Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g90 3/8 kur. 13-15
  • Maoni ya Kikristo Juu ya Kuvuta Sigareti

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maoni ya Kikristo Juu ya Kuvuta Sigareti
  • Amkeni!—1990
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kupenda Mungu na Jirani
  • Kwa Nini Waliacha Kabisa?
  • Je! Inastahiki Kuacha?
  • Unaweza Kuyavunja Mazoea ya Tumbako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Mungu ana maoni gani kuhusu Kuhusu Kuvuta Sigara?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Kwa Nini Uache Kuvuta Sigareti?
    Amkeni!—2000
  • Wauzaji wa Kifo—Je! Wewe Ni Mnunuzi?
    Amkeni!—1990
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1990
g90 3/8 kur. 13-15

Maoni ya Kikristo Juu ya Kuvuta Sigareti

NI WAZI kwamba Biblia haitaji tumbako wala kuvuta sigareti, kwa kuwa vitu hivyo havikujulikana katika nchi ya kale ya Mashariki ya Kati. Sababu sahili ni kwamba mmea wa tumbako ni wa uenyeji wa Amerika Kusini, Meksiko, na West Indies nao haukuanza kukuzwa kwenye sehemu nyingine za ulimwengu mpaka katikati ya karne ya 16.

Je! hiyo yamaanisha kwamba Biblia haisemi jambo lolote kuhusu kuvuta sigareti? Sivyo hata kidogo. Hiyo hutaarifu wazi kanuni zenye kutumika ulimwenguni pote ambazo ni miongozo kwa mwenendo wetu. Ni nini baadhi ya kanuni hizi za msingi?

Kupenda Mungu na Jirani

Ni lazima kani ya msingi yenye kuchochea Mkristo iwe ile ambayo Yesu alieleza: “Mpende Bwana [Yehova, NW] Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote, na kwa akili zako zote; na jirani yako kama nafsi yako.”—Luka 10:27.

Mtu aweza kutoleaje Mungu upendo kwa moyo, nafsi, akili, na nguvu zake zote ikiwa anachakaza kimakusudi nguvu zake za kufikiri kwa kujihusisha katika tabia, zoea ovu, ambalo huongoza kwenye ugonjwa na kifo cha mapema? Mtu huonyeshaje uthamini wa zawadi ya Mungu ya uhai huku akivuta ndani nikotini ambayo ni dawa ya kulevya yenye kumzoeleza uvutaji? Mungu ndiye aliwapa “wote uzima na pumzi.” (Matendo 17:24, 25) Je! yatupasa tuchafue pumzi hiyo tuliyopewa na Mungu? Kwa maoni ya Mungu, kwa kweli hilo zoea ovu, “ni zoea au tabia mbovu, yenye kushusha tabia, au ya ukosefu wa adili.”—The American Heritage Dictionary of the English Language.

Kuvuta sigareti kwaonyeshaje upendo kwa jirani, na hali pumzi mbaya ya mvutaji na moshi wake huchafua nguo na hewa inayozunguka? Namna gani majirani wa karibu zaidi wa mvutaji, mwenzi wa ndoa na watoto wake? Je! ni upendo kufuatia mwendo ambao ungeweza kuongoza kwenye kifo cha mapema cha polepole, kilicho na maumivu ambacho wao watalazimika kuona wewe ukipatwa nacho? Je! ni kuonyesha ufikirio wa Kikristo kwa watu wengine kwa kuwashurutisha wawe wavutaji wasiojivutia wenyewe, huku wakivuta ndani mipumuo yenye sumu ya mvutaji? Si ajabu kwamba mmea wa tumbako umewekwa mahali paufaapo katika sehemu ya mimea yenye sumu, katika ile bustani ya mimea iliyoko Blanes, Hispania!

Namna gani kujipenda binafsi? Ni halali kujipenda mwenyewe kufikia hatua ya kutunza afya yako ya kimwili, ya kiakili, na ya kiroho. Mtume Paulo alitaarifu kwamba “hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza.” Je! kujihusisha katika tabia ambayo pole kwa pole hudhoofisha afya yako ni kujipenda binafsi?—Waefeso 5:28, 29.

Yehova Mungu ameahidi kwamba kutakuwako ‘mbingu mpya na dunia mpya ambamo uadilifu utakaa.’ (2 Petro 3:13, NW) Huo utakuwa ulimwengu mpya ulio safi, usio na uchafuzi wa aina yoyote. Uvutaji sigareti hautaruhusiwa wala kutamaniwa wakati huo, kwa hiyo mbona kuvuta sigareti sasa? Kwa kufaa shauri la Paulo latumika hapa: “Basi, wapenzi wangu, kwa kuwa tuna ahadi hizo, na tujitakase nafsi zetu na uchafu wote wa mwili na roho, huku tukitimiza utakatifu katika kumcha Mungu.” (2 Wakorintho 7:1) Nikotini hutia unajisi wa kihalisi katika mnofu. Kuvuta sigareti hufanya isiwezekane Mkristo kumtolea Mungu mwili wake ukiwa “dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu [zake] za kufikiri.” (Warumi 12:1, NW) Nguvu za akili zaonyesha kwamba kuvuta sigareti kuna madhara na ni dhidi ya kanuni za Kikristo. Basi, hicho ndicho kichocheo cha msingi cha kuacha kabisa kuvuta sigareti ikiwa mtu ataka kufurahisha Mungu.

Kwa Nini Waliacha Kabisa?

Mamilioni ya watu kuzunguka ulimwengu wameacha kabisa kuvuta sigareti. Yawezekana kuacha. Lakini jinsi gani? Ni mambo gani yenye kuhitajiwa kabisa? Ni kichocheo chenye nguvu. Kile ambacho hufanya wengi waache ni afya, hali ya kujistahi, na upendo kwa jamaa. Lakini wengine pia wana kichocheo cha kidini—tamaa ya kufurahisha Mungu.

Kwa hiyo, namna gani kuhusu Ray, Bill, Amy, na Harley, waliotajwa katika makala yetu ya pili? Kwa nini waliacha kabisa kuvuta sigareti?

Bill, ambaye hapo kwanza alikuwa msanii mwenye madevu na nywele ndefu, alijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Halafu ikawaje? “Niliamua kwamba nilitaka kumfurahisha Mungu na kumtumikia nikiwa na mwili na akili safi. Nilijipiga konde la kifua nikaamua kuacha ghafula. Sikuacha pole kwa pole. Siku ya Januari 1, 1975 ilikuwa ndiyo siku yangu ya mwisho kupuliza sigareti halafu nikatupilia mbali pakiti ile ya sigareti. Tangu wakati huo afya yangu imepata maendeleo. Ningali na kiasi kidogo cha kusakamwa na hewa mapafuni. Lakini hata nilipata maendeleo katika nguvu zangu za kutambua rangi baada ya kuacha kabisa kuvuta sigareti.”

Amy, yule muuguzi wa upasuaji, aeleza jinsi alivyoacha kabisa. “Mimi nilisaidia katika upasuaji wa kufungua moyo wazi, nami nimeona mapafu ya aina nyingi weee—ya rangi nyekundu-nyeupe na yenye afya, meusi-meusi na yenye sumu. Hata ingawa niliona mapafu hayo yaliyogonjweka vibaya sana, yenye kuonekana ni kana kwamba yamekolezwa pilipili nyeusi, bado mimi sikuacha kuvuta sigareti. Mimi nilijipumbaza, nikisema, ‘Wewe ungali mchanga. Hilo halitakupata wewe.’

“Halafu katika 1982 nikahisi uhitaji wa kunyoosha maisha yangu, nami nikaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi. Hata ingawa nilikaa pamoja na Shahidi katika kao lake, nilikuwa nikijificha na kwenda nje paani ili nikavute kidogo! Kwa hiyo ilikuwa lazima nijibane mimi mwenyewe. Nilisali sana tena kwa muda mrefu. Lakini mara nilipokwisha kufanya uamuzi ule, ilikuwa rahisi. Siku mbili za kwanza zilikuwa mtihani, lakini sala ya daima ndiyo ilinifungulia njia.”

Harley, ambaye hapo kwanza alikuwa mrukaji wa Jeshi-Bahari, alitatizwa kuvunja tabia hiyo ya kutumia nikotini. “Nilijaribu kupunguza-punguza uvutaji wangu wa sigareti, lakini sikupata mafanikio. Halafu nilipoamua kutaka kubatizwa niwe mmoja wa Mashahidi wa Yehova, nikajipiga konde la kifua nikaamua kuacha ghafula. Nilipita katika siku mbili au tatu za maumivu makali. Nilikuwa mwenye wasiwasi, mwenye kukazika hisia, na asiyestareheka mawazo. Nikatamani sigareti weee! Ndipo Shahidi mmoja akanisaidia kwa shauri fulani zuri. ‘Utakapo kunyoosha mkono uchukue sigareti, hapo ndipo ni lazima umpelekee Yehova sala ya kuomba msaada.’ Mimi nilipata mafanikio kwa kufanya hivyo. Wazo jingine lililonivutia ni kwamba, ‘Je! ningeweza kuwazia Yesu akiwa na sigareti katika kinywa chake?’ Hilo lilikuwa jambo lisilowazika. Lakini mimi nang’amua kwamba mvutaji sigareti huhitaji kichocheo chenye nguvu ili aache kabisa. Mimi nilikuwa nikimwambia mama yangu, ‘Mama, ni mimi mwenyewe tu ninayeumia [kwa sababu ya kuvuta].’ Kwa uhakika nilikuwa nikimuumiza yeye pia, kwa njia nyingi.”

Ray pia, yule ambaye hapo kwanza alikuwa ofisa mtumikia-manahodha wa Jeshi-Bahari, hakuona ikiwa rahisi kuacha kuvuta sigareti. “Nilikuwa nimejaribu mara chache kabla sijakutana na Mashahidi wa Yehova, lakini sikupata mafanikio. Sikuzote nilikuwa nikichangamana na wavutaji wa sigareti, na ilikuwa vigumu kukataa sigareti niliyotolewa. Lakini nilipopata kujua ukweli kutokana na Biblia, nilitaka kutumikia Yehova, sawa na vile Kristo alivyokuwa amefanya. Kwa hiyo nikaacha kwa siku moja. Nilikuwa na masikitiko kwa majuma mawili. Mwili wangu ulikuwa ukiomba sana nikotini. Lakini lo, ulifanya badiliko lililoje! Kwa ghafula nikawa tena na nishati zisizo na mipaka. Nilijihisi vema kwa kufanya hivyo. Nikawa naweza tena kujidhibiti.”

Je! Inastahiki Kuacha?

Fikira za akili nzuri zaonyesha kwamba zoea lolote lenye madhara lapasa kuachwa. Lakini hatusemi kwamba uvutaji sigareti una madhara tu. Bali ni wenye hatari ya kifo, ni wenye kuua. Ni wenye sumu. Kama vile Patrick Reynolds, mrithi wa mali nyingi za tumbako, alivyotaarifu katika ushuhuda wake kwa halmashauri ndogo ya baraza kuu la United States: “Mimi naamini kwamba kutangaza sigareti ni kuendeleza bidhaa yenye sumu na kwamba ni jambo la kiadili, lenye kufaa na lililo jema kukomesha utangazaji wote wa sigareti.”

Kwa Wakristo walio na tamaa ya kufurahisha Mungu, hakika ni jambo la kiadili, lenye kufaa na lililo jema kukomesha, si utangazaji wa tumbako tu, bali pia bidhaa zote za tumbako ili zitoke katika maisha zao. Sigareti (“zilizo salama” na zisizo salama), sigara (sigari), tumbako ya kiko, na ugoro (tumbako-mnuso)—zote hizi hutoka kwenye mmea ule ule mmoja wenye sumu, ufanyizao nikotini. Nawe huhitaji mmea huo ili kuthibitisha kwamba ‘umetoka mbali, ewe kipenzi’ wala ili kuona shangwe na ladha nzuri katika maisha yako. Hata wauzaji wa ugonjwa na kifo wajaribu kukuambia nini, umamboleo wa mtu hauonyeshwi kwa kujitilia sumu yeye mwenyewe!

[Sanduku katika ukurasa wa 15]

Walioacha Biashara ya Sigareti

Katika 1875 R. J. Reynolds alianzisha kampuni ya kutafuna tumbako katika Carolina ya Kaskazini. Katika 1913 walifanyiza sigareti yao ya kwanza—ile aina ya Camel. Kutoka hapo biashara hiyo imepata ufanisi ikawa na mauzo na mapato mengi sana hivi kwamba katika United States hakuna shirika jingine la kuizidi isipokuwa lile la Philip Morris. Kitukuu cha mwanzishi huyo ni Patrick Reynolds, ambaye sasa yumo katika miaka yake ya mapema ya 40. Ingawa hapo kwanza alikuwa mvutaji sigareti kwa miaka 15, yeye aliugutusha sana ulimwengu wa wavutaji tumbako.

Katika 1986 alienda mbele ya halmashauri ndogo ya baraza kuu ili atoe ushuhuda dhidi ya kuvuta sigareti! Tangu wakati huo yeye amekuwa akifanya kampeni ya ukawaida dhidi ya utumizi wa tumbako. Ni nini kilichoanzisha maoni yake ya kutotaka bidhaa iliyoiletea jamaa yao utajiri mkubwa? Ni kwa sababu yeye akumbuka kwamba baba yake, aliyekuwa mvutaji wa kupindukia, aliuawa na ugonjwa wa kusakamwa na hewa mapafuni huku yeye akiwa anamtazama. Patrick alitaarifu hivi: “Kumbukumbu za pekee nilizo nazo ni kwamba baba yangu alikuwa sikuzote akiishiwa na pumzi, akihesabu wakati wake wa kuishi uliobaki.”

Patrick aliamua kutumia maisha yake kwa njia yenye matokeo mazuri. “Niliona kwamba ningeweza kufanyiza tofauti fulani nitumie maisha yangu kwa njia yenye faida.” Yeye alisema kwamba kuzidi kuendeleza “viuaji vilivyothibitishwa” kungekuwa “jambo ambalo ni wazi si la kiadili.”

“Ikiwa mkono ulionilisha wakati mmoja ni ile biashara ya tumbako, basi mkono uo huo ndio umeua mamilioni ya watu na utaendelea kuua mamilioni zaidi ikiwa watu hawataamka wazione hatari za sigareti.”—The New York Times, Oktoba 25, 1986.

David Goerlitz ndiye aliyekuwa akitumiwa kuwa yule mwanamume hodari wa Winston juu ya matangazo ya sigareti za Winston. Yeye amekwisha acha matangazo yake ya sigareti na sasa amekuwa mnenaji kwa niaba ya Sosaiti ya Kansa Amerika. Ni nini kilichombadili? Katika hoji moja katika televisheni, Desemba 29, 1988, alisema hivi: ‘Mimi nilizuru ndugu yangu katika wodi ya kansa kwenye hospitali moja katika Boston. Hiyo ilinionyesha ana kwa ana athari za kazi yangu—wagonjwa wa kansa waliokuwa wakiteseka kwa sababu ya kuvuta sigareti. Nikaziona athari zenye kuwaharibu sana majeruhi wa uvutaji sigareti na wale walio majeruhi wa majeruhi, yaani, jamaa zao. Niliona wanaume wa miaka 40 na kitu wakiwa bila nywele, wakiwa na mirija katika koo na tumbo zao. Nikahisi nikiwa mwenye hatia na kuamua kuacha kabisa kutangaza tumbako.’ ◼

[Picha katika ukurasa wa 14]

“Mimi nilisaidia katika upasuaji wa kufungua moyo wazi, nami nimeona mapafu ya aina nyingi weee”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki