Sura ya 18
“Kutafuta Kwanza Ufalme”
KICHWA kikuu cha Biblia ni kutakaswa kwa jina la Yehova kupitia Ufalme. Yesu Kristo aliwafunza wafuasi wake kutafuta kwanza Ufalme, wakiutanguliza badala ya faida nyinginezo za maisha. Kwa nini?
Mara nyingi Mnara wa Mlinzi limeeleza kwamba kwa sababu ya jambo la kwamba yeye ndiye Muumba, Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima. Yeye ana haki ya kustahiwa kabisa na viumbe vyake. (Ufu. 4:11) Hata hivyo, mapema sana katika historia ya kibinadamu, mwana wa kiroho wa Mungu aliyejifanya Shetani Ibilisi alipinga kwa ukaidi enzi kuu ya Yehova. (Mwa. 3:1-5) Zaidi ya hivyo, Shetani alisingizia kwamba wote waliomtumikia Yehova walifanya hivyo kwa makusudi ya kibinafsi. (Ayu. 1:9-11; 2:4, 5; Ufu. 12:10) Hivyo amani ya ulimwengu wote mzima iliharibiwa.
Kwa muda wa miongo sasa, vichapo vya Watch Tower vimefafanua kwamba Yehova amefanya uandalizi wa kusuluhisha masuala hayo kwa njia inayokuza, si nguvu yake ya uweza yote tu, bali pia ukuu wa hekima yake, haki yake, na upendo wake. Sehemu kuu ya uandalizi huo ni Ufalme wa Mungu wa Kimesiya. Kupitia Ufalme huo, wanadamu wamepewa fursa nyingi kujifunza njia za uadilifu. Kupitia Ufalme huo, waovu wataangamizwa, enzi kuu ya Yehova itatetewa, na kusudi lake litatimizwa la kufanya dunia kuwa paradiso iliyojaa watu wanaopenda Mungu na wenzao kikweli na ambao wanabarikiwa kwa ukamilifu wa uhai.
Kwa sababu ya umaana wao, Yesu alishauri wafuasi wake hivi: “Fulizeni kutafuta kwanza ufalme.” (Mt. 6:10, 33, NW) Mashahidi wa Yehova katika nyakati za kisasa wametoa uthibitisho mwingi kwamba wanajitahidi kufuata shauri hilo.
Kuacha Yote kwa Ajili ya Ufalme
Katika tarehe ya mapema, Wanafunzi wa Biblia walifikiria kile kilichomaanishwa na kutafuta kwanza Ufalme. Walizungumzia kielezi cha Yesu ambacho alilinganisha Ufalme na lulu ya thamani kubwa sana hivi kwamba mtu mmoja ‘aliuza vyote alivyo navyo, akainunua.’ (Mt. 13:45, 46) Walitafakari juu ya umaana wa shauri la Yesu kwa mtawala kijana aliyekuwa tajiri auze kila kitu, agawanye kwa maskini, na kumfuata. (Mk. 10:17-30)a Waling’amua kwamba ikiwa wangestahili kuwa na sehemu katika Ufalme wa Mungu, ni lazima watangulize masilahi ya Ufalme, wakitumia maisha zao, uwezo wao, na mali zao, kwa furaha katika utumishi wao. Vitu vinginevyo vyote maishani vingechukua mahali pa pili.
Charles Taze Russell alitumia binafsi shauri hilo. Aliuza biashara yake ya kuuza nguo za wanaume, akapunguza hatua kwa hatua faida nyinginezo za kibiashara, kisha akatumia mali yake yote ya kidunia kusaidia watu katika njia ya kiroho. (Linganisha Mathayo 6:19-21.) Hilo si jambo alilofanya kwa miaka michache tu. Kufikia kifo chake, alitumia uwezo wake wote—uwezo wake wa kiakili, afya yake ya kimwili, mali zake za kimwili—kuwafunza wengine ujumbe wa maana wa Ufalme wa Mesiya. Kwenye maziko ya Russell, mshirika mmoja, Joseph F. Rutherford, alisema: “Charles Taze Russell alikuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa Mungu, mwaminifu-mshikamanifu kwa Kristo Yesu, na mwaminifu-mshikamanifu kwa kusudi la Ufalme wa Mesiya.”
Katika Aprili 1881 (wakati ambapo mamia machache ya watu walipokuwa wakihudhuria mikutano ya Wanafunzi wa Biblia), Watch Tower lilitangaza makala yenye kichwa “Wahubiri 1,000 Watakwa.” Hiyo ilitia ndani mwaliko kwa wanaume na wanawake ambao hawakuwa na familia zenye kuwategemea waanze kazi wakiwa makolpota waeneza-evanjeli. Kwa kutumia maneno ya kielezi cha Yesu kwenye Mathayo 20:1-16, Watch Tower liliuliza: “Ni nani aliye na tamaa inayowaka ya kwenda kufanya kazi ngumu katika Shamba la Mizabibu, na ambaye amekuwa akisali kwamba Bwana atafungua njia”? Wale ambao wangeweza kutoa angalau nusu ya wakati wao kwa ajili ya kazi ya Bwana kihususa walitiwa moyo watoe maombi. Ili kuwasaidia na gharama za usafiri, chakula, mavazi, na makao, Zion’s Watch Tower Tract Society iliwapa makolpota hao wa mapema fasihi za Biblia ili wazigawanye, ikataarifu mchango wa kiasi ambao ungeweza kuombwa kwa ajili ya fasihi, na kuwaalika makolpota watumie sehemu ya fedha zilizopokewa. Ni nani waliokubali mipango hiyo na kuchukua utumishi wa kolpota?
Kufikia 1885 kulikuwa na makolpota 300 hivi walioshirikiana na Sosaiti. Hatimaye katika 1914 idadi hiyo ilipita 1,000. Haikuwa kazi rahisi. Baada ya kuzuru nyumba nyingi katika miji minne midogo na kupata watu watatu au wanne tu waliopendezwa kwa kiasi fulani, mmoja wa makolpota aliandika: “Ni lazima niseme kwamba nilihisi upweke kidogo kusafiri mbali hivyo, kukutana na wengi sana, na kupata upendezi mdogo sana ulioonyeshwa juu ya mpango wa Mungu na Kanisa. Nisaidieni kwa sala zenu, ili niweze kutoa kweli kwa njia ifaayo na kwa ujasiri, na nisichoke katika kutenda mema.”
Walijitoa Wenyewe kwa Hiari
Makolpota hao walikuwa watanguliza-njia kwelikweli. Waliingia hadi kwenye sehemu za nchi zisizoweza kufikika katika wakati ambapo usafiri ulikuwa wa nyuma sana na sehemu kubwa ya barabara ilikuwa vijia tu vya mikokoteni. Dada Early, katika New Zealand, ni mmoja wa wale waliofanya hivyo. Akianza mapema kabla ya Vita ya Ulimwengu 1, alitumia miaka 34 katika utumishi huo wa wakati wote kabla hajafa katika 1943. Alienda sehemu nyingi za nchi hiyo kwa baiskeli. Hata alipolemaa kwa ugonjwa wa yabisi kavu na hivyo hangeweza kuiendesha, alitumia baiskeli ili aiegemee na kubebea vitabu vyake katika eneo la kibiashara la Christchurch. Yeye angeweza kupanda ngazi, lakini alilazimika kuzishuka kwa kwenda kinyumenyume kwa sababu ya udhaifu wake wenye kulemaza. Hata hivyo maadamu alikuwa na nguvu kidogo, aliitumia katika utumishi wa Yehova.
Watu hao hawakufanya kazi hiyo kwa sababu walijitumainia. Wengine walikuwa wenye woga sana kiasili, lakini walimpenda Yehova. Kabla ya kutoa ushahidi katika eneo la kibiashara, dada mmoja wa namna hiyo aliomba kila Mwanafunzi wa Biblia katika eneo lake asali kwa ajili yake. Baada ya muda, alipata ujuzi, akawa mwenye idili sana katika utendaji huo.
Malinda Keefer alipozungumza na Ndugu Russell katika 1907 kuhusu tamaa yake ya kuanza utumishi wa wakati wote, alisema kwamba alihisi uhitaji wa kupata ujuzi zaidi kwanza. Kwa kweli, ni mwaka mmoja tu uliokuwa umepita alipoona fasihi za Wanafunzi wa Biblia kwa mara ya kwanza. Jibu la Ndugu Russell lilikuwa: “Ikiwa unataka ungoje hadi utakapoyajua yote hutaanza kamwe, bali utajifunza unapoendelea kuifanya.” Bila kusita, yeye alianza upesi katika Ohio, Marekani. Mara nyingi alikumbuka Zaburi 110:3, inayosema: “Watu wako wanajitoa kwa hiari.” Kwa miaka 76 iliyofuata, aliendelea kufanya ivyo hivyo.b Alianza utumishi huo akiwa mseja. Kwa miaka 15 alifurahia kutumikia akiwa ameolewa. Lakini baada ya mume wake kufa, aliendelea tu, kwa msaada wa Yehova. Akikumbuka muda wa miaka iliyopita, yeye alisema: “Nina shukrani kama nini kwamba nilijitoa kwa hiari kuwa painia nilipokuwa mwanamke mchanga na nikatanguliza masilahi ya Ufalme nyakati zote!”
Mikusanyiko ya ujumla ilipofanywa katika siku za mapema, mara nyingi mipango ilifanywa kwa ajili ya vipindi vya pekee pamoja na makolpota. Maswali yalijibiwa, mazoezi yaliandaliwa kwa ajili ya wapya, na kitia-moyo kilitolewa.
Kuanzia 1919 kuendelea, kulikuwa na watumishi wengi zaidi wa Yehova waliothamini Ufalme wa Mungu sana hivi kwamba wao pia walitegemeza maisha zao kikweli juu ya Ufalme. Wengine wao waliweza kuacha kufuatia miradi ya kilimwengu na kujitoa wenyewe kikamili katika huduma.
Kushughulikia Mahitaji ya Kimwili
Walishughulikiaje mahitaji yao ya kimwili? Anna Petersen (baadaye Rømer), mweneza-evanjeli wa wakati wote katika Denmark, akumbuka: “Tulipata msaada kutoka kwa fasihi tulizoangusha ili kulipia gharama za kila siku, na mahitaji yetu hayakuwa makubwa. Kulipokuwa na gharama kubwa zaidi, hizo zililipiwa kwa njia moja au nyingine. Dada walikuwa wakitupatia nguo, marinda au makoti, na tungeyavaa mara hiyo, na hivyo tulivalia vizuri. Na katika nyakati fulani za baridi kali, nilifanya kazi ya ofisi kwa miezi kadhaa. . . . Kwa kununua mavazi wakati bei zilipokuwa chini, ningeweza kununua nguo nilizohitaji za mwaka mzima. Mambo yalienda sawa. Hatukuwa kamwe na uhitaji.” Vitu vya kimwili havikuwa hangaiko lao kuu. Upendo wao kwa Yehova na njia zake ulikuwa kama moto uwakao ndani yao, na ilikuwa lazima wauonyeshe tu.
Ili kupata malazi, wangekodi chumba kidogo huku wakihubiria watu katika eneo hilo. Wengine wao walitumia trela—kitu sahili, mahali tu pa kulala na kulia. Wengine walilala katika mahema na kuhamahama. Mahali pengine, ndugu walipanga kuwa na “kambi za mapainia.” Huenda Mashahidi katika eneo hilo wakaandaa makao, na mtu mmoja angegawiwa kuyasimamia. Mapainia waliotumikia katika eneo hilo wangeweza kutumia makao hayo, na wangeshiriki kulipa gharama zilizohusika.
Wafanyakazi hao wa wakati wote hawakuruhusu ukosefu wa pesa uwazuie watu wenye mfano wa kondoo kupata fasihi za Biblia. Mara nyingi mapainia walibadilishana fasihi kwa mazao kama viazi, siagi, mayai, matunda yaliyotoka kuchumwa au ya mkebe, kuku, sabuni na karibu kitu kingine chochote. Hawakuwa wanakuwa matajiri; badala yake, hiyo ilikuwa njia ya kuwasaidia watu wanyoofu wapate ujumbe wa Ufalme, hali wakati uleule wakipata mahitaji ya kimwili yaliyo ya lazima kwa maisha ili mapainia waweze kuendelea na huduma yao. Walikuwa na uhakika katika ahadi ya Yesu kwamba ikiwa ‘wangetafuta kwanza Ufalme na uadilifu wa Mungu,’ basi chakula na mavazi yanayohitajiwa yangeandaliwa.—Mt. 6:33, NW.
Wenye Nia Kutumika Kokote Kulikokuwa na Uhitaji
Tamaa yao ya moyoni ya kufanya kazi ambayo Yesu alikuwa amewagawia wanafunzi wake iliwaongoza wafanyakazi hao wa wakati wote kwenye maeneo mapya, hata kwa nchi mpya. Frank Rice alipoalikwa aondoke Australia ili akafungue kazi ya kuhubiri habari njema katika Java (sasa ni sehemu ya Indonesia) katika 1931, alikuwa amepata ujuzi wa miaka kumi katika huduma ya wakati wote. Lakini sasa kulikuwa na desturi mpya, kutia na lugha mpya za kujifunza. Angeweza kutumia Kiingereza kutoa ushahidi kwa wengine madukani au maofisini, lakini alitaka kutolea wengine ushahidi pia. Yeye alijifunza kwa bidii, na katika miezi mitatu alijua Kiholanzi cha kutosha kuanza kwenda nyumba hadi nyumba. Kisha akajifunza Kimaleya.
Frank alikuwa na miaka 26 tu alipoenda Java, na kwa sehemu kubwa ya miaka sita aliyokuwa huko na Sumatra, alifanya kazi akiwa peke yake. (Kuelekea mwisho wa 1931, Clem Deschamp na Bill Hunter walikuja kutoka Australia ili kusaidia kazi. Wakiwa kikundi, walifanya ziara ya kuhubiri kuelekea bara, huku Frank akifanya kazi katika jiji kuu la Java. Baadaye, Clem na Bill pia walipokea migawo iliyowapeleka sehemu nyinginezo.) Hakukuwa na mikutano ya kutaniko ambayo Frank angeweza kuhudhuria. Nyakati nyingine alikuwa mpweke sana, na mara kadhaa alishindana na mawazo ya kuacha na kurudi Australia. Lakini aliendelea tu. Jinsi gani? Chakula cha kiroho kilichomo katika The Watch Tower kilimtia nguvu. Katika 1937 alienda kwenye mgawo katika Indochina, ambapo alinusurika kufa wakati wa misukosuko ya jeuri iliyofuata Vita ya Ulimwengu 2. Roho hiyo ya kutaka kutumikia ilikuwa ingali hai katika miaka ya 1970 alipoandika ili kuonyesha shangwe yake kwa sababu familia yake yote ilikuwa ikimtumikia Yehova na kusema kwamba yeye na mke wake walikuwa wakijitayarisha tena kuhamia sehemu fulani katika Australia kulikokuwa na uhitaji mkubwa zaidi.
‘Kumtumaini Yehova kwa Moyo Wao Wote’
Claude Goodman aliazimia ‘kumtumaini Yehova kwa moyo wake wote bila kutegemea akili zake mwenyewe,’ kwa hiyo alichagua utumishi wa kolpota akiwa mweneza-evanjeli Mkristo badala ya fursa ya kufuatia biashara ya kilimwengu. (Mit. 3:5, 6) Akiwa pamoja na Ronald Tippin, aliyekuwa amemsaidia kujifunza kweli, alitumikia akiwa kolpota katika Uingereza kwa zaidi ya mwaka mmoja. Kisha, katika 1929, hao wawili walijitoa ili waende India.c Hilo lilitokeza ugumu kama nini!
Katika miaka iliyofuata, hawakusafiri tu kwa miguu na kwa garimoshi la abiria, na kwa basi bali pia kwa garimoshi la mizigo, gari la kukokotwa na ng’ombe, ngamia, mashua ndogo, riksho, na hata ndege na garimoshi la kukodiwa. Nyakati nyingine walitandika matandiko yao katika vyumba vya kungoja garimoshi, katika zizi la ng’ombe, kwenye nyasi ya msituni, au juu ya sakafu ya samadi ya ng’ombe katika nyumba ndogo, lakini pia kulikuwa na nyakati walipolala katika mahoteli ya starehe na katika jumba la mfalme. Kama vile mtume Paulo, walijifunza siri ya kuridhika iwe walikuwa na vitu vichache ama vitu vingi. (Flp. 4:12, 13) Mara nyingi walikuwa na vitu vichache sana vya thamani, lakini wakati wote walikuwa na vitu walivyohitaji kwelikweli. Wao binafsi waliona utimizo wa ahadi ya Yesu kwamba ikiwa wangetafuta kwanza Ufalme na uadilifu wa Mungu, vitu vya lazima vya maisha vingeandaliwa.
Kulikuwa na maambukizo mabaya ya homa ya kidingapopo, malaria, na homa ya matumbo, lakini utunzi wenye upendo uliandaliwa na Mashahidi wenzi. Kulikuwa na utumishi wa kufanywa miongoni mwa majiji yenye nyumba mbovumbovu kama vile Calcutta, na kulikuwa ushahidi wa kutolewa katika mashamba ya chai katika milima ya Ceylon (sasa yajulikana kuwa Sri Lanka). Ili kujazia mahitaji ya kiroho ya watu, fasihi zilitolewa, rekodi zilichezwa katika lugha za wenyeji, na hotuba zilitolewa. Kadiri kazi ilivyoongezeka, Claude alijifunza pia jinsi ya kuendesha matbaa ya uchapaji na kushughulikia kazi katika ofisi za tawi za Sosaiti.
Katika mwaka wake wa 87, yeye angeweza kutazama nyuma kwenye maisha yaliyojaa maono katika utumishi wa Yehova katika Uingereza, India, Pakistan, Ceylon, Burma (sasa ni Myanmar), Maleya, Thailand, na Australia. Akiwa kijana mseja na mume na baba pia, alitanguliza Ufalme maishani mwake. Haikupita miaka miwili baada ya ubatizo wake ndipo akaingia katika utumishi wa wakati wote, naye aliona huo kuwa kazi-maisha yake kwa maisha yake yote.
Uwezo wa Mungu Wafanywa Kuwa Kamili Katika Udhaifu
Ben Brickell alikuwa mwingine wa wale Mashahidi wenye bidii—aliyekuwa kama watu wengine, kwa vile alikuwa na mahitaji na udhaifu kama wao. Yeye alikuwa mwenye kutokeza katika imani. Katika 1930 alianza kazi ya kolpota katika New Zealand, ambako alitoa ushahidi katika maeneo ambayo hayakuenezwa tena kwa miongo mingi ya miaka. Miaka miwili baadaye, katika Australia, alianza safari ya miezi mitano ili kuhubiri akipitia nchi ya jangwa ambako hakukuwa na ushahidi uliokuwa umepata kutolewa. Alipakia baiskeli yake mzigo mkubwa wa mablanketi, nguo, chakula, na vitabu vilivyojalidiwa vya kuangusha. Ingawa watu wengine walikuwa wameangamia walipojaribu kusafiri kupitia eneo hilo, yeye alijikakamua, akiwa na tumaini katika Yehova. Kisha, akatumikia katika Malasia, ambako alipata matatizo mabaya ya moyo. Yeye hakuacha. Baada ya kupata nafuu, aliendelea na utendaji wa kuhubiri wakati wote katika Australia. Karibu mwongo mmoja hivi baadaye, ugonjwa mbaya ulimfanya alazwe hospitalini, na alipotoka humo aliambiwa na daktari kwamba “hangeweza kufanya kazi kwa asilimia 85.” Yeye hata hangeweza kutembea kwenda dukani bila kupumzikapumzika njiani.
Lakini Ben Brickell aliazimia kuendelea tena, na alifanya hivyo, akitua ili kupumzika kama ilivyohitajika. Upesi akawa anatoa ushahidi katika sehemu za mbali za Australia. Alifanya yote aliyoweza kutunza afya yake, lakini utumishi wake kwa Yehova ndio uliokuwa jambo kuu maishani mwake hadi kifo chake miaka 30 baadaye akiwa na umri wa kama miaka 65.d Yeye alitambua kwamba upungufu uliokuwako kwa sababu ya udhaifu wake ungejazwa na uwezo wa Yehova. Kwenye mkusanyiko katika Melbourne katika 1969, alitumikia kwenye dawati ya painia akiwa na beji kubwa kwenye shavu la koti lake, ikisema: “Ikiwa unataka kujua kuhusu upainia, niulize.”—Linganisha 2 Wakorintho 12:7-10.
Kufikia Vijiji vya Msituni na Kambi za Migodi za Milimani
Bidii katika utumishi wa Yehova ilisukuma si wanaume tu bali pia wanawake kuanza kazi katika mashamba yasiyofikiwa. Freida Johnson alikuwa mmoja wa watiwa-mafuta, mwenye umbo dogo na mwenye umri wa miaka 50 na kitu alipofanya kazi peke yake katika sehemu za Amerika ya Kati, akieneza sehemu kama vile pwani ya kaskazini ya Honduras kwa farasi. Kulitaka imani ili afanye kazi peke yake katika sehemu hiyo, kutembelea mashamba ya ndizi yaliyotapakaa, miji ya La Ceiba, Tela, na Trujillo, na hata vijiji vilivyo peke yavyo vya Carib. Alitoa ushahidi huko katika 1930 na 1931, tena katika 1934, na katika 1940 na 1941, akaangusha maelfu ya fasihi zenye kweli ya Biblia.
Wakati wa miaka hiyo, mfanyakazi mwingine mwenye bidii alianza kazi-maisha yake katika huduma ya wakati wote. Huyo alikuwa Kathe Palm, aliyezaliwa katika Ujerumani. Kilichomsukuma achukue hatua ilikuwa kuhudhuria mkusanyiko katika Columbus, Ohio, katika 1931, ambako Wanafunzi wa Biblia walikubali jina Mashahidi wa Yehova. Ulikuwa wakati huo alipoazimia kutafuta sana kwanza Ufalme, na katika 1992, akiwa mwenye umri wa miaka 89, alikuwa angali akifanya hivyo.
Utumishi wake wa painia ulianza katika New York City. Baadaye katika South Dakota, alikuwa na mwenzi kwa miezi michache kisha akaendelea peke yake, akisafiri kwa kupanda farasi. Alipoalikwa atumikie katika Kolombia, Amerika Kusini, alikubali mara hiyo, akafika huko mwishoni mwa 1934. Kwa mara nyingine tena, alikuwa na mwenzi kwa muda fulani kisha akawa peke yake. Hilo halikumfanya ahisi kwamba ni lazima aache.
Alialikwa na mume na mke mmoja ajiunge nao katika Chile. Huko kulikuwa na eneo jingine kubwa, lililotanuka kilometa 4,265 katika pwani ya magharibi ya bara la Amerika ya Kusini. Baada ya kuhubiri katika ofisi za jiji kuu, alienda kwenye sehemu ya mbali ya kaskazini. Alitoa ushahidi mlango kwa mlango katika kila kambi ya migodi, katika miji ya kampuni, iwe mikubwa au midogo. Wafanyakazi waliokuwa juu ya mlima Andes walishangaa kumwona mwanamke aliye peke yake akiwatembelea, lakini yeye aliazimia asimkose mtu hata mmoja katika eneo hilo alilogawiwa. Baadaye, alihamia kusini, mahali ambapo estancias (malisho ya kondoo) kadhaa yalienea kufikia hektari kama 100,000. Watu huko walikuwa wenye urafiki na wakaribishaji-wageni na walimkaribisha kwenye meza yao wakati wa kula. Kwa njia hiyo na nyinginezo, Yehova alimtunza, hivi kwamba alikuwa na vitu vya kimwili vilivyo vya lazima kwa maisha.
Kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu kumejaa maisha yake.e Alipotazama nyuma kwenye miaka yake ya utumishi, yeye alisema: “Ninahisi kwamba nimekuwa na maisha bora sana. Kila mwaka ninapohudhuria kusanyiko la watu wa Yehova, ninapata hisi changamfu ya uradhi ninapoona watu wengi ambao nimejifunza nao Biblia wakitangaza habari njema, wakisaidia wengine waje kwenye maji ya uhai.” Amekuwa na shangwe ya kuona idadi ya wasifaji wa Yehova katika Chile ikikua kutoka 50 hivi hadi zaidi ya 44,000.
“Mimi Hapa, Nitume Mimi”
Baada ya kusikia mhadhara uliotegemea mwaliko wa Yehova kwenye utumishi kama ulivyorekodiwa kwenye Isaya 6:8 na itikio lenye maoni mazuri la nabii, “Mimi hapa, nitume mimi,” Martin Poetzinger, katika Ujerumani, alibatizwa. Miaka miwili baadaye, katika 1930, aliingia katika huduma ya wakati wote katika Bavaria.f Kabla ya muda mrefu kupita, maofisa huko walizuia kuhubiri kwa Mashahidi, mahali pa kukutania pakafungwa, na fasihi zikachukuliwa. Gestapo walikuwa ni tisho. Lakini matukio hayo katika 1933 hayakukomesha huduma ya Ndugu Poetzinger.
Alialikwa atumikie katika Bulgaria. Kadi za ushuhuda katika Kibulgaria zilitumiwa kutoa utangulizi kwa fasihi za Biblia. Lakini watu wengi hawakujua kusoma na kuandika. Kwa hiyo, Ndugu Poetzinger alianza kujifunza lugha yao, iliyotumia alfabeti ya Kisirili. Familia ilipoangushiwa fasihi, mara nyingi ilikuwa lazima wazazi wasomewe na watoto wao.
Kwa sehemu kubwa ya mwaka wa kwanza, Ndugu Poetzinger alikuwa peke yake, naye aliandika: “Kwenye Ukumbusho, nilitoa hotuba mimi mwenyewe, nikasali mwenyewe, na kufunga mkutano nikiwa peke yangu.” Wakati wa 1934, wageni walifukuzwa, kwa hiyo alienda Hungaria. Huko alilazimika kujifunza lugha nyingine mpya ili aweze kutoa habari njema. Kutoka Hungaria alienda kwenye nchi zilizoitwa wakati huo Chekoslovakia na Yugoslavia.
Alipata maono mengi yenye kufurahisha—kupata wapendao kweli alipoenda sehemu za mashambani na vijijini, na fasihi zikiwa zimepakiwa juu ya mgongo wake; kuona utunzaji wa Yehova wakati wakaribishaji-wageni walipompa chakula na hata malazi ya usiku huo; kuzungumza hadi jioni sana na wale waliokuja mahali alipolala ili wasikie zaidi kuhusu ujumbe wa Ufalme wenye kufariji.
Kulikuwa pia na majaribu makubwa ya imani. Alipokuwa akitumikia nje ya nchi alikozaliwa, na bila fedha, alipatwa na ugonjwa mbaya. Hakuna daktari aliyetaka kumwona. Lakini Yehova aliandaa. Jinsi gani? Hatimaye, mshauri wa cheo cha juu wa hospitali ya mahali hapo alifikiwa. Mtu huyo, aliyeamini sana Biblia, alimtunza Ndugu Poetzinger kama vile ambavyo angefanya kwa mwanae, akifanya hivyo bila malipo. Daktari huyo alivutiwa na roho ya kujidhabihu ya kijana huyo, iliyodhihirika katika kazi ambayo alikuwa akifanya, na alikubali vitabu kadhaa vya Sosaiti kuwa zawadi.
Jaribu jingine kubwa lilikuja miezi minne baada ya kufunga ndoa. Ndugu Poetzinger alikamatwa Desemba 1936 na kufungiwa kwanza katika kambi moja ya mateso kisha katika nyingine, huku mke wake akifungiwa katika kambi nyingine kama hizo. Hawakuonana kwa miaka tisa. Yehova hakuzuia mnyanyaso huo wenye ukatili, lakini alimtia nguvu Martin, na mke wake Gertrud, na maelfu ya wengineo ili wauvumilie.
Baada ya yeye na mke wake kuachiliwa, Ndugu Poetzinger alionea shangwe miaka mingi ya utumishi akiwa mwangalizi asafiriye katika Ujerumani. Alikuwako kwenye mikusanyiko yenye kusisimua iliyofanywa baada ya vita katika viwanja vya Nuremberg vilivyokuwa vya gwaride ya Hitler hapo awali. Lakini sasa viwanja hivyo vilijawa umati mkubwa wa wategemezaji wa Ufalme wa Mungu walio waaminifu-washikamanifu. Alihudhuria mikusanyiko isiyoweza kusahaulika katika Yankee Stadium katika New York. Alionea shangwe kikamili mazoezi yake kwenye Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower. Na katika 1977 akawa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Mtazamo wake, hadi alipomaliza mwendo wake wa kidunia katika 1988, waweza kuelezwa vema zaidi kwa maneno: ‘Jambo hili moja nilifanyalo—kutafuta kwanza Ufalme.’
Kujifunza Yale Yanayomaanishwa Hasa
Kwa wazi roho ya kujidhabihu si jambo jipya miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Buku la kwanza kabisa la Millennial Dawn lilipotangazwa huko nyuma katika 1886, jambo la kujitakasa (au, kama vile tungesema leo, kujiweka wakfu) lilizungumzwa kwa uwazi. Ilionyeshwa kwa msingi wa Maandiko kwamba Wakristo wa kweli “hutakasa” kila kitu kwa Mungu; hiyo hutia ndani uwezo wao, mali zao za kimwili, maisha zao. Ni lazima Wakristo wawe watumishi wa yale “yaliyotakaswa” kwa Mungu, na wakiwa watumishi, ni lazima watoe hesabu—si kwa wanadamu bali kwa Mungu.
Idadi iliyozidi kukua ya Wanafunzi wa Biblia ilijitoa yenyewe kwelikweli katika utumishi wa Mungu. Walitumia kikamili uwezo wao, mali zao, nishati muhimu zao katika kufanya mapenzi yake. Kwa upande ule mwingine, kuna wale waliohisi kwamba kile kilichokuwa cha maana zaidi ni kusitawisha ile iliyoitwa tabia ya Kikristo ili wastahili kushiriki katika Ufalme pamoja na Kristo.
Ingawa daraka la kila Mkristo wa kweli la kutoa ushahidi kwa wengine kuhusu Ufalme wa Mungu lilikuwa limesemwa mara nyingi na Ndugu Russell, hilo lilikaziwa hata zaidi baada ya Vita ya Ulimwengu 1. Kielelezo chenye kutokeza ni makala “Tabia au Agano—Jipi Kati ya Hayo?” katika The Watch Tower la Mei 1, 1926. Lilizungumzia kwa uwazi matokeo mabaya ya kile kilichoitwa usitawishaji tabia kisha likakazia umaana wa mtu kutimiza madaraka yake kwa Mungu kwa njia ya vitendo.
Mapema zaidi, The Watch Tower la Julai 1, 1920, lilikuwa limechunguza unabii mkubwa wa Yesu kuhusu ‘ishara ya kuwapo kwake na ya mwisho wa ulimwengu.’ (Mt. 24:3, KJ) Lilikazia fikira kazi ya kuhubiri ambayo lazima ifanywe kwa utimizo wa Mathayo 24:14 na likatambulisha ujumbe utakaotangazwa, likisema: “Habari njema hapa zinahusu mwisho wa utaratibu wa mambo wa kale na kusimamishwa kwa ufalme wa Mesiya.” The Watch Tower lilieleza kwamba kwa msingi wa mahali Yesu aliposema hayo kuhusiana na sehemu nyinginezo za ile ishara, kazi hii ingetimizwa “kati ya wakati wa vita ile kuu ya ulimwengu [Vita ya Ulimwengu 1] na wakati wa ‘dhiki kubwa’ iliyotajwa na Bwana-Mkubwa katika Mathayo 24:21, 22.” Hiyo kazi ilikuwa ya haraka. Ni nani angeifanya?
Kwa wazi daraka hilo lilikuwa juu ya washiriki wa “kanisa,” kutaniko la kweli la Kikristo. Hata hivyo, katika 1932, kupitia toleo la Agosti 1 la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), hao walishauriwa watie moyo “jamii ya Kiyehonadabu” kushiriki nao katika kazi, kwa kupatana na roho ya Ufunuo 22:17. Jamii ya Kiyehonadabu—ambayo tumaini layo ni uhai wa milele katika dunia-Paradiso—iliitikia, na wengi wao walifanya hivyo kwa bidii.
Umaana mkubwa wa kazi hii umekaziwa sana: “Ni jambo la maana kushiriki katika utumishi wa Bwana kama vile ilivyo kuhudhuria mkutano,” likasema The Watch Tower katika 1921. “Kila mmoja lazima awe mhubiri wa gospeli,” likaonyesha katika 1922. “Yehova amefanya kuhubiri kuwe kazi ya maana sana awezayo yeyote kati yetu kufanya katika ulimwengu huu,” likasema katika 1949. Julisho rasmi la mtume Paulo kwenye 1 Wakorintho 9:16 (NW), limenukuliwa mara nyingi: “Nimewekewa sharti. Kwa kweli, ole wangu mimi ikiwa sikutangaza habari njema!” Andiko hilo limetumiwa kuhusu kila mmoja wa Mashahidi wa Yehova.
Ni Wangapi Wanaohubiri? Kwa Kadiri Gani? Kwa Nini?
Je, kuna wowote waliokuwa wakilazimishwa kushiriki katika kazi hii kinyume cha mapenzi yao? “La,” The Watch Tower likajibu, katika toleo lalo la Agosti 1, 1919, “hakuna yeyote anayeshurutishwa kufanya chochote. Wote ni utumishi wa kujitolea, unaofanywa kwa kumpenda Bwana na kusudi lake la uadilifu. Yehova haandikishi kamwe yeyote kwa nguvu.” Kuhusu kusudi la utumishi huo, The Watch Tower la Septemba 1, 1922, lilisema zaidi hivi: “Mtu ambaye kwa kweli ana shukrani moyoni mwake na anathamini yale ambayo Mungu amemfanyia atataka kufanya jambo fulani kwa upande wake; na kadiri ambavyo uthamini wake kwa fadhili za Mungu uongezekavyo, ndivyo upendo wake utakavyokuwa mkubwa; na kadiri upendo wake ulivyo mkubwa, ndivyo tamaa ya kumtumikia itakavyokuwa kubwa zaidi.” Ilielezwa kwamba kupenda Mungu huonyeshwa kwa kushika amri zake, na mojapo amri hizo ni kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu.—Isa. 61:1, 2; 1 Yoh. 5:3.
Wale ambao wanafanya utendaji huu hawakuvutwa na wazo lolote la kilimwengu la kujitakia makuu. Wameambiwa kinaganaga kwamba wanapoenda nyumba hadi nyumba au kutoa fasihi barabarani, wataonwa kuwa ‘wapumbavu, dhaifu, wa hali ya chini,’ kwamba ‘watadharauliwa, wataudhiwa,’ na kwamba wataonwa kuwa ‘wasiofaa kitu katika maoni ya kilimwengu.’ Lakini wanajua kwamba Yesu na wanafunzi wake wa zamani walitendwa kwa njia iyo hiyo.—Yn. 15:18-20; 1 Kor. 1:18-31.
Je, Mashahidi wa Yehova hufikiri kwamba kwa njia fulani wanastahili wokovu kwa utendaji wao wa kuhubiri? La hasha! Kitabu Wenye Umoja Katika Ibada ya Mungu wa Pekee wa Kweli, ambacho kimetumiwa tangu 1983 kusaidia wanafunzi kuendelea kufikia ukomavu wa Kikristo, kinazungumzia jambo hilo. Kinasema: “Vilevile dhabihu ya Yesu imetufungulia nafasi ya kupata uzima wa milele . . . Hiyo si thawabu tunayojipatia kwa ustahili wa kufanya kazi. Hata tufanye mengi namna gani katika utumishi wa Yehova, hatuwezi kamwe kujifanyia ustahili huo hata Mungu awe na deni kwetu la kutulipa uzima. Uzima wa milele ni ‘zawadi anayotoa Mungu . . . kwa njia ya Kristo Yesu, Bwana wetu.’ (Rum. 6:23; Efe. 2:8-10, NW) Hata hivyo, tukiwa na imani katika zawadi hiyo na kuthamini ni kwa jinsi gani ilifanywa iwezekane, tutaonyesha hilo. Kwa kufahamu namna Yehova ametumia Yesu kwa njia ya ajabu katika kutimiza mapenzi Yake na namna lilivyo jambo la maana sana kwetu sote kufuata sana hatua za Yesu, tutaifanya huduma ya Kikristo iwe mojapo mambo ya maana zaidi katika maisha zetu.”
Je, yaweza kusemwa kwamba Mashahidi wa Yehova wote ni watangazaji wa Ufalme wa Mungu? Ndiyo! Kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova kwamaanisha hivyo. Zaidi ya nusu karne iliyopita, kuna wale waliohisi kwamba haikuwa lazima kwao kushiriki katika utumishi wa shambani, kwenda hadharani na nyumba hadi nyumba. Lakini leo hakuna yeyote kati ya Mashahidi wa Yehova anayedai asihusishwe na utumishi huo kwa sababu ya daraka lake katika kutaniko la mahali au katika tengenezo la ulimwenguni pote. Wanaume na wanawake pamoja na wachanga na wazee hushiriki. Wao huuona kuwa pendeleo lenye thamani, utumishi mtakatifu. Watu wengi hupiga mbiu wajapokuwa na udhaifu mbaya. Na kwa wowote ambao hawawezi kimwili kwenda nyumba hadi nyumba, wao hupata njia nyinginezo za kuwafikia watu na kuwapa ushahidi kibinafsi.
Nyakati nyingine zamani, kulikuwa na mwelekeo wa kuruhusu wapya zaidi washiriki katika utumishi wa shambani mapema mno. Lakini katika miongo ya hivi karibuni, mkazo mkubwa umewekwa juu ya kustahili kabla ya kualikwa. Hilo linamaanisha nini? Halimaanishi kwamba ni lazima waweze kueleza kila kitu katika Biblia. Lakini, kama vile kitabu Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu kinavyofafanua, ni lazima wajue na waamini mafundisho ya msingi ya Biblia. Ni lazima pia wawe wanaishi maisha safi, kupatana na viwango vya Biblia. Ni lazima kila mmoja atake kikweli kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.
Haitazamiwi kwamba Mashahidi wa Yehova wote watafanya kiasi kilekile cha kuhubiri. Hali za watu mmoja-mmoja hutofautiana. Umri, afya, madaraka ya familia, na kina cha uthamini yote ni mambo yanayoamua. Jambo hilo limetambuliwa nyakati zote. Hilo lilikaziwa na toleo la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Desemba 1, 1950, lilipozungumza kuhusu “udongo mzuri” katika kielezi cha Yesu cha mpanzi, kwenye Luka 8:4-15. Kingdom Ministry School Course, waliotayarishiwa wazee katika 1972, ulichanganua takwa la ‘kumpenda Yehova kwa nafsi yote’ na ukaeleza kwamba “lililo la maana si wingi wa yale ambayo mtu anafanya kwa kulinganisha na yale ambayo mwingine anafanya, bali ni kufanya yale ambayo mtu anaweza kufanya.” (Mk. 14:6-8) Hata hivyo, likitia moyo kujichanganua kibinafsi kwa uzito, pia lilionyesha kwamba upendo kama huo humaanisha “kwamba kila jambo la maisha ya mtu linahusika katika kumtumikia Mungu kwa upendo; hakuna utendaji, uwezo au tamaa maishani ambayo haihusiki.” Uwezo wetu wote wa kufikiri, nafsi yetu yote, lazima zisukumwe kufanya mapenzi ya Mungu. Kitabu hicho cha mafunzo kilikazia kwamba “Mungu hutaka, si ushiriki tu, bali utumishi wa nafsi yote.”—Mk. 12:30.
Kwa kusikitisha, mwelekeo wa wanadamu wasio wakamilifu ni kupita kiasi, wakikazia jambo moja huku wakipuuza jingine. Kwa hiyo, huko nyuma katika 1906, Ndugu Russell aliliona kuwa jambo la lazima kutahadharisha kwamba kujidhabihu hakumaanishi kudhabihu wengine. Hakumaanishi kushindwa kuandalia ifaavyo mke wako, watoto wanaokutegemea, au wazazi wazee-wazee ili mtu awe huru kuhubiria wengine. Mara kwa mara tangu wakati huo, vikumbusho kama hivyo vimetokea katika vichapo vya Watch Tower.
Hatua kwa hatua, kwa msaada wa Neno la Mungu, tengenezo zima limetafuta kupata usawaziko wa Kikristo—kudhihirisha bidii kwa ajili ya utumishi wa Mungu, huku mtu akitoa uangalifu ufaao kwa mambo yote ya kuwa Mkristo halisi. Ingawa “usitawishaji wa tabia” ulikuzwa juu ya uelewevu usiofaa, Mnara wa Mlinzi limeonyesha kwamba matunda ya roho na mwenendo wa Kikristo hayapaswi kupuuzwa. Katika 1942 Mnara wa Mlinzi lilisema kwa njia ya waziwazi: “Wengine kwa kukosa hekima wamefikia mkataa kwamba ikiwa wangekuwa wakishiriki katika kazi ya kutoa ushahidi nyumba hadi nyumba wangeweza kufuatia mwendo wowote ambao ungeweza kuridhisha mibetuko na tamaa zao bila kupata adhabu. Mtu apaswa akumbuke kwamba kushiriki tu katika kazi ya kutoa ushahidi si ndilo jambo pekee linalotakwa.”—1 Kor. 9:27.
Kutanguliza Mambo ya Maana Zaidi
Mashahidi wa Yehova wamekuja kuthamini kwamba ‘kutafuta kwanza Ufalme na uadilifu wa Mungu’ kunamaanisha kutanguliza maishani mambo ya maana zaidi. Kunatia ndani kuweka mahali pafaapo maishani, funzo la kibinafsi la Neno la Mungu na hudhurio la kawaida kwenye mikutano ya kutaniko bila kuruhusu faida nyinginezo zichukue mahali pa kwanza. Kunatia ndani kufanya maamuzi yanayoonyesha tamaa ya kweli ya kujipatanisha na matakwa ya Ufalme wa Mungu, kama yanavyoonyeshwa katika Biblia. Hilo linatia ndani kutumia kanuni za Biblia kama msingi wa maamuzi yanayohusu maisha ya familia, tafrija, elimu ya kilimwengu, kazi ya kuajiriwa, shughuli za kibiashara, na uhusiano na wenzetu.
Kutafuta kwanza Ufalme kwatia ndani mengi kuliko kuwa na ushirika fulani kila mwezi katika kuzungumza na wengine kuhusu makusudi ya Mungu. Kwamaanisha kupatia faida za Ufalme mahali pa kwanza katika maisha yote ya mtu, huku akishughulikia ifaavyo madaraka mengine ya Kimaandiko.
Kuna njia nyingi ambazo kwazo Mashahidi wa Yehova waliojitoa huendeleza faida za Ufalme.
Pendeleo la Utumishi wa Betheli
Wengine hutumikia wakiwa washiriki wa familia ya Betheli ya duniani pote. Hao ni wafanyakazi walio wahudumu wa wakati wote ambao wamejitolea kufanya lolote watakalogawiwa kufanya katika kutayarisha na kuchapa fasihi za Biblia, katika kushughulikia kazi ya lazima ofisini, na katika kuandaa utumishi wa kutegemeza shughuli hizo. Hiyo si kazi ambayo wao hujipatia umashuhuri wa kibinafsi au mali za kimwili. Tamaa yao ni kumheshimu Yehova, na wanaridhika na upaji wanaopewa kama vile chakula, malazi, na rudishio la fedha la kiasi kwa ajili ya matumizi ya kibinafsi. Kwa sababu ya aina ya maisha ya familia ya Betheli, wenye mamlaka wa kilimwengu katika Marekani, kwa kielelezo, huwaona kuwa jamii ya dhehebu la kidini ambao wamechukua nadhiri ya umaskini. Wale walio katika Betheli hupata shangwe kuweza kutumia maisha zao kikamili katika utumishi wa Yehova na katika kufanya kazi ambayo hunufaisha idadi kubwa ya ndugu zao za Kikristo na watu ambao wamependezwa karibuni, nyakati nyingine kimataifa. Kama vile wale Mashahidi wa Yehova wengineo, wao pia hushiriki kwa ukawaida katika huduma ya shambani.
Familia ya kwanza ya Betheli (au familia ya Bible House, kama walivyojulikana wakati huo) ilikuwa katika Allegheny, Pennsylvania. Kufikia 1896, wafanyakazi walikuwa 12. Katika 1992, kulikuwa na washiriki wa familia ya Betheli zaidi ya 12,900, wakitumikia katika nchi 99. Kwa kuongezea, wakati nafasi ya nyumba katika majengo ya Sosaiti imekuwa haitoshi, mamia ya wafanyakazi wengine wa kujitolea wamesafiri kwenda kwenye makao ya Betheli na viwanda kila siku ili kushiriki katika kazi. Wao hulihesabu kuwa pendeleo kuwa na sehemu katika kazi inayofanywa. Kunapokuwa na uhitaji, maelfu ya Mashahidi wengineo hujitolea kuacha kazi za kimwili na utendaji mwingineo kwa vipindi vya wakati vinavyotofautiana ili kusaidia katika kujenga vifaa vinavyohitajiwa na Sosaiti vya kutumiwa kuhusiana na kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu duniani pote.
Washiriki wengi wa familia ya Betheli ya duniani pote wameifanya iwe kazi-maisha yao. Frederick W. Franz, ambaye katika 1977 alikuja kuwa msimamizi wa nne wa Watch Tower Society, alikuwa tayari amekuwa mshiriki wa familia ya Betheli katika New York kwa miaka 57, na akaendelea katika utumishi wa Betheli kwa miaka mingine 15, mpaka alipokufa katika 1992. Heinrich Dwenger alianza utumishi wa Betheli Ujerumani katika 1911, baadaye akatumikia kwa unyenyekevu mahali popote alipogawiwa; na katika 1983, mwaka aliokufa, bado alikuwa anafurahia utumishi wake akiwa mshiriki wa familia ya Betheli katika Thun, Uswisi. George Phillips, kutoka Scotland, alikubali mgawo wa kwenda ofisi ya tawi ya Afrika Kusini katika 1924 (ilipokuwa ikisimamia utendaji wa kuhubiri toka Cape Town hadi Kenya) na akaendelea kutumikia katika Afrika Kusini hadi kifo chake katika 1982 (wakati ambapo ofisi za tawi saba za Sosaiti na Mashahidi 160,000 walikuwa watendaji katika eneo hilo). Dada Wakristo, kama vile Kathryn Bogard, Grace DeCecca, Irma Friend, Alice Berner, na pia Mary Hannan, wakiwa watu wazima walitoa maisha zao katika utumishi wa Betheli, wakifanya hivyo hadi kifo chao. Vilevile washiriki wengineo wa familia ya Betheli wamekuwa wakitumikia kwa miaka 10, 30, 50, 70, na zaidi.g
Waangalizi Wasafirio Wenye Kujidhabihu
Ulimwenguni pote, kuna waangalizi wa mzunguko na wa wilaya kama 3,900 ambao, wakiwa na wake zao, hushughulikia pia migawo mahali popote wanapohitajiwa, sana sana katika nchi za kwao. Wengi wao wameacha makao na sasa wanaenda kila juma au kila baada ya majuma machache kutumikia makutaniko waliyogawiwa. Hawapokei mshahara wowote lakini wao hushukuru kwa chakula na malazi mahali wanapotumikia, pamoja na kiasi cha upaji kwa ajili ya matumizi ya kibinafsi. Katika Marekani, ambako waangalizi wa mzunguko na wa wilaya 499 walikuwa wakitumikia katika 1992, wazee hao wenye kusafiri walikuwa na wastani wa umri wa miaka 54, na wengine wao wamekuwa wakitumikia katika daraka hilo kwa miaka 30, 40, au zaidi. Katika nchi kadhaa, waangalizi hao husafiri kwa gari. Eneo katika sehemu ya Pasifiki mara nyingi hutaka ndege na mashua za kibiashara. Katika sehemu nyingi waangalizi wa mzunguko hufikia makutaniko ya mbali kwa kupanda farasi au kwa miguu.
Mapainia Watoa Msaada Mkubwa
Ili kuanza kuhubiri habari njema katika sehemu zisizo na Mashahidi, au kutoa msaada ambao huenda ukahitajiwa kihususa katika eneo fulani, huenda Baraza Linaloongoza likapanga kupeleka mapainia wa pekee. Wao ni waeneza-evanjeli wa wakati wote wanaotumia angalau saa 140 kila mwezi katika huduma ya shambani. Wao hujitolea ili watumikie popote wanapohitajiwa katika nchi yao au, katika visa fulani, katika nchi jirani. Kwa kuwa matakwa ya utumishi wao huwaacha wakiwa na wakati mchache au bila wakati wa kufanya kazi ya kimwili ili kujiandalia mahitaji ya kimwili, wao hupewa rudishio la kiasi kwa ajili ya kugharimia makao na mahitaji mengineyo. Katika 1992, kulikuwa na mapainia wa pekee zaidi ya 14,500 katika sehemu mbalimbali za dunia.
Mapainia wa pekee wa kwanza walipotumwa katika 1937, waliongoza katika kazi ya kuwapigia kinanda wenye nyumba milangoni pao ili wasikilize hotuba za Biblia zilizorekodiwa kisha kutumia rekodi hizo kuwa msingi wa mazungumzo ya Biblia kwenye ziara za kurudia. Hilo lilifanywa katika miji mikubwa ambako tayari kulikuwa na makutaniko. Baada ya miaka kadhaa, mapainia wa pekee wakaanza kuelekezwa hasa kwenye sehemu ambako makutaniko hayakuwako au ambako makutaniko yalikuwa na uhitaji mkubwa wa msaada. Kwa sababu ya kazi yao yenye matokeo, mamia ya makutaniko mapya yalifanyizwa.
Badala ya kueneza eneo na kusonga mbele, wangefanya kazi kwenye eneo hususa kwa kurudiarudia, wakifuatia kupendezwa kote na kuongoza mafunzo ya Biblia. Mikutano ilipangwa kwa ajili ya waliopendezwa. Hivyo, katika Lesotho, kusini mwa Afrika, kwenye juma lake la kwanza katika mgawo mpya, painia wa pekee alialika kila mtu aliyekutana naye aje aone jinsi Mashahidi wa Yehova huongoza Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Yeye na familia yake walifanya programu nzima. Kisha akawaalika wote kwenye Funzo la Mnara wa Mlinzi. Baada ya udadisi wa kwanza kuridhishwa, watu 30 waliendelea kuhudhuria Funzo la Mnara wa Mlinzi, na wastani wa hudhurio kwenye shule ulikuwa 20. Katika nchi ambako wamishonari waliozoezwa Gileadi walifanya mengi kuanzisha kuhubiriwa kwa habari njema, nyakati nyingine ukuzi wa haraka ulitokea wakati Mashahidi wenyeji walipoanza kustahili kutumikia katika utumishi wa painia wa pekee, kwani hao wangeweza kufanya kazi kwa matokeo zaidi miongoni mwa wenyeji.
Kwa kuongezea wafanyakazi hao wenye bidii, kuna mamia ya maelfu ya Mashahidi wa Yehova wanaoendeleza faida za Ufalme kwa juhudi. Hao ni vijana kwa wazee, wanaume kwa wanawake, waliofunga ndoa na waseja. Mapainia wa kawaida hutumia saa zisizopungua 90 kila mwezi kwenye huduma ya shambani; mapainia wasaidizi, angalau saa 60. Wao huamua mahali ambako wangependa kuhubiri. Walio wengi hufanya kazi pamoja na makutaniko yaliyoanzishwa tayari; wengine huhamia sehemu za mbali. Wao hushughulikia mahitaji yao wenyewe kwa kufanya kazi ya kimwili, au huenda washiriki wao wa familia wakasaidia kuwapa upaji huo. Wakati wa 1992, zaidi ya 914,500 walishiriki utumishi huo wakiwa mapainia wa kawaida au wasaidizi kwa angalau sehemu ya mwaka huo.
Shule Zenye Malengo ya Pekee
Ili kuwatayarisha wenye kujitolea kwa ajili ya aina fulani za utumishi, masomo ya pekee huandaliwa. Kwa kielelezo, tangu 1943, Shule ya Gileadi imezoeza maelfu ya wahudumu wenye ujuzi kwenye kazi ya mishonari, na wahitimu wamepelekwa kwenye sehemu zote za dunia. Katika 1987 Shule ya Mazoezi ya Kihuduma ilianza kutenda ili kusaidia kujazia mahitaji ya pekee, kutia na kushughulikia makutaniko na madaraka mengine. Mpango wa kwamba shule hii ifanywe katika mahali tofauti-tofauti hupunguza gharama za usafiri za wanafunzi kwenda mahali fulani pa kati na vilevile uhitaji wa kujifunza lugha nyingine ili kunufaika na shule hiyo. Wote wanaoalikwa kuhudhuria shule hii ni wazee au watumishi wa huduma ambao wamedhihirisha kwamba kwelikweli wao wanatafuta kwanza Ufalme. Wengi wanajitolea kutumikia katika nchi nyinginezo. Roho yao ni kama ile ya nabii Isaya, aliyesema: “Mimi hapa, nitume mimi.”—Isa. 6:8.
Ili kufanya ufanisi wa wale ambao tayari wanatumikia wakiwa mapainia wa kawaida na wa pekee uwe bora zaidi, Shule ya Utumishi wa Painia ilianzishwa katika 1977. Mahali ilipowezekana, shule hiyo ilipangwa katika kila mzunguko kotekote ulimwenguni. Mapainia wote walialikwa wanufaike kutokana na mtaala huo wa majuma mawili. Kwa kuendelea tokea wakati huo, mapainia ambao wamemaliza mwaka wao wa kwanza wa utumishi wamepewa mazoezi ayo hayo. Kufikia 1992, zaidi ya mapainia 100,000 walikuwa wamezoezwa katika shule hiyo katika Marekani pekee; zaidi ya 10,000 walikuwa wakizoezwa kila mwaka. Wengine 55,000 walikuwa wamezoezwa katika Japani, 38,000 katika Mexico, na 25,000 katika Brazili na 25,000 katika Italia. Kuongezea mtaala huo, kwa kawaida mapainia hufurahia mkutano wa pekee na mwangalizi wa mzunguko wakati wa ziara zake za mara mbili kila mwaka kwa kila kutaniko na kipindi cha mazoezi ya pekee pamoja na mwangalizi wa mzunguko na wa wilaya wakati wa kusanyiko la mzunguko la kila mwaka. Hivyo, wale wanaofanyiza jeshi kubwa la wapiga-mbiu wa Ufalme wanaotumikia wakiwa mapainia si wafanyakazi wenye nia tu bali pia ni wahudumu waliozoezwa vyema.
Kutumikia Sehemu Zenye Uhitaji Mkubwa Zaidi
Maelfu mengi ya Mashahidi wa Yehova—wengine wao wakiwa mapainia, na wengine si mapainia—wamejitoa ili kutumikia si katika jumuiya yao ya nyumbani tu bali pia katika maeneo mengine ambako kuna uhitaji mkubwa zaidi wa wapiga-mbiu wa habari njema. Kila mwaka maelfu hutumia kipindi cha majuma au miezi, kulingana na yale ambayo mtu binafsi aweza kupanga, katika maeneo ambayo kwa kawaida huwa mbali na kwao ili kutolea ushahidi watu ambao hawatembelewi kwa ukawaida na Mashahidi wa Yehova. Maelfu zaidi wameondoka wanakoishi na kuishi kwingineko ili kutoa msaada huo kwa kipindi kirefu. Wengi wa hawa ni waume na wake au familia zenye watoto. Kuhama kwao mara nyingi kumehusisha kwenda mwendo mfupi kwa kulinganishwa, lakini wengine wamehamahama hivyo kwa muda wa miaka. Wengi wa hao Mashahidi wenye bidii hata wameanza utumishi katika nchi za kigeni—wengine kwa miaka michache, wengine kwa kudumu. Wao hufanya kazi yoyote ya kimwili inayohitajiwa ili kushughulikia mahitaji yao, na wao huhama kwa gharama yao wenyewe. Tamaa yao kuu ni kushiriki kikamili kueneza ujumbe wa Ufalme kadiri hali zao zinavyoruhusu.
Inapokuwa kichwa cha familia si Shahidi, huenda yeye akahama na familia yake kwa sababu za kikazi. Lakini huenda washiriki wa familia ambao ni Mashahidi wakaona hiyo kuwa fursa ya kueneza ujumbe wa Ufalme. Ilikuwa hivyo kwa Mashahidi wawili kutoka Marekani waliojipata katika kambi ya ujenzi katika msitu wa Suriname mwishoni mwa miaka ya 1970. Mara mbili kwa juma waliamka saa 10:00 za usiku, wakapanda basi ya kampuni kwa safari ya saa moja isiyostarehesha kwenda kwenye kijiji, na kutumia siku wakihubiri. Kabla ya muda mrefu walikuwa wakiongoza mafunzo ya Biblia 30 kila juma na watu wenye njaa ya kiroho. Leo, kuna kutaniko katika sehemu hiyo ya msitu wa mvua ambayo hapo awali haikuwa imefikiwa.
Kutumia Kila Fursa Inayofaa ili Kutoa Ushahidi
Bila shaka, si Mashahidi wa Yehova wote wanaohamia nchi nyingine, au hata kwenye miji mingine, ili kuendeleza huduma yao. Hali zao huenda zisiwaruhusu wapainie. Hata hivyo, wao wanajua vema juu ya himizo la Biblia kutia ‘jitihada yote’ na kuwa ‘na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.’ (2 Pet. 1:5-8; 1 Kor. 15:58, NW) Wao huonyesha kwamba wanatafuta kwanza Ufalme wanapotanguliza faida za huo mbele ya kazi ya kimwili na tafrija. Wale ambao mioyo yao imejaa uthamini kwa ajili ya Ufalme hushiriki kwa ukawaida katika huduma ya shambani kwa kadiri ambayo hali zao huwaruhusu, na wengi wao hubadili hali zao ili waweze kushiriki kwa ukamili zaidi. Pia wako macho wakati wote kutumia fursa zifaazo kutoa ushahidi kwa wengine kuhusu Ufalme.
Kielelezo kimoja, John Furgala, ambaye alikuwa na biashara ya kuuza bidhaa za chuma katika Guayaquil, Ekuado, aliweka fasihi za Biblia dukani mwake kwa wonyesho wa kuvutia. Wakati msaidizi wake angemhudumia mteja, John angemtolea mteja ushahidi.
Katika Nigeria Shahidi mwenye bidii aliyeruzuku familia yake kwa kufanya kazi akiwa mwenye kondrati ya umeme aliazimia pia kutumia vema fursa alizokuwa nazo kukutana na watu na kuwatolea ushahidi. Kwa kuwa yeye ndiye aliyekuwa mwenye biashara, alipanga ratiba ya utendaji. Kila asubuhi, kabla ya kazi ya kila siku, alikusanya mke wake, watoto, wafanyakazi, na wanagenzi (wafunzwa-kazi) kwa ajili ya mazungumzo ya andiko la Biblia la siku hiyo, pamoja na mambo yaliyoonwa kutoka Yearbook of Jehovah’s Witnesses. Mwanzoni mwa kila mwaka, angewapatia wateja wake nakala ya kalenda ya Watch Tower Society, pamoja na magazeti mawili. Kama tokeo, baadhi ya wafanyakazi wake na wateja wamejiunga naye katika kumwabudu Yehova.
Kunao wengi kati ya Mashahidi wa Yehova walio na roho hiyohiyo. Hata iwe wanafanya nini, wakati wote wanatafuta fursa za kushiriki habari njema pamoja na wengine.
Jeshi Kubwa la Waeneza-Evanjeli wa Wakati Wote Wenye Furaha
Bidii ya Mashahidi wa Yehova ya kuhubiri habari njema haijakwisha kwa kupita kwa miaka. Hata ingawa wenye nyumba wengi wamewaambia kwa uthabiti kwamba hawapendezwi, kuna idadi kubwa ya wale ambao wanashukuru kwamba Mashahidi huwasaidia kuelewa Biblia. Azimio la Mashahidi wa Yehova ni kuendelea kuhubiri hadi Yehova mwenyewe atoe mwelekezo wa wazi kwamba kazi hiyo imekamilika.
Badala ya kupunguza mwendo, shirika la ulimwenguni pote la Mashahidi wa Yehova hasa limeongeza utendaji walo wa kuhubiri. Katika 1982 ripoti ya duniani pote ya kila mwaka ilionyesha kwamba muda wa saa 384,856,662 zilitolewa kwenye huduma ya shambani. Miaka kumi baadaye (katika 1992) saa 1,024,910,434 zilitumiwa katika kazi hiyo. Ni nini kilichosababisha ongezeko hilo kubwa la utendaji?
Ni kweli kwamba idadi ya Mashahidi wa Yehova imekua. Lakini si kwa kadiri ileile ya muda wa saa. Wakati wa kipindi hicho, idadi ya Mashahidi ilipoongezeka kwa asilimia 80, idadi ya mapainia ilipanda ikawa asilimia 250. Kwa wastani kila mwezi, 1 kati ya Mashahidi wa Yehova 7 ulimwenguni pote alikuwa katika aina fulani ya kazi ya kuhubiri ya wakati wote.
Ni nani waliokuwa wakishiriki katika utumishi huo wa painia? Kwa kielelezo, katika Jamhuri ya Korea, Mashahidi wengi ni wake wa nyumbani. Huenda madaraka ya familia yasiwaruhusu wote kupainia kwa ukawaida, lakini idadi kubwa wametumia likizo ndefu za shule wakati wa kipupwe kuwa fursa za kufanya utumishi wa painia msaidizi. Kama tokeo, asilimia 53 ya Mashahidi wote katika Jamhuri ya Korea walikuwa katika aina fulani ya utumishi wa wakati wote katika Januari 1990.
Katika miaka ya mapema, ilikuwa ni roho ya upainia wa bidii kwa upande wa Mashahidi Wafilipino iliyowawezesha kufikia mamia ya visiwa vinavyokaliwa na watu katika Filipino kwa ujumbe wa Ufalme. Bidii hiyo imekuwa wazi hata zaidi tangu wakati huo. Katika 1992, kwa wastani kila mwezi, wahubiri 22,205 walikuwa wakishiriki katika huduma ya shambani wakiwa mapainia katika Filipino. Hiyo ilitia ndani vijana wengi waliokuwa wamechagua ‘kumkumbuka Muumba wao’ na kutumia nguvu yao ya ujana katika utumishi wake. (Mhu. 12:1) Baada ya mwongo mmoja wa miaka ya utumishi wa painia, mmoja wa vijana hao alisema: “Nimejifunza kuwa mwenye saburi, kuwa na maisha sahili, kumtegemea Yehova, na kuwa mnyenyekevu. Ni kweli kwamba nimepata magumu na kuvunjika moyo pia, lakini yote hayo si kitu ninapoyalinganisha na baraka ambazo upainia umeniletea.”
Wakati wa Aprili na Mei 1989, Mnara wa Mlinzi lilikazia kufunuliwa kwa Babiloni Mkubwa, ambayo ni dini bandia katika namna yayo mbalimbali ulimwenguni pote. Makala hizo zilitangazwa wakati uleule katika lugha 39 na kugawanywa sana. Katika Japani, ambako idadi ya Mashahidi wanaopainia mara nyingi imekuwa zaidi ya asilimia 40, kilele kipya cha mapainia wasaidizi 41,055 walijiandikisha kusaidia katika kazi hiyo mwezi Aprili. Katika Wilaya ya Osaka, Jiji la Takatsuki, Kutaniko la Otsuka, wahubiri waliobatizwa 73 kati ya 77 walikuwa katika aina fulani ya utumishi wa painia mwezi huo. Mnamo Aprili 8, wahubiri wote katika Japani walipohimizwa kuwa na sehemu katika kugawanya ujumbe huo muhimu, mamia ya makutaniko, kama vile Kutaniko la Ushioda, katika Jiji la Yokohama, yalipanga kuwa na utumishi wa siku nzima kwenda barabarani na nyumba hadi nyumba, kuanzia saa 1:00 asubuhi hadi saa 2:00 usiku, ili kufikia kila mtu katika eneo hilo kwa kadiri ilivyowezekana.
Kama vile ilivyo kila mahali, Mashahidi wa Yehova katika Mexico hufanya kazi ili kushughulikia mahitaji yao ya kimwili. Hata hivyo, kila mwezi wakati wa 1992, kwa wastani 50,095 kati ya Mashahidi wa Yehova huko walipanga mambo yao ili washiriki katika utumishi wa painia ili wasaidie watu wenye njaa ya kiroho wajifunze kuhusu Ufalme wa Mungu. Katika familia nyingine, wote katika nyumba walishirikiana ili kuwezesha kikundi kizima, au angalau baadhi yao, wapainie. Wanaonea shangwe huduma yenye mazao. Wakati wa 1992, Mashahidi wa Yehova katika Mexico walikuwa wakiongoza mafunzo ya Biblia nyumbani 502,017 pamoja na watu mmoja-mmoja na vikundi vya familia.
Wazee wanaotumikia mahitaji ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova wana madaraka mazito. Wengi wa wazee katika Nigeria ni wanaume wenye familia, na ndivyo ilivyo pia na wazee katika mahali pengine pengi. Na zaidi ya kutayarisha ili kuongoza au kushiriki katika mikutano ya kutaniko, pamoja na kufanya uchungaji unaohitajiwa wa kundi la Mungu, baadhi ya wanaume hao hupainia pia. Hilo huwezekanaje? Kuratibu wakati kwa uangalifu na ushirikiano mzuri wa familia mara nyingi huwa mambo ya maana.
Ni wazi kwamba, ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova wamezingatia moyoni himizo la Yesu la ‘kufuliza kutafuta kwanza Ufalme.’ (Mt. 6:33, NW) Yale wanayofanya ni wonyesho wa kutoka moyoni wa upendo wao kwa Yehova na uthamini wao kwa ajili ya enzi kuu yake. Kama vile mtunga zaburi Daudi, wao husema: “Ee Mungu wangu, Mfalme, nitakutukuza, nitalihimidi jina lako milele na milele.”—Zab. 145:1.
[Maelezo ya Chini]
a Watch Tower, Agosti 15, 1906, kur. 267-271.
b Ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), Februari 1, 1967, kurasa 92-95.
c Ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), Desemba 15, 1973, kurasa 760-765.
d Ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), Septemba 1, 1972, kurasa 533-536.
e Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), Desemba 15, 1963, kur. 764-766.
f Ona Mnara wa Mlinzi, (Kiingereza) Desemba 1, 1969, kurasa 729-732; Septemba 15, 1988, ukurasa 31.
g Ona Mnara wa Mlinzi, Mei 1, 1987, kurasa 22-30; Aprili 1, 1964 (Kiingereza), kurasa 212-215; Desemba 1, 1956, kurasa 712-719; Agosti 15, 1970, kurasa 507-510; Oktoba 1, 1960, kurasa 601-605; Juni 15, 1968, kurasa 378-381; Aprili 1, 1968, kurasa 217-221; Aprili 1, 1959, kurasa 220-223.
[Blabu katika ukurasa wa 292]
Mkazo ulioongezwa juu ya daraka la kutoa ushahidi
[Blabu katika ukurasa wa 293]
Wao huona kutoa ushahidi nyumba hadi nyumba kuwa pendeleo lenye thamani
[Blabu katika ukurasa wa 294]
Kuelewa kinachomaanishwa na utumishi wa nafsi yote
[Blabu katika ukurasa wa 295]
Kinachomaanishwa hasa na “kutafuta kwanza Ufalme”
[Blabu katika ukurasa wa 301]
Mashahidi wenye bidii walitanguliza faida za Ufalme mbele ya kazi ya kimwili na tafrija
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 288]
“Where Are the Nine?”
Kwenye Ukumbusho wa kifo cha Kristo, katika 1928, trakti ambayo kila mtu aliyehudhuria alipewa ilikuwa yenye kichwa “Where Are the Nine?” Mazungumzo yayo ya Luka 17:11-19 yaligusa moyo wa Claude Goodman na yakamsukuma kuingia katika kazi ya kolpota, au painia na kustahimili katika utumishi huo.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 296, 297]
Utumishi wa Betheli
Kufikia 1992, kulikuwa na 12,974 waliokuwa wakishiriki katika utumishi wa Betheli katika nchi 99
[Picha]
Funzo la kibinafsi ni la maana kwa washiriki wa familia ya Betheli
Hispania
Kwenye kila Kao la Betheli, siku huanza kwa mazungumzo ya andiko la Biblia
Finland
Kama vile ilivyo na Mashahidi wa Yehova kila mahali, washiriki wa familia ya Betheli hushiriki katika utumishi wa shambani
Uswisi
Kila Jumatatu jioni familia ya Betheli hujifunza “Mnara wa Mlinzi” pamoja
Italia
Kazi hutofautiana, lakini yote hufanywa kwa kutegemeza kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu
Ufaransa
Papua New Guinea
Marekani
Ujerumani
Filipino
Mexico
Uingereza
Nigeria
Uholanzi
Brazili
Japani
Afrika Kusini
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 298]
Wachache Wenye Muda Mrefu wa Utumishi wa Betheli
F. W. Franz—Marekani (1920-1992)
Heinrich Dwenger—Ujerumani (karibu miaka 15 ya 1911-1933), Hungaria (1933-1935), Chekoslovakia (1936-1939), kisha Uswisi (1939-1983)
George Phillips—Afrika Kusini (1924-1966, 1976-1982)
Dada za kimwili (Kathryn Bogard na Grace DeCecca) waliotoa jumla ya miaka 136 kwenye utumishi wa Betheli—Marekani
[Grafu katika ukurasa wa 303]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Mapainia Wanaoongezeka!
Mapainia
Wahubiri
Asilimia ya Ongezeko Tangu 1982
250%
200%
150%
100%
50%
1982 1984 1986 1988 1990 1992
[Picha katika ukurasa wa 284]
Dada Early alisafiri sehemu kubwa ya New Zealand kwa baiskeli ili kushiriki ujumbe wa Ufalme
[Picha katika ukurasa wa 285]
Kwa miaka 76—akiwa mseja, akiwa ameolewa, na kisha akiwa mjane—Malinda Keefer alijitoa mwenyewe kwenye huduma ya wakati wote
[Picha katika ukurasa wa 286]
Magari yenye nyumba sahili yaliandaa malazi kwa baadhi ya mapainia wa zamani walipohama kutoka mahali pamoja hadi pengine
Kanada
India
[Picha katika ukurasa wa 287]
Frank Rice (anayesimama upande wa kulia), Clem Deschamp (aliyeketi mbele ya Frank, pamoja na mke wa Clem, Jean, kando yao), na kikundi katika Java kutia na Mashahidi wenzi na watu waliopendezwa karibuni
[Picha katika ukurasa wa 288]
Maisha ya Claude Goodman ya huduma ya wakati wote yalimpeleka kwenye utumishi katika India na nchi nyinginezo saba
[Picha katika ukurasa wa 289]
Ben Brickell alipokuwa na afya nzuri, alifurahia kuitumia katika utumishi wa Yehova; matatizo mabaya ya afya katika miaka ya baadaye hayakumfanya aache
[Picha katika ukurasa wa 290]
Kathe Palm alitoa ushahidi katika kila aina ya eneo, kuanzia ofisi za majiji makubwa hadi kwenye kambi za migodi na malisho ya kondoo ya mbali katika Chile
[Picha katika ukurasa wa 291]
Azimio la Martin na pia Gertrud Poetzinger linaonyeshwa katika maneno: ‘Jambo hili moja nilifanyalo—kutafuta kwanza Ufalme’
[Picha katika ukurasa wa 300]
Shule ya Utumishi wa Painia (kama inavyoonyeshwa hapa katika Japani) imeandaa mazoezi ya pekee kwa makumi ya maelfu ya wafanyakazi wenye bidii