“Amani ya Mungu Inayoshinda Mawazo Yote”
“Amani ya Mungu inayoshinda mawazo yote italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kupitia kwa Kristo Yesu.”—Flp. 4:7, NW.
1. Sababu gani mtume Paulo alijua kwamba watu watawa hawana sababu ya kuwa na mahangaiko yasiyofaa?
MTUME Mkristo Paulo alijua kutokana na yaliyompata kwamba watawa hawana sababu ya kuwa na mahangaiko yasiyofaa, kwa maana Yehova yuko pamoja nao. Paulo alikuwa amefungwa, amepigwa, amepigwa mawe, na mara nyingi akakaribia kufa, naye alikuwa amepatwa na hatari nyingi, hata kati ya ndugu za uongo. Walakini Mungu hakumwacha wakati wo wote. Wakati wote mtume huyo alimwendea Baba yake wa kimbinguni katika sala ya bidii, akitupa mahangaiko juu yake na bila kukatishwa tamaa wakati wo wote.—2 Kor. 4:7-9; 11:23-27.
2. Matokeo yangekuwa nini kama Wakristo wengine watafuata shauri la Paulo lililoandikwa katika Wafilipi sura ya nne, mstari wa sita?
2 Kwa hiyo Paulo akiwa na uhakika kamili aliwasihi Wakristo wenzake wasihangaikie cho chote, bali wamjulishe Mungu maombi yao, wakimpelekea Yeye kila kitu katika sala na kusihi pamoja na kutoa shukrani. Matokeo ya kufanya hivyo yatakuwa nini? Mtume huyo aliendelea kusema hivi: “Na amani ya Mungu inayoshinda mawazo yote italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kupitia kwa Kristo Yesu.”—Flp. 4:6, 7, NW.
Amani “Inayoshinda Mawazo Yote”
3. (a) “Amani ya Mungu” ni nini? (b) Tukiwa na amani inayotolewa na Mungu, sababu gani hatuna sababu ya kushindwa na mahangaiko?
3 “Amani ya Mungu” ni utulivu unaofurahiwa na mashahidi wa Yehova waliojiweka wakf hata wanapokuwa ndani ya hali ngumu sana. Inatokana na uhusiano wa kibinafsi wa karibu pamoja na baba yetu wa mbinguni. Tukiwa na amani hiyo inayotoka kwa Yehova, twairuhusu roho ya Mungu ituchochee nasi twafuata uongozi wake. Kwa kweli, twaomba tupewe roho hiyo, na tunda lake la amani. (Luka 11:13; Gal. 5:22, 23; Efe. 4:30) Hivyo, hatuna sababu ya kushindwa na mahangaiko, maana twajua kwamba hakuna cho chote kinachoweza kutokea tusiweze kuangaliwa na Mungu. (Linganisha Matendo 11:26.) Hakika, Yehova hufanya watumishi wake ‘wakae katika usalama.’—Zab, 4:8, NW.
4, 5. (a) Wakilinganishwa na Mashahidi wa Yehova wengine wana amani ya namna gani? (b) “Amani ya Mungu” inatofautianaje na amani yo yote wanayoweza kuwa nayo wale wasiomtumikia Yehova kwa uaminifu?
4 Wakilinganishwa na Mashahidi wa Yehova, huenda watu wengi wakawa na elimu zaidi ya kidunia au uwezo zaidi katika mambo fulani ya kibinadamu. Bila shaka, wanakuwa na matatizo, walakini wana hakika kwamba wataweza kupata masuluhisho yanayofaa. Kwa hiyo, wanajiona salama sana, wasihangaikie wakati wao ujao. Wanaonekana kuwa na amani wakifurahia utulivu wa kadiri. Hata Maandiko hutaja “amani ya wasio haki”—Zab. 73:3.
5 Hata hivyo, “amani ya Mungu,” ni tofauti kabisa. Msingi wake si mtu kuwa na hakika juu yake mwenyewe na kuwa na maoni kwamba sikuzote mawazo ya wanadamu yatafaulu. Paulo alisema kwamba amani hiyo inayotolewa na Mungu ‘inashinda mawazo yote’ au ‘inapita kuwaza kote.’ Imeitwa “amani ile ya Mungu, ambayo ni kubwa zaidi ya tunavyoweza kufahamu.” (Flp. 4:7, New World Translation of the Holy Scriptures; The New American Standard Bible: New Testament; The Jerusalem Bible) Ndiyo, wale wanaomtumikia Yehova kwa uaminifu wana utulivu ambao wanadamu wengine hawana wala hawaufahamu.
6. (a) Sana sana inakuwa wazi wakati gani kwamba tuna “amani ya Mungu”? (b) Wakati tunapomngojea Yehova atende juu ya jambo ambalo tumemwomba, je! tunakuwa na msaada wo wote? (c) Je! inatia nguvu kiroho ‘kumtupia Yehova mizigo yetu,’ nawe unajibu hivyo kwa sababu gani?
6 Sana sana inaonekana wazi wale waliojiweka wakf kwa Yehova wana “amani ya Mungu” kweli kweli wakati mambo yanapotokea yanayokuwa na matokeo makubwa sana kwao lakini wasiyoweza kuzuia. Kwa kusema kwa njia ya kibinadamu wanakuwa hawawezi kushindana na mahangaiko hayo. Je! nyakati nyingine tunajipata katika hali kama hizo? Basi inafaa kama nini tuombe kwa bidii, tukiomba mambo kwa kuyataja hasa na kutoa maombi ya waziwazi ya kutaka msaada wa kimungu au uongozi! (Linganisha Waamuzi 6:36-40.) Baada ya hiyo, twapaswa kumngojea Yehova atende. Wakati huo wa kungojea, iwapo tuna “amani ya Mungu,” twaweza kuona msaada wa roho takatifu ya Yehova na kuendelea kuwa watulivu, tukisubiri kuona namna Aliye Juu Zaidi atakavyotatua tatizo hilo. Hakuna upumbavu kuwa na maoni hayo, maana mtunga zaburi Daudi alisema hivi: “Mtupie Yehova mwenyewe mzigo wako, naye atakutegemeza. Hataruhusu kamwe mwenye haki atikisike.” (Zab. 55:22, NW) Pamoja na hayo, wakati tatizo hilo linapokwisha na jaribu hilo kupita, tutajua kwamba “Mungu atoaye amani” amejibu sala zetu.—Rum. 15:33, NW.
Hulinda Mioyo na Nguvu za Akili
7. (a) Katika Maandiko, “moyo” mara nyingi unamaanisha nini? (b) Tukiwa na “amani ya Mungu,” sababu gani ‘hatutakasirika kwa sababu ya watenda mabaya’?
7 Paulo alisema kwamba “amani ya Mungu” ‘italinda mioyo yetu na nguvu za akili.’ (Flp. 4:7, NW) Tafsiri moja ya Biblia huita amani hiyo “ngome ya kulinda mioyo yenu na akili zenu.” (Weymouth) Katika Maandiko, mara nyingi “moyo” humaanisha kikao cha shauku na nia. (Kut. 35:21, 26, 29; Zab. 119:11) Tukipatwa na mahangaiko mabaya, shauku na nia zetu zaweza kuharibiwa nasi twaweza kutenda kwa njia isiyosawazika au isiyofaa. Kwa mfano, huenda ‘tukakasirika kwa sababu ya watenda mabaya,’ hivyo kupoteza utulivu wote. Lakini jambo hilo halitatokea tukiwa na “amani ya Mungu,” maana ndipo tutakapojua kwamba Yehova huona mambo yote naye atatengeneza mambo kwa wakati wake. (Zab. 37:1-11) Kwa hiyo mioyo yetu itaendelea kuwa na utulivu nayo haitatusukuma tutende bila kiasi. Jambo hilo latufaa katika maono ya ndani, kiroho na hata kimwili, maana “moyo mtulivu ni uzima wa mwili.”—Mit. 14:30, NW.
8. (a) Katika Wafilipi 4:7, tofauti kati ya “mioyo” na “nguvu za akili” ni nini? (b) Tukiwa na “amani ya Mungu,” sababu gani haielekei tutakosa usawa wa akili? (c) Je! cho chote kinachoruhusiwa na Baba yetu wa kimbinguni kitatuumiza milele?
8 “Nguvu za akili” si kitu kimoja na “mioyo,” ingawa zinatenda pamoja. Akili inafikiria habari, nao moyo unamchochea mtu. Kwa hiyo ili kuhakikisha kwamba tunafuata mwendo unaofaa, lazima tuwe na maarifa ya Neno la Mungu nasi lazima tumtegemee kwa sala. Iwapo akili zetu zinataabishwa—iwapo tungekuwa na mahangaiko makubwa—tusingeweza kufanya maamuzi yanayofaa. Hata huenda tukakosa usawa wa akili. Hata hivyo, hiyo haitaelekea kutupata tukiwa na “amani ya Mungu,” kwa sababu wakati huo mioyo yetu inaongozwa nazo akili zetu zinakuwa na utulivu. Tunaamini kweli kweli kwamba ‘mkono wa Yehova u pamoja nasi’ na kwamba hakuna cho chote ambacho Baba yetu wa kimbinguni anaruhusu kitatuumiza milele. (Mt. 10:28; Matendo 11:21) Mahali pa kuhangaika na kuingiliwa na mawazo mengi yenye kusumbua, twamtumaini Yehova kweli kweli, na hivyo “nguvu zetu za akili” zinalindwa. Namna gani? “Kupitia kwa Kristo Yesu,” ambaye kupitia kwake uhusiano wa kibinafsi wa karibu pamoja na Baba wa kimbinguni umewezekana.—Gal. 1: 3-5.
9. Ingawa Paulo alikuwa na “amani ya Mungu,” je! alikuwa bila mahangaiko ya moyoni kabisa?
9 Bila shaka, Paulo mwenyewe alijua kwamba Wakristo hawawezi kuwa bila mahangaiko ya moyoni kabisa. Yeye alikubali kwamba kushindwa kwa Wayahudi wenzake kukubali “habari njema” kulimpa “huzuni nyingi na maumivu yasiyokoma moyoni.” Hata hivyo mtume huyo hakushindwa na mahangaiko naye alitosheka kuachilia mambo yawe na Mungu, anayetenda kwa haki katika kuwachagua wale ambao Yeye atawaonyesha rehema. (Rum. 9:1-18) Hivyo, yajapokuwa maono ya moyoni yenye nguvu, Paulo aliruhusu “amani ya Mungu” ilinde moyo na nguvu zake za akili.
10. Basi, amani inayotolewa na Mungu italindaje mioyo na nguvu za akili zetu?
10 Kama Paulo, ambaye bila shaka alihangaikia sana, twaweza kuwa na “amani ya Mungu”—utulivu ule wa ndani unaoletwa na uhusiano wenye thamani pamoja na Yehova. Kweli kweli inaweza kulinda mioyo na nguvu zetu za akili zisihangaikie sana mahitaji yetu. Twaweza kuwa na hakika, kabisa kwamba Yehova huwaangalia watumishi wake naye hujibu sala zao. Mahali pa kuwa katika msukosuko wa wakati wote, mioyo na akili zetu zitakuwa na utulivu kwa sababu tunamtumaini kabisa Baba yetu wa kimbinguni.—Zab. 33:20-22.
Mambo ya Lazima Maishani Yamehakikishwa
11. Tukiwa na “amani ya Mungu,” sababu gani tusihangaike isivyofaa juu ya mambo ya lazima ya maisha?
11 Iwapo kweli kweli tuna “amani ya Mungu” na tukiwa na hakika kwamba yeye ndiye “Msikiaji wa sala,” tutaweza kushindana na mahangaiko. (Zab. 65:2, NW) Sikuzote tutaona tuna msaada wa kimungu, na katika hilo kuna amani nyingi ya moyo na akili. Kwa mfano, hatutahangaikia isivyofaa mambo ya lazima maishani. Yesu aliwaambia wafuasi wake: “Acheni kuhangaikia nafsi [au, “uzima”] kwamba mtakula nini au juu ya miili yenu kwamba mtavaa nini.” Sababu gani tusihangaike hivyo? Kwa sababu Yehova, anayetoa vitu vya kutosha kwa ndege na maua, hakika anaweza naye atalisha na kuvisha watumishi wake waaminifu. “Basi,” akasema Yesu, “acheni kutafuta mtakachokula na mtakachokunywa, na acheni kuhangaika . . . Hata hivyo, tafuteni wakati wote ufalme [wa Mungu], nayo mambo hayo mtaongezewa.” (Luka 12:22-31, NW) Hakika, tukiweka faida za kiroho kwanza maishani, twaweza kuwa na hakika kwamba Baba yetu wa kimbinguni atatuangalia.
12. Ni mfano gani wa Kimaandiko unaoonyesha sababu gani hata wale waliojiweka wakf kwa Yehova wanapaswa kuepuka kukazia sana mali?
12 Hata watu mmoja mmoja waliojitoa kwa Yehova wanapaswa kuepuka kukazia sana mali. Kwa mfano, kwa sababu ardhi isingeweza kuwaruzuku pamoja na kumaliza ugomvi kati ya wachungaji wao, Abrahamu alimpa mpwa wake Loti nafasi ya pale alipopendelea kukaa. Loti alichagua ardhi iliyo bora zaidi, lakini hiyo ilimaanisha kuishi katikati ya watenda mabaya. Muda si muda, alitekwa nyara ikawa lazima aokolewe. (Mwa. 13:1–14:16) Baadaye, Loti aliona lazima ya kuachana na mali yake ili maisha yake yaponywe wakati Yehova alipoharibu Sodoma. Baadaye zaidi, Loti aliona lazima ya kuondoka katika mji wa Soari na kukaa katika pango. (Mwa. 19:1-26, 30-38) Ingawa anaitwa “Loti mwenye haki,” inaonekana alijifunza kwa kupatwa na magumu, upumbavu wa mtu mtawa kukazia sana faida za kimwili. (2 Pet. 2:7, 8, NW) Ni vema zaidi kama nini kuomba uongozi fulani na sikuzote kuweka faida za kiroho kwanza maishani!
13. Sababu gani Wakristo hawapaswi kuhangaikia mambo ya lazima maishani?
13 Tukifanya mambo ya kiroho yawe ya maana zaidi maishani mwetu, hiyo itatuletea amani ya moyo na akili. Bila shaka, twaweza kuwa na hakika kwamba Yeye ambaye dhahabu na fedha yote ni yake anaweza kabisa kuwapa watumishi wake mambo ya lazima maishani. (Hag. 2:8) Bila shaka, inafaa kumwomba Mungu ‘atupe leo riziki yetu,’ na inafaa kufanya kazi kwa bidii ili kuangalia mahitaji ya lazima. (Mit. 6:6-11; 31:10, 13-24; Mt. 6:11) Lakini ‘kwa kuwa hatukuleta cho chote ulimwenguni nasi hatuwezi kuondoa cho chote, twapaswa kuridhika na chakula na mavazi.’ (1 Tim. 6:6-12, NW) Sababu gani kuhangaika? Mtunga zaburi alisema hivi kwa kufaa: “Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, lakini sijamwona mwenye haki ameachwa, wala mzao wake akiomba chakula.”—Zab. 37:25.
Njia Inayoongoza kwenye Kufanikiwa kwa Kweli
14. Sababu gani haifai kwetu, tukiwa mashahidi Wakristo, kukazia sana matendo ya wanadamu na kufanikiwa kunakoshirikishwa nayo?
14 Ni jambo la kawaida kwa watu wa ulimwengu kujiletea mahangaiko kwa kukazia sana matendo ya kibinadamu. Bila shaka, Biblia inatia moyo juhudi na kusitawisha ufundi katika kazi ya mtu. (Mit. 22:29) Lakini kutamani sana kufanya mambo kunakopofusha na mahangaiko mengi juu ya kufanikiwa hayapatani na “amani ya Mungu.” Kwa kweli, kutafuta kutawala wengine kwaweza kumfanya mtu mwenye tamaa hiyo atumie njia mbaya, pengine kuharibu jitihada za wafanya kazi wenzake na kufuatia mwendo mpotovu unaoleta kukosa kibali ya Mungu. (Mit. 3:32; 2 Kor. 4:1, 2) Kweli, wanaotamani sana kufanya mambo wanaweza kushangiliwa na wanadamu, kama vile viongozi wa kidini wa karne 19 zilizopita walivyotoa zawadi, wakaomba na kufunga kula katika njia kama hizo ili wasifiwe. Walakini Yesu Kristo alilaani matendo yao na kusema kwamba wanafiki hao waliokuwa wakijifikiria walikuwa ‘wakipata zawadi yao kamili.’ (Mt. 6:1-18, NW) Ni upumbavu kama nini kwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova kuishi pamoja na mahangaiko ya kujifanyia kwa kujaribu kuwa ‘mkuu,’ na kisha aone kwamba baraka za milele zimepotezwa kwa njia hiyo!—Linganisha Yeremia 45:5.
15. Kwa habari ya kufanikiwa, mtu mtawa anaweza kujifunza nini kutokana na Mhubiri 9:11 na 10:5-7?
15 Kwa mtu anayefurahia “amani ya Mungu,” kweli kweli, njia inayoongoza kwenye kufanikiwa kwa kweli haielekezi kwenye njia mbaya na kujitahidi bure. Kutokana na Maandiko amejifunza kwamba ujamii wa kisasa, ukiwa umejaa wanadamu wasiokamilika na wenye dhambi, “si wenye mbio washindao katika michezo, wala si walio hodari washindao vitani, wala si wenye hekima wapatao chakula, wala si watu wa ufahamu wapatao mali, wala wenye ustadi wapatao upendeleo.” (Mhu. 9:11) Hakika, “upumbavu huwekwa mahali pa juu sana,” na mtu anaweza kuona “watumwa wamepanda farasi, na wakuu wakienda kwa miguu.” (Mhu. 10:5-7) Ndiyo, wakuu au watu wenye cheo huenda wasipewe heshima wanayostahili, hali watumwa—watu wanaostahili kidogo zaidi—huenda ‘wakapanda farasi’ kama watu wenye cheo.
16. Kufanikiwa pamoja na matendo ya kimungu yanategemea nini?
16 Je! umekwisha kuwekwa kando, usifurahie kufanikiwa ambako ulitamani wakati mmoja? Sababu gani uhangaikie hilo? “Amani ya Mungu” na ikae moyoni mwako, na upate utulivu wenye kufariji inaoleta. Endelea kufanya mapenzi ya kimungu nawe umtegemee Baba yako wa kimbinguni abariki jitihada zako katika utumishi wake. Hilo ndilo jambo kubwa maishani. Kufanikiwa kwa kimungu na matendo yanategemea makusudi ya kiroho na maoni pia. Mtunga zaburi alisema hivi kwa kufaa: “Mwenye furaha ni mtu ambaye hakutembea katika shauri la waovu . . . Bali kupendezwa kwake ku katika sheria ya Yehova, na katika sheria yake husoma kwa sauti ndogo mchana na usiku. Naye atakuwa kama mti uliopandwa kandokando ya vijito vya maji, uzaao matunda yake kwa majira yake, wala jani lake halinyauki; na kila alitendalo litafanikiwa.”—Zab. 1:1-3, NW.
17. (a) Ili tufurahie kufanikiwa sana, twapaswa kufanya nini? (b) Unaweza kufanya nini ili usaidie wengine wafurahie “amani ya Mungu inayoshinda mawazo yote”?
17 Hatuwezi kufurahia kufanikiwa sana maishani kuliko kuingia na kuendeleza uhusiano wa kirafiki pamoja na Yehova Mungu. Tamaa nyingi ya kumpendeza itatusukuma tumletee heshima kwa maneno yetu ya utawa na matendo pia, kufanyia wanadamu wenzetu mema na kushiriki pamoja nao “habari njema za utukufu za Mungu mwenye furaha.” (1 Tim. 1:11, NW) Furaha yetu itakuwa nyingi iwapo, tukiwa na baraka ya Baba yetu wa kimbinguni, twaweza kuwasaidia wengine wajifunze juu ya makusudi yake ya ajabu na vilevile kuwa na uhusiano ulio wakf pamoja naye. Kisha, kama sisi, watajifunza kushindana na mahangaiko ya maisha. Wao, pia, watafurahia “amani ya Mungu inayoshinda mawazo yote.”
—Kutoka The Watchtower Nov. 1, 1980.
[Picha katika ukurasa wa 19]
Hata katikati ya hali ngumu zaidi Mkristo anaweza kufurahia “amani ya Mungu”