Je! Wakristo Washike Siku ya Pumziko?
JUNI ulikuwa na mvua nyingi isivyo kawaida. Kwa sababu hiyo, mapokeo ya kilimwengu ya tangu zamani ilivunjwa wakati wa mashindano ya tenisi ya Wimbledon ya 1991. Kwa mara ya kwanza katika historia, mechi zilichezwa Jumapili ili kulipia wakati uliopotezwa. Isipokuwa kupuuzwa kwa kanuni pindi kwa pindi kama wakati huo, Jumapili inaendelea kuwa siku takatifu ya pumziko katika Uingereza, pamoja na katika nchi nyinginezo.
Watu wengine huweka siku tofauti ya pumziko. Wayahudi ulimwenguni pote hushika Sabato sana kutoka kushuka kwa jua Ijumaa hadi kushuka kwa jua Jumamosi. Wakati wa Sabato, ndege za shirika la ndege la kitaifa la Israeli haziruki, na katika miji fulani usafiri wa umma hauendeshwi. Katika Yerusalemu wenye kushika mapokeo huamuru barabara fulani zifungwe ili kuzuia magari yote wanayoona kuwa haramu siku ya Sabato.
Uhakika wa kwamba dini nyingi zingali zinashika siku ya pumziko ya kila juma au sabato unatokeza maswali kadhaa. Je! kuweka Sabato ni kwa Wayahudi pekee? Kwa nini dini nyingi za Jumuiya ya Wakristo zimekuja kukubali siku ya pumziko iliyo tofauti? Je! kushika siku ya pumziko ya kila juma kwaendelea kuwa takwa la Kibiblia leo?
Je! Sabato Imekuwako Sikuzote?
Twapata mtajo wa kwanza wa Kimaandiko wa sabato katika kitabu cha Kutoka. Waisraeli walipokuwa jangwani, walipokea mana, chakula cha kimuujiza kutoka kwa Yehova. Kila siku ya sita ya juma, walihitaji kukusanya kiasi maradufu kwa sababu siku ya saba ilikuwa “sabato ya BWANA [Yehova, NW],” ambamo kazi yote ilikatazwa.—Kutoka 16:4, 5, 22-25.
Isitoshe, Waisraeli walipewa Sabato ili kuwakumbusha kwamba walikuwa wamekuwa watumwa katika bara la Misri. Ukumbusho huo usingalikuwa na maana sana ikiwa wangalikuwa wamefuata sheria hiyo hapo mbeleni. Kwa hiyo, amri za Sabato zilipewa Israeli pekee.—Kumbukumbu la Torati 5:2, 3, 12-15.
Mazoea Madogo-madogo na Yenye Kulemea
Kwa sababu Sheria ya Kimusa haikueleza mambo mengi madogo-madogo kuhusu Sabato, marabi kupitia muda wa karne zilizopita walitokeza makatazo mengi, yaliyokataza hasa namna zote za kazi katika Sabato. Kulingana na Mishnah, kazi zilizokatazwa zilitiwa ndani ya vikundi 39 vikuu, kama vile kushona, kuandika, na kazi za shambani. Nyingi kati ya amri hizo hazitegemei Biblia. Ikitaja Mishnah, Encyclopedia Judaica hukiri kwamba amri hizo ni kama “milima inayoning’inia kwenye unywele, kwani kuna maelezo machache juu ya habari hiyo katika Maandiko na bado kanuni ni nyingi.”
Ili kutumia ile amri kwamba mtu hapaswi “kuondoka mahali pake siku ya saba,” upeo wa mwendo uliamuliwa, na huo uliitwa “upeo wa Sabato.” Kulingana na vyanzo fulani, huo ulilingana na dhiraa elfu mbili, au karibu meta 900. (Kutoka 16:29) Hata hivyo, amri hiyo ingeweza kukiukwa kwa hila: Jioni iliyotangulia, vyakula vya Sabato vingeweza kuwekwa mwendo wa dhiraa elfu mbili kutoka kwa nyumba. Kisha mahali hapo pangeweza kuonwa kuwa urefusho wa nyumba ya familia, na dhiraa elfu mbili nyinginezo zingeweza kuhesabiwa kutoka hatua hiyo.
Vingi kati ya vizuizi hivyo vyenye kufanyizwa na wanadamu vilikuwako katika siku za Yesu. Hivyo, viongozi wa kidini waliwalaumu wanafunzi wake kwa ajili ya kuchuma masuke ya nafaka na kuyala walipokuwa wakipitia mashamba ya nafaka. Walishtakiwa juu ya kuvunja Sabato—kuchuma nafaka kulionwa kuwa kuvuna, na kuisugua kulionwa kuwa kusaga au kuponda. Yesu aliyashutumu maoni yao ya kupita kiasi katika pindi nyingi, kwani waliiwakilisha vibaya roho ya sheria ya Yehova.—Mathayo 12:1-8; Luka 13:10-17; 14:1-6; Yohana 5:1-16; 9:1-16.
Kutoka Kuwa Sabato ya Jumamosi Hadi Kuwa Sabato ya Jumapili
“Siku za Jumapili zitawekwa kwa ajili ya kumtumikia Mungu kwa bidii.” Ndiyo Amri ya Nne juu ya Sabato kama inavyotolewa na Kanisa Katoliki. Catéchisme pour adultes ya Kifaransa iliyotangazwa kwa chapa hivi karibuni hueleza hivi: “Jumapili ya Kikristo husherehekewa siku baada ya Sabato: siku ya nane, yaani, siku ya kwanza ya uumbaji mpya. Inafuata sehemu za maana za Sabato lakini inakazia Sikukuu ya Kupitwa kwa Kristo.” Badiliko hilo kutoka kwa sabato ya Jumamosi hadi sabato ya Jumapili lilitukiaje?
Hata ingawa Jumapili ilikuwa siku ambayo Yesu alifufuliwa, kwa Wakristo wa mapema ilikuwa siku ya kufanya kazi kama nyingine yoyote. Lakini uamuzi wa baraza la kanisa ya Laodicea (katikati hadi mwisho-mwisho wa karne ya nne W.K.) unafunua kwamba wakati ulipopita, mahali pa Sabato ya Kiyahudi ya Jumamosi palichukuliwa na sabato ya Jumapili ya “Kikristo.” Amri hiyo “iliwakataza Wakristo wasifuate desturi za Kiyahudi na kukaa kitako katika siku ya Sabato [ya Kiyahudi], na siku ya Bwana [siku ya juma aliyofufuliwa] ilipaswa iheshimiwe katika njia ya Kikristo.” Kutoka wakati huo na kuendelea wafuasi wa Jumuiya ya Wakristo walipaswa wafanye kazi Jumamosi na kutofanya kazi Jumapili. Baadaye, walitakwa wahudhurie Misa Jumapili.
Kwa kuungwa mkono na mamlaka za kilimwengu, upesi kufanya kazi Jumapili kulikatazwa kotekote katika Jumuiya ya Wakristo. Kutoka karne ya sita na kuendelea, wakiukaji walitozwa faini au kupigwa mjeledi, na ng’ombe-dume zao kunyakuliwa. Pindi kwa pindi, watenda dhambi wasiotubu wangeweza kulazimishwa kuwa watumishi.
Kwa maana fulani, sheria zilizohusu kazi zilizokubalika Jumapili zilikuwa ngumu kama yale mapokeo yaliyoongoza Sabato ya Kiyahudi. Dictionnaire de théologie catholique inatoa maelezo marefu kuhusu habari ya kusuluhishwa kwa maswali juu ya yaliyofaa au yasiyofaa kupitia matumizi ya kanuni na, miongoni mwa mambo yaliyokatazwa, inataja kazi za kiutumwa, kazi za shambani, kesi za kisheria, masoko, na kuwinda.
Kinyume cha hilo, Sabato ya Kiyahudi ilirejezewa ili kutetea makatazo hayo. New Catholic Encyclopedia inataja sheria za Maliki Charlemagne kuhusu Jumapili: “Wazo la Kisabato, lililokataliwa katakata na Mt. Jerome na kulaumiwa na Baraza la Orléans katika 538 kuwa la Kiyahudi na lisilo la Kikristo, lilitaarifiwa waziwazi katika amri ya Charlemagne ya 789, iliyokataza kazi zozote Jumapili kuwa ni uhalifu [wa zile Amri Kumi].” Hivyo, ingawa kanisa lilipendezwa kuona mamlaka za serikali zikifanya Jumapili kuwa siku ya pumziko, liliruhusu mamlaka hizo zitetee makatazo hayo kwenye msingi wa kisheria ambao kanisa lilikatalia mbali, yaani, sheria ya Kimusa kuhusu Sabato.
Msimamo Usio wa Kimaandiko
Karne kadhaa kabla ya hapo, Mababa kadhaa wa Kanisa, na hasa Augustino, walijulisha ifaavyo kwamba Sabato ilikuwa mpango wa muda tu uliowekewa Wayahudi. Kwa kufanya hivyo, Mababa hao wa Kanisa walifuata tu yale ambayo Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanayoeleza, yaani, kwamba Sabato ni sehemu kuu ya agano la Sheria iliyobatilishwa na dhabihu ya Yesu.—Warumi 6:14; 7:6; 10:4; Wagalatia 3:10-14, 24, 25.
Katika Vocabulaire biblique ya wakati huo Oscar Cullmann ananukuliwa kuwa alikubali kwamba “kwa sababu Yesu alikuja, akafa, na akafufuliwa. sikukuu za A[gano] la K[ale] zimetimizwa, na kuzidumisha ‘kunamaanisha kulirudia agano la kale, kana kwamba Kristo hakupata kuja kamwe.’” Baada ya kuona jambo hilo la maana, je, inawezekana kutetea kule kushika Sabato kwa lazima?
Leo, waandikaji Wakatoliki kwa kawaida hujaribu kupata utegemezo kwenye Matendo 20:7, linalosema juu ya “siku ya kwanza ya juma” (Jumapili), wakati Paulo alipokutana na wenzake ili kushiriki chakula pamoja nao. Hata hivyo, hilo lilikuwa jambo la kuongezea habari tu. Hakuna lolote katika andiko hilo wala katika mistari mingine ya Biblia yanayoonyesha kwamba usimulizi huo ulimaanishwa kuwa kielelezo kilichohitaji kufuatwa na Wakristo, kwa hakika huo sio wajibu. Naam, kushika sabato ya Jumapili hakuna utegemezo w a Kimaandiko.
Kuna Pumziko Gani kwa Wakristo?
Ingawa Wakristo hawana wajibu wa kushika siku ya pumziko ya kila juma, bado wanaalikwa washike pumziko la aina nyingine. Paulo aeleza hilo kwa Wakristo Wayahudi wenzake, akisema hivi: “Basi, bado lipo pumziko kwa watu wa Mungu. . . . Basi, tujitahidi kupata pumziko hilo.” (Waebrania 4:4-11, Habari Njema Kwa Watu Wote) Wayahudi hao, kabla ya kuwa Wakristo, walikuwa mbeleni wameifuata Sheria ya Kimusa kwa uangalifu sana wawezavyo. Sasa Paulo hakuwa akiwatia moyo tena wajaribu kupata wokovu kupitia matendo bali ‘wapumzike’ kutoka kazi zao zisizo hai. Kutoka wakati huo, walipaswa wawe na imani katika dhabihu ya Yesu, iliyokuwa njia pekee ya ainabinadamu kuweza kuwa yenye uadilifu machoni pa Mungu.
Sisi leo tunaweza kuonyeshaje ufikirio uo huo kwa maoni ya Mungu? Kama vile wanadamu wenzao, Mashahidi wa Yehova, wakiwa wanadamu wenye usawaziko, huithamini ile siku ya pumziko ya kila juma kutoka kazi za kilimwengu ambayo imewekwa katika nchi nyingi. Hiyo inawaruhusu wawe na wakati wa ushirika wa familia na burudisho. Lakini hasa, imethibitika kuwa kipindi cha ufuatiaji mwingineo wa Kikristo. (Waefeso 5:15, 16) Huo unatia ndani mikutano na ushiriki katika huduma ya peupe, kutembelea majirani wao ili kushiriki habari za Kibiblia juu ya wakati unaokaribia ambapo ainabinadamu yenye kuamini itakapofurahia amani ya duniani pote. Ikiwa ungependa kujua kuhusu hilo, Mashahidi wa Yehova watafurahia kukusaidia, iwe ni Jumamosi, Jumapili, au siku nyingine yoyote ya juma.
[Picha katika ukurasa wa 28]
Yesu alishika sheria ya Sabato kikamilifu, badala ya mapokeo ya Kiyahudi
[Picha katika ukurasa wa 29]
Ufuatiaji wa Kikristo unaandaa burudisho katika siku za pumziko kutoka kazi za kilimwengu