Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 8/15 kur. 19-24
  • Je! Wewe Unathamini “Mtumwa Mwaminifu Mwenye Akili”?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Wewe Unathamini “Mtumwa Mwaminifu Mwenye Akili”?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Nl NANI YULE MTUMWA MWAMINIFU MWENYE AKILI?”
  • “MTUMWA MWAMINIFU” AACHA KUONEKANA WAZIWAZI
  • “MTUMWA MWAMINIFU” AJULIKANA KWA SABABU YA UTENDAJI WAKE
  • USHUHUDA MWINGI SANA
  • “Mtumwa” Ambaye Ni Mwaminifu na Mwenye Busara
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • “Ni Nani kwa Kweli Mtumwa Mwaminifu na Mwenye Busara?”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Wakristo Wanalishwaje Kiroho?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Msimamizi-nyumba Mwaminifu na Baraza Lake Linaloongoza
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 8/15 kur. 19-24

Je! Wewe Unathamini “Mtumwa Mwaminifu Mwenye Akili”?

“NI NANI basi yule mtumwa mwaminifu mwenye akili?” Yesu alianza kutoa mfano wenye maana ya kiunabii kwa kutumia ulizo hilo. Ni sehemu ya “ishara” ambayo alitoa kuhusiana na “mwisho wa taratibu ya mambo,” ambayo tunaishi ndani yake. (Mt. 24:3, NW) Baada ya kuwaagiza wanafunzi wake waendelee kulinda, Yesu alisema hivi:

“Ni nani basi yule mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya nyumba yake, awape watu chakula kwa wakati wake? Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo. Amin, nawaambieni, atamweka juu ya vitu vyake vyote.”​—Mt. 24:42-47.

“Mtumwa” huyo ni nani nao watu wa “nyumba” ni nini? “Vitu” ni nini? Maulizo hayo si ya kutaka kupata elimu tu. Kujua ifaavyo na kushirikiana na “mtumwa mwaminifu mwenye akili” kutamaanisha furaha nyingi na zawadi nyingi za kiroho.

“Nl NANI YULE MTUMWA MWAMINIFU MWENYE AKILI?”

Wengine husema kwamba “mtumwa” anamaanisha wahudumu Wakristo, au cheo chao cha usimamizi, pamoja na daraka la kuangalia mahitaji ya kiroho ya kundi. Kufika kwa “bwana” kunasemekana kuwa ni ama kuja kwa pili kwa Kristo au kifo cha mhudumu mmoja mmoja. Hivyo inasemekana kwamba wahudumu Wakristo wapaswa kuchochewa na mfano huo ili waangalie vizuri vitu walivyokabidhiwa.

Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba mfano huo unahusu kundi moja la kweli la wafuasi wa Yesu Kristo waliotiwa mafuta. Kuanza Pentekoste, 33 W.K., na kuendelea kwa karne 19 tangu wakati huo, kundi hilo linalofanana na mtumwa limekuwa likilisha washiriki wake kiroho, likifanya hivyo kwa akili. Sana sana “mtumwa” huyo amejulikana vizuri zaidi wakati wa kurudi au kuwapo kwa Kristo. “Mtumwa” huyo anajulikana kwa sababu ya kulinda na uhakika wa kwamba anatoa chakula cha kiroho kinachohitajiwa na wote katika kundi la Kikristo. Hakika, “mtumwa” huyo, au kundi lililotiwa mafuta kwa roho, ndiye njia moja pekee inayokubaliwa ya kuwakilisha ufalme wa Mungu duniani “wakati wa mwisho.” (Dan. 12:4) Mashahidi wa Yehova wanafahamu kwamba “mtumwa” ni washiriki wote Wakristo waliotiwa mafuta wakiwa kikundi duniani wakati wo wote ule katika karne 19 tangu Pentekoste. Hivyo, watu wa “nyumba” ni wale wafuasi wa Kristo wakiwa mtu mmoja mmoja.

Huenda wasomaji wengine wakaona kwamba hivyo ni kuangalia mambo kama dhehebu. Au huenda wakakataa wazo la kwamba “mtumwa” na watu wa “nyumba” wanawakilisha jamii ile ile, moja ikiwa ni jamii ya washiriki wote na ile nyingine ikiwa ni watu mmoja mmoja. Watu hao wenye kukataa huenda wakabisha kwamba si wanafunzi wote wa Kristo waliotiwa mafuta wanaoshiriki kutayarisha chakula cha kiroho, hivyo kwamba pengine “mtumwa” anafananisha wale tu wanaoongoza, nao watu wa “nyumba” wanafananisha wale wanaowatumikia katika makundi.

Hakuna sababu ya kujaribu kulazimisha pawe ufasiri mwingine wa mfano huo. Kujidanganya hakufaidi cho chote nako kunaharibu kiroho. Kwa hiyo, lazima tuangalie Maandiko ili tufahamu. Kwa kufanya hivyo, tunaonaje? “Mtumwa” huyo ni mtumishi wa Bwana Kristo Yesu na Babaye, Yehova. (Linganisha Mathayo 10:24, 25.) Na mtumishi aweza kuwa kikundi chenye washiriki wengi. Katika wakati uliopita, taifa lote la Israeli lilikuwa mtumishi wa Yehova, au mtumwa. Yeye aliwaambia hivi: “Nawe, Israeli, [wewe ni] mtumishi wangu.” (Isa. 41:8, 9; 44:21) Mtumishi huyo mmoja, washiriki wake walikuwa watu mmoja mmoja, kama ambavyo Isaya 43:10 linavyoonyesha kwa husema hivi: “Ninyi ni mashahidi wangu [kwa wingi], asema [Yehova] na mtumishi [mmoja] niliyemchagua; mpate kujua, na kuniamini.” Waisraeli hao wa nyakati za kale walikuwa “mali ya pekee” ya Yehova, “taifa takatifu.” (Kut. 19:5, 6, NW) Hata ingawa si kila mtu mmoja mmoja aliyeshiriki kusimamia mambo ya taifa hilo, watu wote ndio waliokuwa washiriki wa taifa hilo moja, “mtumishi” wa Mungu. Ni wachache tu walioshiriki kuandika au kunakili Maandiko Matakatifu, hata hivyo mtume Paulo alisema hivi juu ya watu wa Israeli: “Wamekabidhiwa mausia ya Mungu.” (Rum. 3:1, 2) Maagano, Sheria na ahadi zilikuwa zao. (Rum. 9:3-5) Kwa hiyo taifa lote lilikuwa “mtumishi” aliye jamii, hali wakati uo huo washiriki wake walikuwa watu mmoja mmoja, “mashahidi” wake.

Yesu alipokuwa duniani, aliambia hivi viongozi wa kidini wa Israeli: “Ufalme wa Mungu utaondolewa kwenu, nao watapewa taifa lingine lenye kuzaa matunda yake.” (Mt. 21:43) “Taifa” hilo lenye kuzaa matunda ya Ufalme lazima liwe ni kundi la Kikristo ambalo limeenea sana, na juu yake Petro aliandika hivi: “Ninyi ni . . . ‘taifa takatifu, watu walio mali ya pekee, ili mtangaze mbali sifa’ zake [Mungu] mmoja aliyewaita toka gizani na kuingia kwenye nuru yake ya ajabu. Kwa kuwa wakati mmoja ninyi hamkuwa watu, lakini sasa mu watu wa Mungu.” (1 Pet. 2:9, 10, NW) Kundi hilo linaitwa pia “Israeli wa Mungu” na “nyumba ya Mungu.” (Gal. 6:16; 1 Tim. 3:15) Watu mmoja mmoja katika kundi wanaitwa “washiriki wa nyumba ya Mungu.” (Efe. 2:19, NW) Kuwa ‘mawakili waaminifu’ kwa washiriki hao wa nyumba kunatia ndani kutoa kweli za kiroho, ambazo ndizo “chakula” kinachofaa kwa waamini. (1 Kor. 3:2-5; 4:1, 2) Inafaa kuangaliwa kwamba “mtumwa mwaminifu mwenye akili” anaitwa “wakili” katika Luka 12:42-48.

Walipokuwa wakiishi duniani, mitume waaminifu wa Yesu walikuwa na daraka hasa la kutoa chakula cha kiroho kwa “nyumba ya Mungu.” ‘Wachungaji’ waliowekwa wa “kundi,” pamoja na wengine, vilevile walikuwa na daraka kama hilo. Hata hivyo, mtume Petro anaonyesha kwamba uwakili huo wa kweli za kimungu kwa kweli walipewa wote ‘walioteuliwa.’ Hivyo, kila mshiriki mmoja wa kundi alishiriki katika kuujenga mwili. (Efe. 4:11-16; 1 Pet. 1:1, 2; 4:10, 11; 5:1-3) Hivyo tunaona msingi wa Kimaandiko wa kusema kwamba wafuasi wote wa Kristo Yesu waliotiwa mafuta ni washiriki wa “mtumishi” wa Mungu, naye Yesu akiwa Bwana wao. Hivyo, mtumishi huyo, au “mtumwa,” akiwa ni jamii yenye washiriki wengi anatoa chakula cha kiroho kwa watu mmoja mmoja wa kundi hilo, ambalo washiriki wake ni watu wa “nyumba.” Wao wakiwa mtu mmoja mmoja wanafaidika wakiwa wapokeaji wa chakula hicho.​—1 Kor. 12:12, 19-27; Ebr. 3:5, 6; 5:11-14.

“MTUMWA MWAMINIFU” AACHA KUONEKANA WAZIWAZI

Kuonekana waziwazi kwa jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” hakukuendelea katika karne zote mpaka kurudi kwa Bwana akiwa na uwezo wake wa kifalme. Mitume walionya kwamba ukafiri mkubwa ungetokea baada ya kufa kwao nao ungeendelea mpaka wakati wa kuwapo kwa Kristo. (2 The. 2:1-12; Matendo 20:29, 30; 1 Yohana 2:18, 22; 4:2, 3) Vilevile Yesu alionyesha jambo hilo katika mfano wake wa ‘ngano na magugu.’ Kulingana na mfano huo, mbegu nzuri, ngano, zilipandwa ulimwenguni. “Ngano” ni “wana wa ufalme,” au wanafunzi wa kweli waliotiwa mafuta wa Yesu Kristo. Hata hivyo, “adui” (Ibilisi) alionyeshwa kuwa alipanda “magugu” (“wana wa yule mwovu,” au Wakristo wa uongo) kati ya “ngano,” navyo vyote viwili vingekua pamoja mpaka wakati wa “mavuno.”​—Mt. 13:24-30, 36-43.

Ukafiri huo ulisitawi wakati wa kuleta filosofia zisizo za adili na mafundisho ya uongo. Kundi hilo kafiri likaendelea kuwa sehemu ya ulimwengu zaidi na zaidi, likafuatisha mafundisho yake, desturi na maoni pia. Yesu alitabiri kwamba “ngano” na “magugu” vingekua pamoja mpaka wakati wa “mavuno,” au “mwisho wa taratibu ya mambo,” wakati ambapo “ngano” (Wakristo wa kweli) ingetenganishwa na “magugu” (Wakristo wa uongo) na kuangaza kiroho. (Mt. 13:30, 39-43, NW) Basi kuonekana kwa jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye akili” hakungekuwa wazi mpaka wakati wa kurudi kwa Kristo Yesu.

Wakati huo, wanafunzi waaminifu wa Yesu wangeonekana wazi. Hali yao ya kulishwa vema ingepatana na unabii wa Danieli, ambao ulitabiri kwamba “wakati wa mwisho” wenye ufahamu wangeng’aa kama nyota, wangefurahia maarifa ya Kimaandiko na ufahamu ulioongezeka na kuleta wengi katika haki. (Dan. 12:3, 4, 9, 10) Hiyo inaonyesha kwamba kundi la wanafunzi waliotiwa mafuta wa Kristo, wenye ufahamu, wangekuwa wakilinda ili kuona kurudi kwa Bwana na kupatikana wakitoa chakula cha kiroho kwa uaminifu kwa wakati wake, wakati wa kurudi kwake.​—Mt. 24:43-46.

“MTUMWA MWAMINIFU” AJULIKANA KWA SABABU YA UTENDAJI WAKE

Ingawa “magugu” yalikuwa yametawala sehemu ya kidini wakati wa karne hizo, “ngano” fulani ilikuwa ikitenda na chakula cha kiroho kilitolewa kwa watu wa “nyumba.” Mapema katika miaka ya kuanzia na wa 1870 palikuwako kikundi cha wanafunzi wa Biblia wanyofu ambao walikuwa wanalishwa kiroho vizuri kutosha ili watazamie kurudi kwa Bwana na kutambua uhitaji wa kujifunza kikamilifu Maandiko ili wawe tayari. Uchunguzi wao usio wa kimadhehebu ulitokeza wingi wa maarifa.

Wakati wa miaka hiyo, makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yalikuwa yamefungwa na mapokeo, mafundisho yasiyo na msingi na sherehe zenye kutokana na ukafiri mkuu. Yalishikilia mafundisho ya uongo kama Utatu, kutokufa kwa nafsi na moto wa mateso. Vilevile, yalikuwa sehemu ya ulimwengu. Seminari zao za kufunza dini zilikuwa zinatilia Biblia mashaka. Kisio la mageuzi la Darwin lilikuwa linalinganishwa na masimulizi ya Biblia juu ya uumbaji, sayansi ilikuwa inakataa fundisho juu ya dhambi iliyorithiwa na uhitaji wa ukombozi, na uchambuzi wote juu ya Biblia ulikuwa unapinga kwamba Maandiko yameandikishwa na Mungu nayo hayakosei.

Katikati ya mambo hayo yote, Wanafunzi wa Biblia (ndivyo Mashahidi wa Yehova walivyokuwa wakiitwa wakati huo) walikuwa imara wakiwa mawakili wenye nguvu wa mafundisho ya Biblia. Walishikilia Kimaandiko kwamba Mungu Mwenye Nguvu Zote na aliye Muumba, Yehova, ni mmoja, na kwamba Kristo Yesu ndiye Mwana wake wa pekee na kiumbe wa kwanza, ambaye Mungu alituma duniani ili atoe uhai wake uwe ukombozi kwa wanadamu wenye dhambi. Walipiga vita vya kutetea Biblia yote kuwa Neno la Mungu, lisilokosea na lililoongozwa kwa roho yake nao wakaandika matokeo ya uchunguzi wao wa Biblia ukawa “chakula kwa wakati wake,” hivyo wakashiriki habari hiyo ya maana pamoja na wale wote wenye kutamani kuwa tayari wakati wa kurudi kwa Bwana. Wanafunzi wa Biblia walijulisha fundisho la kweli la Kikristo kwamba nafsi ya kibinadamu inakufa na tumaini kwa wafu ni ufufuo. Walionyesha kwamba kusudi la ukombozi wa Yesu si kufungulia njia tu wale 144,000 ambao wangekombolewa kutoka duniani ili wawe warithi-washirika na Kristo mbinguni bali pia kupatia wazao wengine wa Adamu nafasi ya kupata uzima wa milele duniani wakati wa utawala wa Ufalme wa Kimasihi wa miaka 1,000. Vilevile walitangazia ulimwengu kwamba mwisho wa “nyakati za mataifa zilizowekwa” ungefika mwaka 1914. (Luka 21:24, NW) Kurudishwa huko kwenye kutia nguvu imani kwa kweli za Biblia na kusihi juu ya kuwa macho kuhusiana na kuwapo kwa Kristo Yesu kulitokeza kukusanywa kwa wanafunzi waliotiwa mafuta wa Kristo ambao walionyesha ushuhuda wa kulishwa vema kiroho.

USHUHUDA MWINGI SANA

“Mtumwa mwaminifu mwenye akili” ana ushuhuda mwingi sana. Chini hapa pana sehemu ya maandishi ya Kimaandiko na majina ya kiunabii yanayohusu au yanayowakilisha mabaki ya wafuasi wa Yesu Kristo waliotiwa mafuta tangu mwaka wenye kutokeza wa 1919;

(1) Mke wa Noa, Mwa. 7:7; (2) malaika waliotumwa kwa Loti, Mwa. 19:15; (3) Rebeka, Mwa. 24:64; (4) Yusufu na Benyamini, Mwa. 45:14; (5) mavuno ya kuokotwa yaliyoachwa nyuma, Law. 19:9; (6) wapelelezi wawili waliotumwa kwa Rahabu, Yos. 2:4; (7) Baraka, Amu. 4:14; (8) Yeftha, Amu. 11:34; (9) Naomi na Ruthu, Ruthu 2:2; (10) mashujaa Waisraeli wa Daudi, 2 Sam. 18:1; (11) Yehu, 2 Fal. 10:11, 15 (12) Mordekai na Esta, Esta 4:13; (13) Ayubu, Ayubu 42:10, 13; (14) binti ya Mfalme, Zab. 45:13; (15) watu wenye fadhili za upendo, Zab. 50:5; (16) kikundi cha urafiki, Zab. 89:7, NW; (17) Shear-yashubu, Isa. 7:3; (18) nuru ya mataifa, Isa. 60:3; (19) miti mikubwa ya haki, Isa. 61:3; (20) wahudumu wa Mungu, lsa. 61:6; (21) kichala kilichohifadhiwa, Isa. 65:8; (22) watumishi wenye jina jingine, Isa. 65:15; (23) watu wenye kutetemeshwa na neno la Mungu, Isa. 66:5; (24) taifa jipya lililozaliwa, Isa. 66:8; (25) Yeremia, Yer. 1:10; (26) watu wa Yehova katika agano jipya, Yer. 31:33; (27) mlinzi mwenye kuvumilia, Eze. 3:16-27 (28); mtu aliyevaa kitani, Eze. 9:2; (29) watu waliosafishwa, Eze. 36:29-32; (30) wakaaji katikati ya dunia, Eze 38:12; (31) jeshi la mbinguni, Dan. 8:10; (32) patakatifu parudishwa (pasafishwa), Dan. 8:14; (33) wao walio na hekima, Dan. 11:33; (34) mwenye furaha anayeendelea kungojea, Dan. 12:12; (35) wenye nyama wote wanaopokea roho, Yoeli 2:28; (36) Yona, Yon. 3:1-3 (37) mboni ya jicho la Yehova, Zek. 2:8; (38) mabaki waliokombolewa, Zek. 2:7; (39) Myahudi, Zek. 8:23; (40) wana wa Lawi, Mal. 3:3; (41) ngano, Mt. 13:25; (42) wana wa ufalme, Mt. 13:38; (43) wafanya kazi wa shamba la mizabibu, Mt. 20:1; (44) wale walioalikwa kwenye karamu ya arusi, Mt. 22:3-14; (45) waliochaguliwa, Mt. 24:22; (46) tai, Mt. 24:28; (47) mtumwa mwaminifu mwenye akili, Mt. 24:45; (48) wanawali wenye akili, Mt. 25:2; (49) ndugu za mfalme, Mt. 25:40; (50) kundi dogo la kondoo, Luka 12:32; (51) Lazaro mwenye kuomba-omba, Luka 16:20; (52) kondoo wa “zizi hili,” Yohana 10:1-16; (53) matawi ya mzabibu, Yohana 15:4; (54) nyumba ya kifalme ya Daudi, Matendo 15:16; (55) warithi pamoja na Kristo, Rum. 8:17; (56) mabaki, Rum. 11:5; (57) matawi katika mzeituni, Rum. 11:24; (58) watakatifu, 1 Kor. 6:2; Ufu. 16:6; (59) hekalu, 1 Kor. 6:19; (60) kiumbe mpya, 2 Kor. 5:17; (61) mabalozi wa Kristo, 2 Kor. 5:20; (62) kundi la Mungu, Gal. 1:13; (63) sehemu ya uzao wa Ibrahimu, Gal. 3:29; (64) Israeli wa Mungu, Gal. 6:16; (65) mwili wa Kristo, Efe. 1:22, 23; (66) askari wa Kristo Yesu, 2 Tim. 2:3; (67) nyumba inayosimamiwa na Kristo, Ebr. 3:6; (68) ukuhani mtakatifu, 1 Pet. 2:5; (69) taifa takatifu, 1 Pet. 2:9; (70) ushirika wa kina ndugu, 1 Pet. 2:17; (71) makundi saba, Ufu. 1:20; (72) wazee 24, Ufu. 4:4; (73) Israeli wa kiroho, Ufu. 7:4; (74) nzige, Ufu. 9:3; (75) mashahidi wawili, Ufu. 11:3; (76) mizeituni miwili, Ufu. 11:4; (77) uzao wa mwanamke, Ufu. 12:17; (78) Yerusalemu Mpya, Ufu. 21:2; (79) bibi-arusi wa Kristo, Ufu. 22:17; 19:7; (80) mashahidi wa Yehova, Isa. 43:10.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki