“Mkutano Mkubwa” Wamtolea Mungu Utumishi Mtakatifu Wapi?
“Kwa sababu hii wako mbele ya kiti cha enzi cha Mungu nao wanamtolea utumishi wa kimungu mchana na usiku katika patakatifu pake.”—Ufu. 7:15, “The Emphasised Bible” ya Rotherham.
1. “Mkutano” kwa ujumla ukoje kwa habari ya dini za ulimwengu?
DINI inapungua. Kwa hiyo, hudhurio katika “utumishi wa kimungu” katika majengo ya makanisa, makathedro na mahekalu linapunguka. Sana sana jambo hilo linaonekana katika zile nchi zinazoitwa Jumuiya ya Wakristo. Watu wazushi, wasioamini ukweli wo wote, waaminio kwamba hatuwezi kupata habari zo zote za kweli kuhusu Mungu, wasioamini kuwako kwa Mungu na wapinga dini wanazidi kuongezeka. Hakuna jitihada zo zote za kufufua dini zitakazowarudisha. Ndivyo ilivyo kwa habari ya “mkutano” au umati wa watu kwa jumla.
2. Sisi tunapendezwa na “mkutano” gani, kama vile ulivyotangulia kuonwa na mwanamume mzee aliyekuwa amepelekwa uhamishoni kwenye kisiwa cha Patmo na serikali ya Rumi?
2 Hata hivyo, sisi tunapendezwa na mkutano ulio wa pekee, “mkutano mkubwa” uliotangulia kuonwa na mzee aliyekuwa amepelekwa uhamishoni katika kisiwa cha Patmo na serikali ya Milki ya Rumi. Baada ya yeye kuona katika njozi wale Waisraeli wa kiroho 144,000, yeye anaandika, akisema hivi: “Baada ya mambo hayo niliona, na tazama! mkutano mkubwa ambao hakuna ye yote ambaye angeweza kuuhesabu kutoka kila taifa, na wakiwa wa makabila yote, na jamaa, na lugha, wanasimama mbele ya kile kiti cha enzi, na akiwapo yule Mwana-Kondoo, wamevikwa mavazi marefu meupe, na wakiwa na matawi ya mitende mikononi mwao; nao wanalia kwa sauti kuu, wakisema ‘Wokovu na uhesabiwe huyo Mungu wetu aketiye katika kile kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo.’”—Ufu. 7:9, 10, The Emphatic Diaglott, ya Benjamin Wilson.
3. Ni kwa sababu gani hao wa huo ‘‘mkutano mkubwa” wanaonekana wakiwa wamevalia ifaavyo, na ni kwa sababu gani watu wengi hufikiri kwamba wako mbinguni?
3 Lo! ni cheo chenye heshima kama nini wanachosemekana kuwa nacho, na ni sura yenye kuheshimika kama nini wanayosemekana kuwa nayo hao wa “mkutano mkubwa”! Hata katika nyakati za kisasa ni jambo lenye kufaa mtu asimame anapokuwa mbele ya mfalme ambaye ameketi juu ya kiti chake cha enzi. Walakini hapa, hao wa “mkutano mkubwa” wanaonekana wakisimama mbele ya kiti cha enzi cha Mungu mwenyewe. Na vilevile, ili hali yao ilingane na wakati huo, wamevalia mavazi marefu meupe. Je! wanaonekana wakiwa wamesimama katika kusanyiko lililofanyiwa nje ya nyumba? Hapana, kwa kuwa Ufunuo 7:15 (tafsiri ya Emphatic Diaglott) unasema kwamba “wao . . . wanamtumikia waziwazi mchana na usiku katika hekalu [na·osʹ katika maandishi ya Kigiriki cha asili].” Basi, hiyo yamaanisha kwamba hao wa huu “mkutano mkubwa” wanakwenda mbinguni mwishowe alipo yule Mungu wanaomhesabia “wokovu”? Jibu linalotolewa kwa kawaida ni Ndiyo! Kwa sababu gani? Kwa sababu inasemekana kuwa ni “katika hekalu lake” (ED), au, ni “katika patakatifu pake” (Rotherham), wanamomtolea utumishi wa waziwazi au “utumishi wa kimungu.”
4. Ulizo lahusu neno gani la Kigiriki cha asili, nalo lilitumiwa kuhusiana na jambo gani katika Yohana 2:19-21?
4 Walakini je! maoni hayo yanapatana na mambo yote ya hakika yanayotolewa katika kitabu cha mwisho cha Biblia, Ufunuo? Vilevile, kwa habari ya wale wote wanaojihesabu kuwa sehemu ya huo “mkutano mkubwa” unaofanyizwa sasa, je! wao wanatazamia kwenda mbinguni na kuwa viumbe vya kiroho kama malaika? Wao watakuambia Hasha! nao hawajifikirii kuwa wamezaliwa kwa roho ya Mungu na kuwa na tumaini kama hilo la kimbinguni. Ulizo linahusu neno hilo la Kigiriki cha asili ambalo latafsiriwa katika njia mbalimbali kama “hema,” “hekalu” na “patakatifu.” Kwa mfano, masimulizi ya Biblia kuhusu mahali ambapo kutoka hapo Yesu Kristo aliwafukuza wabadili fedha na wafanya-biashara katika hekalu la Herode, neno la Kigiriki cha asili lililotumiwa ni na·osʹ. Hapo twasoma hivi: “Yesu akajibu, ‘Haribuni patakatifu [na·osʹ] hapa, na katika siku tatu nitapainua’. Wayahudi wakajibu, ‘Imechukua miaka arobaini na sita kujenga patakatifu [na·osʹ] hapa: je! wewe utapainua kwa siku tatu? ’ Lakini alikuwa akisema juu ya patakatifu [na·osʹ] palipokuwa mwili wake.” (Yohana 2:19-21, The Jerusalem Bible) Wayahudi hao walimaanisha nini kwa kusema “patakatifu”?
5. (a) Ni mjengo gani ambao Wayahudi hawangekuwa wakimaanisha waliposema kwamba ulichukua miaka 46 kujengwa? (b) Ni lazima neno na·osʹ katika Isaya 66:6 lihusu nini katika tafsiri ya Septuagint ya Kigiriki?
5 Bila shaka hawakumaanisha patakatifu pa ndani zaidi mlimokuwa ile sebule, vyumba vya Patakatifu na Patakatifu Zaidi. Walimaanisha mjengo wa hekalu kwa ujumla, kutia na nyua zake, ua mmojawapo ambamo hao wabadili fedha na wafanya-biashara walikuwa wakifanyia biashara yao. Hekalu lote la Herode liliharibiwa na Warumi katika mwaka 70 W.K. Tofauti na hekalu la mapema la Sulemani lililoharibiwa katika mwaka wa 607 K.W.K., hekalu la Herode halikujengwa tena hata kidogo. Kwa habari ya hekalu katika Yerusalemu, Isaya 66:6 husema hivi, kwa maana ya kiunabii: “Mngurumo huo kutoka mjini, makelele hayo katika hekalu ‘[na·osʹ katika tafsiri ya Kigiriki ya Septuagint], ni sauti ya BWANA akilipa kisasi juu ya adui zake.” (The New English Bible) “Sikiliza! makelele kutoka mjini, Sikiliza! yanakuja kutoka hekaluni [na·osʹ], Sikiliza! BWANA awapatiliza adui Zake.” (The Jewish Publication Society of America) Kwa wazi sana, hekalu, patakatifu, au na·osʹ, hapamaanishi patakatifu pa ndani zaidi tu, bali sehemu yote ya hekalu pamoja na majengo yake yote.
6. Katika usiku wa mwaka 33 W.K., ni ushahidi gani wa uongo kuhusu Yesu na na·osʹ (hekalu) la Yerusalemu waliotoa Wayahudi?
6 Katika usiku wa Sikukuu ya Kupitwa, Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., Wayahudi fulani walitoa ushuhuda mbele ya wakuu wa makuhani na mbele ya Sanhedrin, walakini ikiwa mashahidi hao waliishi kufikia mwaka 70 W.K. walihakikishiwa kwamba ushuhuda wao waliotoa juu ya Yesu Kristo katika usiku huo wenye msiba ulikuwa wa uongo. Walishuhudia hivi: “Sisi tulimsikia akisema, Mimi nitalivunja hekalu [na·osʹ] hili lililofanyika kwa mikono, na katika siku tatu nitajenga jingine Iisilofanyika kwa mikono.” (Marko 14: 58) Kumfisha Yesu hakukuzuia hekalu lao lisiharibiwe kabisa katika mwaka 70 W.K.
7. (a) Wayahudi walimdhihakije Yesu aliyekuwa ametundikwa huko Kalvari? (b) Mwishowe Yuda msaliti aliitupa wapi ile fedha aliyokuwa amehongwa nayo?
7 Baadaye, katika siku iyo hiyo, wakati Wayahudi wenye uadui walipomwona Yesu akiwa ametundikwa juu ya mti nje ya Yerusalemu, huenda wakawa waliona kwamba alikuwa amezuiwa asitimize yale waliyofikiria kwa uongo kwamba ndiyo aliyokuwa ameyasema. “Nao waliokuwa wakipita njiani wakamtukana, wakitikisa-tikisa vichwa vyao, wakisema, Ewe mwenye kulivunja hekalu [na·osʹ] na kulijenga kwa siku tatu, jiokoe nafsi yako; ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, shuka [mtini wa mateso]”! (Mt. 27:39, 40; Marko 15:29, 30) Lakini kabla ya kutundikwa kwa Yesu, yule mwanafunzi aliyekuwa amemsaliti kwa adui zake wenye kutaka sana kuona damu ikimwagwa kwa vipande 30 vya fedha alijaribu kujiondolea hatia. Huyo alikuwa Yuda Iskariote, mmoja wa wale mitume 12. Alijaribu kurudisha fedha alizohongwa kwazo, lakini waliomhonga walikataa kuzichukua. Aliposhindwa kujiondolea hatia kwa njia hiyo, msaliti huyo alifanyaje? Mathayo 27:5 huripoti hivi: “Yuda aliitupa fedha hiyo kwenye patakatifu [na·osʹ] na kuiacha; kisha akaondoka na kujinyonga.” (Good News Bible; The Jerusalem Bible; Literal Translation of the Bible ya Young) Ni kwa sababu gani tafsiri nyinginezo za Biblia za kisasa hutafsiri na·osʹ kama “hekalu”?
8. Kwa wazi, ni kwa sababu gani wafasiri wengi wa Biblia walitumia hapa neno “hekalu” badala ya “patakatifu”?
8 Kwa wazi sababu ni kwamba walifahamu kwamba neno hilo la Kigiriki halikumaanisha hapa patakatifu pa ndani zaidi pakiwa na ukumbi wake, Patakatifu na Patakatifu Zaidi, ambamo kuhani mkuu alileta damu ya dhabihu kila mwaka katika Siku ya Upatanisho. Lilimaanisha hekalu pamoja na nyua zake zote.
9. (a) Kwa hiyo, je! ni lazima ule “mkutano mkubwa” uwe mbinguni ili wamtumikie Mungu katika na·osʹ (hekalu) lake? (b) Kulingana na Ufunuo 3:12, je! na·osʹ (hekalu) laweza kuwa na maana ndogo?
9 Hivyo ule “mkutano mkubwa” waweza kusemekana kuwa umo katika “hekalu,” au na·osʹ , la Mungu na hata hivyo usiwe katika mbingu wakiwa viumbe vya roho pamoja na wale Waisraeli wa kiroho 144,000 washiriki wa lile “kundi dogo” la Mungu. (Ufu. 7:1-9, 15; Luka 12:32) Na·osʹ laweza vilevile kuwa na maana ndogo, kwa kuwa Yesu Kristo alipeleka ujumbe kwa kundi la karne ya kwanza katika Filadelfia, Asia Ndogo, akasema: “Kwa habari ya yeye ashindaye, mimi nitamfanya yeye kuwa nguzo katika hekalu [na·osʹ] la Mungu wangu; yeye atakuwa salama, naye hatatoka nje tena; mimi nitaandika juu yake Jina la Mungu wangu, naye atakuwa raia katika mji wa Mungu wangu—ule Yerusalemu Mpya, unaoshuka kutoka mbinguni kutoka kwa Mungu wangu; naye atakuwa na Jina langu jipya limeandikwa juu yake.”—Ufu. 3:12, The Living Bible.
10. Ni katika njia zipi Ufunuo 7:9-17 waonyesha kwamba ule “mkutano mkubwa” unashindwa kuwa katika kusanyiko katika na·osʹ (hekalu) hilo lenye maana ndogo?
10 Kuandikwa kama huko juu ya washiriki wa huo “mkutano mkubwa” hata hakutajwi katika Ufunuo 7:9-17, wala hawasemekani kuwa wanafanywa kuwa “nguzo” katika hekalu la Mungu. Wale wanaofanywa kuwa “nguzo” za mfano ni wale Waisraeli wa kiroho 144,000 wa makabila 12.
11, 12. (a) Kikundi hicho chenye hesabu kamili cha Waisraeli wa kiroho kinatofautianaje na ule “mkutano mkubwa” kwa habari ya majina? (b) Kulingana na Ufunuo 14:1-5, jina la ule mji ushukao kutoka kwa Mungu linawafaaje wale 144,000?
11 Tofauti na huo “mkutano mkubwa” usio na hesabu, kikundi hiki chenye hesabu cha Waisraeli wa kiroho kina jina la Yesu na la Baba yake yakiwa yameandikwa juu yao. Vilevile wana jina la mji wa Mungu likiwa limeandikwa juu yao, ule Yerusalemu Mpya, ushukao kutoka mbinguni kutoka kwa Mungu. Kama vile Mlima Sayuni ulivyoshirikishwa na Yerusalemu, vivyo hivyo Mlima Sayuni wa kiroho unashirikishwa na huu Yerusalemu Mpya wa kimbinguni. Kupatana na jambo hilo, mtume Yohana aliona njozi ya pili ya hao Waisraeli wa kiroho 144,000, naye akaandika hivi:
12 “Tazama, huyo Mwana-Kondoo [Yesu Kristo] amesimama juu ya mlima Sayuni, na watu mia na arobaini na nne elfu pamoja naye, wenye jina lake na jina la Baba yake limeandikwa katika vipaji vya nyuso zao. . . . [Nao wanaimba] wimbo mpya mbele ya kile kiti cha enzi . . . wala hapana mtu aliyeweza kujifunza wimbo ule, ila wale mia na arobaini na nne elfu, walionunuliwa katika nchi. . . . Hawa wamenunuliwa katika wanadamu, malimbuko kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo.”—Ufu. 14:1-5.
13. (a) Je! hao wa ule “mkutano mkubwa” ni kama wale 144,000 katika kusimama juu ya Mlima Sayuni wa kimbinguni? (b) Je! wao “wamenunuliwa katika wanadamu, malimbuko kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo”?
13 Je! maelezo hayo yanahusu vilevile na ule “mkutano mkubwa” wa mataifa yote wa Ufunuo 7:9-17? Hapana, kwa kuwa hakuna mahali po pote wanaposemekana wakisimama katika Mlima Sayuni wa kimbinguni. (Ebr. 12:22) Wao hawatiwi ndani ya wale waimbaji wa kwanza wa ule “wimbo mpya.” Wao hawasemekani kuwa “wamenunuliwa katika wanadamu, malimbuko kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo.” Kwa hiyo, hao wa “mkutano mkubwa” wanatazamia kubaki duniani milele na kushiriki kuileta katika hali ya Paradiso. Wao si wa jamii ile ya 144,000 ‘walionunuliwa’ iliyoanza kufanyika katika siku ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K., siku ambayo katika hiyo kuhani mkuu wa Kiyahudi alipeleka “malimbuko” au mazao ya kwanza ya mavuno ya ngano kwenye hekalu katika Yerusalemu. Katika siku hiyo, Yesu Kristo, Kuhani Mkuu Zaidi, alimtolea Mungu mbinguni bei ya ukombozi kwa njia ya damu yake iliyomwagwa, naye Mungu alimtumia kuwa njia ya kumwagia roho takatifu katika siku iyo hiyo wale wanafunzi 120 waliokuwa wakingojea na baadaye Wayahudi wapatao 3,000 pamoja na wafuasi wa Mataifa wa dini ya Kiyahudi waliotubu na kubatizwa siku hiyo.—Matendo, sura ya 2; Yoeli 2:28, 29; Ebr. 4:15, 16.
“MUHURI YA MUNGU ALIYE HAI” YATOFAUTISHA
14. Ijapokuwa wote, wale 144,000 na ule “mkutano mkubwa” wameletwa katika hali ya kuwa wenye kuokolewa, muhuri fulani inawatofautishaje?
14 Jambo moja linalostahili kuangaliwa ambalo hutofautisha wale ‘walionunuliwa’ 144,000 na ule “mkutano mkubwa” wenye kuvalia mavazi marefu meupe ni kile kinachoitwa “muhuri ya Mungu aliye hai.” Ufunuo sura ya 7, ambayo hutoa habari juu ya hao Waisraeli wa kiroho 144,000 pamoja na ule “mkutano mkubwa,” huonyesha kwamba ni hao 144,000 tu wanaotiwa muhuri “juu ya vipaji vya nyuso zao” kwa “muhuri” kuwa wao ni “watumwa wa Mungu wetu.” Jambo hilo laonyesha kwamba kuna tofauti vilevile katika vyeo vyao walivyowekwa katika mpango wa mwisho wa Mungu, kwa habari ya mbingu na dunia. Inakuwa hivyo ijapokuwa wote wanaletwa katika hali ya kuokolewa, kwa sababu wale wa huo “mkutano mkubwa,” pamoja na wale 144,000 wanamkubali Yesu Kristo kuwa “Mwana-Kondoo wa Mungu aichukuaye dhambi ya ulimwengu.” (Yohana 1:29, 36; 1 Yohana 2:1, 2) Katika njia hiyo wale wa huo “mkutano mkubwa . . . wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” (Ufu. 7:9, 14) Jambo hilo linawapa haki ya kumwabudu Yehova katika hekalu lake la kiroho, ambalo lilifananishwa na mjengo wote wa hekalu katika Yerusalemu wa kale.—Yohana 4:21-24.
15. Ni wakati wa kufanya kilio gani cha ulinzi unaokaribia, nao ni upepo gani wenye kuumiza ambao bado unazuiwa, na kwa sababu gani?
15 Wakati unakaribia ambapo watu wote watakuwa ni kama kwamba wanayaambia hivi matengenezo yaliyoinuka sana ya jamii ya kidunia ambayo yamejiimarisha kwa muda mrefu sana: “Tuangukieni, tusitirini, mbele za uso wake yeye aketiye juu ya kiti cha enzi, na hasira ya Mwana-Kondoo. Kwa maana siku iliyo kuu, ya hasira yao, imekuja; naye ni nani awezaye kusimama?” (Ufu. 6:16, 17) Upepo mkali wa uharibifu unakaribia. Hilo laonyeshwa na maneno yanayofuata ya njozi hiyo: “Baada ya hayo [mimi mtume Yohana] nikaona malaika wanne wamesimama katika pembe nne za nchi, wakizizuia pepo nne za nchi, upepo usivume juu ya nchi, wala juu ya bahari, wala juu ya mti wo wote. Nikaona malaika mwingine [wa tano], akipanda kutoka maawio ya jua, mwenye muhuri ya Mungu aliye hai; akawapigia kelele kwa sauti kuu wale malaika wanne waliopewa kudhuru nchi na bahari, akisema, Msiidhuru nchi, wala bahari, wala miti, hata tutakapokwisha kuwatia muhuri watumwa wa Mungu wetu juu ya vipaji vya nyuso zao.”—Ufu. 7:1-4.
16. Ni kwa sababu gani “mkutano mkubwa,” ujapokuwa hautiwi muhuri, hauumizwi na ule upepo mkali unaoachiliwa kama wonyesho wa hasira ya Mwana-Kondoo?
16 Hakuna ye yote wa ule “mkutano mkubwa” anayeripotiwa kuwa akitiwa muhuri kwa hiyo “muhuri ya Mungu aliye hai,” ni wale tu “watumwa wa Mungu wetu” 144,000. Ni kwa sababu gani, basi, hakuna ye yote wa huo “mkutano mkubwa” anayeumizwa na uharibifu huo unaotokea baada ya kuachiliwa kwa hizo “pepo nne” katika zile pembe nne za dunia? Na vilevile, inakuwaje kwamba hao wa huo “mkutano mkubwa” usiotiwa muhuri hawaioni “hasira ya Mwana-Kondoo” baada ya hao 144,000 kumaliza kutiwa muhuri? Aha! ni kwa sababu “wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” (Ufu. 7:14) Sasa wanakubali faida za dhabihu yake ya ukombozi na kutafuta kuwa safi kwa kuoshwa kutokana na dhambi zao katika damu yake yenye kufunika dhambi. Hawatafuti ulinzi wao katika matengenezo yenye fahari na yenye kujiimarisha sana ya wanadamu wanyonge, bali wanamtegemea Yehova Mungu na Mwanawe Yesu Kristo aliye mfano wa mwana-kondoo. Kwa hiyo wakiwa na shukrani nyingi wanalia kwa sauti kuu hivi: “Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo.”—Ufu. 7:9, 10.
17. Kwa habari ya Utawala wa Ulimwengu Wote, “mkutano mkubwa” ni mshikamanifu kwa nani, nao unamtolea nani utumishi mtakatifu, ukiwa wapi?
17 Mpaka kufikia wakati wa kumalizwa kwa suala lenye maana sana la Utawala wa Ulimwengu Wote wao ni washikamanifu kwa Yehova na ufalme wake kupitia kwa Mwana-Kondoo, Kristo. “Hiyo ndiyo sababu wako mbele ya kiti cha enzi cha Mungu; nao wanamtolea utumishi mtakatifu [la·treuʹein, kiarifa cha Kigiriki] mchana na usiku katika hekalu [na·osʹ] lake.” (Ufu. 7:15, NW) Humo wanashirikiana na mabaki yaliyosalia ya wale “watumwa wa Mungu wetu” 144,000 waliotiwa muhuri.
‘KUTOKA KATIKA DHIKI ILE ILIYO KUU’
18. Hao wa huo “mkutano mkubwa” wanasemekana kuwa wanatoka katika kitu gani, na ni ulizo gani linalotokea?
18 “Wokovu” wanaopata hao wa ule “mkutano mkubwa” unatia ndani kutoka katika kile kinachotabiriwa katika Ufunuo 7:14: “Hao ndio wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu, nao wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” Maandishi ya Kigiriki cha asili yanasomeka hivi neno kwa neno: “Kutoka ile dhiki iliyo kuu.” (Tafsiri ya Kingdom Interlinear) Sasa, basi, hii ‘dhiki kuu’ ni nini? Badala ya neno “dhiki,” tafsiri nyingine za Biblia husema: “Taabu,”a “mateso,”b “udhalimu,”c “uonevu,”d na “hatari.”e Lakini Biblia nyingine nyingi (za Kiingereza) husomeka “dhiki.”
19, 20. (a) Ni nini maana ya neno la Kilatini ambalo katika hilo neno “dhiki” linatafsiriwa? (b) Maelezo ya Robertson yasema nini juu ya neno hilo katika Ufunuo 7:14, nao unabii wa Yesu ulilitumiaje neno hilo?
19 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa katika njia hizo mbalimbali ni thlipʹsis. Laonyesha jambo baya ambalo limempata mtu. Neno la Kiingereza “tribulation (dhiki)” latokana na neno la Kilatini tribulum, linalomaanisha “ubao wa kupuria (kitelezeo).”
20 Kuhusu usemi “dhiki ile iliyo kuu” kama vile unavyotumiwa katika Ufunuo 7: 14, Robertson katika kitabu chake Word Pictures in the New Testament (Kitabu cha 6, kurasa 352, 353) anaeleza hivi: “Kwa wazi hatari kubwa imekusudiwa (Mt. 13:19 [maelezo ya chini]; 24:21; Marko 13:19), ijapokuwa mfuatano wote huo huenda ukawa akilini na hivyo huenda hukumu ya mwisho ikawa inatarajiwa.” Mathayo 24:21 huelekeza kwanza kabisa kwenye uharibifu wa Yerusalemu wa kale katika mwaka 70 W.K. nalo lasomeka hivi (HNWW): “Maana wakati huo kutakuwa na dhiki [thlipʹsis] kubwa, ambayo haijapata kuwako tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka leo, wala haitapata kutokea tena.” Marko 13:19 husomeka hivi (HNWW): “Maana wakati huo kutakuwa na dhiki [thlipʹsis] ya aina ambayo haijatokea tangu Mungu alipoumba ulimwengu mpaka leo, wala haitatokea tena.” Dhiki hii ingekuwa sehemu ya “ishara . . . itakayoonyesha kwamba mambo haya karibu yatimizwe.” (Marko 13:4, HNWW) “Mambo haya” yote yangetia ndani kumaliza kutiwa muhuri kwa wale Waisraeli wa kiroho 144,000.—Ufu. 7:1-8.
21. Ni neno gani la Kigiriki lenye maana linalotumiwa katika Septuagint katika kutafsiri Danieli 12:1, naye Mikaeli ni nani?
21 Tafsiri ya Kigiriki ya Septuagint ya Maandiko ya Kiebrania hutumia neno hilo thlipʹsis inapotaja tukio ilo hilo katika Danieli 12:1 na kusema: “Na katika wakati huo Mikaeli yule mwana wa kifalme mkuu ambaye amekuwa juu ya watoto wa watu wako, atasimama, na kutakuwa na wakati wa dhiki [thlipʹsis]—dhiki [thlipʹsis] ya namna ambayo haijapata kuwako tangu kulipokuwapo taifa duniani hata mpaka wakati huu.” (The Septuagint Bible, ya Charles Thomson; The Septuagint Version, chapa ya Samuel Bagster and Sons Limited) Kulingana na Ufunuo 12:7, Mikaeli ni Yesu Kristo aliyetukuzwa.
22. Je! “dhiki” hiyo ni wonyesho wa hasira ya Mungu juu ya ule “mkutano mkubwa,” nako kutoka kwao ndani yake kwamaanisha nini?
22 Kutokana na hayo yote yaliyotangulia kutajwa inaweza kuonekana kwamba hiyo ‘dhiki iliyo kuu’ si wonyesho wa ghadhabu au hasira ya Mungu juu ya ule “mkutano mkubwa,” kwa kusudi la kuwaadibu na kuwatakasa na uhusiano wao na taratibu hii mbovu ya mambo. ‘Dhiki kubwa’ hiyo iliyotabiriwa ni taabu ya ulimwengu, ile “dhiki” ya mwisho inayokuja juu ya ulimwengu huu uliohukumiwa maangamizi. Ndio ule upepo wa mfano uliozuiwa na wale malaika wanne katika zile pembe nne za nchi mpaka wale wa mwisho wa wale Waisraeli wa kiroho 144,000 watiwe muhuri wakiwa mali ya Yehova Mungu ‘iliyonunuliwa,’ wale “watumwa wa Mungu wetu” wasioweza kuwa wa mwingine. “Mkutano mkubwa” wanatoka katika hiyo ‘dhiki iliyo kuu’ ikiwa na maana kwamba wanaiokoka.
23. “Mkutano mkubwa” wenye kuokoka utafanyiza mwanzo wa kitu gani kipya, ukiwa na matazamio gani mbele yao?
23 Litakuwa pendeleo la kupendeza kama nini wakati huo kwa huo “mkutano mkubwa” uliookolewa kuendelea ‘kumtolea [Mungu] utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu lake,’ katika nyua za kidunia za ule mpango wa hekalu lake kuu! Zile “mbingu mpya” zitakuwa zimekwisha wekwa juu yao, nao watakuwa mwanzo wa “dunia mpya” ambayo katika hiyo haki itakaa kwa wakati usio na mwisho. (2 Pet 3:13, NW) Paradiso mpya itakuwa imeanza kuchanua juu ya dunia iliyotakaswa, wala Ibilisi ye yote hatakuwako akijaribu kuwashawishi wageukie udhalimu wa namna yo yote. Ni taraja lenye furaha kweli kweli ambalo limewekwa mbele ya huo “mkutano mkubwa” utakaoiokoka ile “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye Har–Magedoni!—Ufu. 16:13-16.
[Maelezo ya Chini]
a The Emphatic Diaglott.
b Zaire Swahili Bible.
c Habari Njema kwa Watu Wote.
d The New Testament in Modern English ya Philllps.
e The New English Bible.
[Sanduku katika ukurasa wa 13]
Neno la Kigiriki na·osʹ mara nyingi humaanisha patakatifu pa ndani zaidi mbinguni kwenyewe
● WALAKINI ni hekalu (na·osʹ) lote ambalo lilichukua miaka 46 kujengwa
● Ni hekalu (na·osʹ) lote lililoharibiwa kama hukumu kutoka kwa Mungu
● Ni ndani ya sehemu ya nje ya hekalu (na·osʹ) ndimo Yuda alitupa vile vipande 30 vya fedha
● HIVYO inapatana kwamba ule “mkutano mkubwa” wamtumikia Mungu katika ua wa kidunia wa lile hekalu la kiroho
[Sanduku katika ukurasa wa 15]
Wale watiwa mafuta 144,000 ndio peke yao wanao—
● fanywa kuwa nguzo katika hekalu la Mungu
● fanyiza “kundi dogo” lenye hesabu kamili
● andikwa juu yao jina la Baba, la Mwana-Kondoo na la Yerusalemu Mpya
● simama juu ya Mlima Sayuni
● “nunuliwa katika nchi . . . katika wanadamu”
● fanywa kuwa “malimbuko kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo”
● tiwa muhuri kwa ile “muhuri ya Mungu aliye hai”
[Sanduku katika ukurasa wa 16]
Ule “mkutano mkubwa” unapewa pendeleo la—
● kuyakimbia matengenezo ya jamii ya kidunia yaliyohukumiwa maangamizi
● kuuona wokovu kupitia kwa ukombozi wa Mwana-Kondoo
● kusimama wakiwa na kibali mbele ya kiti cha enzi cha Mungu
● kumtolea Mungu utumishi mtakatifu katika hekalu lake la kiroho
● kuiokoka ile “dhiki” ya mwisho inayokuja juu ya ulimwengu huu uliohukumiwa kuwa na hatia
● kuwa msingi wa jamii ya “dunia mpya” iliyo safi
● kushiriki milele dunia ya Paradiso
[Picha katika ukurasa wa 14]
Mpango wa Hekalu la Yehova
PATAKATIFU PA NDANI ZAIDI
“MKUTANO MKUBWA” WAKIWA NA MATAWI YA MITENDE
MADHABAHU IKIWA NA MAKUHANI WAKITUMIKIA