Nina Furahi Kutumikia Mungu Anayekumbuka
ILIKUWA jioni ya Mei 24, 1971. Mkristo aliye wakf alikuwa amekula chakula hotelini pamoja na wengine. Alipokuwa akiondoka, akawa akitelemka kwenye ngazi. Mkono wake wa kuume ukajaribu bila kufaulu kujishikilia ufito wa ngazi ambao haukuwako—na muda si muda akawa anabingirika kasi sana kuelekea chini. Kichwa chake kikagonga kwa nguvu sana chombo fulani cha mapambo cha chuma.
Alex Henderson akawa amejeruhiwa vibaya sana. Kwa kweli, mataraja yake ya kupona yalikuwa yasiyo na matumaini sana hata kwamba mkewe akapelekewa rambirambi na daktari. Na hata hivyo, mumewe aliishi. Matokeo ya kuanguka kwake yalikuwa nini? Fuvu la kichwa chake likawa limevunjika-vunjika vibaya sana, akawa na vivimbe vitatu vilivyojaa damu na upande wa kushoto wa mwili wake ukawa umepooza. Ilikuwa baada tu ya miezi mingi kupita ya kukaa bila fahamu kwamba kulikuwa na maendeleo kidogo sana.
Leo, hali mbaya ya kutojiweza humzuia Alex Henderson asifanye mengi kama vile alivyofanya wakati mmoja katika utumishi wa Yehova Mungu. Hata hivyo, yeye ana furaha, akikumbuka kwamba “Mungu si dhalimu hata aisahau kazi [yako], na pendo lile [u]lilolidhihirisha kwa jina lake.” (Ebr. 6:10) Inafariji kama nini kujua kwamba kazi za imani pamoja na kulipenda jina la Mungu ni mambo anayokumbuka Baba yetu wa kimbinguni!
Walakini, Wakristo wanaweza kushindanaje na matokeo mabaya ya msiba kama huo wenye kuhuzunisha? Ni nini kinachoweza kuwategemeza? Kabla ya kujibu maulizo hayo—ebu tutazame kifupi wakati uliopita. Alex anatusimulia.
DINI KATIKA JAMAA YETU
‘Glasgow ndipo nilipoona nuru ya mchana kwa mara ya kwanza huko nyuma katika mwaka 1921. Jamaa yetu ilifuata Kanisa la Scotland. Mama alikuwa mwanamke mtawa sana, lakini kwa huzuni tulimpoteza alipochukuliwa na adui mauti nilipokuwa kivulana wa miaka 12 tu. (1 Kor. 15:26) Kutunza shamba lililoelekea kusitawi vizuri sana ndiyo inayoonekana kuwa ilikuwa njia kubwa zaidi ya baba kumkaribia Muumba. Kwa kweli, mojayapo ya mara chache sana ambapo baba aliingia kanisani ilikuwa Juni 11, 1943, wakati mimi na Janet tulipooana.
‘Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili nikawa katika utumishi wa kijeshi kwa muda wa miaka mitano. Kiongozi mmoja wa kidini alijitolea afanye mpango niachishwe utumishi huo, mradi tu ningekubali kuingia seminari nikawe mhudumu. Lakini nilichagua kuendelea kutumikia katika jeshi la hewani.
‘Vita ilipomalizika, mimi na mke wangu tulijikuta katikati ya jamii yenye wasiwasi. Janet alikuwa mwalimu wa Sunday-school, na katika maonyesho mbalimbali yaliyodhaminiwa na kanisa tulikuwa tukishiriki kuimba pamoja nyimbo kama ule unaoitwa “bonny Scotland.” Halafu, ijapokuwa kuna wimbo wa kidini wa Kiskochi unaoitwa “Niongoze Ee Yehova Mkuu,” sikumbuki nikisikia jina hilo la kimungu katika siku hizo.’—Zab. 83:18.
KUJIFUNZA JUU YA MUNGU ANAYEKUMBUKA
‘Katika Novemba wa mwaka 1947, sisi pamoja na mwana wetu wa miaka mitatu tulihamia mjini New York. Upesi Janet akaanza kuonyesha kule kupendezwa kwake katika mambo ya kidini. Yeye alikuwa anajua habari fulani juu ya Mashahidi wa Yehova huko Scotland, walakini sasa alianza kujifunza Biblia pamoja nao. Na katika mwaka 1950 alionyesha wakf wake kwa Mungu kwa kubatizwa katika maji.
‘Kwa kuwa mke wangu alikuwa akishirikiana na “hao Mashahidi wa Yehova,” ilielekea inafaa nihudhurie mmoja wa mikutano yao. Nawezaje kusahau huo wa kwanza—ukumbusho wa 1951 wa kifo cha Yesu? (Luka 22:19, 20) Kwanza kila kitu kilikuwa kimya. Ndipo mwanamke mmoja mzee akapaza sauti hivi: “Acheni tumwimbie Yesu wimbo!” Hiyo ikatosha! Wasinitazamie niwepo wakati ujao. Bila shaka, mwanamke huyo alikuwa mgeni, hakuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, nayo mikutano yao inafanywa kwa utaratibu sana hata kwamba asiye mwamini anayehudhuria anaweza kusema, “Kweli Mungu yupo pamoja nanyi.” (1 Kor. 14:23-25, HNWW) Walakini wakati huo hungeweza kunisadikisha hilo.
‘Mara nyingi Janet aliwaalika Mashahidi wachache kwenye makao yetu baada ya mikutano siku ya Jumapili. Walakini, ili niepuke kukutana nao, mara nyingi nilikaa na kuona sinema iyo hiyo mara mbili katika jumba fulani la kuonyeshea sinema la mahali petu, au nikawa nikizurura-zurura huku na huku mpaka wageni hao waondoke ili niweze kurudi nyumbani “salama,” huku nimechoka nazo nyayo za miguu yangu zikiuma kwa kuzurura-zurura. Lo! namna wengine wetu wanavyojiepusha na kweli ya Kimaandiko!
‘Hata hivyo, polepole, “upinzani” wangu ukapunguka. Mwenendo mwema wa mke wangu maneno fulani yaliyochaguliwa vizuri—pamoja na magazeti kama hili yakiwa yamewekwa kwa werevu mahali pafaapo—yalinisadikisha kwamba kumbe Mashahidi “hawakuwa wabaya.” (1 Pet. 3:1-6) Kuugua ugonjwa wa kifua kikuu na kulazwa hospitalini kwa miezi kadha kulinipa wakati wa kufikiri. Kupitia kwa barua, Janet alijibu maulizo yangu mengi juu ya Biblia, na kabla ya muda mrefu kupita nikaikubali imani ya kweli kwa moyo. Na ndivyo na mwana wetu Adam, ambaye leo ni mwangalizi Mkristo. Sote wawili tulibatizwa siku ile ile—Septemba 9, 1957.’
‘Nikifahamu sana hali yangu ya sasa ya kutoweza kutimiza mengi, ninashukuru sana kwa nafasi nilizokuwa nazo wakati uliopita za kumtumikia Mungu ambaye hukumbuka. Upesi nikapata pendeleo la kutumikia kama mwangalizi msimamizi. Licha ya kushiriki kazi ya kuhubiri habari njema pamoja na utendaji mwingine wa kundi, nilifurahia sana kushiriki katika kujenga Jumba la Ufalme ambamo Wakristo wangali wakikutania kwa kawaida.
‘Katika siku hizo, watu fulani waliniita kwa kirafiki “Henderson mwenye kusema-sema.” Kati ya mambo mengine, lilikuwa jambo lenye kuvutia sana kuongoza sherehe za ndoa na kuona furaha iliyoonyeshwa na nyuso za wale waliokuwa wakioana. Kulikuwako vipindi vya huzuni pia—nyakati ambapo ilikuwa lazima kutoa hotuba za mazishi. Kipindi kimojawapo kinakumbukwa waziwazi sana kwa sababu ya tatizo la lugha. Ebu wazia—wasikilizaji Waspania wakisikiliza hotuba ya Kiingereza ikitolewa katika matamshi ya Kiskochi. Lakini kulikuwako mtafsiri, nami najua kwamba walifahamu, kwa sababu polepole zile nyuso zenye huzuni zilianza kuangaza kidogo waliposikia juu ya tumaini la ajabu la ufufuo. Hata hivyo pendeleo langu lililokuwa zuri sana la kusema lilikuwa lile la kutoa hotuba wakati kundi lilipokuwa likiadhimisha Chakula cha Bwana cha Jioni katika mwaka 1959, kwa sababu kulinipa nafasi ya kusema wa moyo wote juu ya wokovu mkuu ambao Yehova Mungu amefanya uwezekane kupitia kwa Mwanawe mpendwa Yesu Kristo.—Mt. 26:26-29; Yohana 3:16; 5:28, 29,
‘Katika mwaka 1963, tulianza kushirikiana na kundi jingine nasi tulikuwa wenye furahi kweli kweli tukiwa jamaa iliyo wakf kwa Yehova. Lakini ndipo ukaja msiba wangu wenye kudhoofisha katika mwaka 1971. Tangu wakati huo kupungukiwa na nguvu za mwili limekuwa fungu langu, lakini furaha yangu imekuwa kuu kwa kuweza kumtumikia Mungu ambaye hukumbuka.’
WAAMINI WENZI WASAIDIA
Alex Henderson hakumbuki mengi juu ya msiba huo pamoja na matokeo yake mabaya yaliofuata mara baada ya msiba huo. Kwa hiyo inaonekana kuwa jambo lenye kufaa kuwaacha wengine waeleze mambo fulani . . . na hivyo tusaidiwe kujibu maulizo kama vile: “Wakristo wanaweza kushindana na msiba? Nini kinachowategemeza? Wengine waweza kusaidiaje? Na je! Mkristo mwenye udhaifu wa mwili aweza kusaidia waamini wenzake?
Kwa Mkristo, huenda msiba mbaya sana ukamhitaji afanye azimio thabiti la ‘kujiepusha na damu.’ (Matendo 15:28, 29) Ndivyo ilivyokuwa kwa akina Henderson, nao mwendo wao thabiti ulikuwa na matokeo kwa wengine, kwa kuwa mshiriki wa karibu alisema hivi: “Kuona Wakristo wenzi wakihatirisha maisha yao ili wasimame imara bila kushindwa na [suala] la kutiwa damu mishipani kunatia imani nguvu.” Ndivyo, hata tunapopatwa na msiba, tunaweza kuwajenga wengine kiroho kwa kuchukua msimamo usio wa woga kwamba ‘tuishi au tufe, sisi tu wa [Yehova].’—Rum. 14:7, 8.
Waamini wenzi wenyewe wanaweza kusaidia. Wakati wa miezi ile, wakati ambapo Alex alikuwa hafahamu lo lote, alihitaji uangalizi wa matibabu wenye gharama nyingi wa usiku na mchana. “Kundi (ndugu na dada za kiroho mmoja mmoja) lilisaidia kuchukua mzigo huo,” aeleza mzee mmoja. Hapa palikuwapo wonyesho unaothaminiwa wa upendo unaowatambulisha wafuasi wa kweli wa Yesu.—Yohana 13:35.
Bila shaka, upendo wa Kikristo waweza kuonyeshwa katika njia nyingi. Akitazama nyuma, mwangalizi mwingine anatamka hivi: “Upasuaji ulifanikiwa. Alex akapelekwa kwenye sehemu ya kutunzia wagonjwa kwa uangalifu sana akakaa humo kwa siku kadha. Nilizuru kila siku . : . Wakati wa ziara hizo, nilikuwa nikimshika Alex mkono na kutoa sala. Kama aliweza kusikia sikuweza kujua. Walakini, kwa kushangaza, waaguzi wa kike walikuwa watulivu nao hawakutembea huku na huku kwa kelele.”
Mzee mwingine anaongeza hivi: “Polepole Alex akaanza kupata nafuu na kupata fahamu. Mwendo ulikuwa wa polepole sana. Hata hivyo aliweza kusema baada ya muda fulani. Wakati ulivyoendelea, udhaifu ulioupata mwili wake ukaanza kuonekana—kupooza kwa upande wa kushoto wa mwili wake pamoja na kuharibika kwa hali ya kuona ya macho yake. Kumbukumbu lake vilevile liliharibiwa sana hasa kwa habari ya matukio yaliyohusiana na kulazwa hospitalini kwake na yale ya wakati wa karibuni uliotangulia tukio hilo. Walakini kumbukumbu lake na maarifa yake juu ya mambo ya kiroho vilionekana kuharibiwa kidogo sana. Maendeleo yake kwa upande huo yalishangaza sana.”
Lo! jinsi ilivyo rahisi kwa mtu asiyejiweza kuacha kujitahidi, na kutokomea katika kukata tamaa! Lakini ni jambo lisilo la hekima kama nini kufanya hivyo, na hasa ikiwa mtu anamtumikia Yehova, “Mungu atoaye tumaini”! (Rum. 15:13, NW) “Alex aliendelea, akasubiri kadiri alivyoweza,” asema mwenzi mmoja Mkristo. “Polepole akaanza kurudiwa na akili zake. Akawa anaweza kusoma, kusema na kufanya mambo kadiri fulani, walakini hali yake ya kupooza upande wake wa kushoto ikaendelea. Akiendelea kupata nafuu polepole, alianza kuhudhuria mikutano na baadaye kushiriki, akiwa jukwaani na kwa kutoa maelezo.”
Kwanza ilikuwa lazima Alex Henderson asaidiwe aweze kufika kwenye mikutano ya Kikristo akiwa katika kiti cha wagonjwa chenye magurudumu. Baadaye, aliweza kutembea kwa miguu yake akitumia vyuma vya kutia miguu nguvu pamoja na bakora ambavyo mpaka sasa analazimika kutumia. Anapoulizwa ni jambo gani limemtegemeza, jambo moja analokuwa tayari kutaja ni “kuhudhuria mikutano.” Ni jambo la maana kama nini kwa Wakristo kuhudhuria mikutano kwa ukawaida na ‘kuhimizana katika upendo na kazi nzuri’!—Ebr. 10:24, 25.
Kuimba kumekuwa sikuzote sehemu yenye maana ya maisha katika jamaa ya Henderson. “Sikuzote nimependa kusikia Alex na Janet wakiimba kwenye Jumba la Ufalme,” asema mmojawapo wa dada zao za kiroho. Walakini kwa sababu ya kuharibika kwa uwezo wake wa kuona, Ndugu Henderson hangeweza kuona maandishi katika kitabu cha nyimbo cha kundi. Kwa hiyo dada huyo alifikiria njia ya kusaidia. “Niliandika kitabu chote cha nyimbo kwa maandishi makubwa,” anasema, “nami nilifurahi sana kumsikia akiimba sifa za Yehova tena.”—Efe. 5:18-20.
NAFASI ZAIDI ZA KUTUMIKIA
“Haielekei kwamba jamaa yetu itasahau kamwe mkutano fulani karibu na mwisho wa mwaka 1975,” anakumbuka Alex: “Ilikuwa furaha kama nini kwetu wakati mmojawapo wa waangalizi aliposoma barua moja ikisema kwamba nilikuwa nimewekwa kuwa mzee! Jambo hilo lilinishangaza kabisa, kwa kuwa ndugu hawakuwa wamezungumza jambo hilo pamoja nami, ijapokuwa walijua kwamba lingekubaliwa kama pendeleo linalothaminiwa sana. Nilionaje mwanzoni? ‘Mimi! Naweza kufaaje mimi?’ Kwa unyenyekevu, lazima nikubali kwamba inawezekana kuchukua daraka kama hilo kwa msaada wa Yehova tu, kwa kuwa naweza kujisifuje katika nguvu zangu mwenyewe?”—Linganisha 1 Wakorintho 1:28-31; Wafilipi 4:13.
Kweli mtu asiyejiweza anaweza kusaidia wengine? Ndiyo, nao uhakika huo waweza kuwa kitia-moyo kwa mtu anayepatwa na msiba kwa sababu ya kutojiweza. Kijana mmoja alisema hivi: “Nafurahia sana mambo mengi juu ya kweli ambayo Ndugu Henderson hutumia kufanya maelezo na hotuba zake kuwa tamu.” Mwingine asema hivi: “Ni wazi kwamba yeye ana utajiri mwingi wa maarifa ambayo anataka sana kushiriki na sisi sote. . . . Inashangaza sana namna anavyokuwa na bidii kutia moyo anapokabili magumu haya ya mwilini!”
Kwa hiyo Mkristo ye yote aliye na udhaifu wa mwilini asione kwamba jitihada zake za kumsifu Yehova na kujenga waamini wenzake kwa unyenyekevu hazina matokeo. Mzee mmoja anaeleza hivi: “Ndugu Henderson alianza kusimama jukwaani karibuni tu, hali wakati uliopita alikuwa akiketi na kuzungumza na kundi. . . . Uhakika huo mwepesi umekuwa wenye kutia nguvu imani na kunitia moyo kwa sababu ninaona kwamba mtu aliye mwaminifu katika utumishi wa Yehova, na ambaye amepatwa na msiba wenye kudhoofisha na kukatiza utumishi wake, ameyashinda mambo hayo kwa msaada wa roho ya Yehova.”
NILISAIDIWA NA MUNGU ANAYEKUMBUKA
Kweli kweli, ni kwa msaada wa Yehova tu kwamba Wakristo wanaweza kuushinda msiba, hata uwe wa namna gani. “Msaada wangu utatoka wapi?” akauliza mtunga zaburi. “Msaada wangu u katika [Yehova], aliyezifanya mbingu na nchi.” (Zab. 121:1, 2) “Yehova alinisaidi kusubiri—kuvumilia,” asema Alex. ‘ Alitoa msaada wenye upendo akanipa nguvu za kushikamana na ukamilifu wangu chini ya magumu.’ Janet anaongeza hivi: “Matatizo yalipozuka nilimpelekea Yehova kwa sala, bila kuomba mwujiza bali kwamba Yeye anionyeshe njia ya kukabiliana nayo na kutosheka na matokeo, hata yaweje.”—1 Pet. 5:6, 7.
Wakristo hawatumikii Mungu anayesahau. Yehova hawaachi wale wanaompenda kweli kweli, naye ameweka mbele yao tumaini lenye furaha la uzima wa milele. (Zab. 94:14; Yohana 3:16; 2 Pet. 3:13) Hivyo, akiwa na maoni yanayofaa ajapokuwa hajiwezi, Alex anasihi hivi:
“Changamkeni, ‘dumuni katika sala’ na kuendelea katika imani. Siku fulani iliyo karibu, vipofu wataona, viziwi watasikia, ulimi wa wasionena utaimba kwa furaha—na, ndiyo—vilema wataruka-ruka kama vile anavyofanya kulungu mwepesi. Bila shaka, nautamani sana wakati huo mzuri sana. Kwa wakati huu, kumtumikia Yehova, Mungu anayekumbuka, kunaleta furaha ya kweli.”