Je! Wakumbuka?
Je! umefikiria kwa uangalifu mambo ambayo yamezungumzwa katika matoleo ya hivi karibuni ya “Mnara wa Mlinzi”? Ikiwa ndivyo, bila shaka unakumbuka yafuatayo:
● Ni kwa sababu gani uhakika wa kwamba “mkutano mkubwa” waonyeshwa wakimtumikia Mungu katika “na·osʹ,” au “patakatifu,” haumaanishi kwamba wanakwenda mbinguni?
Neno la Kigiriki “na·osʹ” laweza kumaanisha si “patakatifu” pa ndani pa hekalu peke yake, bali vilevile katika maana kubwa zaidi eneo lote au mpango wa hekalu. (Isa. 66:6, “Septuagint”; Mt. 27:5, 39, 40; Marko 15:29, 30; Yohana 2:19-21) Hapa ndipo katika ua wa kidunia wa hekalu la Mungu la kiroho unapoonekana ule “mkutano mkubwa” usiohesabika ukifanya “utumishi mtakatifu” wao. Huo “mkutano mkubwa” kama kikundi wanaokoka “ile dhiki iliyo kuu,” nayo ahadi inayotimizwa kwao hata sasa kupatana na uhusiano wao wa kiroho pamoja na Yehova ni: “Mungu atayafuta machozi yote katika macho yao.”—Ufu. 7:9-17.—2/1, kur. 11-18.
● Wazazi wasio na wenzi wanaweza kushindaje matatizo katika ulimwengu wa leo?
Wanaweza kufanya hivyo kwa kumtumaini Mungu na ahadi zake, kudumisha uhusiano mwema pamoja na Yehova, pamoja na kuendelea kujishughulisha sana katika kazi yenye kufaa. Wengine katika kundi la Kikristo wanaweza kusaidia kufurahisha mioyo yao kwa kuwapa msaada wenye upendo na wenye kufaa.—3/1, kur. 4-10.
● Je! “utumishi mtakatifu” unatia ndani utendaji wa maisha ya kila siku, kama vile kuangalia jamaa zetu, kuendeleza adili bora na mambo kama hayo?
Hapana. “Utumishi mtakatifu” unapasa yale yanayohusiana moja kwa moja na ibada yetu kwa Mungu. Unatia ndani kutoa ushuhuda kwa kawaida na vivi hivi, kushiriki ibada kwenye Jumba la Ufalme, kutunza mahali petu pa mikutano, utendaji wote unaohusiana na kutoa Biblia na vitabu vya kujifunza Biblia, pamoja na kujinyima ko kote tunakojinyima katika kuwatia moyo na kuwasaidia ndugu zetu, kiroho na kwa mambo ya kimwili, waendelee kuwa watendaji katika kazi ya Yehova.—2/1, kur. 21-26.
● Tuna ushuhuda gani ulio wazi kwamba tumekuwa tukiishi katika “siku za mwisho” tangu mwaka 1914?
“Ishara” aliyotoa Yesu katika Mathayo 24 na 25 imekuwa na utimizo wenye kusadikisha. Kazi ya duniani pote ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova imetimiza kusudi la Mungu la kuonya mataifa na kukusanya “mkutano mkubwa” utakaookoka na kuingia katika “taratibu mpya” ya Mungu. Kutangazwa huku kwa Ufalme kufikiapo upeo wake, “ndipo,” asema Yesu, “ule mwisho utakapokuja.”—3/15, ukur. 20.
● Kupunguka kwa maji ya Mto Frati kabla tu ya kuangushwa kwa Babeli kuna maana gani ya kiunabii?
Leo, “Babeli Mkuu,” milki ya ulimwenguni pote ya dini ya uongo, ‘anaketi juu ya maji mengi,’ yaani, “jamaa” wanaomwunga mkono. Lakini katika nyakati za kisasa kumekuwako na upungufu mkubwa katika hesabu ya washiriki pamoja na viongozi wa kidini na wafanyakazi, na zaidi katika Jumuiya ya Wakristo. Kutegemezwa huko kunakopungua kwa “Babeli Mkuu” kunaonyesha kwamba Yehova anakaribia kumtuma Koreshi Mkuu Zaidi, Yesu Kristo, atekeleze hukumu juu ya huyo “kahaba mkuu.” (Ufu. 17:1, 4, 15-17)—4/1, kur. 13-20.