Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 4/15 kur. 13-17
  • “Msihangaikie Cho Chote”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Msihangaikie Cho Chote”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Pasipo Mahangaiko Kabisa?
  • Baba Mwenye Upendo wa Matendo Makuu
  • ‘Mjulisheni Mungu Maombi Yenu’
  • “Pamoja na Shukrani”
  • “Amani ya Mungu Inayoshinda Mawazo Yote”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • ‘Tumia Kila Namna ya Sala na Kusihi’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Mtwikeni Yehova Hangaiko Lenu Lote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Mtupie Yehova Mahangaiko Yako Yote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 4/15 kur. 13-17

“Msihangaikie Cho Chote”

“Msihangaikie cho chote, bali katika kila jambo kwa sala na kusihi pamoja na shukrani, Mungu na ajulishwe maombi yenu.”—Flp. 4:6, NW.

1. Twaweza kusema Yehova ni “Mungu wa amani” kwa sababu gani za Kimaandiko?

YEHOVA ndiye “Mungu wa amani.” (Flp. 4: 9) Hapatwi na mahangaiko yenye kutaabisha, wasiwasi wa akilini wala hofu. Hakuna cho chote—hata vitendo viovu vya waovu—kinachoweza kumwondolea Mungu utulivu wala kumfanya akose usawa. Sikuzote sifa zake ni zenye kusawazika kabisa. Kwa mfano, akitenda kwa upendo, Yehova “huwaangazia jua lake waovu na wema.” (Mt. 5:44, 45; 1 Yohana 4:8) Hapotoi haki ya hukumu kamwe. (Mwa. 18:25) Hekima ya Mungu isiyolinganika inamwezesha kuona ‘mwisho tangu mwanzo’ na kukabiliana na tukio lo lote. Vilevile, uwezo wake usio na kikomo, ambao hautumiwi vibaya kamwe, sikuzote unatokeza kutimizwa kwa mapenzi yake ya haki.—Ayubu 12:13; Isa. 40:26; 46: 9, 10.

2. Yehova anapaswa kuonwaje na waabudu wake?

2 Huyu “Mungu wa amani” asiyelinganika anapaswa kuonwaje na wale walio katika jamaa ya ulimwengu wote ya waabudu wake? (Linganisha Waefeso 3:14, 15.) Kwa kuwa Baba yao wa kimbinguni anaweza kukabiliana na hali yo yote, wasifaji wa Yehova wana kila sababu ya kuwa watulivu. Wanaweza kujiona kuwa na usalama wa kweli katika uhusiano wao pamoja naye.

Pasipo Mahangaiko Kabisa?

3. Sababu gani haishangazi kwamba watumishi wa Yehova wanapaswa kupata mahangaiko fulani?

3 Bila shaka, hiyo haimaanishi kwamba ‘wanaompenda Yehova’ wanakuwa bila mahangaiko kabisa. (Zab. 97:10, NW) Wana hali ya kutokamilika waliyorithi kutoka kwa Adamu nao wana lazima ya kuishi kati ya wazao wengine wasiokamilika wa mwanamume huyo wa kwanza. (1 Fal. 8:46; Rum. 5:12) ‘Siku za maisha yao’ ni zenye taabu, nao wanadamu wote wasiokamilika wana “siku chache nazo zimejawa na kufadhaika.” (Ayubu 14:1, NW; Zab. 90:10) Kwa hiyo si jambo la kushangaza kwamba watumishi wa Yehova wanalazimika kupatwa na mahangaiko fulani.

4. Ni maandiko gani yanayoonyesha sababu gani watu wanaomwogopa Mungu hawawezi kuwa bila mahangaiko kabisa?

4 Kwa mfano, kwaweza kuwa taabu za maono ya ndani, kama vile wake Wahiti wa Esau ‘walivyojaza uchungu roho’ za wazazi wake wenye kumwogopa Mungu, Isaka na Rebeka. (Mwa. 26:34, 35) Maradhi yanatokeza mahangaiko kwa watumishi wa Mungu leo, kama ilivyokuwa katika maisha ya Wakristo waaminifu Timotheo na Trofimo. (1 Tim. 5:23; 2 Tim. 4:20) Kama vile “Loti mwenye haki,” wasifaji wa kisasa wa Yehova wanataabishwa na mwendo wa uasherati wa watu wenye kumkaidi Mungu. (2 Pet. 2:7, NW) Nyakati nyingine, watu mmoja mmoja waliojitoa kwa Yehova wanalazimika kujiruzuku kwa chakula kidogo, bila shaka hiyo ikiwa inahangaisha sana. (Flp. 4:12) Na kama vile mtume Paulo, wanaume wengi Wakristo wa nyakati zetu wanahangaikia waamini wenzao. (2 Kor. 11:28) Kuongezea hayo kuna taabu mbalimbali zinazowapata watu binafsi wanaomwogopa Mungu na inaonekana wazi kwamba hawawezi kuwa pasipo mahangaiko kabisa.

5. (a) Watu wa Yehova wana msaada gani wa pekee wa kushindana na mahangaiko? (b) Kama inavyotumiwa katika Maandiko, “amani” inamaanisha nini?

5 Hata hivyo, watumishi wa Yehova wana msaada wa kimungu wa kushindana na mahangaiko yao yote—msaada wenye thamani usiofurahiwa na mtu ye yote asiye wa kiroho. (Linganisha Yuda 17-21.) Si kwamba Yehova ni “Mungu wa amani” tu, bali pia, kwa furaha yeye ni “Mungu atoaye amani.” (Rum. 15:33, NW) Katika Maandiko, “amani” inamaanisha mengi zaidi ya kuwa bila ugomvi. Kati ya mambo mengineyo, inaonyesha ‘hali njema, furaha, fanaka na wema wa kila namna.’ (Mwa. 41:16, Authorized Version; Marko 5:34; Luka 1:79) Bila shaka, kuwa na amani hiyo yenye kutia ndani mambo yote kwapaswa kuzuia au kupunguza mahangaiko ya maisha.

6. Twapaswa kufanya nini iwapo twataka kupata na kuendeleza amani inayotolewa na Mungu?

6 Lakini ili kupata na kuendeleza amani hii inayotolewa na Mungu, lazima mtu awe na upendo mwingi kwa Yehova na Neno lake. Hiyo inatia ndani kumpenda Mungu, kutii amri zake, kuamini jina la Mwanawe Yesu Kristo, na kuwapenda wengine. (1 Yohana 3:19-24; 5:2-4) Bila shaka, ili kutii amri za Mungu twapaswa kuzijua. Hiyo inataka tujifunze Maandiko kila siku. (Yos. 1:8) Na, bila shaka, tunapotumia wakati zaidi tukiwa na Neno la Yehova, ‘tutalitamani’ zaidi. Hiyo, nayo, itatuletea amani zaidi ya moyo na akili.—1 Pet. 2: 1-3, NW.

Baba Mwenye Upendo wa Matendo Makuu

7. Maarifa yaliyoongezeka ya Neno la Mungu yanakuwa na matokeo gani juu ya uhusiano wetu pamoja naye, nalo jambo hilo linatuondoleaje mahangaiko?

7 Maarifa yetu yaliyoongezeka ya Neno la Mungu yatatuvuta karibu zaidi na Aliye Juu Zaidi, mradi tunamfikia kwa unyenyekevu kama wa mtoto na tamaa ya kutoka moyoni ya kupata “hekima itokayo juu.” (Yak. 3:17, 18) Tutavutiwa na uhakika wa kwamba Yehova ni “Mungu mwenye rehema na neema, asiye mwepesi wa hasira na mwingi wa fadhili za upendo na kweli.” (Kut. 34:6, NW) Tutajua kabisa kwamba yeye ni ‘mwema na yu tayari kusamehe.’ (Zab. 86:5) Tukiwa hatujakamilika na wenye dhambi, tutakosea katika njia yetu, walakini tunahakikishiwa hivi: “Kama ambavyo baba huonyesha wanawe rehema, Yehova amewaonyesha rehema wale wanaomwogopa. Maana yeye mwenyewe ajua vema tulivyoumbwa, akikumbuka kwamba sisi tu mavumbi.” (Zab. 103:13, 14, NW) Lo! hilo linaondoa mioyoni mwetu na akilini pia hangaiko ambalo kama sivyo lingetuponda! Nalo ni tendo la upendo lisiloweza kuwazwa na wanadamu kwamba Yehova alitoa mpango wa ukombozi, uliotolewa kupitia kwa Mwanawe mpendwa “ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16; 1 Tim 2:5, 6.

8, 9. (a) Ni maandiko gani yanayotuambia namna Yehova alivyo Mfanya “matendo makuu”? (b) Sababu gani unaweza kusema kwamba vitendo vya Mungu vya wakati uliopita vyathibitisha kwamba watu wake wanaweza kutazamia msaada wake katika kushindana na mahangaiko ya maisha?

8 Vilevile Baba yetu wa kimbinguni ndiye Mfanyizaji wa “matendo makuu,’ (Zab. 106:1, 2; 145:4, 11, 12) Akiomba kibali ya Mungu, Musa aliweza kusema hivi: “Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, wewe mwenyewe umefanya mtumishi wako aanze kuona ukuu na mkono wako wenye nguvu, maana ni nani aliye mungu mbinguni au duniani anayefanya vitendo kama vyako na matendo makuu kama yako?” (Kum. 3: 23, 24, NW) Musa aliweza kukumbuka namna Yehova alivyofungua watu Wake toka utumwani Misri na kuwaongoza kupitia sakafu kavu ya Bahari ya Shamu. (Kut. 12:29-42 14:5-31) Vilevile, nabii huyo alikuwa ameona matendo ya Yehova katika kupatia Israeli ushindi juu ya Waamori, waliokuwa chini ya Wafalme Sihoni na Ogi. Pamoja na hayo, kwa kuwa Yehova alikuwa akipigania Waisraeli, Musa alikuwa na uhakika kwamba Mungu angepindua falme nyingine za maadui na kuwapa watu Wake nchi ya ahadi. (Kum. 3:1-22) Ndiyo, Mungu alifanya hivyo, kwa kuwa yeye ni Mtimiza Ahadi. (Yos. 23:1-5) Basi, “wampendao Yehova” wanapaswa kuonaje wanapofikiria kutegemeka kwa Mungu na matendo yake ya kuokoa? Je! kuna sababu ya kuwa na mahangaiko yenye kutaabisha kwa habari ya watu wake leo? Hata kidogo, maana Yehova ni mwaminifu, naye “ajua jinsi ya kuokoa watu wenye utawa.”—2 Pet. 2:5-9, NW.

9 Bila shaka, vitendo vya Mungu kwa ajili ya wale waliojitoa kwake kabisa havihusu tu matendo ya kuokoa. Hata hivyo, matendo hayo yanathibitisha kwamba “Yehova hatawaacha watu wake.” (Zab. 94:14, NW) Kwa hiyo twaweza kuwa na hakika kwamba yeye atawasaidia kushindana na mahangaiko ya maisha.

‘Mjulisheni Mungu Maombi Yenu’

10. Kulingana na maneno ya mtume Paulo katika Wafilipi 4:6. 7, twaweza kutiaje nguvu kifungo chetu pamoja na “Mungu wa amani”?

10 Funzo la kawaida la Neno la Mungu litavuta watu wanyofu wamkaribie Yehova. Vilevile kutafakari juu ya njia za upendo za Baba wa kimbinguni pamoja na matendo yake makuu kwa ajili ya wale wanaomtumikia kwa uaminifu. Hata hivyo kuna njia nyingine ya kutia nguvu kifungo chetu pamoja na “Mungu wa amani.” Mtume Mkristo Paulo alikionyesha wazi alipowasihi hivi waamini wenzake: “Msihangaikie cho chote, bali katika kila jambo kwa sala na kusihi pamoja na shukrani, Mungu na ajulishwe maombi yenu.” Hiyo inatokeza utulivu unaotolewa na Mungu usiowazika kwa wanadamu.—Flp. 4:6, 7, NW.

11. Unaweza kutoa mifano gani ya Biblia kuthibitisha kwamba Yehova ni “Msikiaji wa sala”?

11 Muda mrefu kabla Paulo hajaandika maneno hayo, Yehova alikuwa amethibitisha kuwa ni mwenye upendo, “Msikiaji wa sala” mwenye kutegemeka. (Zab. 65:2, NW) Waabudu wake wangeweza kumtupia mahangaiko yao mbalimbali, wakiwa na uhakika kwamba maombi yao yatasikiwa. Kuonyesha jambo hilo kwa mfano: Sala ya mtumishi wa Abrahamu, Eliezeri ilijibiwa alipoongozwa apate mke wa Isaka, mwana wa bwana yake. (Mwa. 15:2; 24:10-27, 62-67) Hana aliye tasa (asiyeweza kuchukua mimba) ‘alisali sana’ pamoja na machozi naye akapewa mwana, Samweli, ambaye kwa kushukuru ‘akampa Yehova wakati wote atakaokuwa hai.’ (1 Sam. 1:4-28) Kwa kulia sana, Mfalme Hezekia aliyekuwa mgonjwa mahututi alimsihi Yehova naye akaponywa. (2 Fal. 20:1-11) Kwa siku nyingi Nehemia alifunga kula na kusali—na kwa dakika ya hatari alimwomba “Mungu wa mbinguni” akiwa amenyamaza—matokeo ya furaha yakawa kwamba alipewa mamlaka ya kifalme akajenge upya Yerusalemu ulioharibiwa. (Neh. 1:1-2: 8) Huko hekaluni Ana mwaminifu alitoa utumishi mtakatifu usiku na mchana “kwa kufunga na kuomba” naye alithawabishwa kwa kuwapo wakati mtoto Yesu alipoletwa hapo. (Luka 2: 36-38) Usiku wa mwisho wa kifo chake cha kidunia, Kristo alimsihi Yehova naye akatiwa nguvu na Babaye wa kimbinguni apate kunywea “kikombe” kilichokusudiwa kwa ajili yake.—Mt. 26:36-47.

12. Sababu gani watumishi wa Yehova wanaweza kusali kwa uhakika kwake wanapopata mahangaiko?

12 Vilevile, fikiria, sala nyinginezo nyingi zilizoandikwa katika Maandiko—zile za kuungama makosa, kusifu, kutoa shukrani. Kisha uulize hivi: Je! watumishi wa kisasa wa Yehova hawapaswi kumgeukia wawe ni wenye furaha, shukrani, taabu au mahangaiko? Hakika wanapaswa, wakiwa na hakika kwamba Baba yao wa kimbinguni husikia kusihi na maneno yao ya unyenyekevu na unyofu.

13. Sababu gani mtume Paulo angeweza kusihi Wakristo wenzake wasihangaikie “cho chote”?

13 Muda mfupi tu kabla Paulo hajashauri Wakristo wamjulishe Mungu maombi yao, mtume huyo alisihi hivi: “Msihangaikie cho chote.” (Flp. 4:6, NW) Katika kufanya hivyo alikuwa akirudia shauri la Yesu, aliyesema hivi: “Acheni kuhangaikia nafsi zenu” na “msitangulie kuhangaikia mtakayosema.” (Mt. 6:25, NW; Marko 13:11, NW) Mtume huyo alijua kwamba Baba wa kimbinguni angeangalia waabudu Wake na kwamba wangepata msaada kutoka kwa roho takatifu ya Yehova katika kila kitu chenye kukubaliwa na Mungu.

14. Kwa habari ya sala, “maombi” ni nini?

14 Tukijua kwamba Yehova ndiye “Msikiaji wa sala,” sisi tunaofuata maisha ya utawa leo twaweza kutii shauri la Paulo tukiwa na uhakika: “Bali katika kila jambo kwa sala na kusihi pamoja na shukrani, Mungu na ajulishwe maombi yenu.” Mara nyingi sala zetu zinakuwa maombi.” Yaani, zinatia ndani kuomba kwa kuyataja hasa mambo unayoomba au kutoa maombi ya kuyasema waziwazi mambo yenyewe. Eliezeri na Hana walikuwa kati ya watu waaminifu ambao maombi yao yalisikiwa na Mungu kwa sababu walitaja waziwazi walichoomba. Naye Yesu alionyesha kwamba inafaa kutaja kitu chenyewe unachomwomba Mungu. Kwa mfano, Kristo aliwaambia wanafunzi wake wamwombe Baba: “Utupe siku kwa siku riziki yetu.”—Luka 11:2, 3.

15. (a) Kwa habari ya sala, “kusihi” kunamaanisha nini? (b) Waebrania 5:7 linatufundisha nini juu ya sala za Yesu Kristo?

15 Kuhangaika sana kunaweza kutokea kwa ajili ya mambo mengi, na nyakati nyingine hiyo inaweza kuhitaji “sala za kusihi.” Neno hilo linakazia kuomba kwa bidii, kwa uhitaji na unyenyekevu. Kwa hiyo si kuzungumza na Mungu kwa njia ya kuabudu katika sala ya kawaida. Maombi ya bidii na kusihi yanakuwa ya lazima nyakati nyingine. “Katika siku za mwili wake,” twasoma, “Kristo alitoa sala za kusihi na maombi pia kwa Yule aliyekuwa na uwezo wa kumwokoa katika mauti, kwa kulia sana na machozi, naye alisikiwa kwa kibali kwa sababu ya woga wake kwa kimungu.” (Ebr. 5:7, NW) Akikubali mahitaji ya kweli, Yesu aliomba sana kutoka moyoni, akimsihi Babaye kwa bidii. Pamoja na hayo, Kristo alimwomba Yehova, akitaja hasa mambo yenyewe aliyotaka.—Yohana 17:9, 10, 15-21.

16. Kwaweza kuwa na matokeo gani kwa Mkristo sala zake zinapojibiwa?

16 Maombi ya Mkristo ya kutaja waziwazi anachotaka yakitimizwa, nako kuomba kwake kwa bidii kukijibiwa, anajua kwamba Yehova yu pamoja naye. Kuona msaada huo wa kimungu kwaweza kutokeza itikio kama lile la Ayubu, ambaye alitamka hivi baada ya kuvumilia jaribu: “Nilikuwa nimesikia habari zako [Yehova Mungu], kwa kusikia kwa masikio; bali sasa jicho langu linakuona.” (Ayubu 42:5) Kama Ayubu, kwa jicho la ufahamu, imani na kuthamini twaweza kutazama matendo ya Yehova yaliyo pamoja nasi tuweze ‘kumwona’ kama tusivyomwona hapo mbeleni. Ni amani ya moyo na akili kama nini inayotokana na uhusiano huo wa karibu na Baba yetu wa kimbinguni!

“Pamoja na Shukrani”

17. Sababu gani twapaswa kumshukuru Mungu katika sala?

17 Paulo alisihi waamini wenzake wamjulishe Mungu maombi yao kwa sala na kusihi “pamoja na shukrani,” (Flp. 4:6, NW) Hakika, kuna sababu nyingi za kumshukuru na kumsifu Aliye Juu Zaidi. (1 Nya. 29:10-13) Yesu aliwekea wafuasi wake mfano alipotoa shukrani kwa ajili ya chakula na kwa ajili ya mkate na divai iliyokuwa mfano iliyotumiwa katika Chakula cha Bwana cha Jioni. (Mt. 15:36; 26:26, 27; Luka 22:19, 20) Zaidi ya kumtolea Mungu shukrani kama hizo, twapaswa “kumshukuru Yehova” kwa ajili ya “matendo yake ya ajabu kwa wana wa watu,” kwa ajili ya ‘maamuzi yake ya haki ya hukumu,’ na kwa ajili ya mengi zaidi. (Zab. 33:2-5, NW; 92:1, 2, NW; 100:4, 5; 107:1, 8, 15, 21, 31, NW; 119:62, NW) Inafaa kama nini kumshukuru Mungu kwa ajili ya Neno lake la kweli lisilolinganika! Nasi twapaswa kuwa wenye shukrani kama nini kwa ajili ya dhabihu ya Mwanawe ambayo imefanya iwezekane kupatanishwa na Yehova!—Rum. 5:6-11.

18. Iwapo tunafanya mapenzi ya Mungu kwa uaminifu kwa nini hatuna sababu ya kushindwa na mahangaiko?

18 “Wanaompenda Yehova” wanaweza kumshukuru, pia, kwa sababu yeye anawajali kweli kweli. Mtume Petro aliandika hivi: “Jinyenyekezeni, basi, chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu, ili aweze kuwakweza kwa wakati wake; huku mkimtupia mahangaiko yenu yote; kwa sababu anawajali.” (1 Pet. 5:6, 7, NW) Hivyo Petro na Paulo waliwasihi waamini wenzao wasihangaikie cho chote bali wampe Yehova mahangaiko yao yote. Nalo shauri hilo linafaa kama nini! Hakuna kitu cho chote asichoweza kufanya au asichoweza kuongoza Aliye Juu Zaidi kwa ajili ya wale waliojitoa kwake kwa moyo wote. (Marko 10:27; 12:29, 30) Cho chote anachoruhusu Mungu, walio waaminifu wanaweza kuvumilia kwa sababu yeye huwapa ‘nguvu katika mambo yote,’ (Flp. 4:13; 1 Kor. 10:13) Akiwa na sababu nzuri, mtunga zaburi Daudi alisema hivi: “Umkabidhi [Yehova] njia yako, pia umtumaini, naye atafanya.” (Zab. 37:5) Ndiyo, kwa uaminifu fanya mapenzi ya Mungu na hakuna sababu ya kuwa na wasiwasi na kushindwa na mahangaiko. Mahali pake, kuna sababu nzuri ya kuwa na amani ya ndani, hata katikati ya dhiki na msukosuko. Walakini amani hiyo ni kubwa kadiri gani?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki