“Waweza Kuacha—Sisi Tuliacha!”
NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA JAPANI
Kulingana na masimulizi fulani, meli za Ulaya zilizotia nanga Japani miaka ya mwisho-mwisho ya 1500 zilibeba wageni waliokuwa wakivuta sigareti, ambao walionekana kana kwamba “wanachochea moto ndani ya tumbo.” Mshangao huo ukawa udadisi, hivi kwamba kufikia miaka ya 1880, zoea la tumbaku lilikuwa limekuwa la kawaida katika Japani. Ni nani ambaye angefikiria kwamba wazao wa Wajapani hao waliokuwa wameshangaa leo wangekuwa miongoni mwa wavutaji wakubwa zaidi wa sigareti ulimwenguni?
“TULITAKA tujihisi kuwa watu wazima, tuzifahamu hisia-moyo za utu mzima.”—Akio, Osamu, na Yoko.
“Nilitaka kupunguza uzani.”—Tsuya.
“Ulikuwa udadisi tu.”—Toshihiro.
“Hatukufikiri kwamba tumbaku ingetuathiri vibaya.”—Ryohei, Junichi, na Yasuhiko.
“Sikutaka nihisi vibaya kutokana na kichefuchefu nilipokuwa na mimba ya pili.”—Chieko.
“Niliivuta ili nisione fedheha katika nyakati za kufedhehesha kwenye mikutano ya kikazi.”—Tatsuhiko.
Hizo ndizo sababu zilizotolewa wakati kikundi kimoja cha watu hapa kilipoulizwa kwa nini kilianza kuvuta sigareti. Maelezo hayo yanaeleweka vizuri, kwa kufikiria kwamba wengine huiita Japani paradiso ya wavutaji-sigareti. Ingawa hivyo, kwa kustaajabisha, hao watu wote waliotajwa wameacha zoea la tumbaku. Huo ni utimizo mkubwa sana unapofikiria vizuizi vinavyotokana na mazingira yao. Je, wajiuliza jinsi walivyoacha? Ebu tuchunguze kwanza jinsi ambavyo zoea la tumbaku limeenea sana Japani leo.
Tumbaku Leo
Karibu asilimia 56 ya wanaume Wajapani huvuta sigareti, wakilinganishwa na asilimia 28 tu ya wanaume Wamarekani walio na umri wa miaka 15 au zaidi. Wavutaji-sigareti wa Japani wapatao 34,000,000 wanatia ndani asimilia 22 ya wanawake, wengi wao wakiwa vijana. Vielelezo vya watu wazima na matangazo ya werevu yamechangia sana ongezeko la haraka la vijana wavutaji-sigareti. Matangazo ya sigareti kwenye televisheni na redio, ambayo yalipigwa marufuku Marekani zaidi ya miongo miwili iliyopita, sasa yamepigwa marufuku Japani.
Zaidi ya hilo, sigareti hupatikana kwa urahisi katika mashine nyingi za kuuzia za pembeni za barabara za Japani. Mara washikapo pakiti hiyo mkononi, ni wachache tu ambao hutii ujumbe dhaifu na wa kijuu-juu tu uliochapwa juu yake. Huenda kibandiko kikasema tu: “Tusivute sigareti sana; inaweza kudhuru.” Na kuongezea uhakika wa kwamba hatari mbaya za tumbaku mara nyingi huendelea, kielelezo kibaya cha watu wengi mashuhuri pia hutia moyo Wajapani wavute sigareti, ikiwahadaa kuwa wana aina fulani ya usalama.
Si ajabu, kwamba wapinzani wa uvutaji-sigareti hulaumu uzembe wa Japani wa kutofanya raia wake wengi waache kutumia tumbaku. Lakini waelimishaji wanaanza kuona umaana na kuonya watu kwamba kuvuta sigareti huhatarisha afya yao na uhai wao. Naam, wavutaji-sigareti Wajapani hupatwa na magonjwa yaleyale kama wavutaji-sigareti kwingineko—kichefuchefu, kutopumua vizuri, kukohoa daima, kuumwa na tumbo, kupoteza hamu ya kula, kushikwa na homa kwa urahisi, na labda baada ya muda fulani, kifo cha mapema kutokana na kansa ya mapafu, maradhi ya moyo, au matatizo mengineyo.
Tangu Aprili 1, 1985, utengenezaji wa tumbaku nchini Japani ulifanywa uwe biashara ya kibinafsi, ikikomesha miongo kadhaa ya kudhibitiwa na serikali. Hata hivyo, bado huo hufurahia uhusiano wa karibu na serikali ambao huzuia hatua zozote kubwa za kukataza kuvuta sigareti. Hiyo ndiyo sababu vikundi vya kupinga tumbaku huona Japani leo kuwa mahali salama pa wavutaji-sigareti. Na yaonyesha sababu inayofanya The Daily Yomiuri liripoti kwamba madaktari hapa wanasikitikia kwamba Japani “ni jamii inayotia moyo uvutaji-sigareti.”
Ili kuona jinsi wengine walivyofanikiwa kuacha, ona sanduku “Jinsi Tulivyoacha.”
Waweza Kuachaje?
Shauri kutoka kwa wapenda-tumbaku wa zamani, kama wale walio katika sanduku kwa ufupi ni hili: Nuia kabisa kuacha. Kumpenda Mungu na tamaa ya kumpendeza ndilo jambo bora zaidi. Na kumpenda jirani yako ni jambo jingine zuri. Weka mradi, na uushikilie. Julisha hadharani kwamba unaacha—ambia rafiki zako, pata msaada wa washiriki wa familia yako. Acha kwa ghafula, ikiwezekana. Na ufanye yote uwezayo kuepuka mazingira ya uvutaji-sigareti.
Ikiwa unajifunza Biblia, endelea kushirikiana na Mashahidi wa Yehova. Ukiwa miongoni mwao, utapoteza tamaa yako ya kuvuta sigareti upesi. Kwa upande mwingine, ikiwa wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova unayejifunza Biblia na mvutaji-sigareti, usikate tamaa juu yake. Msaidie ampende Yehova zaidi ya zoea lake lenye kudhuru.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 16, 17]
“Jinsi Tulivyoacha”
Mieko: “Nilipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, nilikuwa na uhakika kwamba singeweza kuacha kuvuta sigareti. Nia yangu ya kujifunza ilikuwa kwamba angalau watoto wangu wajifunze njia ya kupata uhai. Lakini punde si punde nikatambua kwamba lazima mzazi aweke kielelezo chema, kwa hiyo nikaanza kusali kwa bidii kwa Yehova Mungu anisaidie. Ilihitaji jitihada kufanyia kazi sala yangu, nami nilihisi vibaya sana kwa muda fulani. Lakini sitasahau kamwe hisia nzuri ajabu ya dhamiri safi ambayo niliiona hatimaye nilipoacha uovu huu mchafu.”
Masayuki: “Baada ya kuwa mvutaji-sigareti wa pakiti tatu kwa siku na baada ya kujaribu sana na kushindwa, hatimaye nilizima sigareti yangu ya mwisho na kuacha tumbaku. Familia yangu, Mashahidi wenzangu, na Yehova Mungu walinisaidia kuacha. Katika benki ambako nilifanya kazi, hakuna aliyeamini kwamba nimeacha. Nilidokeza kwamba, kwa kuwaheshimu wateja wetu, wafanyakazi wa ofisi katika sehemu ya watu wote ya benki wasivute sigareti saa za kazi. Dokezo langu lilikubaliwa, hata ingawa asilimia 80 ya wafanyakazi walikuwa wavutaji-sigareti. Zoea hilo sasa limeenea katika matawi 260 ya benki yetu.”
Osamu: “Nilipokuwa nikijifunza kweli ya Neno la Mungu, Biblia, nilijua ni lazima niache kuvuta sigareti. Ilinichukua mwaka mmoja hivi. Hata nilipoacha, kwa miezi sita mingine, ilinibidi nipigane na tamaa ya kuvuta sigareti. Nilijua moyoni mwangu kwamba ni lazima nitake kuacha.”
Toshihiro: “Dhabihu ya fidia ya Yesu ilinivutia sana hivi kwamba nikahisi ningeweza angalau kujidhabihu kuacha kuvuta sigareti.”
Yasuhiko: “Uamuzi wangu wa kumtii Yehova Mungu na kuacha kuvuta sigareti uliokoa uhai wangu. Siku moja, chumba ambacho nilikuwa nikifanyia kazi kilijaa gesi ya propani iliyokuwa ikivuja. Kwa kawaida, ningewasha sigareti, ambayo ingesababisha mlipuko. Lakini kwa kuwa nilikuwa nimeacha kuvuta sigareti siku chache kabla ya hapo, leo niko hai kuzungumzia jambo hilo.”
Akio: “Nilipoanza kuhisi kichefuchefu mara kwa mara, nilikisia kwamba uvutaji-sigareti ulikuwa unaniumiza. Lakini sikuacha. Nilipata habari ya hakika ya kwanza kuhusu hatari za uvutaji-sigareti kwa mke wangu, ambaye alikuwa amekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Upesi nikaanza kujifunza Biblia, nikajifunza kutokana na vichapo vya Watch Tower kwamba mvutaji-sigareti hajiumizi mwenyewe tu bali pia huumiza washiriki wa familia yake. Nikakoma mara moja!”
Ryohei: “Mke wangu alikuwa akininunulia sigareti—pakiti 20 mara moja. Lakini baada ya kujifunza Biblia na Mashahidi, alikataa kununua kitu ambacho alijua kingenidhuru. Basi nikafungua duka langu mwenyewe la tumbaku. Nilikuwa nikivuta pakiti tatu na nusu kwa siku. Kisha nikaanza kujifunza Biblia na Mashahidi. Punde si punde nikataka kuwa msemaji mzuri wa habari za Biblia. Kwa hiyo, nikaacha kuvuta sigareti ili nistahili mazoezi haya katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.”
Junichi: “Binti yangu mdogo ambaye ni Shahidi, alihangaikia maisha yangu. Alinifanya niahidi kuacha kuvuta sigareti, nikaacha.”
Tsuya: “Nilipotembelea Jumba la Ufalme kwa mara ya kwanza, niliomba kisahani cha kuwekea jivu na kiberiti nilipokuwa nikiingia. Nilishangaa nilipoambiwa kwamba watu hawavuti sigareti huko. Nilijua ni lazima niache kuvuta sigareti. Siku nane nilizokaa hospitalini zilinisadikisha kwamba sikutaka kamwe kuhisi uchungu wa kuacha tena.”
Yoko: “Nilijifunza jambo hilo katika magazeti na vichapo vingine vya Mashahidi wa Yehova, vikionyesha jinsi Yesu alivyokataa dawa za kulevya alizopewa wakati alipokuwa karibu kupigiliwa msumari kwenye mti wa mateso. Nilisali kwa Yehova Mungu, nikimwambia kwamba nataka kuwa msifaji safi wa jina lake. Baada ya hapo, sikuvuta sigareti tena. Watu waliokuwa karibu nami walipovuta sigareti, nilikuwa karibu kutaka kuvuta moshi wao, lakini niliondoka penye moshi haraka, kwa kuwa sikutaka hamu yangu ya kuvuta sigareti inirudie.”
Hawa wavutaji-sigareti wa zamani wameazimia kutovuta sigareti tena kamwe. Je, wewe ni mvutaji-sigareti anayetaka kuacha zoea hilo?
Mieko
Osamu
Yasuhiko
Akio na mkewe, Sachiko
Junichi na bintiye Meri
Yoko