Ubukuzi wa Mambo ya Kale Waithibitisha Biblia
KWA WATU wenye kiburi ambao kwa kushupaza shingo zao walikataa kukubali kuwa yeye ni Masihi wakapuza wanafunzi wake, Yesu alisema hivi: “Nawaambia ninyi, wakinyamaza hawa, mawe yatapiga kelele.” (Luka 19:40) Kwa furaha, Yesu alikuwa, na angali na wanafunzi wanaokataa kunyamaza. Hata hivyo, kwa njia fulani, mawe ambayo yalikuwa mashahidi walionyamaza wa matukio ya Kibiblia yamefanywa yapige kelele, yakishuhudia kwamba Biblia ni ya kuaminika. Sayansi ambayo imeruhusu mawe hayo yaseme katika kuunga Biblia mkono inaitwa ubukuzi wa mambo ya kale, ambao unaelezwa kuwa “masomo ya kisayansi ya mambo yenye kuonekana yaliyobaki ya wakati uliopita.”
Katika kazi yake ya utaalamu katika kitabu Light from the Ancient Past, Jack Finegan anatuarifu kwamba “ubukuzi wa mambo ya kale wa kisasa unaweza kusemwa kwamba ulianza katika mwaka 1798, wakati ambapo wataalamu na mafundi Wafaransa karibu mia moja waliambatana pamoja na Napoleon wakati wa kuiteka Misri.” Katika mwaka 1822 Mtaalamu wa Mambo ya Kale ya Misri Mfaransa Champollion alifaulu kufunua fumbo ya maandishi ya picha yaliyokuwa juu ya jiwe liitwalo Rosetta. Kufikia mwisho wa karne ya 19 ubukuzi ulikuwa ukifanywa kwa mpango fulani na wabukuzi wa mambo ya kale katika Misri, Ashuru, Babeli na Palestina, nao wameendelea kufanya hivyo mpaka wakati huu. Je! uvumbuzi wa wabukuzi wa mambo ya kale umethibitisha maandishi ya Biblia?
CHANZO CHA ULIMWENGU NA WANADAMU
Uvumbuzi mmoja uliofanywa katika makaburi ya Misri unatuwezesha tulinganishe maelezo ya Biblia juu ya chanzo cha wanadamu pamoja na masimulizi ya uumbaji yaliyomo katika kitabu cha Misri ya kale kinachoitwa Book of the Dead, ambacho kimo katika sanduku la kioo katika Jumba la Kuhifadhi Mambo ya Kale la Louvre, Paris (Ufaransa). Akiandika katika kitabu cha maarifa Supplement au Dictionnaire de la Bible, Louis Speleers, mwangalizi wa Jumba la Kuhifadhi Mambo ya Kale la Cinquantenaire katika Brussels, Ubelgiji, anaeleza hivi: “[Kitabu] Book of the Dead kinasimulia kwamba siku moja [mungu-jua] Ra aliacha Jicho lake la kimungu liking’aa mbinguni. Shu na Tefnut wakamletea Jicho lake, nalo likaanza kulia, nao watu wakatokea katika machozi ya Ra.”
Uvumbuzi mwingine wa mambo ya kale yaliyobukuliwa ambao unawezesha ulinganifu wenye kupendeza pamoja na masimulizi ya Biblia ni mfululizo wa mabamba ya udongo saba yenye Enuma elish, au “Utenzi wa Uumbaji” wa Wasumeri na Wababeli. Kulingana na maandishi hayo ya kale, Marduki, mungu wa mji wa Babeli, alimshinda mungu wa kike wa kale Tiamat na kumkata vipande viwili. “Kwa kipande kimoja akatengeneza kuba la mbinguni, na kwa kile kingine dunia. Akiisha kufanya hivyo, akatengeneza ulimwengu. . . . Kisha ‘ili miungu waishi katika ulimwengu wafurahishe mioyo yao’ Marduki akaumba wanadamu.”—Larousse Encydopedia of Mythology.
Je! unaamini kwamba wanadamu walitoka katika machozi ya Ra? Wamisri wengi wastaarabu na wenye elimu waliamini hivyo. Au unaweza kukubali wazo la kwamba mwili uliokatwa wa mungu mke ulitokeza mbingu na dunia? Hiyo ni mifano miwili tu ya hadithi za uumbaji ambazo ziliaminiwa na watu wa vizazi vilivyofuatana katika nyakati zilizopita.
Leo, watu wengi wenye elimu nyingi wanataka tuamini kwamba ulimwengu wote mkubwa na namna zote za uhai, vyote hivyo vilitokea ghafula, pasipo tendo la Mtu ye yote mkuu zaidi mwenye uhai, ujapokuwa uhakika wa kwamba mwanasayansi Mfaransa Louis Pasteur alithibitisha bila shaka kwamba uhai unatokana na uhai. Je! si jambo la akili zaidi kukubali masimulizi ya Biblia yanayosema kwa wazi kabisa kwamba ulimwengu mkubwa ni wonyesho wa ‘nguvu nyingi mno’ (kwa kuwa Einstein na wengine wameonyesha kwamba vitu ni namna fulani ya nguvu)? Na je! si jambo la akili zaidi kuamini Maandiko Matakatifu, ambayo yanaonyesha kwamba namna zote za uhai zimetoka kwa Mungu, Chanzo kikubwa cha uhai, na kwamba wanadamu waliumbwa “kwa mfano wa Mungu”?—Mwa. 1:27; Zab. 36:9; Isa. 40:26-28; Yer. 10:10-13.
UBUKUZI WA MAMBO YA KALE PAMOJA NA ABRAHAMU
Mtu mashuhuri katika Biblia ni Abrahamu. Si kwamba yeye ni babu ya waandikaji wote wa Biblia, wa Wayahudi na Waarabu wengi, bali pia anaitwa “baba yao wote waaminio.” (Rum. 4:11) Pamoja na hayo, watu wa mataifa yote wanapaswa kupendezwa kujua kama masimulizi ya Biblia juu ya Abrahamu ni ya kweli. Sababu gani? Kwa sababu ni yeye aliyeahidiwa na Mungu hivi: “Kupitia kwa uzao wako mataifa yote ya dunia yatajibarikia hakika.” (Mwa. 22:16-18, NW) Iwapo tunataka kuwa kati ya wale “waaminio” ambao watabarikiwa kupitia kwa uzao wa Abrahamu, ushuhuda unaoonyesha usahihi wa habari nyingi inayotolewa katika Biblia juu ya maisha na nyakati za Abrahamu wapaswa kutupendeza sana.
Biblia inatuarifu kwamba Abrahamu (ambaye wakati huo aliitwa Abramu) alilelewa katika “Uru wa Wakaldayo.” (Mwa. 11:27, 28) Je! hapo ni mahali pa kuwazia? Mavumbuzi ya wabukuzi wa mambo ya kale yamefunua nini? Mapema katika mwaka 1854, J. E. Taylor akijaribia alitambulisha Uru kuwa Tell el-Muqayyar (“Chungu ya Lami”), maili chache tu magharibi mwa Frati. Katika mwaka 1869, Mfaransa wa kutoka Mashariki Jules Oppert alitoa ripoti katika Chuo Kikuu cha Ufaransa, katika Paris, akaonyesha mahali hapo kwa uhakika kuwa Uru, msingi wake ukiwa ni mitungi ya udongo yenye maandishi ya michoro kama kabari iliyopatikana huko na Taylor. Kisha, muda mrefu baadaye, tangu mwaka 1922 mpaka 1934, mbukuzi wa mambo ya kale wa Uingereza Sir Leonard Woolley si kwamba tu alithibitisha jambo hilo bali pia alivumbua kwamba Uru ulioachwa na Abrahamu ulikuwa mji wenye kusitawi na wenye ustaarabu, wenye nyumba nzuri na mnara mkubwa wa hekalu, au zigareti, uliotumiwa kwa ibada ya mungu-mwezi Nanna, au Sini. Wanahistoria walikuwa wametilia mashaka kwa muda mrefu juu ya mji wa Uru unaotajwa katika Biblia kuhusiana na Abrahamu. Walakini uvumbuzi wa mbukuzi wa mambo ya kale ulithibitisha Biblia ni ya kweli.
Vilevile wabukuzi wa mambo ya kale wamethibitisha mila nyingi zinazotajwa katika masimulizi ya Biblia kuhusiana na Abrahamu. Kwa mfano, katika Nuzu, au Nuzi, mji wa kale wa Uru upande wa kusini-mashariki wa Ninawi, mabamba ya udongo yamepatikana ambayo yanaonyesha mila kama hizi ni za kweli: Watumwa kuwa warithi wa wazazi wasiokuwa na watoto (linganisha maneno ya Abrahamu juu ya mtumwa wake Eliezeri—Mwanzo 15:1-4); mke asiyeweza kuzaa akiwa na lazima ya kumpa mume wake suria (Sara, au Sara, alimpa Abrahamu Hajiri—Mwanzo 16:1, 2); na mikataba ya biashara ilifanyiwa kwenye lango la mji (linganisha Abrahamu akinunua shamba na pango la Makpela, karibu na Hebroni—Mwanzo 23:1-20). Mifano ya namna ubukuzi uliofanywa Nuzi unavyounga mkono Biblia unajaza zaidi ya safu nane zenye maandishi madogo katika kitabu cha kitaalamu cha Kifaransa Supplement au Dictionnaire de la Bible. (Kitabu cha Tano, safu 663-672) Kitabu Encyclopaedia Britannica kinaeleza hivi: “Vifaa hivyo vya Nuzi vimeeleza wazi vifungu vingi vigumu katika masimulizi ya Mwanzo ya wakati uo huo wa mababu.”
MAJINA YATHIBITISHWA
Mbukuzi wa mambo ya kale Mfaransa Andre Parrot alifanya ulimaji mkubwa mahali ulipokuwa mji wa kale wa kifalme wa Mari, katika Frati ya Kati. Mji ulio taifa wa Mari ulikuwa mmojawapo wa mamlaka zenye kutawala katika Mesopotamia ya Juu katika mwanzo wa mileani (miaka elfu) ya pili K.W.K., hata ulipotwaliwa na kuharibiwa na Mfalme Hammurabi wa Babeli. Katika magofu ya jumba kubwa la mfalme lililovumbuliwa hapo, kikundi cha wabukuzi wa mambo ya kale Wafaransa kilipata mabamba ya udongo zaidi ya 20,000. Baadhi ya mabamba hayo yenye maandishi ya michoro kama kabari yanataja miji kwa majina haya Pelegi, Serugi, Nahori, Tera na Harani. Kwa kupendeza, majina yote hayo yanapatikana katika masimulizi ya Biblia yakiwa ni majina ya watu wa ukoo wa Abrahamu.—Mwa. 11:17-26.
Akieleza juu ya ufanani huo wa majina ya kale, John Bright anaandika hivi katika kitabu History of Israel: “Katika yote hayo . . . hakuna mzee wa ukoo wa Kibiblia anayetajwa. Walakini ushuhuda huo mwingi kutoka kwa maandishi ya wakati huo unaonyesha waziwazi kwamba majina yao yanapatana kabisa na utaratibu wa majina wa watu wa Amori wa mwanzo wa mileani ya pili, wala si katika majina yale ya wakati wo wote wa baadaye. Kwa hiyo masimulizi juu ya mababu kwa habari hii ni ya kweli kabisa.”
Hivi karibuni katika mwaka 1976, wabukuzi wa mambo ya kale Waitalia na Washami walipata, katika upande wa kaskazini wa Shamu, mji ulio taifa wa kale wa Ebla. Kama vile Mari, Ebla hautajwi katika Biblia, walakini majina yote mawili yanaonekana katika vitabu vya zamani vya kipindi cha wazee wa ukoo. Kwa hiyo uvumbuzi wa wabukuzi wa mambo ya kale unafunua nini katika mahali hapa papya? Katika maktaba ya makao ya kifalme, maelfu ya mabamba ya udongo yalipatikana, yakiwa ya wakati wa mileani ya tatu au mwanzo wa mileani ya pili kabla ya Wakati wa Kawaida. Likiripoti juu ya uvumbuzi huo katika toleo lake la Machi 19, 1979, gazeti la Kifaransa la kila juma Le Point lilisema hivi: “Kwa kushangaza majina yanafanana [na yale yaliyo katika Maandiko]. Katika Biblia twapata ‘Abrahamu;’ katika mabamba ya Ebla, ‘Ab-ra-um;’ Esau—E-sa-um; Mikaeli—Mi-ki-ilu; Daudi—Da-u-dum; Ishmaeli—lsh-ma-ilum; Israeli—Ish-ra-ilu. Vilevile maandishi hayo ya Ebla yana majina ya Sodoma na Gomora, miji inayotajwa katika Biblia, walakini ambayo kuwapo kwayo kulikuwa kunapingwa kwa muda mrefu na wataalamu. . . . Na zaidi, mabamba hayo yanapanga miji kwa utaratibu ule ule ambao intajwa katika Agano la Kale: Sodoma, Gomora, Adma, Seboimu na Bela [Mwa. 14:2].” Kulingana na Boyce Rensberger, akiandika katika gazeti New York Times, “wataalamu wengine wa kibiblia wanaamini [mabamba ya Ebla] yanalingana na vile Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi katika kuonyesha ukweli na kuongeza maarifa ya maisha katika . . . nyakati” za Kibiblia.
MILA NA SHERIA
Ubukuzi wa mambo ya kale umefanya mengi katika kueleza mila zinazotajwa katika Biblia, hivyo kuonyesha usahihi wa maandishi ya Biblia. Jambo moja ni masimulizi katika Mwanzo, sura ya 31, ambapo panaripotiwa kwamba mke wa Yakobo, Raheli ‘aliiba vinyago vya babaye,’ Labani. (Mst. 19) Inaelezwa hapo sababu gani Labani alijisumbua akimfuata bintiye na mume wake kwa siku saba. Kusudi lilikuwa kuipata “miungu” yake. (Mist. 23, 30) Kwa kupendeza, uvumbuzi wa wabukuzi wa mambo ya kale katika mji wa kale wa upande wa kaskazini wa Mesopotamia wa Nuzi umefunua kulikuwako sheria ya mababu kwamba mtu akiwa na miungu ya jamaa alipata haki za kumiliki shamba la baba-mkwe wake aliyekufa. Mtu akikumbuka kwamba Labani alikuwa mkaaji wa upande wa kaskazini-magharibi wa Mesopotamia na namna alivyokuwa amemdanganya Yakobo, maarifa ya sheria hiyo yanaonyesha kwa njia nzuri wizi usio wa kawaida wa Raheli na jitihada za bidii za Labani kupata “miungu” yake. Jumba la Kuhifadhi Mambo ya Kale la Louvre, katika Paris, linayo ‘miungu ya jamaa’ iliyovumbuliwa katika miji mbalimbali ya Mesopotamia. Udogo wayo (inchi nne mpaka sita [centimetre 10 mpaka 15]) vilevile unasaidia kueleza namna Raheli aliweza kuficha vinyago hivyo kwa kukalia kikapu kilichokuwa navyo na kukataa kusimama Labani alipokuwa akitafuta.—Mist. 34, 35.
Mojawapo cha vitu vyenye thamani sana katika Jumba la Kuhifadhi Mambo ya Kale la Louvre ni bamba jeusi la jiwe la futi karibu nane (metre 2.25) urefu na linalojulikana kwa kawaida kama “Orodha ya Sheria za Hammurabi.” Chini ya picha yenye kumwonyesha Mfalme Hammurabi wa Babeli akipokea mamlaka kutoka kwa mungu-jua Shamashi, kuna sheria 282 zilizoandikwa katika safu zenye maandishi ya michoro kama kabari. Kwa kuwa inasemekana kwamba Hammurabi alitawala tangu mwaka 1728 mpaka 1686 K.W.K., wachambuzi wengine wa Biblia wamesema kwamba Musa, aliyeandika sheria za Israeli karne moja na nusu baadaye, alitumia orodha ya sheria za mfalme huyu wa Babeli. Akitoa maelezo ya kupinga shtaka hilo, W. J. Martin anaandika katika kitabu Documents from 0ld Testament Times hivi:
“Ujapokuwa ufanani mwingi, hakuna msingi wa kudhani kwamba Waebrania walitumia cho chote kutoka kwa Wababeli. Hata wakati orodha hizo mbili za sheria zinapotofautiana kidogo katika maandishi, zinatofautiana sana katika maana. Kwa mfano, katika Orodhi ya Sheria za Hammurabi, wizi na kupokea bidhaa zilizoibwa ulileta adhabu ya kifo (Sheria za 6 na 22), walakini katika sheria za Israeli adhabu ilikuwa kulipa. (Kut. 22:1; Law. 6:1-5) Sheria ya Musa ilikataza kurudisha mtumwa aliyetoroka kwa bwana zake (Kum. 23:15, 16), sheria za Wababeli zilimwadhibu kwa kifo mtu ye yote aliyemchukua mtumwa aliyetoroka.—Sheria za 15, 16, 19.
Katika kitabu Supplement au Dictionnaire de la Bible, Mfaransa wa Mashariki Joseph Pless aliandika hivi: “Haielekei mtungaji wa sheria za Kiebrania alitumia sheria mbalimbali za Babeli na Ashuru. Hakuna cho chote katika utungaji wake kinachoweza kuthibitishwa kilitolewa hapo. Ingawa kuna ufanani wenye kupendeza, unaweza kuelezwa na utaratibu wa sheria za mila ambazo zapatikana kati ya watu waliotoka mahali pale pale.”
Ingawa Orodha ya Sheria za Hammurabi inaonyesha roho ya kulipa kisasi, sheria ya Musa inasema hivi: “Usimchukie ndugu yako moyoni mwako. . . . Usifanye kisasi, wala kuwa na kinyongo juu ya wana wa watu wako; bali umpende jirani yako kama nafsi yako.” (Law. 19:17, 18) Kwa hiyo si kwamba tu imethibitishwa Musa hakutumia sheria za Hammurabi bali pia ulinganishi wa sheria za Biblia na zile zilizoandikwa juu ya mabamba ya mawe yaliyochimbuliwa na wabukuzi wa mambo ya kale unaonyesha sheria hizo za Kibiblia ni bora zaidi kuliko zile zilizokuwa zikiongoza watu wengineo wa kale.
UBUKUZI WA MAMBO YA KALE NA MAANDIKO YA KIGIRIKI
Namna gani Maandiko ya Kigiriki, ambayo kwa kawaida yanajulikana kama “Agano Jipya”? Je! ubukuzi wa mambo ya kale umethibitisha usahihi wa sehemu hiyo ya maana ya Biblia? Vitabu vizima vimeandikwa kuonyesha kwamba kuna uthibitisho kama huo. Mapema katika mwaka 1890, Mtaalamu wa Biblia Mfaransa F. Vigouroux alichapisha kitabu chenye zaidi ya kurasa 400 chenye kichwa “Le Nouveau Testament et les decouvertes archeologiques modernes’’ (Agano Jipya na Mavumbuzi ya Ubukuzi wa Mambo ya Kale wa Kisasa). Katika kitabu hicho alitoa uthibitisho mwingi kuunga mkono zile Injili, Matendo ya Mitume na barua zinazopatikana katika Maandiko ya Kigiriki. Katika mwaka 1895, W. M. Ramsay alichapisha kitabu chake ambacho ni kizuri sana cha sasa St. Paul the Traveller and the Roman Citizen, ambacho kinatoa habari nyingi iliyo bora inayoonyesha usahihi wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.
Hivi karibuni zaidi, vitabu vingi vingine na makala ya wataalamu vimechapishwa kuonyesha namna ubukuzi wa mambo ya kale umeonyesha ukweli wa Biblia nzima. Katika kitabu chake The Archaeology of the New Testament, ambacho kwanza kilichapishwa katika mwaka 1970, E. M. Blaiklock anaandika hivi: “Mambo ya kutokeza yanayotetea uandikaji wa historia ya kibiblia yamefunza wanahistoria waheshimu ukweli wa Agano la Kale na Jipya pia, na kuvutiwa na usahihi wake, kupendezwa sana na kweli, na ufahamu wa kihistoria ulioongozwa kwa roho wa waandikaji mbalimbali ambao waliipa Biblia vitabu vyake vya historia.”
Ndiyo, ubukuzi wa mambo ya kale unaunga mkono waziwazi Biblia.
[Ramani katika ukurasa wa 6]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Harani
Ebla
Mari
Nuzi
Babeli
Lagashi
Uru
Sumeri
Ghuba la Uajemi
[Picha katika ukurasa wa 6]
Zigareti iliyofukuliwa katika Uru wa Ukaldayo wa zamani
[Picha katika ukurasa wa 7]
mungu wa jamaa (aliyepatikana katika Lagashi)
Orodha ya Sheria za Hammurabi