Amani ya Kweli ya Akili Inaletwa na Nini?
AMANI ya akili. Nani anayeweza kuipata katika ulimwengu wa leo wenye msukosuko? Magaidi (watu wajeuri) mara nyingi wanahatirisha maisha ya wanadamu wenzao. Wakimbizi wanakimbia nchi yao na kwenda nchi nyingine. Silaha za nuklea zimejaa nazo zasimama kama walinzi zikiwa zaweza kuua jamii yote ya kibinadamu. Infuleshoni inamaliza haraka sana fedha zilizowekwa akiba, na mara nyingi akiba zilizowekwa muda wote wa maisha ya mtu. Kuongezea hayo kuna “vita” vingi vya kibinafsi vya matatizo ya afya, huzuni inayoletwa na kifo cha mpendwa—na maelfu ya mahangaiko yaliyo kawaida ya watu kila mahali—na hakika amani ya kweli ya akili ni haba katika jamii ya kisasa.
Walakini wengi wanatumainia nini kilete usalama na amani ya akili inayotakiwa? Mara nyingi kuwa na fedha na mali nyingi. Lakini, je! hiyo inaleta amani ya kweli ya akili?
Huenda ikaonekana ndivyo. Walakini kwa unyamavu—bila kufahamika—thamani ya mali itapungua kwa kadiri miaka inavyopita. Kwa mfano, huenda mtu tajiri akawa na mavazi mengi ya bei. Lakini ungekuwa upumbavu kutunuka (kuwekea thamani kubwa) mavazi ya mtu! Mdudu mwenye mabawa manne—sana anapokuwa buu—anaweza kuharibu mavazi yanayothaminiwa sana. Ndiyo, nondo wanaweza kuharibu na, kwa kadiri fulani, wanaweza kupoteza hali ya mtu kujiona salama na amani yake ya akili. Kwa habari hiyo, hata yasipoharibiwa na nondo, mavazi yanachakaa au mwizi aweza kuyaiba.
‘Hazina Isiyopungua’
Nabii wa Mungu, Isaya alionyesha kwamba matokeo ya mwisho ya wapinzani wake waliopotoka yatalinganika na yale ya vazi lililochakaa au lililoliwa na nondo. Lakini katika habari iyo hiyo Isaya alitaja chanzo cha kweli cha usalama na amani ya akili, akisema hivi: “Tazama! Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mwenyewe atanisaidia. Ni nani aliyeko anayeweza kunitangaza kuwa mwovu? Tazama! Wote, kama vazi, watachakaa. Nondo atawala.” (Isa. 50:7-9, NW) Hakika, ingawa mali ni yenye thamani ya muda, uhusiano wa karibu wa kibinafsi pamoja na Mungu unategemeza. Unaleta amani ya kweli ya akili.
Yesu Kristo alizungumza jambo hilo zaidi aliposema hivi: “Msiogope, enyi kundi dogo! Kwa kuwa Baba yenu amependa kuwapeni huo utawala. Uzeni mali zenu zote mkawape maskini. Jifanyieni mifuko isiyochakaa, na jiwekeeni hazina mbinguni ambako haitapungua. Huko wevi hawakaribii, wala nondo hawaharibu. Pale hazina yako ilipo, ndipo pia na moyo wako utakapokuwa.” (Luka 12:32-34, HNWW) Wakati huo Yesu alikuwa akizungumza na wafuasi wake waliotiwa mafuta ambao wangekuwa warithi-washirika wake katika ufalme wa kimbinguni. (Rum. 8:12-17) Walakini kanuni iliyopo hapo inahusu Wakristo wote. Mambo ya kiroho ni ya thamani kubwa sana.
‘Uhusiano wa Karibu na Yehova’ Wenye Thamani
Hata hivyo, chenye thamani zaidi ya vitu vinginevyo vyote ni uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu Aliye Juu Zaidi. Kuhusu “hazina” hiyo, mtunga zaburi Daudi alisema hivi: “Wale wanaomwogopa Yehova ndio wenye uhusiano wa karibu naye.” (Zab. 25:14, NW) Nalo ni jambo bora kama nini kushirikiana na wale wanaofurahia uhusiano wa kibinafsi wa karibu pamoja na Mungu wakiwa watu wake!—Zab. 35:18.
Hata ingawa kuwa pamoja na watu wa Mungu ni jambo la maana, utumishi wetu hauwezi kuwa desturi au jambo la kawaida tu iwapo utakubaliwa na Mungu. Kwa kweli, amani ya kweli ya akili inaweza kukosekana iwapo mtu anashiriki katika utendaji wa Kikristo bila kusudi zuri. Kabla ya kuweka maisha yake wakf kwa Mungu, mwanamke mmoja kijana alipendezwa kushirikiana na Mashahidi wa Yehova. Walakini anakubali hivi:
“. . . Nilivutiwa na watu wa dini hiyo mpya. Walikuwa wenye furaha, watu wenye urafiki waliofurahia kufuata kanuni bora za adili za Biblia. Nilifurahi kuwa pamoja nao. Nilikwenda kwenye mikutano yao na hata nikashiriki kwenda nyumba kwa nyumba nikazungumze na wengine juu ya Biblia.
“Kisha siku moja ulizo zito likaja akilini mwangu. Je! dini inapaswa kuwa uhusiano pamoja na watu wengine au inapaswa kuwa uhusiano pamoja na Mungu? Nikajua kwamba nilikuwa natenda kama mmoja wa Mashahidi wa Yehova kwa sababu nilifurahia sana watu hao na pia nilitaka kupendeza mama-mkwe wangu [aliyekuwa Shahidi], si kwa sababu nilimpenda Mungu. Nilikwenda nyumba kwa nyumba nikiwa na Biblia, walakini sikujua sababu gani nilifanya hivyo. Nikaacha niliyokuwa nikifanya.”
Miezi ilipoendelea, mwanamke huyo kijana alichanganua “yanayomaanishwa na kuwa na uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova Mungu.” Vilevile, alipata msaada wa Kimaandiko kutoka kwa mwanamke mmoja Mkristo naye akahangaikiwa kwa upendo na kundi la kwao la Mashahidi wa Yehova. Matokeo? ‘Akapata tumaini lenye uzima katika uhusiano [wake] wa kibinafsi pamoja na Yehova.’ Mwanamke huyo kijana alibatizwa katika wonyesho wa wakf wake kwa Mungu naye akaanza kumtumikia Yehova kwa furaha pamoja na watu wake.
Amani ya akili na hali ya kujiona salama kweli kweli inafurahiwa na wale walio na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Na yajapokuwa mahangaiko ya maisha, wao, pamoja na waamini wenzao, ‘wanamtumikia [Yehova] kwa furaha.’ (Zab. 100:2) Walakini tuchunguze kwa ndani zaidi na tujifunze sababu gani Wakristo wa kweli wanafurahia amani ya kweli ya akili na moyo katika ulimwengu huu wenye msukosuko.