Je! Ni Vibaya Kufanya Kazi Siku ya Saba ya Juma?
AMRI ya nne kati ya Amri Kumi ambazo Mungu alilipa taifa la Israeli inasema hivi: “Ikumbuke siku ya sabato uitakase. Siku sita fanya kazi, utende mambo yako yote; lakini siku ya saba ni sabato ya [Yehova], Mungu wako, siku hiyo usifanye kazi yo yote.”—Kut. 20:8-10.
Neno “sabato” linatokana na neno la asili ya Kiebrania lenye maana ya “kupumzika, kuacha, kuacha kufanya kazi.” Biblia ilisema wazi kwamba Mwisraeli ye yote hakupaswa kupika wala kuoka, kukusanya kuni, kuchukua mizigo wala kufanya biashara siku ya sabato. (Kut. 16:23, 29; Hes. 15:32-35; Neh. 13:15) Mwisraeli ye yote aliyefanya kazi siku ya sabato ‘hakika yake angeuawa.’—Kut. 31:15.
Wengi wanadai kwamba sheria ya Mungu kushika sabato ya kila juma ingali inatumika. Wengine wanasema kwamba takwa hili lilishikwa na wazee wa ukoo Ibrahimu, Isaka na Yakobo, na kwa kweli, lilianza huko nyuma katika bustani ya Edeni.
Maoni ya Biblia juu ya jambo hili ni nini? Je! bado ni vibaya kufanya kazi siku ya saba ya juma?
Uchunguzi wa uaminifu unaonyesha kwamba Maandiko hayasemi kushika sabato ya kila juma kulianza huko nyuma wakati wa Adamu na Hawa katika bustani ya Edeni. Na, ingawa Ibrahimu alishika “amri” fulani, “hukumu” na “sheria” fulani za Mungu, hakuna mahali Biblia inakomtaja kuwa alishika sabato ya kila juma.—Mwa. 26:5.
Muda mfupi tu kabla ya Mungu kutoa agano la torati ya Musa katika Mlima Sinai, karibu miaka 2,500 baada ya kuumbwa kwa Adamu na Hawa na karne nyingi baada ya kufa kwa Ibrahimu, ndipo Mungu alipoamuru kwa mara ya kwanza sabato ya kila juma ishikwe. Kulingana na Kutoka, sura ya kumi na sita, Mungu aliwaambia Waisraeli waokote mana iliyotolewa kwa mwujiza siku sita kwa juma lakini si siku ya saba. Hii ilipaswa iwe ‘sabato takatifu kwa Yehova.’—Kut. 16:23.
Akionyesha kwamba sheria ya sabato ilikuwa mpya, Musa alisema hivi: “[Yehova] hakufanya agano hili na baba zetu, . . . Nawe utakumbuka ya kuwa wewe ulikuwa mtumwa katika nchi ya Misri, na ya kuwa [Yehova], Mungu wako, alikutoa huko kwa mkono wenye nguvu, na mkono ulionyoshwa; kwa sababu hiyo [Yehova], Mungu wako, alikuamuru uishike sabato.”—Kum. 5:3, 15.
Je! sabato ya kila juma ilipaswa iendelee kushikwa milele? Biblia haionyeshi hivyo, bali inaeleza kwamba Yesu Kristo alikuja ‘kutimiliza torati.’ (Mt. 5:17) Kwa hiyo tunasoma hivi: “Kwa mwili wake [Kristo] akaondoa kabisa . . . Torati ya amri zenye maagizo.”—Efe. 2:15, NW; tazama pia Warumi 6:14; 7:4, 6.
Wengine wanabisha kwamba maandiko haya yanatumika kwa “sheria ya sherehe” peke yake pamoja na sabato zake za pekee kama vile Kupitwa, sikukuu ya Pentekoste, Siku ya Upatanisho, mwaka wa saba na mwaka wa Yubile au wa 50. Wanashikilia kwamba Amri Kumi, pamoja na takwa lake la kushika sabato ya kila juma, zinatofautiana na “sheria ya sherehe” iliyomalizika. Wengine wanasema kwamba, kwa kuwa amri ya kushika sabato ya siku ya saba ilitolewa muda mfupi kabla ya torati ya Musa, amri hii haikumalizika pamoja na Torati hiyo. Je! Biblia inaunga mkono maoni haya?
Linalopendeza ni kwamba, wakati Yesu alipokuwa akizungumza juu ya Torati aliyokuja aitimize, alitia ndani amri ya sita na ya saba ya Amri Kumi, amri ambazo zilikataza kuua na kufanya uzinzi. (Mt. 5:17, 21, 22, 27, 28) Mtume Paulo alitia amri ya kumi ya amri hizi kama sehemu ya Torati ambayo Wakristo ‘wamefunguliwa katika hiyo,’ akisema hivi: “Singalitambua dhambi ila kwa sheria; kwa kuwa singalijua kutamani, kama torati isingalisema, Usitamani.” (Rum. 7:6, 7; linganisha Yakobo 2:10, 11.) Kama ilivyokuwa kwa sheria ya kushika sabato ya kila juma iliyopewa kabla ya Torati, ndivyo tohara ilivyokuwa; lakini Biblia inaonyesha kwamba tohara pia si ya lazima kwa Wakristo.—Mwa. 17:9-14; 1 Kor. 7:19.
Walakini, hii haimaanishi kwamba Wakristo hawako chini ya sheria yo yote ya adili. Maandiko ya Kikristo yanatia moyo kwa nguvu wazazi waheshimiwe na mambo kama vile ibada ya sanamu, uuaji, uzinzi, wizi na kutamani yaepukwe. (Efe. 4:28; 6:2; 1 Yohana 5:21; 1 Pet. 4:15; Ebr. 13:4; Kol. 3:5) Hata hivyo, hakuna mahali vitabu vya “Agano Jipya” vinakosema kwamba lazima Wakristo washike sabato ya kila juma.
Kwa sababu gani, basi, Yesu mwenyewe alishika sabato akatia wasikiaji wake moyo washike “amri” zote za Mungu? (Mt. 5:19) Kwa sababu, Yesu alipokuwa hai duniani, yeye na wanafunzi wake walikuwa chini ya agano la torati ya Musa kwa kuwa walikuwa Waisraeli. (Gal. 4:4) Torati iliondolewa kabisa, mahali pake pakachukuliwa na “agano jipya” baada ya kufa na kufufuliwa kwa Yesu, wakati ambapo alikuwa amekwisha toa “mwili” wake uwe dhabihu.—Luka 22:20; Ebr. 8:13.
Kwa sababu agano lote la Torati, kutia na amri ya kushika sabato ya kila juma, lilimalizwa na Yesu Kristo, mtume Paulo angeweza kuandikia Wakristo hivi: “Mtu asiwahukumu ninyi katika vyakula au vinywaji, au kwa sababu ya sikukuu au mwandamo wa mwezi, au sabato; mambo hayo ni kivuli cha mambo yajayo; bali mwili ni wa Kristo.” (Kol. 2:16, 17) Muda fulani kabla ya hapo, Paulo alionyesha masikitiko kwamba ‘alikuwa amejitaabisha bure’ kwa habari ya Wakristo fulani wa jimbo la Galatia, kwa maana wao walikuwa wangali ‘wanashika siku, na miezi, na nyakati, na miaka kwa uangalifu sana.’—Gal. 4:10, 11.
Hata hivyo, Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yana maana gani katika Waebrania 4:9 yanaposema hivi: “Imesalia raha ya sabato kwa watu wa Mungu”? Je! hii inaonyesha kwamba ni vibaya kwa Wakristo kufanya kazi siku ya saba ya juma?
Sivyo, kwa maana maneno yanayozunguka mstari huo yanaonyesha kwamba “raha ya sabato” (au “pumziko la sabato,” NW) yamaanisha kwamba lazima Wakristo waache nia ya kutoamini kama ile iliyozuia wingi wa Waisraeli waliotoka Misri wasiingie katika ‘raha ya Mungu’ (au ‘pumziko la Mungu, NW) katika Nchi ya Ahadi. (Ebr. 3:12, 18, 19; 4:3) Pia, lazima Wakristo wapumzike kutokana na “kazi” za kutoamini, hasa jitihada za kujionyesha kuwa wenye haki mbele za Mungu ati kwa kufanya tu matendo mema au ya fadhili. (Ebr. 4:10; Rum. 3:20) Kulingana na Biblia, kuwa na hali inayofaa mbele za Mungu kunapatikana kwa kumwamini Yesu Kristo tu. (Rum. 3:28) Lazima Wakristo washike pumziko kama hilo la sabato, si siku moja kwa juma, bali kila siku.
Bila shaka, hakuna ubaya kuchagua siku moja kati ya saba iwe ya kupumzika. Hii inaweza kuleta burudisho la kimwili linalohitajiwa, nafasi ya kujifunza Neno la Mungu na ya utendaji mwingine wenye kusisimua kiroho. Ni juu ya kila mtu kuamua atachagua siku gani kwa ajili ya makusudi ya pekee.
Lakini sasa mtu akitaka kufanya kazi siku ya saba ya juma, hakuna katazo la Maandiko la kutofanya hivyo. Kama vile mtume Paulo alivyosema: “Mtu mmoja afanya tofauti kati ya siku na siku; mwingine aona siku zote kuwa sawasawa. Kila mtu na athibitike katika akili zake mwenyewe.”—Rum. 14:5.