Neno la Mungu Li Hai
Je! Wewe Waweza Kuona Yasiyoonekana?
JE! WEWE umepata kuwa katika taabu ya kweli kweli? Je! ilielekea kwamba hakukuwa na njia ya kutokea, ikaelekea kuwa hakuna uwezekano wa kuondolea taabu hiyo? Hivyo ndivyo kijana mmoja alivyoona katika siku za Elisha, nabii wa Mungu.
Tukitazama nyuma katika wakati huo, twaona kwamba Washami wanapigana na Waisraeli. Hata hivyo, sikuzote mfalme wa Israeli alielekea kutangulia kujua sehemu ambayo Washami wangeshambulia. Kwa hiyo Mfalme wa Washami anawaita maafisa wake, kama unavyoweza kuona, na kuwauliza: ‘Ni nani kati yetu anayetoa siri ya miendo ya majeshi yetu kwa mfalme wa Israeli?’
‘Hapana ye yote,’ ajibu afisa mmoja. ‘Ni Elisha, yule nabii Mwisraeli. Yeye anajua unayosema hata katika faragha ya chumba chako mwenyewe, naye anamwambia mfalme wa Israeli.’
‘Mtafuteni,’ aamuru mfalme, ‘ili twende na kumkamata.’ Baadaye, mfalme apelekewa ripoti hivi: “Yuko [huko, katika mji wa] Dothani.” Kwa hiyo anatuma jeshi kubwa huko likiwa na farasi na magari yao. Askari hao wafika katika mji huo usiku na kuuzingira.
Mapema asubuhi iliyofuata mtumishi wa Elisha atoka nje, na tazama! kuzunguka mahali pote liko jeshi la Washami! Kijana huyo akiogopa sana amwambia Elisha: “Ole wetu! bwana wangu, tufanyeje”?
“Usiogope,” akajibu Elisha kwa utulivu. Kisha asema jambo linalosikika kuwa lenye kushangaza sana kwa mtumishi wake. “Walio pamoja nasi ni wengi kuliko wale walio pamoja nao.” Lakini hilo laweza kuwaje?
Elisha anaomba: “Ee [Yehova], nakusihi, mfumbue macho yake, apate kuona.” Na mara hiyo macho yake yanafumbuliwa yapate kuona yasiyoonekana kwa kawaida. Huko vilimani kuna farasi na magari yenye moto kuzunguka pande zote. Ndiyo, Yehova afumbua macho yake kwa mwujiza apate kuona majeshi Yake ya kimbinguni!—2 Fal. 6:8-23.
Je! hiyo yamaanisha kwamba malaika za Mungu wako tayari kusaidia watumishi wake leo? Ndiyo, inamaanisha hivyo! Wapo kweli kweli, ijapokuwa hatuwezi kuwaona. Nao wanaweza kutusaidia, kama vile walivyomlinda Elisha na mtumishi wake wasipate umizo lo lote. Je! wewe waona, kupitia kwa jicho lako la fahamu, majeshi ya Mungu ya kimbinguni?