Jinsi Mimi Nilivyoshinda Tamaa ya Kutaka Sana Kusifiwa
Kama ilivyosimuliwa na Waikato Gray
KUZALIWA kwangu katika Desemba 2 1928, kulihusiana na tukio kubwa. Mimi nilizaliwa nikiwa nimeketi badala ya kuwa nimelala, na karibu jambo hilo limalize uhai wangu na pia ule wa mama. Kwa sababu hiyo, nilizaliwa nikiwa na miguu iliyopindika. Uzuri ni kwamba, shangazi wangu mkubwa alijihusisha katika jambo hilo na mwishowe akainyoosha miguu. Kwa kufikiria maisha ambayo ningeishi nikiwa Maori katika New Zealand, msaada wake ulikuwa wa maana sana.
Baba yangu, Clark Gray, alikuwa wa kabila la Wamaori wa Ngati-Tuwharetoa na mama, Hore Teree, alitoka katika kabila la Ngati-Kahungunu. Kulingana na ukoo wa vizazi vya Wamaori wa kale, mimi nilikuwa na urithi mzuri, kwa maana nilikuwa nimetokana na ukoo wa machifu wawili wa kabila waliokuwa na tamaa ya kutaka sana kusifiwa. Basi tamaa ya makuu ikawa kani yenye kusukuma maisha yangu pia.
Kuinuka na Kuacha Umaskini
Mimi nilikuwa wa tatu katika ile ambayo baadaye ikawa jamaa yenye watoto wanane. Ilikuwa kipindi cha ule Mshuko Mkuu wa thamani ya pesa, na wazazi wangu walikuwa maskini sana. Sisi sote kumi tuliishi katika nyumba yenye vyumba viwili katika Bay View, karibu na Napier, North Island, New Zealand. Mimi nakumbuka vizuri kwamba kila siku nilikuwa nikifanya kazi ya kuokota kuni karibu ya ufuo wa bahari na kuchukua maji ya lita 15 yakiwa katika debe la mafuta-taa niliyoyachota katika kisima cha jirani. Tulikuwa tukitembea kilometa nane miguu mitupu kwenda shuleni, wakati wa kiangazi na wa baridi pia.
Umaskini huo uliongeza tamaa yangu ya kutaka sana kusifiwa nijitengenezee wakati ujao ulio bora—kupata elimu bora na kuwa mtu mashuhuri. Mahali pa kuanzia palikuwa shuleni. Ingawa niliendelea vizuri katika masomo yangu, niliwazidi wengine pia katika michezo ya riadha na mpira wa ragbi. Nikawa ndimi mkimbiaji mwenye haraka zaidi katika shule yetu ya sekondari na baada ya muda mfupi nikafanywa mshiriki wa timu ya ragbi. Sifa yangu ya kucheza ragbi nikiwa mchezaji-upande wa robo tatu za uwanja aliye mmoja wa walio hodari zaidi katika shule zote ilienea katika sehemu zote za North Island.
Nilipotoka shule nilienda chuo cha mazoezi ya walimu kule Wellington na pia nikatumia mwaka mmoja katika Chuo Kikuu cha Victoria kabla ya kuanza cheo cha ualimu kwenye Shule ya Sekondari ya Wilaya ya Manutahi. Nilipokuwa kule, nilichaguliwa niwe mchezaji wa kujaribiwa wa timu ya ragbi ya Weusi Wote Wamaori. Wamaori wengi wanaishi wakitazamia sana siku ambayo wataweza kuchezea timu ya ragbi ya taifa la New Zealand. Nilijisikia nimependelewa sana kushiriki katika majaribio hayo.
Tamaa zangu za kutaka sana kusifiwa zilikuwa zikitimia. Mimi nilikuwa mwalimu Mmaori na kwa sababu hiyo nilikuwa nimepata kutambuliwa katika masomo na michezo pia. Umaskini ulikuwa umepungua—lo, tofauti kubwa kama nini na jinsi mimi nilivyokuwa mvulana Mmaori maskini katika miaka ya 1930!
Je! Unalijua Jina la Mungu?
Karibu na wakati ule nilipokuwa chuoni, nilikuwa na sababu ya kuchunguza dini kwa uangalifu mwingi. Nilikuwa nimelelewa nikiwa Mwanglikana. Kwa kweli, ibada za kanisani ziliendeshwa katika nyumba yetu wakati mmoja. Jaribu la kweli kweli lilikuja wakati baba alipokufa. Nikaendelea kujiuliza ni kwa sababu gani Mungu alichukuwa baba hali alihitajiwa sana sana na mama na watoto wake wanane. Lilionekana kuwa jambo lisilo la haki kufanya hivyo.
Karibu na wakati huo mama akaanza kuhudhuria mafunzo ya Biblia ambayo Mashahidi wa Yehova walikuwa wakiongoza kwa majirani fulani. Mimi nilichukizwa sana. Sisi tulikuwa na imani yetu wenyewe, kwa hiyo mbona yeye ajihangaishe na Mashahidi hao?
Halafu siku moja Rudolph Rawiri, Shahidi wa eneo hilo, akaja kunitembelea. Niliamua kwamba ningemnyosha awe laini kabisa. Lakini tabasamu yake na tabia yake yenye kufurahisha watu ilinimaliza nguvu za kumpinga. Yeye aliuliza ulizo rahisi: Je! unalijua jina la Mungu? Nikajibu, “Yesu.” Yeye akaniomba nifungue Biblia yangu ya King James kwenye Zaburi 83:18. Lo, mshangao gani! Mle mle ndani ya Biblia yangu mwenyewe nikaona jina la Mungu; “Kwamba watu wapate kujua kwamba wewe, ambaye jina lake pekee ni YEHOVA, ndiwe Aliye Juu Zaidi Sana ya dunia yote.”
Nilivutwa na jambo hilo. Mbona kanisa langu halikuwa limekazia jina takatifu hilo? Baadaye, Shahidi mwingine Mmaori, Charles Tareha, alikuja nyumbani kwetu akaongoza funzo la Biblia la kawaida pamoja nasi. Sisi tulitambua kwamba huo ulisikika kuwa ndio ukweli wa Biblia nasi tukakata uhusiano wote na Kanisa la Uingereza. Mimi nikawa Shahidi aliyebatizwa 1955.
Kilichofanya Ukweli Univute Mimi
Kwa kuwa mimi nilikuwa nimelelewa nikiwa Mwanglikana, kwa sababu gani mafundisho ya Mashahidi wa Yehova yakanivutia? Walipokuwa wakieleza Neno la Mungu, nilivutwa na urahisi wa maelezo yao na sababu za kiakili walizotumia. Bila shaka, urahisi wenyewe huo unakuwa kipingamizi cha kuzuia watu wengi. Lakini mimi nilipata kuona kwamba Biblia ina kanuni za msingi, sheria, na mielekezo kwa tatizo lo lote linalotokea maishani.—Linganisha Zaburi 119.
Ndivyo ilivyokuwa hasa katika maisha ya ndoa. Katika Biblia, nilipata miongozo ya kuwa na ndoa yenye mafanikio. Ilinisaidia kuona mahali ambapo mimi ningeweza kufanyia maendeleo nikiwa mume na baba kwa kukubali madaraka yangu. Bila shaka, lilikuwa tukio zuri sana nikaweza kupata mke mwema kama Hinewaka, wa Kabila la Pwani ya Mashariki la Ngati-Porou. Tulifunga ndoa 1954. Yeye aliukubali ukweli wa Biblia kwa utayari, nasi tumekuwa wenye ushirikiano katika kutumia kanuni za Neno la Mungu.—Ona Mithali 31:10-31.
Nilivutwa sana pia na viwango bora vya maadili ambavyo Mashahidi wanafuata. Ili kuwa na msimamo unaokubaliwa na Yehova, ni lazima mtu aache mwenendo wote wa ukosefu wa adili—matendo yote ya uasherati, uzinzi, kusema uwongo, kuiba, kutenda jeuri, uuaji, chuki na ukabila yamekatazwa na Neno la Mungu. Niliweza kuona faida za mwenendo mwema kwangu na kwa wengine. Mwenendo huo haukuleta matunda yo yote mabaya ya kufanya nisikitike.—1 Wakorintho 6:9, 10.
Ninawekwa Huru Niache Ushirikina
Mambo ya ushirikina wa Wamaori yaliambatana kabisa na urithi wangu wa Kimaori. Sisi tulikuwa tukiogopa sana nafsi za waliokufa, na mafundisho ya Kianglikana juu ya nafsi isiyoweza kufa yalisaidia tu kuniongezea woga wa Kimaori niliokuwa nao kuhusu mambo mbali-mbali. Lakini nilipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi, nikajua kwamba Yesu alikuwa amesema: “Tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.” (Yohana 8:32) Ndiyo, maarifa sahihi ya Neno la Mungu yaliniweka huru nikatoka katika utumwa wa mambo ya ushirikina wa Wamaori.
Nakumbuka kisa kimoja. Babu yangu alikufa, na katika muda wa saa 48 baada ya hapo nyanya yangu akafa pia kwa sababu ya kuvunjika moyo. Yeye alilazwa katika sakafu ya chumba cha maongezi, karibu na babu aliyekuwa ndani ya jeneza. Wamaori wengi wenye umri mkubwa walikuwa wakisimama kando-kando ya maiti ile, lakini wakati mtunza-maiti alipowaomba msaada wa kumwingiza nyanya katika jeneza, wote waliondoka katika chumba hicho! Kama isingalikuwa ni kwa sababu ya maarifa yangu ya kuujua ukweli, hata mimi ningalikimbia. Kwa kujua kwamba wafu wamelala tu katika kifo, mimi sikusita-sita kumsaidia kuinua mwili wa nyanya yangu mpendwa tuingize katika jeneza lake.
Tangu wakati huo, nikiwa mhudumu wa Mashahidi wa Yehova, nimeendesha vipindi vingi vya maziko na nikaweza kufariji watu wengi kwa mafundisho yale rahisi juu ya Biblia kuhusu wafu. Nafikiri ule urahisi wa masimulizi yaliyo katika Yohana 11:11-44 unafanya suala hilo lieleweke wazi kweli kweli. Yesu alilinganisha kifo na usingizi. Hakuna kutaabika, bali ni kungojea ufufuo tu, kama kwamba mtu amelala usingizi.
Jaribu la Ushikamanifu
Maarifa yenye kina zaidi juu ya Biblia na mfano wa Kristo yalianza kunitia jaribuni. Bado tamaa ya kutaka sana kusifiwa ilikuwa ndiyo kani yenye kusukuma maisha yangu. Kazi yangu ya maisha ya kufundisha na michezo ilikuwa imenitimizia mambo yote niliyotaka. Sasa uchaguzi ulikuwa mbele yangu—ama nichague yale maisha rahisi-rahisi ya unyenyekevu nikiwa shahidi Mkristo wa Yehova, ama nijaribu kuchanganya tamaa zangu za kutaka sana kusifiwa pamoja na imani niliyokuwa nimepata karibuni.
Mwaka 1957 nilikabili uamuzi mgumu, jaribu la kweli kweli la ushikamanifu wangu kwa Mungu. Nilipewa mgawo wa kutoa hotuba ya Biblia kwenye mkusanyiko wa wilaya wa Mashahidi wa Yehova ambao ungefanywa katika Lower Hutt. Lakini kwa kuwa nilikuwa mwalimu, ilinipasa kuomba ruhusa ya pekee nihudhurie mkusanyiko huo. Baraza la Elimu la Hawke’s Bay lilikataa ombi langu.
Nikawa katika njia panda—je! nibaki shuleni na kukataa mgawo huo wa mkusanyiko? Au nijasirie kupoteza kazi yangu kisha nihudhurie mkusanyiko bila ruhusa? Halikuwa jambo rahisi kuamua. Mimi nilipenda kufundisha, na watoto na wazazi wangu walinitegemea mimi. Mwalimu mkuu alinisihi sana nibaki shuleni. Lakini nikakumbuka maneno ya Yesu, “Mtu ye yote asiyekubali mti wa mateso wake na kunifuata mimi hanistahili mimi.” (Mathayo 10:38, NW) Je! nilikuwa na nia ya kutoa dhabihu ya kimwili ili nipate baraka ya kiroho? Au tamaa yangu ya kutaka sana kusifiwa iliyonisukuma sana ingenizuia kufanya hivyo?
Mimi niliiacha tamaa yangu ya kutaka sana kusifiwa na kazi niliyokuwa nimeipenda tangu utoto wangu, ile ya kufundisha watoto. Nilienda kwenye mkusanyiko wa Kikristo na nikapoteza cheo changu cha kufundisha. Hata hivyo, ninapotazama nyuma ninajua kwamba uamuzi huo ndio uliofaa. Niliacha kufundisha watoto, na kufanya hivyo kukaniongoza mwishowe kwenye kazi ya kufundisha watu wazima katika eneo lililo pana zaidi. Ili kuruzuku jamaa yangu, nikaanza kazi ya usafi na kutunza bustani. Mwishowe nilifanya kazi ya nusu-siku katika afisi na maduka, ikaniwezesha kutumia wakati mwingi zaidi katika huduma.
Jaribu Kali la Afya
Mwaka 1962 hali yangu ilishuka kweli kweli. Nilipokuwa mwanariadha, sikuzote nilikuwa nimeutunza mwili wangu. Halafu, kwa ghafula, nikalazwa na ile tauni nyeupe—kifua kikuu. Niliwekwa katika hospitali ya wenye kusumbuliwa na mapafu katika Waipukurau katika jitihada ya kuponya ugonjwa wangu. Pafu langu halikuponywa na matibabu hayo. Uamuzi wa daktari ukawa kwamba nipasuliwe ili sehemu ya juu ya pafu langu la kushoto iondolewe. Daktari mpasuaji hakutaka kunipasua bila kunitia damu mishipani. Kanuni zangu za Biblia hazingeniruhusu nikubali damu ya mtu mwingine iingizwe katika mfumo wangu. (Matendo 15:28, 29) Nikamdokezea daktari kwamba anitie mishipani vitu vingine vyenye kufanya kazi ya damu ambavyo nilikuwa na nia ya kuvikubali. Yeye akakataa. Nikampelekea Yehova sala kuhusu jambo hilo.
Madaktari waliamua kukomesha matibabu yote ya kutumia dawa. Badala ya hayo, nilipewa matibabu ya kufanyisha mwili kazi kwa mazoezi ya kutembea muda wa majuma mawili. Baada ya hapo nilipigwa picha ya eksirei kisha nikaitwa niingie afisini mwa msimamizi wa hospitali niambiwe uamuzi. Jinsi nilivyoungoja kwa wasiwasi! “Pafu lako limekuwa safi. unaweza kwenda nyumbani,” akasema. Sala yangu ilijibiwa, nami nikarudi nyumbani kwa mke wangu na mtoto wangu.
Kuridhika Katika Utumishi, Si Tamaa ya kutaka Sana Kusifiwa
Nilipozidi kufanya maendeleo nikiwa Shahidi, nikaja kuridhika na vitu vilivyo vya lazima maishani badala ya kutaka sana kusifiwa kwa kuwa na vitu vya kujionyesha nje-nje kwamba nina mafanikio ya kilimwengu. Kwa muda wa miaka 28 nilitumikia nikiwa mzee katika Kundi la Wairoa la Mashahidi wa Yehova. Wairoa ni mji wenye wakaaji 5,000 tu, ambako pia kuna wakaaji wa shambani kama 7,000 au zaidi. Sana-sana wao ni Wamaori, na wao ni wenye urafiki, wanaopenda sana kushirikiana na watu, na ni wakarimu kama watu wengine wote wa Polinesia. Roho hiyo ilionyeshwa katika kundi letu, ambalo lilikua likawa na wahubiri watendaji zaidi ya 90 wa habari njema.
Sehemu moja ya pekee ya huduma yangu ilikuwa kusaidia waume wasioamini. Mmoja wa namna hiyo alikuwa John McAndrew, mvutaji sigareti wa kupindukia na mlevi, aliyejulikana mjini kuwa ndiye mtu mjeuri na mwenye kichwa kigumu zaidi ya wote. Hata hivyo ukweli wa Biblia ulimgeuza, na sasa yeye anatumikia akiwa mwangalizi-msimamizi katika Kundi la Wairoa.
Mume mwingine asiyeamini alikuwa John Salmon, mfanya biashara, aliyehamia Wairoa ili amwondoe mke wake karibu na Mashahidi. Niipomkuta, yeye alikuwa na nia ya kuongea ikiwa tu ningetumia Biblia ya King James. Hilo halikuwa tatizo hata kidogo. Ingawaje, hiyo ndiyo tafsiri kuu ambayo Mashahidi wa Yehova walitumia kabla ya 1950, kabla New World Translation haijatokea kwa mara ya kwanza. Hivyo, kwa kutumia Biblia yake mwenyewe, alisaidiwa autambue na kuukubali ukweli.
Mtu wa kutokeza alikuwa Tutura Waihape, Mmaori kijana aliyeoa, mwenye matumaini mazuri sana ya kufanya mchezo wa ragbi uwe kazi yake ya maisha. Nilipoanza kujifunza Biblia pamoja naye, alikuwa ndiye mwanamume mwenye nywele ndefu zaidi ambazo nimepata kuona. Alipokuwa akisonga mbele katika maarifa ya kujua Yehova na Kristo Yesu, mwelekeo wake ulibadilika. Kupenda ukweli kulikuwa jambo la maana zaidi kwake kuliko kujulikana na watu kwa sababu ya nywele zake ndefu, basi akazikata. Leo, yeye anatumikia katika kundi akiwa mtumishi wa huduma.
Kazi Yangu ya Kufundisha Wakati Wote
Kwa muda wa miaka kumi iliyopita, mimi nimetumikia nikiwa mhudumu painia wa kawaida, nikitumia wastani ya saa 90 kwa mwezi katika huduma. Mke wangu amekuwa painia kwa miaka 15, na watoto wangu watatu wameonja upainia pia baada ya kumaliza shule.
Upeo wa utumishi wetu kwa Yehova ni kwamba mke wangu na mimi sasa tunatumikia mahali ambako pana uhitaji mkubwa zaidi katika Niue Island, njia ya kwenda kaskazini mwa New Zealand, kule mbali katika Bahari Kuu Pasifiki. Tumeona kwamba idadi ndogo ya wakaaji karibu 2,800 ni wenye maelekeo ya kufuata dini, na wengi wanapenda kuzungumza juu ya Biblia. Wakati ambao tumekuwa hapa tumesaidia pia kundi moja dogo liwe na mipango mizuri zaidi ya kitengenezo.
Ile tamaa yangu ya kutaka sana maendeleo na utukufu wa kibinafsi imemalizika. Nimekuja kutambua kwamba utukufu ambao wanadamu wanapasa kumhesabia Yehova Mungu ndio wa maana zaidi. Ni kama vile Mfalme Daudi alivyoeleza jambo hilo: “Mpeni [Yehova], enyi jamaa za watu. Mpeni [Yehova] utukufu na nguvu. Mpeni [Yehova] utukufu wa jina lake.” Hivyo ndivyo sisi tunavyojaribu kufanya hapa katika kisiwa chetu kidogo cha Niue.—1 Mambo ya Nyakati 16:28, 29.
[Picha katika ukurasa wa 12]
Kavalia vazi la asili ya Kimaori