SIMULIZI LA MAISHA
“Sasa Ninaipenda Huduma!”
NILILELEWA katika mji wa Balclutha, kwenye Kisiwa cha Kusini cha New Zealand. Nilipokuwa mtoto, nilijihisi nikiwa karibu na Yehova na nilipenda kuwa katika kweli. Sikuiona mikutano kuwa jambo lenye kuchosha, na kutaniko lilikuwa mahali pazuri nilipohisi nikiwa salama na mwenye furaha. Ingawa sikuwa mzungumzaji sana, nilifurahia kushiriki katika huduma kila juma. Sikuogopa kuwahubiria wanafunzi wenzangu na watu wengine. Nilijivunia kuwa Shahidi wa Yehova, na nikiwa na umri wa miaka 11, nilijiweka wakfu kwa Mungu.
NAPOTEZA SHANGWE YANGU
Inasikitisha kwamba nilipokuwa na umri wa miaka 13 hivi, uhusiano wangu wa karibu pamoja na Yehova ulipoa. Wanafunzi wenzangu walionekana kana kwamba wana uhuru mwingi, nami nilitaka kuwa na uhuru kama huo. Nilihisi nimelemewa na sheria za wazazi wangu na viwango vya Kikristo, na utendaji wa kiroho ulionekana kuwa kazi ngumu. Ingawa sikuwahi kutilia shaka uwepo wa Yehova, sikuhisi nikiwa karibu naye.
Hata hivyo, nilimtolea Yehova utumishi wa kijuujuu ili kuepuka kuwa mhubiri asiyetenda. Nilipoenda kuhubiri sikujitayarisha, hivyo haikuwa rahisi kwangu kuanzisha au kuendeleza mazungumzo. Kwa sababu hiyo sikupata matokeo mazuri na shangwe katika huduma yangu, jambo lililofanya nisifurahie huduma hata zaidi. Ningejiuliza, ‘Mtu anawezaje kuendelea kufanya kazi ya kuhubiri juma baada ya juma, mwezi baada ya mwezi?’
Nilipofikisha umri wa miaka 17, nilikuwa na tamaa kubwa ya kuishi maisha ya kujitegemea. Hivyo nilifungasha vitu vyangu, nikaondoka nyumbani, na kuhamia Australia. Wazazi wangu walihuzunika nilipokuwa nikiondoka. Walikuwa na wasiwasi, lakini walidhani kwamba ningeendelea na ratiba yangu ya mambo ya kiroho.
Nikiwa Australia, hali yangu ya kiroho ilizorota hata zaidi. Nilihudhuria mikutano mara chache sana. Nilivutiwa na vijana ambao kama mimi, waliona ni sawa kuhudhuria mikutano leo, lakini kesho wangeenda kunywa na kucheza muziki kwenye klabu za usiku. Ninapokumbuka wakati huo, ninatambua kwamba nilikuwa nimekanyaga mguu mmoja kwenye kweli na mguu mwingine ulimwenguni, lakini sikujihisi huru upande wowote.
SOMO LISILOTARAJIWA LAKINI MUHIMU
Miaka miwili baadaye, nilikutana kwa kifupi na dada ambaye bila kujua alinifanya nianze kufikiria kuhusu mahali ambapo maisha yangu yalikuwa yakielekea. Nilikuwa ninaishi kwenye nyumba moja pamoja na dada watano waseja, na tulimwalika mwangalizi wa mzunguko na Tamara, mke wake, waje wakae nasi kwa juma moja. Mume wake alipoenda kushughulikia mambo ya kutaniko, Tamara alitumia muda wake pamoja nasi wasichana na kucheka nasi. Nilifurahia jambo hilo. Alikuwa mtu wa watu na ilikuwa rahisi kuzungumza naye. Nililiona kuwa jambo lenye kupendeza kwamba mtu mwenye hali nzuri hivi ya kiroho, anaweza pia kuwa mtu ambaye unaweza kufurahia kutumia wakati pamoja naye.
Tamara alikuwa mwenye shauku sana. Upendo wake kuelekea kweli na huduma ulinichochea nimwige. Alifurahia sana kumpa Yehova kilicho bora, wakati mimi sikuwa na furaha nilipomtolea Yehova utumishi wa kijuujuu. Mtazamo wake mzuri na furaha yake ya kweli ilinichochea sana maishani. Mfano wake ulinifanya nifikirie kuhusu kweli hii ya msingi ya Kimaandiko: Yehova anatamani sisi sote tumtumikie “kwa kushangilia” na “kwa kelele za shangwe.”—Zab. 100:2.
NACHOCHEA UPYA UPENDO WANGU KUELEKEA HUDUMA
Nilitaka kuwa na shangwe kama ya Tamara, lakini nilihitaji kufanya mabadiliko fulani makubwa. Ilinichukua muda, lakini hatimaye nilianza kupiga hatua moja ndogo baada ya nyingine. Nilianza kujitayarisha kwa ajili ya huduma, na kufanya upainia msaidizi pindi kwa pindi. Jambo hilo lilinisaidia kupunguza wasiwasi na kufanya nijiamini zaidi. Kadiri nilivyoitumia mara nyingi zaidi Biblia katika huduma, ndivyo nilivyofurahia zaidi huduma. Baada ya muda mfupi, nilikuwa nikifanya upainia msaidizi kila mwezi.
Nilianza kuchagua marafiki wa umri mbalimbali ambao walikuwa wanafanya vizuri katika kweli na waliofurahia utumishi wao kwa Yehova. Mfano wao mzuri ulinisaidia kufikiria upya mambo niliyotanguliza na kusitawisha ratiba nzuri ya mambo ya kiroho. Nilianza kufurahia huduma hata zaidi, na hatimaye nikaanza kutumikia nikiwa painia wa kawaida. Kwa mara ya kwanza baada ya miaka mingi, nilikuwa mwenye furaha na nilijihisi huru kutanikoni.
NAPATA MWANDAMANI WA KUDUMU WA KUFANYA NAYE UPAINIA
Mwaka mmoja baadaye, nilikutana na Alex, Ndugu mwenye fadhili na mnyoofu, aliyempenda Yehova na huduma. Alikuwa akitumikia akiwa mtumishi wa huduma na alikuwa ametumikia akiwa painia wa kawaida kwa miaka sita. Pia, Alex alikuwa ametumikia kwa muda fulani kwenye eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri nchini Malawi. Akiwa huko alishirikiana na wamishonari ambao walimwekea kielelezo kizuri na kumtia moyo aendelee kutanguliza masilahi ya Ufalme maishani mwake.
Mwaka wa 2003, nilifunga ndoa pamoja na Alex, na tumeendelea katika utumishi wa wakati wote tangu wakati huo. Tumejifunza mambo mengi mazuri, na Yehova ametubariki kwa njia nyingi sana.
MLANGO ULIOONGOZA KWENYE BARAKA NYINGI ZAIDI
Tukiwa katika utumishi wa shambani huko Gleno, Timor-Leste
Mwaka wa 2009, tulialikwa tukatumikie tukiwa wamishonari nchini Timor-Leste, nchi ndogo iliyo miongoni mwa visiwa vya Indonesia. Tulishtuka, tulisisimka, na kuogopa kwa wakati uleule mmoja. Miezi mitano baadaye tuliwasili katika mji mkuu wa nchi hiyo, Dili.
Kuhama kulihusisha mabadiliko makubwa katika njia yetu ya maisha. Tulihitaji kuzoea utamaduni, lugha, chakula, na hali mpya za maisha. Tukiwa kwenye huduma, mara nyingi tulijionea athari za umaskini, elimu duni, na ukandamizaji. Na tulikutana na watu wengi ambao walikuwa wameathirika kimwili na kihisia kwa sababu ya vita na ukatili.a
Huduma ilikuwa nzuri sana! Kwa mfano, pindi moja nilikutana na msichana mwenye umri wa miaka 13 aliyeitwa Mariab na alikuwa mwenye huzuni. Mama yake alikuwa amekufa miaka michache iliyopita, na alimwona baba yake mara chache sana. Kama tu ilivyokuwa kwa watoto wengi wa umri wake, Maria hakuwa na mwelekeo wowote maishani mwake. Ninakumbuka wakati mmoja alipolia huku akinieleza hisia zake. Hata hivyo, sikuelewa mambo aliyokuwa akisema kwa sababu bado nilikuwa sijui kuzungumza kwa ufasaha lugha yake. Nilisali kwa Yehova, nikimwomba anisaidie nimtie moyo, kisha nikaanza kumsomea maandiko yenye kufariji. Kwa miaka michache iliyofuata, niliona jinsi kweli ilivyobadili mtazamo, mwonekano, na maisha ya Maria. Alibatizwa, na sasa anaongoza mafunzo yake ya Biblia. Leo, Maria ana familia kubwa ya kiroho, naye anahisi kwamba anapendwa.
Yehova amebariki kazi ya kuhubiri nchini Timor-Leste. Ingawa wahubiri wengi wamebatizwa ndani ya miaka kumi tu iliyopita, wengi wanatumikia wakiwa mapainia wa kawaida, watumishi wa huduma, au wazee. Wengine wanatumikia katika ofisi ya utafsiri na wanasaidia kwenye kazi ya kutokeza chakula cha kiroho katika lugha za wenyeji. Nilifurahi sana kusikia wakiimba kwenye mikutano, kuona nyuso zao zenye tabasamu, na kuona ukuzi wao wa kiroho.
Pamoja na Alex, tukielekea kwenye eneo ambalo halijagawiwa kutaniko lolote ili kugawa mialiko ya Ukumbusho
SIWEZI KUWAZIA MAISHA YENYE FURAHA ZAIDI
Mgawo wetu nchini Timor-Leste ulikuwa tofauti kabisa na maisha yetu nchini Australia, lakini siwezi kuwazia maisha yenye furaha zaidi kuliko hayo. Nyakati nyingine, tulipanda basi dogo lililojaa watu, pamoja na samaki wakavu na rundo la mboga kutoka sokoni. Baadhi ya siku, tungeongoza funzo la Biblia kwenye nyumba ndogo isiyo na sakafu iliyokuwa na joto sana, huku kuku wakikimbizana. Lakini licha ya changamoto hizo, mara nyingi nilijiambia ‘Ninafurahia sana maisha haya!’
Tukiwa tunaelekea kwenye eneo la kuhubiri
Ninapokumbuka wakati uliopita, ninashukuru sana kwamba wazazi wangu walifanya yote waliyoweza ili kunifundisha njia za Yehova na kunitegemeza, hata katika kipindi kigumu cha utineja. Methali 22:6 imethibitika kuwa kweli katika kisa changu. Baba na Mama yangu wanatuonea fahari mimi na Alex, wanafurahi kuona tukitumiwa na Yehova. Tangu mwaka 2016, tumekuwa tukitumikia katika kazi ya kuzungukia makutaniko katika eneo la ofisi ya tawi ya Australasia.
Nikiwaonyesha watoto wa Kitimori wenye furaha video za Caleb na Sophia
Ni vigumu kuamini kwamba pindi moja niliona kazi ya kuhubiri inachosha. Sasa ninaipenda huduma! Nimekuja kutambua kwamba licha ya panda shuka za maisha, shangwe ya kweli inatokana tu na kumtumikia Mungu kwa moyo wote. Kwa hakika, miaka 18 ya kumtumikia Yehova pamoja na Alex imekuwa yenye furaha zaidi maishani mwangu. Sasa ninaelewa ukweli wa maneno ya mtunga Zaburi Daudi, aliyemwambia hivi Yehova: “Wale wote wanaokukimbilia watashangilia; watapaza sauti kwa shangwe daima. . . . Na wale wanaolipenda jina lako watashangilia kwa sababu yako.”—Zab. 5:11.
Ni shangwe iliyoje kujifunza Biblia pamoja na watu hawa wanyenyekevu!
a Kuanzia mwaka wa 1975, nchi ya Timor-Leste ilipitia miaka 20 ya vita vya kupambania uhuru wa kisiasa.
b Baadhi ya majina yamebadilishwa.