Zaburi
Kusudi la Ufalme wa Mungu Lashinda
MUNGU ana kusudi. Mataifa wana kusudi. Makusudi haya mawili yanatofautiana sana kwa sababu, kwa maneno ya Mungu, “kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi; kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu.” Na ndivyo kusudi la Mungu kwa wanadamu lilivyo bora zaidi.—Isa. 55:9.
Kupingana huku kwa makusudi kunaelezwa na mtunga zaburi, aliyeandika hivi: “Mbona mataifa wanafanya ghasia, na makabila wanatafakari ubatili? ” Kusudi lao ni la bure, la ubatili, halina budi kushindwa, hata hivyo wanaendelea kulifuatia. Hawawezi kuleta amani na upatano duniani. Hata hivyo, wanaendelea na matendo yao kwa kadiri ya kuupinga utawala wa Mungu, kwa kuwa, asema mtunga zaburi: “Wafalme wa dunia wanajipanga, na wakuu wanafanya shauri pamoja, juu ya [Yehova], na juu ya masihi wake.”—Zab. 1:1, 2.
MFALME WA MUNGU
Masihi huyo ni Yesu Kristo, mfalme wa Mungu. Mtume aliitumia Zaburi 2:1, 2 juu ya Yesu. (Matendo 2:24-27) Mataifa wangeweza kumkubali, walakini wanaona kwamba hawangetaka kujitia chini ya matakwa na vizuizi ambavyo wangewekewa na Yehova na mfalme wake mwekwa, na kwa hiyo wanasema hivi: “Na tuvipasue vifungo vyao, na kuzitupia mbali nasi kamba zao.”—Zab. 2:3.
Je! jitihada hizo za mataifa za kuendelea na enzi kuu zao wenyewe na namna ya utawala wao wenyewe zinampa Mungu wasiwasi? Yeye anasema hivi: “Yeye aketiye mbinguni anacheka, [Yehova] anawafanyia dhihaka.” Yeye anaendelea na kusudi lake kama kwamba watawala hao si kitu. Hata hivyo, yeye hafurahishwi na maoni yao, kwa kuwa, wanapofanya jitihada za kulipinga kusudi lake, “ndipo atakaposema nao kwa hasira [kama sauti ya radi yenye mngurumo wenye kuogopesha] yake, na kuwafadhaisha kwa ghadhabu [kama pigo kuu la umeme] yake.” Analotangaza lawafadhaisha sana: “Nami nimemweka mfalme wangu juu ya Sayuni, mlima wangu mtakatifu.” Kiti cha enzi juu ya dunia kimekwisha kukaliwa na mfalme mwekwa wa Mungu mwenyewe, chaguo lake. Hakuna nafasi kwa kingine.—Zab. 2:4-6.
Kisha Mfalme Yesu Kristo mwenyewe anaongea: “Nitaihubiri [Acha niitaje, NW] amri ya [Yehova Mungu alikuwa ametangulia kufanya pamoja na Mwanawe agano la huo Ufalme] aliniambia, Ndiwe mwanangu, Mimi leo nimekuzaa.” Kwa hiyo Mfalme ni Mwana wa Mungu mwenyewe, aliye na cheo cha pili Kwake, Yule wake aliyejaribiwa na aliye mshikamanifu, na mwenye kutegemeka. Kwa hiyo Mfalme huyo anataja cheo chake cha kifalme, kwa kuwa Mungu amemwambia hivi: “Uniombe, nami nitakupa mataifa kuwa urithi wako, na miisho ya dunia kuwa milki yako.” Yeye anakuwa na urithi kama yeye ambaye Mungu amemfanya mzaliwa wa kwanza; analotakiwa kufanya peke yake ni kuomba tu, jambo ambalo anafanya kwa sababu ya tamaa yake kubwa ya kuona mapenzi ya Mungu juu ya dunia yakitimizwa.—Zab. 2:7, 8.
AMRI YA MUNGU JUU YA MATAIFA
Hivyo, basi, mataifa wako katika hali gani leo, pamoja na silaha zao zote za vita? Mfalme atatimiza amri ya Mungu kwake: “Utawaponda kwa fimbo ya chuma, na kuwavunja kama chombo cha mfinyanzi.” Fimbo za wafalme wa kale zilikuwa za mti, pembe (ya ndovu) au vitu vingine. Nyingine zilikuwa za chuma, kama vile hii. Wazo hapa laonyesha namna Kristo Mfalme atakavyowaharibu mataifa kabisa kabisa kwa urahisi.—Zab. 2:9.
Je! ni lazima watawala hao wa kitaifa wapatwe na kuvunjwa-vunjwa huko hata kuharibiwa? Hapana, kwa kuwa mtunga zaburi anawasihi hivi: “Na sasa, enyi wafalme, fanyeni akili, enyi waamuzi wa dunia, mwadibiwe.” Wanaombwa watii, wafikirie ubatili wa mipango yao ikitofautishwa na yale yatakayofanywa na ufalme wa Mungu kwa faida ya wanadamu, waugeuze mwendo wao.—Zab. 2:10.
Wafalme wa dunia wanaonywa kwa upole “mtumikieni [Yehova] kwa kicho, shangilieni kwa kutetemeka.” Ikiwa wangechukua tendo hilo, badala ya kufanya ghasia, wangeshangilia kwa ajili ya mataraja ambayo Mfalme anaweka mbele yao. Lakini wangehitaji kuachia mbali majivuno na kiburi chao, ambavyo wamekuwa wakivionyesha katika wakati uliopita katika utawala wao. Na ingewapasa kufanya hivyo sasa, kabla haijakuwa kuchelewa mno. Ingekuwa lazima waonyeshe ufahamu juu ya ukuu ulio mkubwa sana wa enzi kuu ya Mungu pamoja na kutoshindika kwa Yehova na Masihi wake.—Zab. 2:11.
MWALIKO WENYE REHEMA
Kwa hiyo watawala wanashauriwa kwamba, badala ya kujikusanya pamoja katika kumpinga Mungu, wapaswa ‘kushika yaliyo bora [au wambusu mwana, NW], [ili Mungu] asije akafanya hasira nanyi mkapotea njiani.’ (Zab. 2:12) Yehova Mwenye Enzi Kuu aliye mkuu afanyapo amri inapaswa kufuatwa. Wakati alipomketisha Mwanawe kwenye kiti cha enzi, watawala wa dunia walipaswa kuacha ‘kutafakari ubatili.’ Walipaswa kumkubali Mfalme huyo mara moja, wakimtii kabisa.
Wale wanaokataa kutambua mamlaka ya Mfalme aliyechaguliwa na Mungu kwa kweli huwa wanamtukana Aliye Juu Zaidi. Wao wanakataa enzi yake kuu ya ulimwengu wote pamoja na uwezo wake na mamlaka yake ya kuchagua mfalme aliye mtawala bora zaidi kwa ajili ya wanadamu. Watu kama hao wataona kwamba hasira ya Yehova itawajilia kwa haraka sana, wanapofuatia njia ya kutimiza makusudi yao wenyewe, “kwa kuwa hasira yake itawaka upesi,” au inawaka kwa haraka, na bila kuzuiwa. Bila shaka hili ni onyo linalofaa na ambalo wanapaswa kulikubali kwa shukrani, kwa kuwa lamaanisha uzima kwao wakilitii.—Zab. 2:12a.
Kwa hiyo, bado kuna wakati wa kupata usalama kwa wale ambao wamekuwa wakiikubali mipango ya mataifa hata bila kutenda lo lote hata kwa wale ambao huenda wakawa wamekuwa wakiupinga ufalme wa Yeye aliyewekwa na Mungu. Kwa sababu ya hatari inayokaribia, hao wanaweza kumkimbilia Yehova, kwa kuwa yeye anatoa kimbilio kwa nia chini ya ufalme wa Mwanawe, kabla ufalme huo haujayaponda-ponda mataifa yenye kuupinga.
Kimbilio hilo laweza kufikiwaje, na itakuwaje kwa yeye anayetafuta ulinzi ndani yake? Mtunga zaburi anamalizia hivi: “Wenye furaha ni wale wote wanaotafuta kimbilio katika yeye [Yehova].” (Zab. 2:12b, NW) Si vigumu kupata ulinzi huo. Lakini unapatikanaje? Lazima mtu aone uhitaji wa jambo bora zaidi ya kile wanachotoa mataifa ya kilimwengu. Kisha, ni lazima aiangalie Biblia kwa unyofu ili aone namna maisha yake yanavyoweza kupatanishwa na njia za Mungu. Hiyo haimaanishi kuishi maisha yasiyo ya kawaida hata kidogo.
Wale wanaojifunza Biblia mahali ambapo uongozi wa Mungu unapatikana, wanaweza kuishi maisha yenye kuridhisha zaidi. Kufuata shauri la Biblia huwapa uhusiano wa jamaa wenye furaha zaidi, uhuru kutokana na woga na wasiwasi unaowazunguka watu ulimwenguni leo, pamoja na maarifa na uhakika wa kwamba wanampendeza Muumba wao. Hakuna mwingine ila Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote anayeweza kutoa uthibitisho wa “uzima wa sasa, na [wa] ule utakaokuwapo baadaye [hasira yake ikiisha kuiondolea dunia wale wote wanaopinga yaliyo mema kwa kuukataa utawala wake].” (1 Tim. 4:8) Yeye akiwa Muumba, anayejua yanayowafaa watu, atatimiza kusudi lake la kuwabariki kwa amani, usalama wenye kudumu pamoja na uradhi chini ya ufalme wa Mwanawe. (Mt. 6:33) Kweli kweli, ni wakati unaofaa sana wa ‘kufanya akili,’ ndiyo, ‘kumbusu Mwana,’ kabla Yehova Mungu hajaharibu watawala wa dunia na falme zao, katika hasira yake.