Je! Ni Kweli kwamba “Wote Wamefanya Dhambi”?
JE! UMEPATA kuuliza sababu gani, zijapokuwa jitihada zote za watu wanyofu, kufikia wakati huu wanadamu wameshindwa na mengi ya matatizo yao yenye uharaka? Sababu gani, ingawa wanaona vizuri mambo wanayotaka—amani, fanaka, furaha, kutokuwa na magonjwa— wanaonekana wakienda mbali zaidi na zaidi kutoka kwa miradi hiyo?
Sababu kubwa inapatikana katika maneno haya ya mtume Paulo: “Wote wamefanya dhambi, na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Rum. 3:23) Ndiyo, jitihada nyingi za wanadamu zinaharibiwa na hali ya dhambi ya wanadamu.
Huenda wengine wakatilia shaka maneno ya mtume Paulo. Huenda wakasema: ‘Unaweza kuaminije kwamba mimi ni mkosaji? Simfanyii jirani yangu mabaya. Naishi maisha ya utulivu nami sifanyi matata yo yote. Ninafanya dhambi gani?’ Ukweli ni kwamba, yajapokuwa hayo, dhambi inatia ndani zaidi ya kuumiza jirani zetu au kufanya matata. Ndiyo, mambo hayo ni dhambi, na kuyaepuka ni jambo la kusifika. Walakini neno “dhambi” lina matumizi makubwa zaidi. Paulo alishirikisha jambo hilo na “kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” Hivyo, inashirikishwa na uhusiano wetu na Muumba wetu, Yehova Mungu.
Maneno yanayotafsiriwa “dhambi” katika Biblia zetu za kisasa hapo awali yalikuwa na wazo la “kukosa lengo” la utii mkamilifu. Kutii nini? Mapenzi ya Mungu. Kwa hiyo, kamusi ya kisasa ya Biblia inasema: “Dhambi ni kukengeuka kuacha uhusiano wa uaminifu kumwelekea Mungu na vilevile kutokutii amri na sheria.” Kwa kuwa ndivyo ilivyo, ni Mungu peke yake anayeweza kutuambia kwa kufaa anayoona kuwa dhambi, naye amefanya hivyo katika Biblia.
Kutatua Tatizo Hilo
Kwanza kabisa, mambo mengi yanayokubaliwa katika ulimwengu wa kisasa kwa kweli ni makosa. Biblia inasema hivi: “Waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi.” (1 Kor. 6:9, 10) Ndiyo, uzinzi, uasherati na kulalana kwa watu wa namna moja ni dhambi. Ndivyo kulivyo kuiba.
Kweli, watu wengi huepuka uasherati na kuiba, nalo hilo ni jambo zuri. Walakini kuna dhambi nyingine. Usemi wetu, pamoja na matendo yetu, yanaweza kuwa yenye dhambi. Kudanganya ni dhambi. Ndivyo kulivyo kusengenya, kusema kwa kukasirika na kutukana. (Kol. 3:9; Zab. 101:5; Efe. 4:31) Pamoja na hayo, Paulo alisema hivi: “Msinung’unike, kama wengine wao walivyonung’unika, wakaharibiwa na mharabu.” (1 Kor. 10:10) Yakobo alilaani kujivuna, naye Paulo akatushauri tuepuke mazungumzo ya kipumbavu na kufanya mzaha kwa mambo machafu. (Yak. 4:16; Efe. 5:4) Je! ye yote wetu anaweza kusema kwa unyofu kwamba yeye hajafanya dhambi kamwe katika mojayapo ya njia hizo? Hakuna. Yakobo, ndugu ya Yesu, alisema hivi: “Mtu asiyejikwaa katika kunena, huyo ni mtu mkamilifu.” (Yak. 3:2) Je! ye yote wetu anaweza kudai kuwa mkamilifu? Hasha.
Mwanafunzi uyo huyo alitaja njia nyingineyo ambayo twaweza kufanya dhambi. Alisema hivi: “Basi yeye ajuaye kutenda mema, wala hayatendi, kwake huyo ni dhambi.” (Yak. 4:17) Hiyo yaweza kuwaje hivyo? Mwazie mwanamume anayetembea katika kijia cha kando kisha ghafula mtoto atimue mbio kutoka shamba lililo mbele yake aingie kwenye barabara yenye motokaa nyingi. Vipi iwapo mtu huyo yuko katika hali ya kuweza kumwokoa mtoto huyo asikanyagwe lakini ampuze na kupita. Ni kweli, yeye hafanyi jambo lo lote baya. Walakini uhakika wa kwamba anashindwa kufanya jambo fulani kusaidia mtoto huyo, hiyo ni dhambi kwake. Ni mara ngapi tumeshindwa sisi sote kutenda katika njia ya upendo kweli kweli kwa wanadamu wenzetu, au kwa Mungu? Kila mara tunaposhindwa, hiyo ni dhambi.
Vilevile nia mbaya zaweza kuwa dhambi. Kujikweza na shingo ngumu kunalaaniwa na Biblia, kuwa woga. (Mit. 21:4; Ufu. 21:8) Hata mawazo mabaya ni dhambi. Ya mwisho ya zile Amri Kumi inasema hivi: “Usiitamani nyumba ya jirani yako, usimtamani mke wa jirani yako; wala mtumwa wake, wala mjakazi wake, wala ng’ombe wake, wala punda wake, wala cho chote alicho nacho jirani yako.”—Kut. 20:17.
Twaweza kuzuiaje tamaa mbaya zisiingie akilini mwetu? Pengine kwa kushughulika na kitu kinachofaa. Walakini iwapo hiyo inashindwa, twapaswa kuzijua na kupigana nazo. (1 Kor. 9:27) Tamaa hizo mbaya ni dhambi machoni pa Mungu.—Mit. 21:2.
Mwishowe, dini ya uongo inaweza kutuongoza kwenye dhambi. Licha ya rnazoea mabaya kama vile kuabudu sanamu na uchawi, ambayo yanakatazwa waziwazi katika Biblia, kuwa mshiriki wa dini ya uongo kunaonyeshwa kuwa ni dhambi. Kikisimulia dini ya uongo kuwa mji mkuu wa ulimwenguni pote kitabu cha Biblia cha mwisho kinasema hivi: “Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake.” (Ufu, 18:4) Dini ya uongo ina hatia ya dhambi kubwa. Imemsingizia Mungu wa kweli wa pekee, ikatesa watumishi wa kweli wa Mungu na kujiingiza katika siasa. Wote walio washiriki wa dini ya uongo wanashiriki dhambi hizo kwa kuwa wanaunga mkono matengenezo yanayofanya hayo.
Sababu Gani Tu Wenye Dhambi?
Tumetaja njia chache tu ambazo katika hizo twaweza kutumbukia katika dhambi. Nyingine nyingi zimeandikwa katika Biblia. Baada ya kuzifikiria, huenda ukakata kauli kwamba haiwezekani kuepuka kufanya dhambi katika njia hii au hii. Bila shaka unakubaliana na Mfalme Sulemani aliyesema hivi: “Hakuna mtu asiyetenda dhambi.” (1 Fal. 8:46) Mungu mwenyewe alisema hivi: “Mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake.” (Mwa. 8:21) Ndiyo, mambo mengi yanatufanyisha dhambi, lakini sana sana udhaifu wa mwili wetu.
Sababu gani iwe hivyo? Ni jambo la kurithi. Hapo kwanza, wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, hawakuwa na tatizo hilo. Walikuwa wakamilifu nao wangeweza kufanya maamuzi yaliyosawazika, ya kiasi kwa habari ya dhambi. Walakini walifanya uchaguzi mbaya, wakaamua kumwasi Mungu, na, hivyo, wakaangukia kutokamilika toka ukamilifu. Kwa sababu hiyo, wakaachia watoto wao wote urithi wa dhambi, maelekeo mabaya. Mtume Paulo alieleza jambo hilo hivi: “Kwa mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.”—Rum. 5:12.
Hivyo, hata tukiwa na nia bora zaidi ulimwenguni, hatuwezi kuepuka kufanya dhambi. Sababu gani? Mtume Paulo mwenyewe alikubali hivi: “Lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo.” (Rum. 7:19) Sote tuna tatizo ilo hilo.
Matokeo yamekuwa yenye msiba kwa wanadamu. Nia bora za wanadamu zimeharibiwa na kukosea kwao. Choyo na pupa yanatokeza uchafuaji wa hewa na maji, umaskini na udhalimu. Kutilia mashaka na kutotumainiana kunatokeza ukosefu wa imara katika uhusiano wa mataifa yote pia kati ya jamaa. Rushwa na uhalifu yanazuia jitihada za nchi za kufanya maendeleo. Nao wanadamu hawawezi kufanya mengi kuhusiana na jambo hilo.
Kuongezea hayo, kwa sababu wanadamu wamerithi hali ya dhambi, amri inayotajwa katika Warumi 6:23 inaning’inia juu ya vichwa vyetu kama wingu lenye kuogopesha: “Mshahara wa dhambi ni mauti.” Hakuna lo lote tunaloweza kufanya kwa uwezo wetu tuepuke kupata adhabu ya mauti kwa ajili ya dhambi zetu, kwa kuwa hakuna lo lote tunaloweza kufanya tuepuke kufanya dhambi kabisa. Kwa sehemu kubwa tunaongozwa na kutokamilika kwetu.
Je! ni hayo tu? Je! sikuzote wanadamu watazuiwa na udhaifu wao wasitimize tamaa zao za kutazamia na kutaka mambo makubwa? Sivyo. Maana kuna Mmoja anayeweza kutusaidia. Baada ya mtume Paulo, kukubali kushindwa kwake mwenyewe kuepuka kuanguka katika dhambi, anaendelea kusema hivi: “Ole wangu, maskini mimi! ni nani atakayeniokoa na mwili huu wa mauti?” Jibu lake ni hili: “Namshukuru Mungu, kwa Yesu Kristo Bwana wetu!” (Rum. 7:24, 25) Ndiyo, kukubali namna tulivyo chini ya uwezo wa dhambi na kuwa kwetu hoi tusiweze kujiokoa kunatufanya tuthamini upendo na huruma nyingi ya Mungu ambaye ametusaidia. Walakini amefanyaje hivyo?