Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 5/15 kur. 8-13
  • Barabara Inayoongoza kwenye Afya Yafunguliwa na Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Barabara Inayoongoza kwenye Afya Yafunguliwa na Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mambo Aliyoona Mungu Kuhusu Unafiki wa Kidini
  • Wale Ambao Wamechukua Njia Inayoongoza Kwenye Kuponywa
  • Mahubiri ya Mlimani—“Ufungapo, Jipake Mafuta Kichwani”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Unafiki Wafichuliwa!
    Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
  • Je, Kufunga Ni Njia ya Kumkaribia Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Biblia Inasema Nini Kuhusu Kufunga?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 5/15 kur. 8-13

Barabara Inayoongoza kwenye Afya Yafunguliwa na Mungu

Kabla ya kujifunza makala hizi tatu zinazofuata msomaji atafanya vema akifahamiana kwanza na habari iliyo msingi wa makala hizo, yaani, unabii wa Isaya, sura za 58 na 59

Afya yako itatokea mara.”​—Isa. 58:8.

1. Kwa sababu gani wanadamu wanahitaji kuponywa katika hali yao ya afya kwa jumla?

JE! WANADAMU wote wanahitaji afya—kuponywa? Watu ambao hujipatia habari kwa njia zote za kisasa za kukusanya habari kutoka mbali na karibu hawatasita kujibu Ndiyo! Ulizo ni hili, Ni nani kati yetu sisi wanadamu anayeweza kuleta afya hiyo inayohitajika sana? Watu wenye fadhili wanaendelea kujaribu wakiwa na matumaini, lakini jitihada zao za unyofu zimeshindwa kuzuia hali ya afya ya wanadamu inayoendelea kuharibika kijamii, kiadili, kiuchumi, kinyumbani. Kilio cha kulalamika kutoka kwa wanadamu wenye kuugua chaendelea kuwa kikubwa zaidi na zaidi!

2, 3. (a) Ni nani aliye na sababu kubwa zaidi kuliko wanadamu wenyewe ya kulalamika juu ya kadiri ya wanadamu walivyoanguka? (b) Hali iliyoshuka ya wanadamu inaelezwaje katika Warumi 3:9-18?

2 Ikiwa sisi wanadamu wa kawaida tunaona sababu nyingi za kulalamika, je! Muumba mwenye nguvu zipitazo za wanadamu hatapata sababu hata zaidi ya kulalamika! Bila shaka yeye hakujiharibia sifa yake ya uwezo wa kuumba kwa kuanzisha kuumba kwa kibinadamu na kukuacha katika hali mbaya kama ile tuliyo nayo leo. Yeye anasema kweli kwamba kuingia kwa dhambi ndiko kulikosababisha hayo yote. Karne kumi na tisa zilizopita yeye alionyesha kadiri wanadamu walivyoanguka kutoka kwa ule ukamilifu wa kwanza kwa kumwongoza mmoja wa waandikaji wa vitabu vya Biblia aandike maneno haya ya maelezo:

3 “Ni nini basi? Tu bora kuliko wengine? La! hata kidogo. Kwa maana tumekwisha kuwashitaki Wayahudi na [Wagiriki] ya kwamba pia wamekuwa chini ya dhambi; kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Hakuna mwenye haki hata mmoja. Hakuna afahamuye: hakuna amtafutaye Mungu. Wote wamepotoka, wameoza wote pia; hakuna mtenda mema, la! hata mmoja. Koo lao ni kaburi wazi, kwa ndimi zao wametumia hila. Sumu ya fira i chini ya midomo yao. Vinywa vyao vimejaa laana na chungu. Miguu yao ina mbio kumwaga damu. Uharibifu na mashaka yamo njiani mwao. Wala njia ya amani hawakuijua. Kumcha Mungu hakupo machoni pao.”​—Rum. 3:9-18.

4. (a) Katika kuandika hayo, Paulo alikuwa akitumia maneno kutoka wapi? (b) Kwa hiyo, basi, leo twaona hali ya mambo ikiwaje, karne 19 baadaye?

4 Katika sehemu hiyo ya barua yake aliyoliandikia kundi la Kikristo katika Rumi wa kale, mtume Paulo alikuwa akitumia maneno kutoka katika Maandiko ya Kiebrania ambayo yote yaliandikwa chini ya uongozi wa roho ya Mungu zaidi ya miaka 450 kabla ya yeye kuandika barua yake wapata mwaka wa 56 hivi. Kwa mfano, Paulo alitumia maneno kutoka Isaya 59:7-20. Hiyo yaonyesha kwamba tayari hali ilikuwa mbaya sana huko nyuma katika wakati wake, wala si kwa habari ya wanadamu kwa jumla tu, lakini sana sana kwa habari ya wale waliodai kuwa watu wa Yehova Mungu, yaani, Wayahudi, au Waisraeli. Hivyo, basi, leo, zaidi ya karne 19 baada ya Paulo kuliandikia kundi la Kikristo mambo kama hayo katika mji mkuu wa milki, Rumi, inatupasa kutazamia hali ya kiadili na ya kidini ya ulimwengu kuwaje, na bila kusahau ile sehemu inayojulikana kama Jumuiya ya Wakristo? Yale tunayofunuliwa kwa wingi na magazeti yanayosema waziwazi yanashtua, ndiyo, yanaogopesha.

5, 6. (a) Kulingana na chanzo cha jina Jumuiya ya Wakristo, mataifa walio washiriki wa eneo lake wanapaswa kujiendeshaje? (b) Tunaposoma unabii wa Isaya ulioelekezwa kwa Israeli, inatupasa kukumbuka utimizo gani mkubwa zaidi?

5 Kulingana na chanzo cha jina lake, Jumuiya ya Wakristo yapaswa kuwa ikimwiga Kristo Yesu na kuishi kulingana na mafundisho yake. Mataifa ambayo ni washiriki wa jumuiya hiyo yapaswa kujua jinsi ya kufanya hivyo. Kati ya hayo yanayoitwa mataifa ya Kikristo, Biblia, na sana sana nakala za “Agano Jipya,” huenezwa kwa mamia ya mamilioni katika lugha zote zinazojulikana katika maeneo yao. Wengi wa wakazi wa maeneo hayo wanajua kusoma Maandiko hayo yaliyoongozwa kwa roho ili wajifunze namna ya kuwa Wakristo. Kwa kuwa Jumuiya ya Wakristo inajidai kuwa na uhusiano na Kristo na hudai kuwa kundi lake, kushindwa kufuata mfano wa Kristo huionyesha kuwa ya kinafiki. Hali yake ya kijamii, kiadili, kidini iko kama ile ya watu ambao wakati mmoja walikuwa ‘watu wateule’ wa Yehova Mungu katika siku za nabii Isaya miaka 800 kabla ya Ukristo kuonekana duniani.

6 Kwa kweli, hali yenye kusikitisha ya Jumuiya ya Wakristo inalingana na ile ya Israeli wa siku za Isaya, kwa kuwa inadai kuwa ndiyo iliyochukua mahali pa Israeli kama watu wateule wa Mungu. Kwa hiyo, tusomapo sura fulani za unabii wa Isaya, inatupasa tukumbuke kutimizwa kwake kwa kadiri kubwa katika Jumuiya ya Wakristo. Je! Mungu wa Isaya aliona Israeli wa siku za Isaya kuwa wa kinafiki na kuwa akihitaji kuponywa kiroho? Mwache Yehova Mungu aeleze alivyoona!’

Mambo Aliyoona Mungu Kuhusu Unafiki wa Kidini

7. Kulingana na Isaya 58:1, ni mambo gani aliyoyaona Yehova ambayo nabii huyo alipaswa kutangazia watu wake wateule?

7 Yaja amri ya Mungu kwa Isaya: “Piga kelele, usiache, paza sauti yako kama tarumbeta; uwahubiri watu wangu kosa [“uasi,” NW] lao, na nyumba ya Yakobo dhambi zao.”​—Isa. 58:1.

8. Isaya alipaswa kutangaza mambo aliyoyaona Yehova kwa sauti kubwa kadiri gani, na ni sababu gani ilimpasa ajione kusukumwa atabiri?

8 Kulingana na amri hiyo, Yehova Mungu alikuwa ameona Israeli akiwa na hatia ya “uasi,” na “dhambi” nyinginezo ambazo hazikutajwa waziwazi. Yeye alimtumia Isaya kama mnenaji wake ili atangaze yale aliyoyaona, naye nabii huyo aliambiwa atangaze mashtaka ya Mungu kwa sauti kuu kama ile ya “tarumbeta” au pembe. Kwa kuambiwa, “usiache,” huenda Isaya akawa alikuwa akijisikia kama alivyojisikia Amosi, wakati nabii huyo wa wakati uliotangulia aliposema: “Simba amekwisha kunguruma, ni nani asiyeogopa? [Yehova] Mungu amenena, ni nani awezaye neno ila kutabiri?”​—Amosi 3:8.

9. Ujumbe mgumu wa Yehova wapaswa kutangazwa kadiri gani leo, nao wapaswa uwasaidie wasikilizaji wafanye nini?

9 Watu walio wakf na kubatizwa wa Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova leo wanapaswa kujisikia vivyo hivyo kuhusiana na jambo hilo. Inawapasa kusukumwa wauchukue ujumbe wa kimungu wa siku za leo na kuutangaza na kuueneza kote kote. Wakiwa Mashahidi wa Yehova, acheni watangaze kwamba kuna uasi wa ulimwenguni pote juu ya Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote, ambaye huwataka watu wake kuwa washikamanifu na kujiepusha na dhambi ya ulimwenguni. Hiyo inaeleza sababu gani ujumbe huu mgumu unatangazwa duniani pote. Kwa kuutii wale wanaousikia wanaweza kusaidiwa wapate kuponywa.

10, 11. Katika wakati ule ule Waisraeli walipokuwa wakijionyesha kupendezwa na Yehova kwa kufunga na kujitaabisha, ni jambo gani jingine walilokuwa wakifanya bila kujizuia?

10 Katika yale ambayo Isaya aliambiwa atangaze kwa sauti kuu kwa “nyumba ya Yakobo,” aliufunua wazi unafiki wake kwa kusema hivi:

11 “Walakini wanitafuta kila siku; hupenda kujua njia zangu; kama vile taifa waliotenda haki, wasioacha sheria ya Mungu wao, hutaka kwangu amri za haki; hufurahi kumkaribia Mungu. Husema, Mbona tumefunga, lakini huoni? Mbona tumejitaabisha nafsi zetu, lakini huangalii? Fahamuni, siku ya kufunga kwenu mnatafuta anasa zenu wenyewe, na kuwalemea wote watendao kazi kwenu. Tazama, ninyi mwafunga mpate kushindana na kugombana, na kupiga kwa ngumi ya uovu.

12. Je! namna ya siku ya kufunga iliyokubaliwa na Yehova ulikuwa wakati wa mtu kujionyesha utawa wake na kujitaabisha?

12 “Hamfungi siku hii ya leo hata kuisikizisha sauti yenu juu. Je! kufunga namna hii ni saumu niliyoichagua mimi? Je! ni siku ya mtu kujitaabisha nafsi yake? Ni kuinama kichwa kama unyasi, na kutanda nguo za magunia na majivu chini yake? Je! utasema ni siku ya kufunga, na ya kukubaliwa na [Yehova]?’​—Isa. 58:2-5.

13. Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema nini, pasipo yeye kuwa mnafiki, juu ya kufunga kwa upande wa watu wa Mungu?

13 Ni kweli kwamba, Yesu Kristo, baada ya kutiwa mafuta kwa roho ya Yehova, alifunga kula kwa siku 40, walakini hilo lilikuwa jambo ambalo halikuwa likionwa na wanadamu, nalo lilifanywa katika jangwa la Uyahudi. Na kwa hiyo baadaye katika Mahubiri yake ya Mlimani yeye aliweza kusema bila unafiki wo wote hivi: “Tena mfungapo, msiwe kama wanafiki wenye uso wa kukunjamana maana hujiumbua nyuso zao, ili waonekane na watu kuwa wanafunga. Amin, nawaambia, wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe ufungapo, jipake mafuta kichwani, unawe uso; ili usionekane na watu kuwa unafunga, ila na Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.”​—Mt. 6:16-18.

14. (a) Katika Jumuiya ya Wakristo, kufunga kwa kidini ni mipango ya namna gani, na kwa sababu gani? (b) Katika Israeli wa kale, kufunga kikawaida tu na kujitaabisha hakungefunika jambo gani jingine?

14 Wanafunzi wa Kristo hawakuamriwa wawe na siku za kufunga; kufunga ni jambo la hiari; uchaguzi wa mtu mwenyewe. Jumuiya ya Wakristo inazo siku zake za kufunga zilizoamriwa, walakini hiyo ni mipango ya wanadamu tu. Katika siku za nabii Isaya, ikiwa siku za kufunga walizojichagulia “nyumba ya Yakobo” zingekuwa na wazo linalofaa pamoja na kusudi, hazingekataliwa. Walakini ebu na tukumbuke yale yaliyokuwa yakiendelea katika “nyumba ya Yakobo” wakati ule ule wa siku za kufunga au kabla na baada ya siku za kufunga. Kushindana, kugombana, kupigiana kelele kwa sauti kubwa zaidi, kupigana kwa “ngumi ya uovu.” Kufunga kwa kikawaida tu pamoja na kujitaabisha hakungeweza kufunika uovu huo wote usionwe na macho ya Yehova Mungu yenye kuona sana. Haishangazi kwamba ilionekana kama kwamba yeye hakuwa akiona kufunga kwao!

15. (a) Katika Israeli, utawa wa kujionyesha nje-nje na kujinyima kulipingana na matendo gani waliyowatenda jamii ya wafanya kazi? (b) Hali kama hiyo inapatikana wapi leo, na kwa sababu gani hilo halifai?

15 Ili waonyeshe utawa wao wa nje-nje, Wayahudi hao wenye kufuata ukawaida walikuwa wakiinamisha vichwa vyao kama unyasi, au walikuwa wakitanda nguo za magunia na majivu chini yake kana kwamba walikuwa wakiomboleza kweli kweli. Walakini maonyesho hayo hayakuwa ishara ya unyofu ya toba la moyo wote juu ya dhambi na uasi wao, juu ya Mungu pamoja na kukosa kwao ukawaida na utaratibu. Ikiwa kufunga kwao kulikuwa kwa namna ya kweli kweli, kujinyima mambo ya kawaida yaliyokuwa haki yao, kwa sababu gani wakati ule ule walikuwa wakiwalemea bila huruma “watendao kazi” wao, ndugu zao wenyewe, na kwa njia hiyo wakitaabisha kwa kuwaonea? Kujinyima kikawaida tu katika siku za kufunga kwa hao wenye kuajiri waliokuwa wakiwalemea hao waliokuwa wakiwafanyia kazi kulikuwa unafiki kweli kweli. Hakukuwapatia kibali kutoka kwa Mungu, wala hakukumfurahisha. Ndivyo ilivyo kwa habari ya Jumuiya ya Wakristo, inayoshika siku za kufunga leo, kwa kuwa inadai kuwa yamwabudu Mungu yule yule aliyemwongoza Isaya aujulishe uasi na dhambi za watu wa Mungu walioteuliwa.

16. Ni mambo gani yenye kufariji ambayo, kama wangefanya Waisraeli, yangempendeza Mungu zaidi kuliko kule kufunga kwao kikawaida?

16 Ni kufunga kwa namna gani, ni mwendo wa kujinyima wa namna gani, unaokubaliwa na Mungu wa Isaya, Mungu ambaye Jumuiya ya Wakristo inadai kuwa inamwabudu? Tunaweza kusoma maneno ya Yehova kama vile yalivyoandikwa na Isaya ili tupate kujua. Kwa faida ya wale wanaoona uhitaji wa kuponywa kiroho au wanaotaka kufanya maendeleo katika uhusiano wao pamoja na Mungu wa Biblia Takatifu, yeye asema hivi: “Je! saumu niliyoichagua, siyo ya namna hii? kufungua vifungo vya uovu, kuzilegeza kamba za nira, kuwaacha huru walioonewa, na kwamba mvunje kila nira? Je! siyo kuwagawia wenye njaa chakula chako, na kuwaleta maskini waliotupwa nje nyumbani kwako? umwonapo mtu aliye uchi, umvike nguo; wala usijifiche na mtu mwenye damu moja nawe?”​—Isa. 58:6, 7.

17. Maneno hayo ya Isaya 58:6, 7 yanaonyesha ni mambo gani yaliyokuwa yakiendelea katika Israeli, na kwa hiyo walihitaji kuponywa kutokana na nini?

17 Katika njia isiyo ya moja kwa moja maneno hayo yenye kueleza ya Yehova yanafunua kwamba Waisraeli walikuwa wakifungwa nira isivyo haki, kwa uovu. Wengine walifungiwa nira wapate kuichukua kama kwamba walikuwa wanyama wenye kufanya kazi. Bado wengine walikuwa wakilemewa na mizigo waliyokuwa wakiwekelewa. Waisraeli wasio katika hali nzuri walikuwa wakiachwa waone njaa au bila makao yanayofaa. Wale waliokuwa na uwezo wa kuwaondolea taabu walijifanya kwamba hawakuwa wakijua hali yenye kuhuzunisha ya Waisraeli wenzao. Aa, ndiyo, walifuata kawaida yao ya kufunga kama taifa, walakini hawakuwa na upendo wa kidugu wa kutosha kuweza kuwaondolea matendo yasiyo ya haki na uonezi wale waliokuwa wa damu moja pamoja nao. Kule kufunga kwa vivi hivi tu hakukuondoa mazoea hayo yasiyo ya huruma, wala hakukupatana na amri hii ya Mungu: “Umpende jirani yako kama nafsi yako; mimi ndimi [Yehova].” (Law. 19:18) Ikiwa walihitaji cho chote, Waisraeli hao walihitaji kuponywa ugonjwa wa kiroho ambao ungemaanisha kwamba uhusiano wao na Mungu ungekufa hakika!

18. Ni kwa sababu gani hakungekuwa kutia maneno chumvi kusema kwamba, kama ugonjwa wa kidini wa Israeli ungeachwa bila kuzuiwa, ungalimaanisha kifo kwa uhusiano wao pamoja na Yehova?

18 Kusema hivyo si kutia mambo chumvi, kwa kuwa katika karne iliyofuata unabii wa Isaya taifa la Israeli liliipoteza nchi ya kwao nao wakawa kama kwamba wamezikwa huko Babeli wasionekane, kuanzia mwaka wa 607 mpaka 537 K.W.K. (Eze. 37:1-11) Na ijapokuwa walirudishwa katika nchi ya kwao kwa fadhili zisizostahilika za Yehova, taifa hilo lilipoteza uhusiano wake wa agano pamoja na Yehova Mungu miaka 569 baadaye, katika mwaka 33 W.K. Katika mwaka 70 W.K. Warumi wakiwa chini ya Jemadari Tito waliuharibu Yerusalemu wenye kuasi, nao Wayahudi wakatawanywa ulimwenguni pote wawe vyombo vya kushutumiwa. Hayo yote ni onyo kwa Jumuiya ya Wakristo ambayo ina ugonjwa wenye kuleta mauti.

Wale Ambao Wamechukua Njia Inayoongoza Kwenye Kuponywa

19. Je! Isaya mwenyewe alikuwa na ugonjwa wa kiroho waliokuwa nao Waisraeli wenzake, nayo maneno yake yaliyotumiwa katika kitabu cha Waebrania yanaonyesha nini?

19 Ye yote na asidhani kwamba nabii Isaya alikuwa mgonjwa kiroho akiwa na ugonjwa wa unafiki wa kidini uliokuwa ukitaabisha taifa lake. Mtu ambaye Yehova Mungu angeweza kumtumia afunue unafiki kama huo alihitaji kuwa na uhusiano mzuri pamoja Naye. Isaya alionyesha afya yake ya kiroho pamoja na ile ya jamaa yake aliposema hivi: “Angalieni, mimi na watoto hawa niliopewa na [Yehova] tu ishara na ajabu katika Israeli, zitokazo kwa [Yehova] wa majeshi, yeye akaaye katika mlima Sayuni.” (Isa. 8:18) Mtume Mkristo Paulo anatumia maneno hayo anapoandika barua yake kwa Waebrania na kuyatumia kuhusiana na Yesu Kristo na wanafunzi wake waliotiwa mafuta na kuzaliwa kwa roho kwa maneno haya: “Akisema, Nitalihubiri jina lako kwa ndugu zangu; katikati ya [kundi] nitakuimbia sifa. Na tena, Nitakuwa nimemtumaini yeye. Na tena, Tazama, mimi nipo hapa na watoto niliopewa na Mungu”​—Ebr. 2:12, 13.

20. Kwanza ni nani waliokuwa “watoto” ambao Yehova alimpa Isaya Mkuu Zaidi, Yesu Kristo?

20 “Watoto” wa Yehova Mungu aliompa Yesu Kristo wakati wa Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. walikuwa wanaume na wanawake waliokuwa washiriki wa tengenezo la Kiyahudi lililokuwa na Yerusalemu kama mji wake mkuu. Kwa hiyo, kabla ya kutiwa mafuta kwa roho ya Mungu wakati wa Pentekoste, walikuwa wakishirikiana na taratibu hiyo ya mambo iliyokuwa na ugonjwa wa kiroho na ambayo ndani yake walikuwamo wale ambao Yesu Kristo aliwaita “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” (Mt. 10:6; 15:24) Walakini tangu Pentekoste na kuendelea hawakuwa tena washiriki wa tengenezo hilo la kidini ambalo kwalo nabii Isaya aliamriwa atangaze maneno ya Yehova ya kulilaumu. Chini ya uongozi wa Yesu Kristo walikuwa wameichukua njia inayoongoza kwenye kuponywa aliyoiahidi Yehova katika Isaya 58:8. Waliliacha tengenezo ambalo miongoni mwa washiriki wake mlikuwamo wale Mafarisayo wenye kujitakia haki, na ambao katika sala katika hekalu, walisema kwa kujisifu: “Mimi nafunga mara mbili kwa juma.”​—Luka 18:11, 12.

21. Kwa sababu ya kutoka katika mfano wa kisasa wa Israeli asiyeaminika, ni faida gani walizoahidiwa kiunabii wanafunzi wa Kristo katika Isaya 58:8?

21 Hali moja na hiyo, mashahidi wa Yehova walio wakf na kubatizwa wa leo, wametoka sana sana katika madhehebu ya Jumuiya ya Wakristo, mfano wa kisasa wa taifa la Israeli la siku za Isaya na za Kristo. Kama thawabu yao kwa sababu ya kutoka katika Jumuiya ya Wakristo yenye ugonjwa wa kiroho na iliyo na giza, ahadi ya kiunabii ya Isaya 58:8 imetimizwa juu yao, kama isemavyo: “Ndipo nuru yako itakapopambazuka kama asubuhi, na afya yako itatokea mara; na haki yako itakutangulia; utukufu wa [Yehova] utakufuata nyuma ukulinde.”

22. “Afya” iliyoahidiwa ilianza kutokea wakati gani kwa ajili ya wanafunzi waliotoka katika Jumuiya ya Wakristo?

22 Mara moja, katika mwaka wa 1919 W.K. uliofuata vita, unabii huo ulianza kutimizwa juu ya mashahidi Wakristo wa Yehova ambao katika wakati huo walivunja kabisa uhusiano na Jumuiya ya Wakristo yenye kufuata imani zilizotungwa, yenye kufuata mapokeo na yenye kutawalwa na viongozi wake wa kidini. Kwa ajili ya hao waliokombolewa nuru juu ya kweli ya Biblia pamoja na unabii wake vilianza kupambazuka “kama asubuhi.” “Afya” au kuponywa kwao kwenye afya nzuri ya kiroho kuhusiana na Yehova Mungu kupitia kwa Kristo kulitokea kukawa na maendeleo ya haraka sana. Kama vile Isaya hekaluni, wao wamesafishwa ili watumikie wakiwa Mashahidi wa Yehova.​—Isa. 6:1-10; 43:10-12.

23. Ni ulinzi gani unaowatangulia na ‘ulinzi wa nyuma’ gani ambao wamekuwa nao, hata wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili?

23 “Haki,” wala si upotovu wa Jumuiya ya Wakristo, imewatangulia iwaongoze katika njia zilizo nyofu machoni pa Yehova. Ili awalinde, amewafuata nyuma mpaka sasa. Kwa sababu hiyo wameendelea kuwa na kibali yake nao wamelindwa wasipate kuangamizwa kama vile adui zao walivyotisha kufanya katika wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili ya 1939 mpaka 1945.​—Mt. 24:9-14.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki