Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 6/1 kur. 13-19
  • Je! Wewe Ni Mtangazaji Mshikamanifu wa Ufalme wa Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Wewe Ni Mtangazaji Mshikamanifu wa Ufalme wa Mungu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Habari Zinazolingana
  • Bariki Jina Takatifu la Yehova!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Yehova Ni Mkuu Katika Upendo Mshikamanifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Ni Nani Atakayemsifu Mfalme?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Yehova Astahili Sifa ya Milele
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 6/1 kur. 13-19

Je! Wewe Ni Mtangazaji Mshikamanifu wa Ufalme wa Mungu?

“Kazi zako zote zitakusifu, Ee Yehova, na washikamanifu wako watakubariki. Watasema juu ya utukufu wa ufalme wako, na juu ya ukuu wako watanena.”—Zab. 145:10, 11, NW.

1. Yesu aliutangaza ufalme wa Mungu kadiri gani?

TANGU siku za Habili sikuzote Yehova Mungu amekuwa na watumishi fulani washikaminifu duniani wakimsifu. Mshikaminifu wa Yehova aliyekuwa mwenye kutokeza zaidi, Mwanawe mzaliwa pekee, Yesu Kristo, aliongoza katika kusema juu ya ukuu wa Yehova na ufalme wake utakaowafaidi wanadamu wote. Yesu alikuja akiwa Yeye Aliyetumwa, mzao aliyeahidiwa wa Yese na Daudi, Mfalme mkusudiwa, naye alifanya ufalme wa Mungu kuwa fundisho lake kuu la kidini. (Isa. 11:1, 10; Mt. 21:1-17) Yeye alileta habari njema za Ufalme. Kwa kuwa alikuwamo miongoni mwa watu, aliweza kuwaambia juu ya kukaribia kwa Ufalme huo kwa kuwa yeye aliuwakilisha, akiwa Mfalme-mkusudiwa, na kufundisha wafuasi wake wautafute Ufalme kwanza. (Luka 17:20, 21) Alipokuwa akifundisha wanafunzi wake kusali, alitilia mkazo kuja kwa Ufalme huo na kwamba ungelitakasa jina la Mungu, na mapenzi ya Mungu kufanywa duniani kama vile mbinguni.—Mt. 4:23; 6:9, 10, 33.

2. Aliwavutaje wengine wajitie katika suala hilo la ufalme wa Yehova?

2 Yesu aliwaalika wengine wajiunge naye katika kusema juu ya habari njema za Ufalme huo uliokuwa ukija. (Luka 9:1-6; 10:1-12) Wafuasi wa Yesu walifahamu kwamba kuwapo kwake akiwa mfalme kungekuwa katika wakati ujao, kama vile tunavyoweza kuona katika ulizo walilomwuliza katika Mathayo 24:3, NW: “Tuambie, Mambo haya yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo [au, parousia, Kigiriki] kwako na ya mwisho wa taratibu ya mambo? ” Naye Yesu aliendelea kuonyesha kwamba wakati wa kuwapo kwake ungekuwa wakati wa pekee wa kusema juu ya Ufalme, akionyesha kwamba jambo hilo lingefanywa duniani pote panapokaliwa na watu kuwa ushuhuda. Tunajua kwamba kuwapo kwa Yesu akiwa mfalme mwenye mamlaka, akitawala katikati ya adui zake, ni jambo la hakika tangu mwaka 1914, kwa sababu tumeona ile “ishara.”—Zab. 110:1; Ebr.10:12, 13; Mt. 24:14.

3. Paulo alishirikije kutangaza ufalme wa Mungu?

3 “Ili kuwajulisha wana wa watu matendo yake makuu na utukufu wa adhama ya ufalme wake. Ufalme wako ni ufalme wa nyakati zote zisizojulikana na utawala wako ni wa vizazi vyote vyenye kufuatana.” (Zab. 145:12, 13, NW)

Wanafunzi wa Yesu walikuwa wenye kutokeza sana katika kuwaelekeza Watu kwenye ufalme wa Mungu mikononi mwa Yesu Kristo. Mfano mzuri sana wa jambo hilo umeandikwa katika Matendo 28:23 30, 31, ambapo tunaambiwa juu ya Paulo akihubiri Ufalme alipokuwa gerezani huko Roma. Hapo mbeleni alikuwa amewaandikia Wakorintho kwamba Wakristo ni “mabalozi badala ya Kristo” na kwamba walikuwa wakiwasaidia watu ‘wapatanishwe na Mungu.’ (2 Kor. 5:20, NW ) Akiwa balozi Paulo alitazamiwa aseme mambo mazuri juu ya Ufalme na mfalme aliyemwakilisha, naye alifanya hivyo. Je! wewe umejitoa kwa utumishi kama huo wa ushikamanifu? Ikiwa ndivyo, je! unaendelea kusema juu ya Mfalme na Ufalme huo?

4. Ni mambo gani ambayo Paulo na Yohana walisema na kuandika tuwezayo kuwajulisha wengine tukiwa waabudu washikamanifu wa Yehova Mungu?

4 Paulo alipokuwa akieleza mafundisho ya Ufalme alikuwa akionyesha uhusiano wa Yesu Kristo na Yehova Mungu katika mpango wa Ufalme na kwamba Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote. “Kichwa cha Kristo ni Mungu.” (1 Kor. 11:3) Vilevile Paulo alieleza yatakayotokea mwishoni mwa utawala wa miaka 1,000 wa Kristo. (1 Kor. 15:24-28) Karibu na mwisho wa karne ya kwanza W.K., mtume mshikamanifu Yohana vile-vile aliandika maneno akielekeza mbele kwenye matendo makuu ya Yehova Mungu ya wakati ujao, kuonyesha utukufu wa ufalme wake. (Angalia Ufunuo 12:9, 10; 19:6; 20:10, 14; 21:3, 4, 22-24.) Hayo ni mambo ambayo sisi leo, tukiwa waabudu washikamanifu wa Yehova, tunaweza kuwajulisha wana wa watu, tukitilia mkazo umuhimu wa ufalme wa Mungu na yale utakayowafanyia wanadamu, yote yamletee Yehova sifa. Lazima Ufalme ufafanuliwe na uelezwe kwa wana wa watu, na kuwaonyesha kwamba ufalme wa Mungu ndio tumaini lao pekee. Utaendelea na kudumu wakati wote wa vizazi vyote vinavyokuja.a

5. (a) Mara nyingi watumishi wa Yehova wanaelekeana na nini? (b) Ujapokuwapo upinzani katika kipindi cha vita ya Ulimwengu ya Kwanza, ni jambo gani ambalo watu wa Yehova wameweza kufanya tangu wakati huo?

5 Chini ya herufi ya alfabeti samekh, herufi ya 15 katika alfabeti za Kiebrania, Zaburi 145:14 inaendelea kusema hivi:

“Yehova anawapa tegemezo wote wanaoanguka, naye anawainua wale wote walioinama chini.” (Zab. 145:14, NW)

Wale wanaomwabudu Yehova kwa ushikamanifu na kuutangaza ufalme wake mara nyingi wanakutana na upinzani na magumu kwa sababu ya ushikamanifu wao kwa Yehova. (Mwa. 3:15) Lakini ushuhuda wa nyakati zilizopita unaonyesha namna Yehova, kulingana na ukweli wa ahadi zake, alivyotoa msaada na kuwategemeza wale waliokuwa waabudu wake washikamanifu na kuwainua walipopatwa na upinzani. (Mwa. Sura ya 15; angalia pia mifano mingi katika kitabu cha Waamuzi.) Katika karne hii ya 20 na hata kufikia mwaka huu wa 1981 tumeona jinsi Yehova amewaokoa mabaki ya watiwa mafuta na wale “kondoo wengine” kutokana na uonevu wa Kibabeli. Kulikuwako mikazo mikubwa juu ya mabaki watiwa mafuta katika wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Walakini Yehova aliwainua kwa roho yake na neno la kweli. Muda mfupi baada ya hapo, katika kusanyiko lao la mwaka 1922 huko Cedar Point, Ohio, waliazimia kwa ushikamanifu kutangaza Mfalme na Ufalme. Yehova amekuwa akiwaongoza tangu wakati huo, hivi kwamba jina lake na ufalme wake vimepata kujulikana ulimwenguni pote.

6. Ni mpango gani wa chakula ambao Yehova anawafanyia watu wake?

6 “Kwako wewe macho ya wote yanaelekea kwa tumaini, nawe unawapa chakula chao katika majira yake.” (Zab. 145:15, NW)

Sana sana waabudu washikamanifu wa Yehova wanahitaji chakula chao cha kiroho katika siku hizi. Wao “wanaona uhitaji wao wa kiroho.” (Mt. 5:3, NW ) Wameutumaini mpango wa Yehova wa kutoa chakula cha kiroho chenye kufaa. (Mt. 24:45-47) Matumaini ya watu wa Mungu kuhusiana na jambo hili yanatoshelezwa kweli kweli nao wana tumaini hakika kwamba Yehova ataendelea kutoa chakula cha kiroho wanachohitaji kwa ukawaida, “kwa wakati wake.”

7. Yehova ni Mtoaji namna gani, na zaidi kuhusiana na mambo ya ibada?

7 Kupatana na hilo, Zaburi 145:16 inaendelea kusema:

“Unaufumbua mkono wako na kutosheleza tamaa ya kila kilicho hai.”

Yehova Mungu ndiye mtu peke yake katika ulimwengu wote ulio mkubwa mno ambaye hana kikomo akiwa Mtoaji. Yeye ndiye Baba wa kimbinguni na Mpaji-Uzima. Ukarimu wake na fadhili zake za upendo huonekana katika kazi zake zote za kuumba na katika mipango mizuri ambayo amefanya kwa ajili ya wanadamu pamoja na viumbe wengine wote walio duniani. Kwa kuwa alitupa uwezo wa kuabudu, kwa ukarimu Yehova amejifunua mwenyewe na makusudi yake kwa wanadamu, nao wale ambao wamejiweka wakf kwa Yehova Mungu wamepata kuona ukarimu wa Yehova zaidi na zaidi. Mambo hayo yote waliyoyaona ni yenye kutia moyo sana nasi twaweza kuwa na tumaini hakika kwamba Yehova ataendelea kuwapa watumishi wake roho yake naye hataacha kamwe kuwatosheleza kwa kuwapa kumbukumbu, uongozi na msaada wa kiroho, hata katika hizi siku za mwisho zenye hatari.—Zab. 119:129.

8. Yehova anaonyeshaje ushikamanifu?

8 Kwa sababu sisi tu washikamanifu kwa Yehova yeye naye ni mshikamanifu kwetu. Na kwa hiyo,

“Yehova ni mwenye haki katika njia zake zote na mshikamanifu katika kazi zake zote.” (Zab. 145:17, NW)

Tukiisha kuwa watumishi wa Yehova walio wakf na wategemezaji washikamanifu wa ufalme wake, sikuzote tunaweza kumtumaini Mungu. Yeye anashughulika na watumishi wake kwa haki na kwa huruma. Sifa zake za ajabu hazibadiliki. Kwa hiyo tukiisha chukua utumishi wa Yehova na ibada yake tumehakikishiwa kwamba yeye hatatuaibisha. Kweli kweli yeye ni “mshikamanifu kwa kazi zake zote.” Na kwa hiyo hapa tuna sababu nyingine nzuri ya kuwaambia wengine juu ya Yehova na sifa zake za ajabu na kuwaalika wajiunge nasi katika kuishi maisha yaliyo wakf ya kumsifu Yehova kwa ushikamanifu.—Linganisha Zaburi 107.

9. Imani inashiriki sehemu gani katika kumwita Yehova, nako huko kumwita Yehova kunapaswa kufanyweje?

9 Kupatana na hilo, twaweza kutangaza maneno haya yafuatayo katika kumsifu:

“Yehova yuko karibu na wale wote wanaomwita, na wale wote wanaomwita kwa ukweli.” (Zab. 145:18, NW)

Kumwita Yehova ni jambo la maana. Na ni lazima jambo hilo lifanywe katika imani ya kweli. (Rum. 10:10-15) Mtunga zaburi anatilia mkazo namna Yehova anavyokaribia wale wanaomwita ifaavyo, jambo linalotia ndani kuonyesha imani. (Ebr. 11:6) Nako huku kumwita Yehova si jambo linalofanywa sirini, bali kwa kweli ni tangazo la waziwazi mbele ya wanadamu kwamba sisi tunamwamini Yehova na kumtegemea yeye. Paulo anakazia uhitaji wa kutangaza “habari njema” za mambo mema na kuhubiri kwa faida ya wengine. Sauti ya kumsifu Yehova ya wale wanaomwita huongezeka kadiri hesabu inavyoongezeka ya wahubiri waaminifu wa “habari njema” wanapowaambia wengine zaidi habari za Yehova. Kwa kuwajulisha Yehova na utukufu wake na ukuu wake, pamoja na ufalme wake, wasifaji hao wanajenga imani katika watu hao ili kwamba wao nao, waweze kujiunga nao katika kuliitia jina la Yehova na kumkaribia. Njia ya wokovu i wazi kwa wote wanaotaka kuifikilia, hakuna ubaguzi kwa sababu ya kabila, rangi au taifa, wala wale wanaomwamini Yehova na kumwita kwa kweli hawatakatishwa tamaa. Yehova ni mwema kama nini kwa kuturuhusu tuwe na uhusiano naye na kuwa karibu naye! Na zaidi ndivyo ilivyo katika hizi siku za mwisho zenye hatari wakati inapokuwa wazi zaidi kuliko wakati mwingine wo wote kwamba ni jambo la lazima kumtegemea Yehova kabisa, Mungu wa wokovu.

10. Ni kwa sababu gani Yehova atafanya tamaa ya wale wanaomwogopa?

10 “Tamaa ya wale wanaomwogopa atafanya, na kilio chao cha kutaka msaada atasikia, naye atawaokoa.” (Zab. 145:19 NW)

Wale wanaomwogopa Yehova kweli kweli wanajiweka wakf kwake nayo tamaa yao ni kufanya mapenzi yake. Tuna kila sababu ya kumtumaini Yehova akiwa chanzo cha msaada na wokovu wetu, tunapojitahidi kufanya mapenzi yake. “Na huu ndio [uhakika] tulio nao kwake, ya kuwa, tukiomba kitu sawasawa na mapenzi yake, atusikia. Na kama tukijua kwamba atusikia, tuombacho chote, twajua kwamba [tutapata tulichomwomba].” (1 Yohana 5:14, 15) Tunajua kwamba, katika siku hizi, ni mapenzi ya Yehova kwamba tuzitangaze habari njema za Ufalme na kuendeleza ibada yake safi. Tamaa yetu yapaswa iwe kujulisha watu lile suala kuu linalohusiana na enzi kuu ya Yehova katika ulimwengu wote, ijapokuwa tunapata upinzani mkali tufanyapo hivyo. Hivyo nafasi inafunguliwa kwa watu wa namna zote waukubali ujumbe wa Yehova na kumwamini, wajifunze juu ya subira yake kwa wanadamu na tamaa yake ya kuona wanadamu wakipata kutubu na kujipatia wokovu.

11. Yehova anaitikiaje kilio cha watumishi wake?

11 Kwa hiyo ni tamaa yetu kubwa kuona kazi hii ya Ufalme ikitimizwa. Hatuifanyi peke yetu. Sisi ni watumishi wa Yehova nasi tunafanya kazi pamoja naye. Katika hizi “siku za mwisho” lazima tumwite atupe msaada, na wakati tutakapofikia upeo wa lile suala naye “Gogu wa Magogu” afanye shambulio lake, kama vile ilivyotabiriwa katika Ezekieli 38 na 39, itakuwa lazima tumtegemee Yehova na kumwita yeye ili atulinde na kutuokoa. Mfalme Daudi aliokolewa katika njia zenye kutokeza sana wakati adui zake walipokuwa wakimfuatia. Ilikuwa lazima Kristo Yesu atoe uhai wake kuhusiana na mapenzi ya Yehova, lakini Yehova alimfufua. Kwa hiyo Yehova anaweza kushinda mikazo yote au upinzani unaoweza kuletwa na adui za kweli, hata kuitikia kilio cha kutaka msaada cha watumishi wake ambao huenda wakaingia kwenye mauti na ambao huenda wakahitaji kuokolewa kupitia kwa ufufuo.

12. Ni kwa sababu gani sisi hatuhitaji kuogopa wakati waovu wanapoangamizwa?

12 Kwa hiyo, kweli hii inaendelea kwamba,

“Yehova huwalinda wale wote wanaompenda, bali waovu wote atawaangamiza.” (Zab. 145:20, NW)

Kwa kuwa tumefikia upeo wa uovu nayo “dhiki kubwa” i mbele yetu tu, ni baraka kuwa na maneno kama hayo yanayotuhakikishia kwamba Yehova huwalinda wale wote wanaompenda. (Mt. 24:21) Wakati umefika wa kuwaangamiza waovu wote, nao ni lazima wapewe onyo. Lakini watumishi wa Yehova kama kikundi wataipita “dhiki ile iliyo kuu” itakayoletwa juu ya waovu, na katika njia hiyo wauone wokovu watakaoletewa na Yehova. Yehova anawapenda kweli kweli wale walio washikamanifu kwake naye hatawasahau wakati wa hasira yake kuu atakayoileta juu ya waovu. Tuna mifano mingi ya Kimaandiko kuonyesha matendo makuu ya Yehova ya kuwahifadhi na kuwaokoa watu wake katika nyakati zile zile alizowaadhibu waovu. Kweli kweli, tunaungojea kwa hamu sana wakati waovu watakapoangamizwa nao wale wote wanaopinga ufalme wa Yehova kuondolewa.

13. (a) Yehova amewalindaje watumishi wake wa kisasa? (b) Yehova amewawekea nini akiba wale wanaompenda?

13 Katika kipindi hiki chote cha “siku za mwisho” watumishi wa Yehova wamekuwa wakimwita awape msaada nao wamemwonyesha upendo wao. Yehova amewahifadhi na kuwalinda watumishi wake kupitia katika magumu mengi, na zaidi wakati wa kipindi cha Vita ya Ulimwengu ya Pili wakati kazi yetu ilipopigwa marufuku katika sehemu nyingi mbalimbali za dunia nao maelfu mengi wakatiwa kwenye kambi za mateso na gerezani. Vikundi vyenye kutumia jeuri vilishambulia katika sehemu nyingi za dunia pia. Walakini kutangazwa kwa habari njema za Ufalme kulisonga mbele, naye Yehova aliwafadhili watumishi wake, akawapa ongezeko, akawafariji kwa kuongeza hesabu yao ulimwenguni pote. Ni kusudi la Yehova kwamba utawala wa Ufalme kupitia kwa Kristo Yesu uenee duniani pote. Kutakuwako raia za ufalme huo duniani kwa kuwa “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wataipita ile dhiki kuu, na baada ya hapo wale wengi watakaotoka makaburini kwa kufufuliwa watajiunga pamoja nao. Hivyo, kuangamizwa kwa waovu hakutawaletea watumishi wa Yehova msiba. Badala yake, Yehova ataitikia upendo alioonyeshwa na watumishi wake naye atawalinda na kuwaonyesha upendo wake, rehema na fadhili. Na katika upendo wake, amewawekea akiba “kondoo wengine” wake paradiso ya kidunia nzuri sana watakapoweza kujifurahisha uzima wa milele. (Luka 23:43 ZSB) Kumalizwa kwa suala kuu juu ya ufalme wa Yehova wa ulimwengu wote kutamaanisha baraka kwa wale wanaompenda Yehova nako kutatokeza nafasi ya kumthamini Yehova zaidi na zaidi kadiri miaka itakavyokuwa ikipita. Litakuwa jambo zuri kama nini kuishi wakati wa kutimizwa kwa mstari wa mwisho wa Zaburi ya 150 wakati ambapo “kila kitu kipumuacho” kitakapokuwa kikimsifu Yehova nao waovu wote watakapokuwa hawapo!—Mst. wa 6. 

14. Ni baraka gani kutoka kwa Yehova tunazoweza kusema juu yake?

14 Tazama nyuma, ukiweza na kuona baraka nyingi alizotupa Yehova. Uone namna alivyotushibisha kwa chakula kinono cha kiroho. Uthamini hata zaidi pendeleo zuri sana ambalo ametupa la kuwa watumishi wake sasa pamoja na mataraja yote mazuri sana ya wakati ujao. Kwa kuwa tunalo taraja la kuwa waokokaji wa Har–Magedoni, shangilia kwa kutazamia mbele kwenye wakati wa ufufuo pamoja na kazi nzuri sana ya wakati huo ya kuwaarifu na kuwaelimisha wale watakaokuja kutoka makaburini. Itakuwa lazima wengi wao wajifunze kwa mara ya kwanza juu ya Mfalme Mkuu Yehova. Itakuwa lazima wajue nani aliyewawezesha kuwa hai kwa mara nyingine tena. Ni nani atakayewaambia? Je! Kila mmoja wetu hangefurahia kufanya hivyo? Ndiyo, tunatazamia mbele kuweza kumsifu Yehova milele.

15. Tuna pendeleo gani kuhusiana na ufalme wa Mungu?

15 Lakini namna gani juu ya wakati uliopo sasa? Wewe unafanya nini juu ya suala kuu la ufalme wa Yehova? Je! Wewe u miongoni mwa washikamanifu wanaomtumaini Yehova na kusema juu ya utukufu wa ufalme wake siku baada ya siku? Kila mmoja wetu na awe mtegemezaji mshikamanifu wa ufalme wa Yehova kupitia kwa Mwanawe aliyetawazwa, Yesu Kristo, Daudi Mkuu Zaidi, na tuazimie sisi binafsi kwa moyo wetu wote kumsifu Yehova waziwazi kama alivyoazimia Mfalme Daudi aliyesema:

Sifa ya Yehova kinywa changu kitanena; nao wote wenye mwili na walibariki jina lake takatifu mpaka wakati usiojulikana, hata milele.”—Zab. 145:21, NW.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa kuwa Zaburi ya 145 ni zaburi ya alfabeti, kila mstari unaofuata ukianza kwa herufi inayofuata katika alfabeti za Kiebrania, tafsiri ya New World chapa ya 1971, ina maneno haya ya chini: “Mstari unaoanzia na herufi nun ya Kiebrania unakosekana baada ya mstari wa mem. Katika hati nyingine za Kiebrania mstari huo wa nun unasomwa hivi: ‘Yehova ni mwaminifu katika maneno yake yote, na mwenye kupenda kwa fadhili katika kazi zake zote.’ Hiyo inathibitishwa na LXXVgSy.”

[Picha katika ukurasa wa 17]

Walio washikamanifu wanasema juu ya utukufu wa ufalme wa Yehova

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki