Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Je! Mashahidi wa Yehova huepuka kusherehekea siku za kuzaliwa kwa sababu zoea hilo lilikuwa na maana fulani ya kidini katika nyakati za kale?
Mwanzo wa kusherehekea siku za kuzaliwa ni ushirikina na dini bandia, lakini hiyo si sababu kuu au ya pekee ya kwa nini Mashahidi wa Yehova huepuka zoea hilo.
Mazoea mengine yaliyokuwa yenye asili ya kidini hayako hivyo tena katika mahali pengi. Kwa mfano, wakati mmoja pete ya arusi ilikuwa na umaana wa kidini, lakini katika mahali pengi leo, haina umaana huo tena. Kwa hiyo, Wakristo wengi wa kweli hukubali zoea la kwao la kuvaa pete ya arusi ili kutoa ushuhuda kwamba mtu amefunga ndoa. Katika mambo ya jinsi hiyo, jambo linaloongoza mambo kwa ujumla ni kama zoea hilo linafungamana na dini bandia sasa.—Ona “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1973, na Oktoba 15, 1991.
Lakini, haiwezi kukanushwa kwamba vitabu vingi vya marejezo hufunua asili za kishirikina na za kidini za kusherehekea siku za kuzaliwa. The Encyclopedia Americana (chapa ya 1991) huonyesha hivi: “Ulimwengu wa zamani wa Misri, Ugiriki, Roma, na Uajemi ulisherehekea siku za kuzaliwa za miungu, wafalme, na wakuu.” Inasema kwamba Waroma waliadhimisha kuzaliwa kwa Artemi na siku ya Apolo. Tofauti na hilo, “ingawa Waisraeli wa kale walidumisha rekodi za umri za raia wao wa kiume, hakuna ushuhuda wowote kuonyesha kwamba walikuwa na sherehe kwenye tarehe ya kuzaliwa ya kila mwaka.”
Vitabu vingine vya marejezo hueleza sana kuhusu asili ya sherehe za siku ya kuzaliwa: ‘Karamu za siku ya kuzaliwa zilianza zamani katika Ulaya. Watu waliamini katika roho wazuri na waovu, walioitwa nyakati nyingine majini wazuri na waovu. Kila mtu aliwaogopa roho hao, kwamba wangemdhuru mwenye kusherehekea siku yake ya kuzaliwa, na kwa hiyo alizungukwa na marafiki na watu wake wa ukoo ambao kwa kumtakia mema, na kuwapo kwao hasa, kungemlinda dhidi ya hatari zisizojulikana zilizoletwa na siku ya kuzaliwa. Kutoa zawadi kulikuwa ulinzi mkubwa hata zaidi. Kula pamoja kuliandaa ulinzi wa ziada na kulisaidia kuleta baraka za roho wazuri. Kwa hiyo karamu ya siku ya kuzaliwa mwanzoni ilikusudiwa imlinde mtu ili asipatwe na uovu na kuhakikisha kwamba mwaka ujao ungekuwa mzuri.’—Birthday Parties Around the World, 1967.
Hicho kitabu hueleza pia, asili ya desturi nyingi za siku ya kuzaliwa. Kwa mfano: “Sababu ya [kutumia mishumaa] hurudi nyuma hadi wakati wa Wagiriki na Waroma wa mapema waliofikiri kwamba mishumaa ilikuwa na sifa za ajabu. Walikuwa wakitoa sala na kusema haja zao zipelekwe kwa miungu kupitia miale ya mishumaa. Kisha hiyo miungu ingepeleka baraka zao na labda kuzijibu sala.” Habari zaidi juu ya hayo imekusanywa kwenye kurasa 357 na 358 ya kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, kilichotangazwa kwa chapa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
Hata hivyo, kama ilivyotajwa, zaidi yanahusika katika swali hilo kuliko kama kusherehekea siku za kuzaliwa kulikuwa au bado ni jambo la kidini. Biblia huzungumzia habari ya siku za kuzaliwa, na Wakristo wakomavu kwa hekima huitikia kwa vyepesi madokezo yoyote inayotoa.
Watumishi wa Mungu wa zamani waliandika habari wakati ambapo watu mmoja mmoja walizaliwa, jambo lililowaruhusu wahesabu umri. Twasoma kwamba: “Nuhu alikuwa mwenye miaka mia tano, Nuhu akawazaa Shemu, Hamu, na Yafethi.” “Katika mwaka wa mia sita wa maisha ya Nuhu, . . . chemchemi zote za vilindi vikuu zilibubujika kwa nguvu.”—Mwanzo 5:32; 7:11; 11:10-26.
Sawa na alivyotaja Yesu, miongoni mwa watu wa Mungu kuzaliwa kwa mtoto kulikuwa tukio la furaha, lenye baraka. (Luka 1:57, 58; 2:9-14; Yohana 16:21) Hata hivyo, watu wa Yehova hawakuadhimisha tarehe ya kuzaliwa; waliaadhimisha sikukuu fulani za kila mwaka lakini si siku za kuzaliwa. (Yohana 10:22, 23) Encyclopaedia Judaica husema hivi: “Kusherehekea siku za kuzaliwa hakujulikani katika mazoea ya Kiyahudi ya kimapokeo.” Customs and Traditions of Israel huonelea hivi: “Kusherehekea siku za kuzaliwa kumeazimwa kutoka kwa mazoea ya mataifa mengine, kwani hakuna mtajo wowote wa desturi hiyo miongoni mwa Wayahudi ama katika Biblia, Talmudi, ama katika maandishi ya Watu Wenye Hekima wa baadaye. Kwa kweli, ilikuwa desturi ya Misri ya zamani.”
Uhusiano huo wa Misri ni wa wazi kutokana na sherehe ya siku ya kuzaliwa inayosimuliwa katika Biblia, moja ambayo waabudu wa kweli hawakuwa wakiadhimisha. Ilikuwa karamu ya siku ya kuzaliwa ya Farao aliyetawala wakati Yusufu alipokuwa katika gereza la Misri. Baadhi ya wapagani hao huenda ikawa walifurahia karamu hiyo, hata hivyo siku hiyo ya kuzaliwa ilifungamana na kukatwa kichwa kwa mkuu wa waokaji wa Farao.—Mwanzo 40:1-22.
Habari kama hiyo isiyofaa inatolewa kuhusu sherehe ile nyingine ya siku ya kuzaliwa inayoelezwa katika Maandiko—ile ya Herode Antipasi, mwana wa Herode Mkuu. Sherehe hiyo ya siku ya kuzaliwa haionyeshwi hata kidogo katika Biblia kuwa karamu tu isiyo na hatia. Badala ya hivyo, ulikuwa wakati wa kukatwa kichwa kwa Yohana Mbatizaji. Kisha, “wanafunzi wake wakaenda, wakamchukua yule maiti, wakamzika; kisha wakaenda wakampasha Yesu habari,” ambaye “aliondoka huko katika chombo, akaenda mahali pasipo watu, faraghani.” (Mathayo 14:6-13) Je! wawazia kwamba wanafunzi hao au Yesu walihisi kuvutiwa na zoea la sherehe za siku ya kuzaliwa?
Kwa sababu ya mwanzo ujulikanao wa kusherehekea siku za kuzaliwa, na la maana zaidi, jinsi habari isiyofaa kuhusu kusherehekea huko inavyotolewa katika Biblia, Mashahidi wa Yehova wana sababu za kutosha za kuepukana na zoea hilo. Hawahitaji kufuata desturi hiyo ya kilimwengu, kwani wanaweza kuwa na wanayo milo yenye furaha wakati wowote katika mwaka. Kutoa kwao zawadi si jambo la lazima au linaloshurutishwa na kikusanyiko cha kijamii; ni kushiriki zawadi kwa hiari wakati wowote kwa sababu ya ukarimu na shauku ya kweli.—Mithali 17:8; Mhubiri 2:24; Luka 6:38; Matendo 9:36, 39; 1 Wakorintho 16:2, 3.