Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 9/1 kur. 26-30
  • Yehova Amenitunza Vema

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Amenitunza Vema
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Maisha ya Mapema
  • Kuwatolea Watu wa Ukoo Ushahidi
  • Baraka Ujapokuwa Upinzani
  • Ushuhuda Mwingineo wa Utunzaji wa Yehova
  • Mgawo Ng’ambo
  • Mapendeleo ya Utumishi ya Ziada —Na Jaribu
  • 1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • “Kutafuta Kwanza Ufalme”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Nahodha James Cook—Mvinjari Hodari wa Pasifiki
    Amkeni!—1995
  • Jinsi Mimi Nilivyoshinda Tamaa ya Kutaka Sana Kusifiwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 9/1 kur. 26-30

Yehova Amenitunza Vema

NILIANZA kumtumikia Yehova katika njia isiyo ya kawaida, kwa kusema machache. Nilikua katika eneo zuri la mashambani la sehemu ya kaskazini kabisa ya New Zealandi, lililokaliwa hasa na Wamaori kama mimi. Nilipokuwa nikisafiri juu ya farasi siku moja, nilikaribiwa barabarani na binamu yangu Ben. Ilikuwa 1942, katika vuli (Kizio cha Kusini, masika katika Kizio cha Kaskazini). Nilikuwa na miaka 27 na wakati huo nikiwa mshiriki mwenye bidii wa Kanisa la Uingereza.

Kwa miaka mingi Ben alikuwa amekuwa akisoma vitabu vya Judge Rutherford, ambaye wakati huo alikuwa msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society, na sasa Ben alikuwa na barua mkononi mwake kutoka kwenye ofisi kuu ya New Zealandi ya Watch Tower Society iliyokuwa ikimwomba awaalike watu wa huku kwenye mahali ambapo wangeweza kuadhimisha Chakula cha Jioni cha Bwana pamoja. Zaidi ya hayo, Ben alitakwa apange ili mtu fulani aje kuongoza mkutano huo. Akinitazama nikiwa juu, Ben alisema hivi: “Wewe ndiye mtu huyo.” Nikionea fahari kuonwa kuwa mwenye kustahili—na nikiwa mtu aliyeshiriki mkate na divai katika komunyo kanisani—nilikubali.

Katika jioni hiyo, watu karibu 40 walikusanyika katika nyumba ya Ben kwa ajili ya mwadhimisho wa kifo cha Bwana wetu, na hakuna hata mmoja wao aliyekuwa Shahidi wa Yehova. Nilipowasili binamu yangu alinipa muhtasari wa hotuba hiyo. Niliuacha wimbo uliodokezwa nikamwomba ndugu mkwe wa Ben afungue kwa sala. Kisha nikaanza kutoa habari iliyotolewa muhtasari, iliyokuwa na mfululizo wa maswali pamoja na majibu yenye msingi wa Kimaandiko. Kasisi wa huku aliyekuwako alikatiza-katiza kwa mabishano, lakini hayo yalijibiwa kwa kusoma Maandiko yaliyotajwa katika muhtasari.

Ninakumbuka kwamba mojawapo la maswali katika muhtasari huo lilihusu wakati wa mwaka ambapo tukio hilo lingeadhimishwa. Iliridhisha kama nini wakati wote waliokuwako walipotazama nje ya dirisha na kuona mwezi mpevu. Kwa wazi, tarehe ilikuwa Nisani 14.

Huo ulikuwa usiku ulioje! Mwadhimisho wetu uliendelea kwa muda wa saa nne! Maswali mengi yalitokea na kujibiwa kutokana na Maandiko katika muhtasari wa Sosaiti. Nikikumbuka yaliyotukia, najua ya kwamba nisingeweza kuokoka ono hilo bila utunzaji wa Yehova wenye upendo—ingawa wakati huo sikuwa mmoja wa Mashahidi wake waliojiweka wakfu. Hata hivyo, katika usiku huo wa ukumbusho katika 1942, nilivumbua kusudi langu maishani.

Maisha ya Mapema

Nilizaliwa katika 1914. Baba yangu alikuwa amekufa miezi minne hivi kabla ya kuzaliwa kwangu, na ninakumbuka nikiwa mtoto mchanga nikiwaonea wivu watoto wengine waliokuwa na akina baba wa kuwapenda. Nilikosa hilo sana. Kwa mama yangu maisha bila mume yalikuwa magumu sana, yakizidiwa na matokeo mabaya sana ya Vita ya Ulimwengu 1.

Nikiwa kijana, nilimwoa mwanamke mchanga aitwaye Agnes Kope, naye amekuwa mwenzi wangu maishani kwa miaka zaidi ya 58. Mwanzoni tulijitahidi pamoja ili kufanikiwa maishani. Nilikosa kufaulu kuwa mkulima kwa sababu ya ukame mkali. Nilipata kitulizo fulani katika michezo, lakini mpaka Ukumbusho ule wa 1942, sikuwa na kusudi maishani.

Kuwatolea Watu wa Ukoo Ushahidi

Baada ya Ukumbusho huo, nilijifunza Biblia kwa bidii, nikizungumza na baadhi ya binamu zangu vichapo vya Biblia vilivyotangazwa kwa chapa na Watch Tower Society. Katika Septemba 1943 baadhi ya Mashahidi wa Yehova kutoka eneo tofauti walikuja kutembelea jumuiya yetu iliyokuwa peke yayo. Tulikuwa na mazungumzo yenye mambo mengi ya muda wa saa nne. Halafu, nilipopata kujua kwamba wangeondoka asubuhi ifuatayo, niliuliza hivi: “Ni nini kinachonizuia nisibatizwe sasa?” Wawili wa binamu zangu na mimi tukazamishwa majini saa saba na nusu za usiku.

Baadaye, nilisafiri sana kuwatolea watu wangu wa ukoo ushahidi. Baadhi yao waliitikia, na kwao nilitegemeza mazungumzo yangu kwenye Mathayo sura 24. Wengine hawakuitikia, na katika visa hivyo niliyatumia maneno ya Yesu kwa Mafarisayo yaliyorekodiwa katika Mathayo sura 23. Lakini baadaye, nilijifunza kuwa mwenye busara zaidi, kwa kumwiga Baba yetu wa kimbingu mwenye fadhili na upendo.—Mathayo 5:43-45.

Mwanzoni mke wangu alipinga tamaa yangu ya kutaka kumtumikia Yehova. Hata hivyo, upesi alijiunga nami, na katika Desemba 1943 akawa msaidizi wangu aliyejiweka wakfu na kubatizwa. Waliojiunga na yeye katika ubatizo siku hiyo yenye kukumbukwa walikuwa wengine watano kutoka kijiji chetu cha Waima, wakiongeza jumla ya wahubiri wa Ufalme katika eneo hilo hadi tisa.

Baraka Ujapokuwa Upinzani

Wakati wa 1944 tulitembelewa tena na ndugu kutoka eneo tofauti, na wakati huu waliandaa mazoezi yaliyohitajiwa katika huduma rasmi ya nyumba kwa nyumba. Kuwapo kwetu katika jumuiya hiyo kulipokuwa wazi zaidi, upinzani kutoka kwa wawakilishi wa Jumuiya ya Wakristo uliongezeka. (Yohana 15:20) Kulikuwako kukabiliana tena na tena na makasisi wa huku, kukitokeza mazungumzo marefu ya kimafundisho. Lakini Yehova alitoa ushindi, na washiriki wengine wa jumuiya hiyo, kutia na dada yangu, wakaja chini ya utunzaji wa Yehova wenye upendo.

Kundi lilifanyizwa Waima katika Juni 1944. Mnyanyaso na chuki ya kidini iliongezeka. Mashahidi wa Yehova walikataliwa maziko katika makaburi ya huku. Nyakati nyingine upinzani ulikuwa wenye jeuri. Kulikuwako makabiliano ya kimwili. Gari langu na nyumba lilimoegeshwa viliteketezwa kabisa. Hata hivyo, kwa baraka ya Yehova, katika muda usiozidi miezi mitatu, tuliweza kununua lori. Na nilitumia mkokoteni mkubwa wenye kuburutwa na farasi ili kuichukua kwenye mikutano, familia yangu iliyokuwa ikiongezeka.

Idadi ya washiriki yenye kuongezeka ilimaanisha kwamba tulikuwa na uhitaji wa muhimu wa kupata mahali pakubwa zaidi pa kukutania, kwa hiyo tuliamua kujenga Jumba la Ufalme katika Waima. Hilo lilikuwa Jumba la Ufalme la kwanza katika New Zealandi. Miezi minne baada ya miti ya kwanza kukatwa katika Desemba 1, 1949, kusanyiko la pamoja na kuweka wakfu lilifanywa katika jumba hilo jipya lenye kutosha watu 260. Katika siku hizo hilo lilikuwa fanikio kubwa, lililotimizwa na msaada wa Yehova.

Ushuhuda Mwingineo wa Utunzaji wa Yehova

Kwa kuwa idadi ya wapiga mbiu ya Ufalme katika sehemu ya kaskazini kabisa ya New Zealandi iliendelea kukua, waangalizi wasafirio waliokuwa wakitembelea walitoa kitia-moyo cha kutumikia mahali penye uhitaji mkubwa zaidi. Katika 1956, kwa kuitikia hilo, niliihamisha familia yangu Pukekohe, kusini tu mwa Auckland. Tulitumikia huko kwa miaka 13.—Linganisha Matendo 16:9.

Mifano miwili ya utunzaji wa Yehova katika wakati huo hujitokeza katika kumbukumbu yangu. Nilipoajiriwa kazi na baraza la wilaya nikiwa dereva wa lori na mwenye kuendesha mashine, nilialikwa kwenye mtaala wa majuma manne wa Shule ya Huduma ya Ufalme kwenye ofisi ya tawi ya Watch Tower Society katika Auckland. Niliomba liziko la majuma manne kwa kusudi hilo, na mhandisi mkuu akasema: “Bila shaka. Natamani watu wote wawe kama wewe. Unaporudi njoo unione ofisini mwangu.” Nilipotembelea ofisi yake baadaye, nilipokea mshahara wa yale majuma manne ambayo sikuwako. Hivyo, mahitaji ya kimwili ya familia yangu yalitunzwa.—Mathayo 6:33.

Huo ulikuwa mfano wa kwanza. Wa pili ulitukia baada ya mke wangu na mimi kuingia utumishi wa upainia wa kawaida katika 1968. Tena, tulimtegemea Yehova ili kupata utegemezo, naye alituthawabisha. Asubuhi moja baada ya kiamshakinywa, mke wangu alifungua mlango wa friji na hakupata chochote ila robo kilogramu ya siagi. “Sarn,” akasema, “hatuna chakula. Je! tungali twaenda nje katika utumishi leo?” Jibu langu? “Ndiyo!”

Kwenye nyumba yetu ya kwanza tuliyotembelea, mwenye nyumba alikubali vichapo tulivyomtolea na kwa fadhili akatupa sisi mayai kumi na mawili yakiwa upaji. Mtu wa pili tuliyemtembelea alitupa zawadi ya mboga—kumara (viazi vitamu), koliflawa, na karoti. Vyakula vingine tulivyorudi navyo nyumbani siku hiyo vilikuwa nyama na siagi. Maneno ya Yesu yalikuwa ya kweli kama nini katika kisa chetu: “Waangalieni ndege wa angani, ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao. Ninyi je! si bora kupita hao?”—Mathayo 6:26.

Mgawo Ng’ambo

Rarotonga katika Visiwa vya Kuk! Huo ndio uliokuwa mgawo wetu wa upainia wa pekee katika 1970. Vingekuwa makao yetu kwa miaka minne ambayo ingefuata. Tatizo la kwanza huko lilikuwa kujifunza lugha mpya. Hata hivyo, kwa sababu ya maneno yanayofanana katika Kimaori cha New Zealandi na Kimaori cha Kisiwa cha Kuk, niliweza kutoa hotuba yangu ya watu wote ya kwanza majuma matano baada ya kuwasili.

Katika Visiwa vya Kuk, kulikuwako wahubiri wa Ufalme wachache, na hatukuwa na mahali pa kukutania. Tena, kwa kujibu sala, Yehova aliandaa mahitaji yetu. Mazungumzo ya vivi hivi pamoja na mwenye duka mmoja yalitokeza kukodi kwetu shamba lililofaa, na katika mwaka mmoja tulikuwa na nyumba ndogo na Jumba la Ufalme lililoweza kutosha watu 140. Kufikia wakati huo na kuendelea tulipokea baraka baada ya baraka, kwa sifa ya Yehova.

Jambo lililothaminiwa hasa lilikuwa ule ukaribishaji-wageni wa kisiwa tulioonyeshwa. Mara nyingi, tulipokuwa hudumani, tulipewa vinywaji vya kuburudisha—vilivyokaribishwa sana katika hali ya anga hiyo yenye joto na uchepechepe. Mara nyingi tungewasili nyumbani na kupata ndizi, mapapai, maembe, na machungwa yakiwa yameachwa mlangoni petu bila mtajo wa nani aliyeyaacha.

Katika 1971 mke wangu na mimi, tuliandamana na wahubiri wengine watatu kutoka Rarotonga, tukasafiri kwenda kisiwa cha Aitutaki, kilichojulikana kwa wangwa wacho wenye kupendeza. Tuliwapata wapendao Neno la Mungu miongoni mwa wakazi wa huko ambao ni wakaribishaji-wageni tukaanza mafunzo ya Biblia nyumbani manne, tuliyoendelea nayo kwa barua baada ya kurudi kwetu Rarotonga. Baadaye wanafunzi hao katika Aitutaki walibatizwa, na kundi likafanyizwa. Katika 1978 Jumba la Ufalme la pili katika Visiwa vya Kuk likajengwa huko. Yehova aliendelea kukuza mambo kwa kuitikia kupanda na kutilia maji kwetu.—1 Wakorintho 3:6, 7.

Nilikuwa na pendeleo la kutembelea visiwa kumi katika kile kikundi cha Visiwa vya Kuk, mara nyingi chini ya hali zenye kujaribu. Safari moja kwa mashua kwenda Atiu, kilichokuwa mwendo wa kilometa 180 kutoka hapo, ilihitaji muda uliozidi siku sita kwa sababu ya pepo zenye nguvu na bahari iliyochafuka. (Linganisha 2 Wakorintho 11:26.) Hata ingawa ugavi wa chakula ulikuwa mdogo na wengi waliokuwa karibu nami walikuwa na ugonjwa wa bahari, nilishukuru kwa ajili ya utunzaji wa Yehova, ulionifanya nifike salama nilikokuwa nikienda.

Katika 1974 tulinyimwa ruhusa ya kukaa katika Visiwa vya Kuk na kwa hiyo tulihitaji kurudi New Zealandi. Kufikia wakati huo kulikuwako makundi matatu kwenye visiwa hivyo.

Mapendeleo ya Utumishi ya Ziada —Na Jaribu

Katika New Zealandi, milango mipya ya fursa ilifunguka. (1 Wakorintho 16:9) Sosaiti ilihitaji mtu ambaye angeweza kutafsiri Mnara wa Mlinzi na vichapo vya Biblia katika Kimaori cha Visiwa vya Kuk. Nilipewa pendeleo hilo, nalo limekuwa langu hadi siku ya leo. Halafu nilikuwa na pendeleo la kufanya ziara za kawaida za kuwarudia ndugu zangu katika Visiwa vya Kuk, kwanza nikiwa mwangalizi wa mzunguko, kisha nikiwa mwangalizi wa wilaya badala.

Kwenye mojawapo ya ziara hizo, Ndugu Alex Napa, painia wa pekee kutoka Rarotonga, alienda pamoja na mimi kwenye safari ya baharini ya siku 23 iliyotupeleka Manahiki, Rakahanga, Penrhyn—visiwa katika sehemu ya kaskazini ya Visiwa vya Kuk. Katika kila kisiwa, Yehova aliisukuma mioyo ya watu wa huko wenye ukaribishaji-wageni watuandalie makao na wakakubali vichapo vingi vya Biblia. (Linganisha Matendo 16:15.) Katika visiwa hivyo, chaza watokezao lulu ni wengi sana, na mara nyingi watu walitoa lulu kuwa michango ya gharama za kazi ya kuhubiri ya ulimwenguni pote. Kwa hiyo, tulipotoa lulu za kiroho, tulipokea lulu halisi.—Linganisha Mathayo 13:45, 46.

Upande huo wa ulimwengu uliokuwa pekee ni wenye kupendeza kama nini! Ebu wazia papa weupe wakubwa wakiogelea pamoja na watoto katika wangwa! Anga za usiku zilitokeza mandhari mzuri ajabu kama nini! Maneno ya mtunga zaburi ni ya kweli kama nini: “Mchana husemezana na mchana, usiku hutolea usiku maarifa.”—Zaburi 19:2.

Halafu miaka tisa iliyopita, jaribu halisi la uaminifu-maadili likaja. Mke wangu alilazwa hospitali akiwa na mtoko wa damu ubongoni. Upasuaji ulihitajiwa, lakini daktari huyo hakuweza kukubali kuufanya bila damu. Mke wangu na mimi tusingeweza kwa kudhamiria kukubali utaratibu ambao ungevunja sheria ya Mungu. Lakini dhamiri ya daktari-mpasuaji huyo ilielekeza kwamba kila njia iwezekanayo, kutia na damu, itumiwe ili kuokoa uhai.

Afya ya mke wangu ilidhoofika, naye aliwekwa katika wadi yenye utunzaji mkubwa, akiruhusiwa kutembelewa mara chache tu. Alipoteza uwezo wake wa kusikia kwa ajili ya mbano kwenye viwambo vya masikio. Hali ikawa ya hatari sana. Baada ya ziara moja daktari mmoja alinifuata hadi gari langu, akisisitiza kwamba nafasi ya mke wangu ya pekee ilikuwa upasuaji kwa kutumia damu na akinisihi nikubali ufanywe. Hata hivyo, mke wangu na mimi tulimtumaini Yehova—hata ingawa kutii sheria yake kungetokeza kupoteza miaka michache katika uhai wa sasa.

Kwa ghafula, kukawa na maendeleo yenye kutokeza katika hali ya mke wangu. Niliwasili siku moja na kumpata akiketi kitandani akisoma. Siku zilizofuata alianza kutoa ushahidi kwa wagonjwa na wauguzi. Kisha, nikaitwa kwenda kwenye ofisi ya daktari-mpasuaji. “Bw. Wharerau,” akasema, “wewe kwa kweli ni mtu mwenye baraka! Twaamini kwamba tatizo la mke wako limepona.” Bila kutazamiwa, msukumo wake wa damu ulikuwa umesawazika. Mke wangu na mimi, tukiwa pamoja, tulimshukuru Yehova tukafanya upya azimio letu la kufanya kadiri tuwezavyo katika utumishi wake.

Sasa nimepewa tena mgawo wa kwenda kwenye Visiwa vya Kuk na ninatumikia tena katika Rarotonga. Ni pendeleo lenye baraka kama nini! Tunapokumbuka yaliyopita mke wangu na mimi hushukuru kwa ajili ya utunzaji wa Yehova kwa muda uliozidi miongo karibu mitano katika utumishi wake. Kimwili, hatujawa kamwe bila riziki za maisha. Kwa maana ya kiroho, baraka zimekuwa nyingi mno kuhesabu. Yenye kutokeza ni idadi ya watu wangu wa ukoo wa kimnofu ambao wamekubali kweli. Naweza kuhesabu zaidi ya 200 ambao sasa ni Mashahidi wa Yehova waliobatizwa kutia na wazao wa moja kwa moja 65. Mwana mjukuu mmoja ni mshiriki wa familia ya Betheli ya New Zealandi, huku binti mmoja pamoja na mume wake na wana wawili wakiwa wanafanya kazi ya ujenzi kwenye matawi.—3 Yohana 4.

Ninapotazama mbele, ninathamini sana lile taraja la kuishi katika paradiso ambayo, duniani pote, uzuri utapita hata ule wa lile bonde lenye kupendeza la majani mabichi nilikozaliwa. Litakuwa pendeleo lililoje kuwakaribisha mama na baba yangu wakati wa ufufuo na kuwaarifu juu ya fidia, Ufalme, na ushuhuda mwingine wote wa utunzaji wa Yehova.

Azimio langu, likitegemezwa na maarifa ya kwamba Mungu hunitunza, ni kama alivyotaarifu mtunga zaburi kwenye Zaburi 104:33: “Nitamwimbia BWANA [Yehova, NW] maadamu ninaishi; nitamshangilia Mungu wangu nikiwa hai.”—Kama ilivyosimuliwa na Sarn Wharerau.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Jumba la Ufalme la kwanza lililojengwa katika New Zealandi, 1950

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki