Je! Unaweza Kumpenda Jirani Yako na Bado Uvute Sigara?
BINADAMU wanaovuta sigara wanachafua hewa ambayo wengine wanapumua ndani na pia wanaharibu afya yao wenyewe. Wangekuwa wenye afya bora zaidi kama wangeacha kuvuta sigara. Na pia wangeokoa fedha nyingi kwa kutotokeza uchafu—kufika shilingi 5,520 kwa mwaka mmoja au karibu na hizo za gharama ya sigara. Kwa hiyo mwendo pekee unaofaa kwa mvutaji sigara ni kuacha kuvuta sigara.
Ebu wazia uchafu mwingi ulioko katika moshi unaojiviringa kutoka katika sigara. Ni wenye sumu zaidi kuliko moshi ule unaopumuliwa ndani na mvutaji sigara. Moshi unaotoka sigarani una lami na sumu ya sigara maradufu, hewa yenye sumu ya carbon monoxide mara tano zaidi na mvuke wa ammonia unaozidi mara 50 ule unaotoka kinywani wakati wa kuvuta sigara, licha ya sumu nyingine.
Sigara 10 zilizowaka ndani ya motokaa iliyofungwa zinaongeza hewa yenye sumu ya carbon monoxide mara 100 kwa kila sehemu milioni moja, zaidi ya inavyoruhusiwa na kanuni za hewa nzuri za United States. “Katika karamu ya kawaida ya chuo kikuu,” likasema gazeti New York Times, “vitu vinavyokuwamo hewani kutokana na moshi wa sigara ni mara 40 zaidi ya kanuni ya hewa nzuri ya United States.” Na kama ilivyotangulia kutajwa dhara linalowapata wale wanaolazimika kupumua ndani moshi huo kwa limekwisha thibitishwa vizuri.
JE! HIYO INAPATANA NA KUMPENDA JIRANI?
Biblia inasema kwamba “amri ya kifalme” ni “mpende jirani yako kama unavyojipenda wewe mwenyewe,” hivyo inakazia maana ya sheria hiyo. (Yak. 2:8) Je! ingekuwa kuonyesha jirani yako upendo kutup takataka makusudi katika uwanja wake au kumtema mate usoni? “Bila shaka sivyo! ” huenda ukasema. Je! kufanyia jirani yako mambo hayo ingekuwa ni dhambi?
Ufafanuzi wa dhambi unasaidia kujibu ulizo hilo. “Dhambi ni kuvunja sheria” —sheria ya Mungu—ndivyo Biblia inavyosema. (1 Yohana 3:4, Today’s English Version) Kwa hiyo kumfanyia jirani yako jambo baya kama vile kumtema mate usoni au kutupa takataka katika uwanja wake ingekuwa ni dhambi. Ingekuwa kuvunja “amri ya kifalme” inayosema “Mpende jirani yako kama unavyojipenda wewe mwenyewe.”
Lakini hiyo inahusianaje na kuvuta sigara? Dakt. Isaac Asimov, katika makala ya mhariri ya gazeti Cancer News, alikazia namna ilivyo hivyo. “Mtu anapovuta sigara mahali nilipo,” akasema, hafanyi uovu peke yake. Moshi mbaya anaotokeza unaingia katika mapafu yangu na katika damu. Ninanuka kama yeye na mnuko wake unanikwamilia. Naye, anaongeza uwezekano wangu wa kupatwa na maradhi ya moyo na donda baya la mapafu.”
Katika kujibu wavutaji sigara ambao wanaweza kudai wana uhuru wa kuvuta sigara mahali palipo wengine, Dakt. Asimov alisema hivi: “Iwapo ana maoni ya kwamba ana lazima ya kuvuta sigara na kwamba ninapokataa jambo hilo ninamnyang’anya uhuru wake, basi je! yeye ana nia ya kunivumilia iwapo naona nina lazima ya kumpiga teke manenani (katikati ya paja na tumbo) na kwamba akikataa ananinyang’anya uhuru wangu? Na tuseme kwa njia hii: Uhuru wako wa kuvuta sigara unakoma mahali yalipo mapafu yangu.”
Bila shaka, kumpiga mtu teke manenani, kumtema mate usoni, au tutupa takataka katika uwanja wake hakupatani na kumpenda jirani. Wala kuvuta sigara. Ni kuingilia uhuru wa wengine—kuwaumiza badala ya kuwapenda. Ndiyo, kuvuta sigara ni dhambi.
Hata hivyo, huenda mvutaji sigara akasema hivi: “Nakubali kwamba kuvuta sigara kunaumiza. Ndiyo sababu sivuti sigara mahali walipo watu.” Kwa hiyo, mtu akivuta sigara akiwa peke yake, je! hiyo ni dhambi? Hakuna mtu mwingine anayeumizwa.
NI DHAMBI KUVUTA SIGARA UKIWA PEKE YAKO?
Lakini ebu fikiri: Maisha ya mvutaji sigara mwenyewe yanapata umizo. Naye ni nani aliye chanzo cha uhai wetu? “Kwako Wewe [Yehova Mungu] iko chemchemi ya uzima,” ndivyo Biblia inavyojibu. “Ndiye anayewapa wote uzima na pumzi na vitu vyote.” (Zab. 36:9; Matendo 17:25) Ndiyo, maisha yetu ni zawadi bora sana kutoka kwa Mungu.
Twaweza kuonyeshaje kuthamini zawadi aliyotupa Mungu ya uzima? Kwa kufanya mambo yanayoweza kuiharibu? Bila shaka sivyo! Kufanya hivyo kwa makusudi ni kosa! Kwa habari hiyo, angalia usemi wa Joseph Califano, aliyekuwa zamani Katibu wa Afya, Elimu na Ujamii wa United States: “Leo hapawezi kuwa shaka kwamba kuvuta sigara ni kujiua pole-pole kwa hakika.”
Kuharibu uhai wa kibinadamu kwa makusudi ni kosa—ni dhambi. Biblia inawaamuru Wakristo wasiichafue hata miili yao. “Tujitakase nafsi zetu na uchafu wote wa mwili,” ndivyo inavyosihi. (2 Kor. 7:1) Ili mvutaji sigara atii amri hiyo, lazima aondoe zoea la kuvuta tumbako, kwa kuwa inachafua kweli kweli. Inachafua vidole, meno, harufu, mavazi ya mvutaji sigara—karibu kila kitu ambacho kinakaribiana nayo.
Lakini vipi mvutaji sigara akitaka kuacha, hata hivyo awe ni mzoelevu sana asiweze? Je! Mungu atafahamu kwa rehema kwamba ‘roho ina nia walakini mwili ni dhaifu,’ ati kwa kuwa Yesu Kristo alisema hayo?—Mt. 26:41, NW.
JE! UNAWEZA KUSAMEHEWA KWA AJILI YA UDHAIFU?
Bila shaka, kuacha kuvuta sigara ni jambo gumu sana. “Lilikuwa jambo rahisi zaidi kuacha kuvuta heroin (inafanana na bhangi) kuliko sigara,” wazoelevu wake wamesema. Dalili zinazofuatana na kuacha kuvuta tumbako zinaendelea kwa muda mrefu zaidi. “Kwa wengi, kutamani kunaendelea kwa angaa mwezi mmoja,” ndivyo lilivyosema gazeti Science 80, “na kwa sehemu moja ya tano kunaendelea kwa miaka mitano kufika tisa baada ya kuacha.”
Hiyo inaonyesha sababu gani wengi wanaacha kuvuta sigara kwa muda, halafu wanaanza tena. Wavutaji sigara tisa kati ya 10 wanataka kuacha. Walakini kuacha tumbako ni vita ya mchana na usiku, nyakati nyingine ikiendelea kwa miaka mingi. Mamilioni wameshinda vita hiyo. Makumi ya mamilioni wamepigana na kushindwa. Iwapo mtu amejaribu kuacha akashindwa, je! ni jambo la hekima kuwaza kwamba Mungu atafahamu na kusamehe kosa hilo?
Chanzo cha tatizo hilo chaweza kuwa kwamba mtu anafurahia kuvuta sigara. Walakini hiyo haifanyi zoea hilo linalolaumiwa na Mungu lisiwe baya. Biblia inasema kwamba, “kuliko kujifurahisha katika dhambi kwa kitambo,” kwa hekima Musa alichagua kumtumikia Mungu. (Ebr. 11:24-26) Mungu anatazamia watumishi wake wapigane na mazoea yanayopingana na sheria zake, wakiwa na msaada wake, nao wayashinde.
Kwa mfano chukua uasherati. Ni zoea ambalo wengi wanaelekea kulifurahia kwa kitambo. Na unapozoewa, tamaa ya mtu kufanya ngono pamoja na wenzi mbali-mbali inakuwa yenye nguvu kama tamaa ya kutaka sigara. Hata hivyo uasherati ni kuvunja sheria ya Mungu, nao wazoelevu wa makusudi wa uasherati, wasiotubu, hawatapata pendeleo la kupata zawadi ya Mungu ya uzima wa milele. Wala wale wanaoendelea kuvuta sigara.—Ebr. 13:4. Rum. 6:23.
Inataka jitihada kweli kweli ili kutii sheria za Mungu. Ndivyo ilivyokuwa kwa Mwana wa Mungu, Yesu Kristo. Aliteseka vikali sana, mwishowe akafa kifo kibaya. Hata hivyo aliendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu. Kwa watu wengine, maumiuvu yanayowapata ili waache kuvuta sigara yaweza kuonekana kuwa magumu kuvumilia kama vile mateso aliyopata Kristo. Hata hivyo zoea la kuvuta tumbako laweza kushindwa. Namna gani?