Unaweza Kuyavunja Mazoea ya Tumbako
KWA nini mamilioni ya watu wanavuta sigara na hali kuna ushuhuda mwingi sana wa kwamba kunadhuru afya? Kwa nini wengi sana wanaonyesha tamaa ya kuacha, na hali wanaendelea tu kuvuta sigara? Kama ilivyoandikwa katika toleo la majuzi la Science World, ni kwa sababu kuvuta sigara “kunazoeza.” Na hali, lijapokuwa ongezeko la idadi ya wavuta sigara, wako watu walio huru kabisa na mazoea ya tumbako.
Watu hawa ni mashahidi wa Yehova. Habari katika Courier la Evansille, Indiana, ilisema hivi juu ya kusanyiko lao katika mji huo: “Huenda ikawa ndio uliokuwa wakati wa kwanza tangu kuwapo kwa uwanja wa michezo ambapo watu 6,000 au 7,000 walikaa katika viti vyote wala ukungu wa moshi haukumfunika msemaji.”
Kwa nini yaonekana sana kwamba hamna uvutaji wa sigara kati ya mashahidi wa Yehova? Je! ni kwa sababu wale wanaokuwa mashahidi wa Yehova hawajapata kuwa wazoevu wa sigara?
Hata kidogo. Wale wanaokuwa mashahidi wa Yehova wametoka kati ya watu wa kawaida, ambao juu yao Guardian Weekly lilisema hivi: “Wawili kati ya kila wanaume watatu ni wavutaji wa sigara, ijapokuwa ni mmoja tu anayevuta kati ya wanawake wanne.” Kwa hiyo ni jambo la akili kusadiki kwamba karibu kiasi kile kile cha mashahidi wa Yehova walivuta sigara wakati fulani.
Je! ilikuwa vyepesi kwa makumi haya ya maelfu ya Mashahidi kuacha kuvuta sigara? Waliwezaje kufanya hivyo? Ikiwa wewe ni mtu unayetaka kuyavunja mazoea hayo, waliyoyaona yaweza kukusaidia.
WAVUTAJI WANAKUWA NA MATOKEO MBALIMBALI
Si kila mvutaji anayeona ugumu mwingi anapoacha. Watu wengine wanavuta kidogo, nao wanafanya hivyo ili wawe wakunjufu. Hivyo Waamerika milioni 10.2 waliacha kuvuta sigara kwa kipindi fulani kilichopita cha miaka minne, kulingana na uchunguzi mmoja. Wingi wa hawa labda hawakuona ugumu mwingi kuacha.
Mfano wa wavutaji hao ni mwanachuo aliyehitimu wa Harvard ambaye, alipokwisha kuvuta sigara kiasi kwa miaka kadha, mwishowe aliamua kuyaacha mazoea haya machafu. Alizitupa sigara zake naye hakuvuta tena. Lilikuwa jambo jepesi kwake; yeye hakukosa, raha, na nyumaye hakutamani sana kuvuta sigara. Lakini visa vingine vinakuwa tofauti sana.
Mtu mmoja aliyekuwa mvuta sigara wa Saskatchewan, Canada, alieleza: “Kuusafisha mwili wangu kwa kutotumia tumbako kulikuwa mateso makali kwangu yasiyoelezeka. Nyakati nyingine kifua changu kilikuwa kikikazika sana, kana kwamba minofu ilikuwa imefunganishwa katika fundo. . . . Nyakati nyingine, ugumu huu ulikuwa mwingi sana hata nikadhani nitakufa.” Mvutaji sigara mkubwa wa West Virginia alisema kwamba alipoacha kuvuta sigara alipata kuwa mgonjwa sana na dhaifu hata ikampasa kulala kitandani kwa siku mbili. Maono hayo ya masumbufu na ugonjwa wakati mtu anapoacha kutumia tumbako si jambo lisilo la kawaida. Ni vizuri wale wanaotaka kuyavunja mazoea ya tumbako wafahamu hili.
KUFAULU
Pengine wewe ni mtu aliyejitahidi kwa miaka mingi kuacha kuvuta sigara, lakini bila ya kufanikiwa, na huenda ukajisikia kukata tamaa sana. Usichoke! Wengine, ambao nao wamekuwa wazoevu wa tumbako, wameyashinda mazoea hayo.
Daktari mmoja mwenye umri wa miaka 56 ambaye ni mpasuaji vile vile alisema hivi majuzi: “Naikumbuka siku nilipoacha. Ilikuwa Jumatatu, Mei 15, 1950, katika Santa Barbara, California. Maono haya yamenipa ujasiri. Kwa maana tangu wakati huo, ninapopatwa na magumu au hali zenye shida, nawaza, ‘Ikiwa niliweza kuacha kuvuta sigara, hata hili nalo naweza.’ Ushindi juu ya kuvuta sigara ulikuwa wenye maana sana kwangu, kwa kuwa nilikuwa nimeshindwa mara nyingi sana.
“Kila mara nilipokwisha kuamua kuacha, mwishowe nilianza kuzunguka nyumba yote nikitafuta-tafuta vipande vya sigara. Nikawa nikivalia usiku na kwenda nje nikanunue sigara kadha. Nyumaye nilikuwa nikifadhaika kwa mara nyingine.
“Karibu wakati huo nilianza kujifunza Biblia na mashahidi wa Yehova. Karibuni nikaona kwamba mambo niliyokuwa nikijifunza hayakupatana na mazoea ya tumbako. Na hali nilizidi tu kuvuta sigara. Wakati wa mikutano nikawa nanyata-nyata kuelekea dukani nikapate sigara. ‘Upumbavu gani huo,’ nikawaza, ‘kwa mwanamume mzima kunyata-nyata hapa na pale kama kitoto kidogo, nikivuta sigara hali nimejificha.’ Nisingeweza hata kidogo kuendelea kuishi hivyo, kama mnafiki. Kwa kuwa nilikuwa nimesadiki mashahidi wa Yehova ndio wenye kweli ya kufanya uchaguzi—niache kutumia tumbako au niiache kweli.
“Naikumbuka Jumapili hiyo mwaka wa Neno la Mungu, nilijua kwamba ilinipasa 1950—kama kawaida nilivuta sigara mkutano ulipovunjika kwa kitambo. Lakini jioni hiyo sigara yangu ya mwisho ilikwisha, nami nikaweka nadhiri kutoleta nyingine nyumbani. Lakini, niliweka sigara katika afisi yangu mjini. Nilipofika asubuhi yake nilizipata chache zilizosalia. Nikazivuta, nikizimaliza karibu saa tano ya asubuhi. Lakini nilikuwa nimekwisha kata maneno kutovuta nyingine tena, nami sijapata kuvuta sigara tangu wakati huo.”
KUMTEGEMEA YEHOVA
Daktari huyu hakuusahau ubora wa sala. (Zab. 55:22) Na kwa msaada wa Yehova, Mungu wa kweli, nawe vile vile waweza kufaulu kuyashinda mazoea ya tumbako. Mtume Paulo alisema: “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.” (Flp. 4:13) Maono ya mwanamume aliyeanza kuvuta sigara akiwa mvulana mwenye umri wa miaka sita katika South Dakota yaonyesha vizuri namna uwezo huu kutoka kwa Yehova Mungu unavyotosha kumsaidia mtu ayashinde mazoea ya tumbako. Alieleza hivi karibuni:
“Mimi nilikuwa nikivuta pakiti mbili kwa siku, na kumaliza sanduku la sigara 50 kwa juma. Mikono yangu, meno, pumzi—mwili wangu wote—ulikuwa umechafuliwa na tumbako. Mimi nisingeweza kumaliza kula bila ya kukoma nipate sigara. Jambo la mwisho nililokuwa nikifanya mbele ya kwenda kulala lilikuwa ni kuvuta sigara; nikawa nikiamka wakati wa usiku nipate sigara; nalo jambo la kwanza nililokuwa nikifanya asubuhi ni kuvuta sigara.
“Mama yangu akahangaika juu yangu. Kwa hiyo nilipokaribia umri wa miaka 21 alisema angenipa shilingi 7,000 nikiacha kuvuta sigara kwa siku mbili. Nikamwambia sikutaka niache, na kwamba sikuwa na nia ya kuacha kitu kilichoniletea raha sana.
“Nyumaye nilianza kuhudhuria mikutano ya mashahidi wa Yehova, nami nikaamua kwamba ili nimpendeze Mungu na watu wake yanipasa kuacha kuvuta sigara. Lakini sikuweza. Nilizidi kulivunja azimio langu. Nakumbuka wakati mmoja nilimwuliza Shahidi shauri juu yake. Akauliza: ‘Je! umesali upate msaada?’ Nikamwambia bila shaka nilikuwa nimefanya hivyo.
“Akauliza: ‘Wewe unasali wakati gani?’ Nikasema jioni mbele ya kulala, asubuhi niamkapo, na ninapokwisha kudhoofika na kuvuta sigara, namwambia Yehova kwamba nasikitikia nililolifanya.
“Akasema: ‘Je! wakati unapohitaji msaada wa Mungu hasa si dakika ile unaponyosha mkono upate sigara? Huo ndio wakati inapokupasa kusali kwa Yehova akutie nguvu.’
“Tangu wakati huo na kuendelea lilo hilo ndilo nililolifanya, naye Yehova alinitia nguvu. Niliweza kuacha kuvuta sigara, ijapokuwa niliendelea kuzitamani kwa miaka mingi.”
Mvutaji, kama vile mzoevu wa dawa ya kutia usingizi inayoitwa heroin, anakuza katika utaratibu wake ‘haja’ ya tumbako. Nyuma ya muda mfupi bila ya kuvuta, anakuwa na masumbufu, nyakati, nyingine hata akianza kutokwa jasho kwa ghafula iwapo amekosa kuvuta kwa muda mrefu mno. Hivyo, kwa sababu ya kitulizo hiki kunacholeta, kuvuta sigara kunamfurahisha mvutaji, nako kwaweza kuwa jitihada kubwa sana kuacha. Kinachoonyesha hili ni kisa cha mwanamke mmoja kijana, aliyelelewa Denmark na sasa anayeishi katika mji wa New York. Alianza kuvuta sigara akiwa mwenye umri wa miaka kumi na minne, na mwishowe akaacha Novemba 28, 1970. Alikuwa amekuwa akijaribu kwa miezi mingi, lakini kila mara alikuwa akirudia hali ile ile. Anasema hivi:
“Nilikuwa nikisali juu ya jambo hili, lakini sikuwa mwaminifu kabisa. Nikawa nikimwambia Yehova kwamba sikupenda kuvuta sigara na kwa hiyo nilitaka niache. Lakini ukweli ni kwamba, mimi nilifurahia kuvuta sigara. Kwa hiyo mwishowe nilikubali katika sala kwa Yehova kwamba kwa kweli nilifurahia kuvuta sigara, lakini kwamba nilitaka niache kabisa nimpendeze Yeye. Halafu, nilipozidi kukazia akili yangu kwenye kumpendeza Mungu, mwishowe niliyavunja mazoea haya.”
YAWEZEKANA!
Ikiwa wahofu kwamba huenda usiweze kuacha kuvuta sigara, ujue kwamba si wewe peke yako. Mke mmoja wa Brooklyn, New York, aliyevuta pakiti tatu au nne kila siku, alijiona hivyo. Alikuwa ameendelea kuvuta sigara ajapokuwa alibatizwa na mashahidi wa Yehova mwaka wa 1968. Anaeleza:
“Siku moja mume wangu aliniambia: ‘Sababu gani usiache kuvuta sigara?’ Nami nikamtolea maneno makali, ‘Wawezaje kuniambia nifanye hivyo? Waniambia niutoe uhai wangu.’ Nilipopata fahamu za niliyokuwa nimeyasema nilishtuka na kuaibika. Nami nilijua kwamba nisingeweza kuendelea kujidai kuwa Shahidi kwa unafiki na kuendelea kuvuta sigara. Kwa hiyo siku iliyofuata nikamwambia mume wangu kwamba ningeacha—lakini nyuma ya mwezi mmoja, Jumamosi ya mwisho ya mwezi wa Februari 1971.
“Jumamosi hiyo nilivuta sigara mchana kutwa na usiku. Juma iliyofuata ilikuwa ndoto. Mikono yangu ilitetemeka. Nililia karibu wakati wote. Nilikuwa mgonjwa; tamaa ilikuwa yenye maumivu makali. Lakini nilikuwa nimekwisha kata maneno, na kwa msaada wa Yehova nikaushikilia mkataa wangu. Sasa mimi nasadiki kwamba watu wasiofaulu, hawataki kweli kuacha. Wangali wanapenda kuvuta sigara zaidi kuliko wanavyompenda Yehova.”
Kwa kweli ikiwa wampenda Yehova Mungu waweza kuyashinda mazoea ya tumbako. Linalopendeza ni kwamba, mkaaji mmoja wa Synanon, mtaa wa California ulioanzishwa kwa ajili ya utabibu wa wazoevu wa dawa za kulevya na watumiao vileo vikali, ambapo kuvuta sigara kulipigwa marufuku mwaka wa 1970, alisema hivi: “Ikiwa sisi tulio waovu katika jamii twaweza kuacha kuvuta sigara, basi huko nje katika unaoitwa ulimwengu wenye akili unaojiangamiza na dawa ya kulevya iliyo hatari kupita zote [tumbako], watu wenye madaraka wanaweza kuvumilia.”
Onyesha kwamba wampenda Yehova kweli na kanuni zake za haki. Jiondoe katika utumwa wa kuvuta sigara sasa! Unaweza kufanya hivyo.