Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Katika kutimiza unabii wa kwanza, katika Mwanzo 3:15, kichwa cha “nyoka” kitapondwa wakati gani na “uzao” wa mwanamke wa Mungu?
Tafsiri ya The Jerusalem Bible inasomwa hivi katika Mwanzo 3:15: “Mimi nitawafanya ninyi kuwa maadui ninyi kwa ninyi: wewe na mwanamke, uzao wako na uzao wake. Utaponda kichwa chako nawe utapiga kisigino chake.” The Emphasized Bible ya Rotherham inasomwa hivi: “Yeye ataponda kichwa chako, lakini wewe utaponda kisigino chake.” Kupondwa kwa kisigino cha “uzao” wa mwanamke wa Mungu kulitokeza kifo cha Bwana Yesu Kristo. Kulipa kisasi, Yesu Kristo aliyetukuzwa atamponda nyoka wa mfano, Shetani Ibilisi.
Baada ya ufalme wa Mungu “kuzaliwa” mwishoni mwa Nyakati za Mataifa katika mwaka 1914, Ufunuo sura ya 12 wasema juu ya Mikaeli na malaika wake wakipigana vita na joka wa mfano na malaika zake walio mashetani na kuwafukuza mbinguni wasiweze kurudi huko tena, na kuongeza hivi: “[Kwa hiyo] yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye.”—Ufu. 12:5, 7-9.
Baada ya maelezo ya vita kwenye Har–Magedoni katika Ufunuo 19:11-21 ambayo katika hiyo Yesu ayaongoza majeshi ya kimbinguni kwenye ushindi juu ya wapinzani wote wa kidunia, Yohana anaona katika njozi Shetani akitupwa katika shimo lisilo na mwisho: “Kisha nikaona malaika [bila shaka Mikaeli malaika mkuu] akishuka kutoka mbinguni, mwenye ufunguo wa [shimo lisilo na mwisho], na mnyororo mkubwa mkononi mwake. Akamshika yule joka, yule nyoka wa zamani, ambaye ni Ibilisi na Shetani, akamfunga miaka elfu; akamtupa katika [shimo lisilo na mwisho], akamfunga, akatia muhuri juu yake, asipate kuwadanganya mataifa tena, hata ile miaka elfu itimie.”—Ufu. 20:1-3.
Hakika Yesu Kristo, akiwa ndiye “uzao” wa mwanamke wa Mungu, angaliweza wakati huo kumponda kabisa kabisa, na kumwangamiza kabisa, “yule nyoka wa zamani,” badala ya kumtia tu katika shimo hilo lisilo na mwisho. Lakini Yehova, katika hekima yake, ameazimia kwamba wanadamu waliokamilishwa wapaswa wajaribiwe na yule yule aliyetokeza upinzani juu ya enzi yake kuu ya ulimwengu wote, baada ya utawala wa Kristo wa miaka 1,000. Jambo hilo litaondoa shaka lo lote linaloweza kutokea juu ya ukamilifu wa wale watakaokataa kupotoshwa na Ibilisi.
Wakiongozwa na Shetani, wapinzani wa dunia wanafanya jaribio la mwisho la kunyakua dunia. Yohana anaeleza matokeo kama kwamba yalikuwa tayari yametokea, akisema: “Moto ukashuka kutoka mbinguni, ukawala.” Na kwa habari ya kupondwa kwa kichwa cha “yule nyoka wa zamani,” masimulizi hayo yasema hivi: “Na yule Ibilisi, mwenye kuwadanganya, akatupwa katika ziwa la moto na kiberiti.” (Ufu. 2:9, 10) Hilo lamaanisha kuangamizwa kwake kabisa. Hivyo, kuhusiana na kupondwa kichwa kwa mpinzani wa Mungu aliye mkubwa zaidi si kwamba tu ulimwengu wote waondolewa wapinzani wa Mungu aliye mkubwa zaidi,si kwamba tu ulimwengu wote waondolewa wapinzani bali pia jina Lake lililo takatifu zaidi linatakaswa kabisa. Hilo latimiza kabisa ahadi katika Warumi 16:20 kwa warithi washirika wa Kristo kwamba “naye Mungu wa amani [atamponda] Shetani chini ya miguu yenu upesi.”—Ebr. 2:14, 15.