Hali ya Afya Ambayo Wanadamu Wangekuwa Nayo
1. Ni kwa sababu gani kuna uhitaji wa mganga (daktari) wa kuponya ulimwengu, nayo ni kanuni gani iliyotajwa na Kristo inayoweza kutumiwa kuhusiana na matabibu na mipango ya kitiba?
HALI ya afya ya wanadamu ni mbaya sana! Kuliko wakati mwingine wo wote uliotangulia wanadamu wanahitaji daktari, kwa kuwa maradhi mapya yanavumbuliwa nayo yanaua watu. Utabibu pamoja na mipango ya kuleta afya vyote pamoja vimeshindwa kuponya maradhi yote ya ulimwengu. Hatungetazamia iwe vingine, kwa kuwa kanuni hii inatumika; “Mganga jiponye mwenyewe.” Ni nani aliyetumia maneno hayo? Ni Mwanamume ambaye aliweza kuponya kila namna ya maradhi, hata kumfufua mtu aliyekuwa amekufa kwa muda wa siku nne. Mwanamume aliyekuwa na sifa kama hiyo ya kuponya alikuwa Yesu Kristo. (Luka 4:23; Marko 6:4-6) Kifo chake mwenyewe katika mwaka 33 W.K. hakikuwa cha kawaida. Aliuawa na wauaji. (Matendo 7:52) Hali ya afya ya wanadamu ingekuwaje leo kama wangalimkubali huko nyuma?
2, 3. (a) Twauliza ulizo gani juu ya Yehova kuwa Mponyaji? (b) Yehova alileta nini juu ya Misri ya kale ili kuwakomboa watu wake, naye aliwaonya Israeli juu ya nini ikiwa hawangesikiliza sauti yake?
2 Tukirudisha ulizo hilo wakati wa nyuma zaidi, twauliza hivi, Ingekuwaje kama watu wangekubali utumishi wa Yeye ambaye aliambia watu wake hivi katika siku za nabii Musa: “Mimi ndimi [Yehova] nikuponyaye”?—Kut. 15:26.
3 Akikusudia kuwakomboa watu wake wateule kutoka utumwani katika Misri ya kale, Yehova alileta mapigo ya mwujiza juu ya nchi hiyo. Baadaye aliyaondoa mapigo hayo tisa ya kwanza. Aliwaleta watu wake waliokombolewa kwenye agano la kitaifa ambalo lingewaletea hali njema ya mwilini, kiakili na kiroho. Yeye alimtumia Musa awaonye Waisraeli hao juu ya yale ambayo yangewapata ikiwa wangeendelea kuvunja sheria za agano hilo, akisema: “Tena kila ugonjwa, na kila pigo yasiyoandikwa katika kitabu cha torati hii, atakutia nayo [Yehova] juu yako, hata utakapokwisha kuangamizwa. Nanyi mtasalia wachache kwa hesabu, ninyi mliokuwa mfano wa nyota za mbinguni kwa wingi; kwa kuwa hukuisikiza sauti ya [Yehova], Mungu wako.”—Kum. 28:61, 62.
4, 5. (a) Kwa kuwa Wayahudi ambao wangali wakiishi wako katika hali mbaya sana leo, ni ulizo gani tunaloweza kuuliza juu ya mfano wa kisasa wa Israeli? (b) Kwa kutengeneza njia zao, hali ingalikuwaje kulingana na Isaya 58:9-12?
4 Leo si wale Wayahudi milioni kadha peke yao ambao wangali wanaishi wanaoteseka kutokana na maradhi ya mwilini, bila kutaja vilevile machafuko ya kiakili, kidini, kijamii na kiuchumi, bali vilevile wanadamu wote wanateseka pia. Kuhusiana na mambo hayo hata Jumuiya ya Wakristo haina lo lote la kuwapita Wayahudi wa asili. Kwa kweli, Jumuiya ya Wakristo ina hatia kubwa zaidi mbele za Mungu. Ikiwa Israeli wa kale walipatwa na mabaya sana hivyo kwa sababu ya kutotengeneza njia zake kama vile Yehova alivyowaambia wafanye kupitia kwa Isaya, twaweza kutarajia Jumuiya ya Wakristo ipatwe na nini mwishowe, na hilo likitokea hivi karibuni? Vile ambavyo ingekuwa, nabii Isaya anaonyesha kama ifuatavyo:
5 “Ndipo utaita, na [Yehova] ataitikia; utalia, naye atasema, Mimi hapa. Kama ukiiondoa nira; isiwepo kati yako, wala kunyosha kidole [kwa kudharau au kulaumu], wala kunena maovu; kama ukimkunjulia mtu mwenye njaa nafsi yako, na kuishibisha nafsi iliyoteswa; ndipo nuru yako itakapopambazuka gizani; na kiwi chako kitakuwa kama adhuhuri. Naye [Yehova] atakuongoza daima, ataishibisha nafsi yako mahali pasipokuwa na maji, na kuitia nguvu mifupa yako; nawe utakuwa kama bustani iliyotiwa maji, kama chemchemi ambayo maji yake hayapungui. Na watu wako watapajenga mahali palipokuwa ukiwa; utaiinua misingi ya vizazi vingi; nawe utaitwa, Mwenye kutengeneza mahali palipobomoka; na, Mwenye kurejeza njia za kukalia.”—Isa. 58:9-12.
6. Kwa sababu ya uwezekano uliowekwa mbele ya Israeli wa siku za Isaya, tunalazimika kuuliza ulizo gani juu ya uwezekano kwa habari ya mfano wa kisasa wa Israeli?
6 Oh, hali ya kitaifa ya Israeli wa kale ingekuwa namna gani kama ingalifuata shauri lililo wazi aliloipa Yehova! Kwa kuwa yeye ni Mwenye nguvu zote yeye angeweza kwa urahisi kutokeza hali kama zile alizosema zingetokea ikiwa Israeli ingeondoa katikati yake yale mambo yasiyopendeza na ambayo yaliwaharibu na kuharibu uhusiano wao wa agano pamoja na Mungu. Kwa sababu ya kukosa kufanya hivyo, Israeli iliendelea kuharibika. Israeli ilipatwa na adhabu mbaya sana katika karne iliyofuata unabii wa Isaya. Kwa sababu ya hayo yote yakiwa mfano, tunalazimika kuuliza, Namna gani mfano wa kisasa wa Israeli, Jumuiya ya Wakristo? Hali yake ya afya ingalikuwaje kijamii, kiuchumi, kiadili, na kidini kama ingalifuata shauri la Mponyaji wa Kimungu, Yehova, na kuukubali ujumbe wa Ufalme ambao umekuwa ukitangazwa na mashahidi Wakristo kwa muda wa zaidi ya karne moja sasa?
7. Ni mfano gani wa leo wenye kuonyesha kwa matendo namna hali ingalikuwa kwa Jumuiya ya Wakristo?
7 Namna hali ya Jumuiya ya Wakristo ingekuwa imeonyeshwa kwa mfano. Jinsi gani? Kwa yale ambayo yametokea leo kwa wale waliofananishwa na wana wa Isaya, “watoto” aliopewa na Yehova na ambao Yehova alitumia kufananisha wanafunzi watiwa mafuta kwa roho wa Yesu Kristo. (Isa. 8:18; Ebr. 2:13) Kwa muda wa zaidi ya miaka 65 wametangazia ulimwengu kwamba sasa ufalme wa Kimasihi wa Yehova upo begani mwa Mwana wa Mungu aliyetawazwa, Yesu Kristo akiwa Mkuu wa Amani. (Isa. 9:6, 7) Kwa njia hiyo wameondolea mamia ya maelfu ya watu wanaokata tamaa hali ya giza isiyo na tumaini inayofunika ulimwengu wote. Kwa njia ya habari njema za Ufalme kama vile Yesu alivyotabiri katika Mathayo 24:14 wamekuwa wakiwalisha kiroho watu wenye njaa kitu chenye kuendeleza uhai kuliko chakula cha kimwili. Matokeo yamekuwa kuponywa kiroho.
8. Wale walioponywa kiroho sasa wanatii maneno gani mengine ya Yehova, juu ya Sabato, kwa sababu ya ahadi gani?
8 Wale wote walioponywa kiroho wanatii sasa maneno haya zaidi ya Yehova ambayo Israeli wa kale hakutii: “Kama ukigeuza mguu wako usiihalifu sabato, usifanye anasa yako siku ya utakatifu wangu; ukiita sabato siku ya furaha, na siku takatifu ya [Yehova] yenye heshima; ukiitukuza, kwa kutokuzifanya njia zako mwenyewe, wala kuyatafuta yakupendezayo, wala kusema maneno yako mwenyewe; ndipo utakapoinuka; nitakulisha urithi wa Yakobo baba yako; kwa maana kinywa cha [Yehova] kimenena hayo.”—Isa. 58:13, 14.
9. Je! Wakristo walio wakf na kubatizwa wamo sasa chini ya mpango wa kushika Sabato kila juma, nao wanakaribia kwa haraka sana kipindi gani cha Sabato?
9 Wakristo walio wakf na kubatizwa, kama vile walivyo Mashahidi wa Yehova leo, hawana wajibu wa kushika Sabato yenye kuanzia wakati wa machweo katika siku ya Ijumaa na kumalizika wakati ule ule katika siku ya Jumamosi, kwa kuwa wao hawamo chini ya orodha ya sheria iliyotolewa na mpatanishi Musa. (Kut. 20:1-11) Wala Yesu Kristo, aliye Mpatanishi wa lile agano jipya, hakuwaamuru wanafunzi wake wawe wakishika Jumapili iwe siku ya Sabato. Wao wanajua kwamba wanaishi katika siku ya saba ya juma ya uumbaji wa Yehova Mungu, siku ambayo katika hiyo amekuwa akipumzika kwa habari ya kazi za moja kwa moja za kuumba kuhusiana na dunia yetu. (Mwa. 1:1 mpaka 2:4) Matukio ya ulimwengu pamoja na elimu ya tarehe ya Biblia huonyesha kwamba tunakaribia sasa kwa haraka sana wakati wa kuanza kwa ule utawala wa Yesu Kristo wa miaka elfu. Utawala wake wa miaka elfu kwa baraka ya wanadamu wote utachukua miaka elfu moja ya mwisho ya siku ya Yehova ya mapumziko au siku ya Sabato ya miaka elfu saba. Utawala wa Kristo utakuwa siku ya Sabato ya furaha kuu kwa wanadamu wote.
10. Je! “sabato” ya kila juma ya Jumuiya ya Wakristo ni ya Kibiblia, nayo sana sana inatumiwa kwa makusudi gani leo?
10 Kwa muda wa zaidi ya miaka 1,500 Jumuiya ya Wakristo imekuwa na kawaida ya kushika Jumapili kama namna ya sabato ya Kikristo. Walakini Jumapili si ya Kikristo wala ya Kiyahudi. Kama vile jina lake (Sunday katika Kiingereza) linavyoonyesha, kwa kweli ni sikukuu ya kipagani inayoadhimishwa kwa ajili ya mungu-jua. Leo Jumuiya ya Wakristo bila shaka haishiki Jumapili yake kama siku ya mapumziko kwa heshima ya Yehova na kwa faida ya mwili wa kibinadamu. Kwa sehemu kubwa, huitumia kwa faida yake kama siku ya michezo, kwenda kwenye pikiniki (mandhari), kwenda sinema, na kufanya mambo mengine yasiyo ya kidini, pamoja na mambo mengine ya kichoyo ya kujifurahisha, bila kutaja kucheza kamari na matendo mbalimbali ya uasherati.
11. Mashahidi Wakristo wa Yehova wanashikaje “sabato” ya kweli hivyo wakijipatanisha na mfano wake?
11 Mashahidi Wakristo wa Yehova wanashika “sabato” yenye kuendelea kwa Yehova. Namna gani? Kwa kumpumzika au kuachana na kazi zao wenyewe za kujitahidi kujionyesha haki mbele za Mungu hivyo wajipatie wokovu wao wa milele. Kwa imani wanapumzika kwa kuiamini thamani yenye kukomboa ya dhabihu ya ukombozi ya Kristo kuwa msingi wa wokovu wao wa milele. Katika njia hiyo wanajipatanisha na ile “siku” kuu ya saba ya Juma ya Uumbaji wa Yehova, “siku” ya mfano ambayo katika hiyo yeye mwenyewe amekuwa akipumzika.
12. Ni nini ‘mapumziko ya sabato’ yaliyopo ambayo ‘yamesalia,’ kwa watu wa Mungu, na kwa hiyo Mashahidi wa Yehova wanatumiaje sabato ya Kiyahudi na Jumapili ya Jumuiya ya Wakristo?
12 Kwa habari ya Mkristo kupumzika kwa imani katika “sabato” ya Yehova ya mileani saba, twasoma hivi: “Kwa maana ameinena siku ya saba mahali fulani hivi, Mungu alistarehe siku ya saba, akaziacha kazi zake zote. . . . Basi, imesalia raha ya sabato kwa watu wa Mungu. Kwa maana yeye aliyeingia katika raha yake amestarehe mwenyewe katika kazi yake, kama vile Mungu alivyostarehe katika kazi zake.” (Ebr. 10:4-10) Mashahidi wa Yehova wanastarehe au kupumzika kwa kuiamini dhabihu ya Kristo kuwa mpango wa Mungu wa kuwaokoa wanadamu. Kwa hiyo wanaweza wakiwa na dhamiri safi kutumia sabato ya Wayahudi na Jumapili ya Jumuiya ya Wakristo kuhubiri habari njema za ufalme wa Mungu nyumba kwa nyumba.
Mtengano Kati ya Jumuiya ya Wakristo na Mponyaji Anayehitajiwa
13. Kulingana na Isaya 59:1-4, ni mwenendo wa namna gani wa watu wanaodai kuwa watu wa Mungu ambao umeleta mtengano kati yake nao?
13 Namna ambavyo hali ingekuwa kwa Jumuiya ya Wakristo badala ya namna ilivyo leo si kwa sababu Mungu Mwenye Nguvu Zote anakosa uwezo. Kwa sababu gani, basi, Israeli wa kale hakupata wokovu, na, hali moja na hiyo, kwa sababu gani Jumuiya ya Wakristo au sehemu nyingine ya ulimwengu haijapata wokovu? Sababu inatolewa katika maneno haya: “Tazama, mkono wa [Yehova] haukupunguka, hata usiweze kuokoa; wala sikio lake si zito, hata lisiweze kusikia; lakini maovu yenu yamewafarikisha ninyi na Mungu wenu, na dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone, hata hataki kusikia. Kwa maana mikono yenu imetiwa unajisi kwa damu, na vidole vyenu vimetiwa unajisi kwa uovu; midomo yenu imenena uongo, ndimi zenu zimenong’ona ubaya. Hapana adaiye kwa haki, wala hakuna atetaye kwa kweli; hutumainia ubatili, hunena uongo; hupata mimba ya madhara, na kuzaa uovu.”—Isa. 59:1-4.
14. Kama vile Israeli wa siku za Isaya, ni kwa sababu gani Jumuiya ya Wakristo ya karne ya 20 haingeweza kujiondolea hatia katika mahakma ya haki ya kimungu?
14 Kutazama hivyo namna mambo yalivyokuwa katika Israeli wa siku za Isaya kunafunua mambo mengi. Yehova angewezaje kukaa karibu na watu wa taifa kama hilo na kuwabariki? Taifa hilo ndilo lililokuwa likileta mtengano kati ya Yeye nalo. Na ndivyo ilivyo kwa habari ya mtengano kati yake na wale watu wanaodai kuwa wake, yaani, Jumuiya ya Wakristo. Mikono, vidole, midomo, ndimi vyote hivyo vinashiriki katika kutenda mabaya, na kuiletea Jumuiya ya Wakristo uharibifu. Baada ya vita viwili vya ulimwengu, si kwamba tu vidole vyake tayari vimejaa damu ya wanadamu, bali pia inapanga kumwaga damu ya kibinadamu kwa wingi hata zaidi, inaelekea katika wakati ujao kwa kutumia makombora ya atomiki na ya nuklea licha ya njia nyinginezo zenye ukatili sana za kuleta kifo chenye maumivu makali sana kwa idadi isiyojulikana ya watu. Bila shaka kupelekea Umoja wa Mataifa au Mahakma ya Haki ya Mataifa Yote matatizo yake huko Hague, Netherlands, si sawasawa na kupelekea mahakma ya haki ya kimungu mambo katika “haki” mbele ya mbingu yote na dunia. Katika mahakma kama hiyo ya kimungu Jumuiya ya Wakristo haiwezi kujiondolea hatia!
15, 16. Kutokana na yale yanayotungwa na mataifa yote, matokeo yangetazamiwa kuwa nini, nayo mazungumzo yote ya kuleta mapatano ni maneno ya nini?
15 Katika Umoja wa Mataifa yale mataifa yasiyo ya Kikristo tayari ni mengi kuliko yale ya Jumuiya ya Wakristo. Hata hivyo viongozi wake wa kidini wanauona mwigizo huo wa ufalme wa Mungu kuwa “tumaini pekee la ulimwengu” nao wanaendelea na kutenda kama kwamba ndivyo ulivyo. Ikiwa kufanya hivyo si ‘kuutumainia ubatili,’ basi ni kupi? Nayo mazungumzo yote ya hadharani na ya faraghani juu ya kuutumainia Umoja wa Mataifa na matengenezo mengineyo kwa ajili ya amani na usalama wa ulimwengu—je! huko si ‘kunena uongo,’ hasa kwa upande wa Jumuiya ya Wakristo? Ikiwa sivyo, mazungumzo hayo yote yamekuwa nini?
16 Kwa kuwa “ubaya,” ndio unaotungwa na mataifa yote, wala si uhusiano wa amani pamoja na Yehova Mungu, “uovu” peke yake ndio unaotazamiwa kuzaliwa. Nacho kinakuwa ‘kitoto matata’ namna gani! Kwa maoni ya Yehova, mazungumzo yote ya kuleta mapatano kati ya mataifa, yale ya Kikristo na yasiyo ya Kikristo, yamekuwa ‘kusema uongo’ tu na ‘manong’ono ya ubaya.’
17. Ni kana kwamba watu wa Mungu wanatiwa sumu kwa kitu gani, na ni kwa sababu gani mwendo waliouchukua haukuwa njia yenye usalama kwa wasafiri?
17 Leo watu ndani na nje ya Jumuiya ya Wakristo wanatiwa sumu, si kwa matumizi ya namna mbalimbali za dawa peke yake, bali kiroho pia. Kulingana na Isaya 59:5-8, wenye kulalamika wangeweza kusema hivi mbele ya Mungu, Hakimu wa wote: “Huangua mayayi ya fira, na kusuka wavu wa buibui; yeye alaye mayayi yao hufa, na hilo livunjikalo hutoka nyoka. Nyavu zao hazitakuwa mavazi, wala hawatajifunika kwa kazi zao; kazi zao ni kazi za uovu, na vitendo vya udhalimu vimo mikononi mwao. Miguu yao hukimbilia mabaya, nao hufanya haraka kumwaga damu isiyo na hatia; mawazo yao ni mawazo ya uovu; ukiwa na uharibifu zaonekana katika njia kuu zao. Njia ya amani hawaijui; wala kila apitaye katika njia hizo hajui amani.”
18. Jumuiya ya Wakristo imekuwa mfano wa namna gani kwa habari ya kuhifadhi amani?
18 Ikiwa Jumuiya ya Wakristo haiwezi kuhifadhi amani ndani yake yenyewe, tungewezaje kutazamia ile sehemu nyingine ya ulimwengu ifanye hivyo? Imekuwa mfano mbaya, ikiusingizia Ukristo wa kweli vibaya sana. Imekuwa yenye kusema-sema sana katika kusihi kuwe na amani na usalama, walakini bila shaka kule kujilundikia silaha sana kwa ajili ya vita katika kusingizia jirani zake za kilimwengu siyo njia ya kuleta amani.
19. Hali ya kinafiki iliyokuwako katika Israeli wa kale ilikuwa na matokeo gani kwa habari ya haki na kuona njia inayofaa ya kufuata?
19 “Kwa sababu hiyo hukumu ya haki i mbali nasi,” aendelea kusema nabii wa Yehova, “wala haki haitufikilii; twatazamia nuru, na kumbe! latokea giza; twatazamia mwanga, lakini twaenda katika giza kuu. Twapapasa-papasa kutafuta ukuta kama kipofu, naam, twapapasa kama watu wasio na macho; twajikwaa wakati wa adhuhuri, kama kwamba ni wakati wa ukungu wa alfajiri; kati yao waliowanda tumekuwa kama wafu.
20. (a) Je! uasi, makosa na dhambi ya Israeli yalikuwa yakionekana waziwazi? (b) Kwa hiyo, ikiwa hivyo, hukumu ya haki, haki na kweli vilikuwaje?
20 “Sisi sote twanguruma kama dubu; twaomboleza kama hua; twatazamia hukumu ya haki, lakini hapana; na wokovu, lakini u mbali nasi. Maana makosa yetu yamezidi kuwa mengi mbele zako, na dhambi zetu zashuhudia juu yetu; maana makosa yetu tunayo pamoja nasi, na maovu yetu tumeyajua; katika kukosa na kumkana [Yehova], na katika kugeuka tusimfute Mungu wetu, tukinena jeuri na uasi, na kukusudia maneno ya uongo na kuyatoa moyoni. Na hukumu imegeuka ikaenda nyuma, na haki inasimama mbali sana; maana kweli imeanguka katika njia kuu, na unyofu hauwezi kuingia. Naam, kweli imepunguka kabisa, na yeye auachaye uovu ajifanya kuwa mateka.”—Isa. 59:9-15; Rum. 3:15-18.
21. Maelezo hayo ya Israeli katika siku za Isaya yanalingana vizuri sana na nini leo, nao wanadamu wangelikuwaje na matumaini bora?
21 Lo! Namna maelezo hayo ya kale yanavyolingana na namna hali ilivyo katika Jumuiya ya Wakristo leo! Tangu mwisho wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza katika mwaka 1918 Mashahidi wa Yehova wamekuwa wenye kutokeza sana ulimwenguni, yajapokuwapo mateso makali sana. Namna gani ikiwa ujumbe wa ufalme wa Yehova ulio mikononi mwa Kristo aliyetukuzwa ungalipokewa vizuri badala ya kupingwa kwa kutumia njia zisizo za haki na kuwatesa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote? Hali ya afya ya wanadamu na sana sana ile ya Jumuiya ya Wakristo ingalikuwa bora kama nini katika kila njia! Kungalikuwa na matumaini maangavu kama nini kwa wanadamu!