Wakristo Wanalishwaje Kiroho?
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1, 2. (a) Twaweza kuuliza maulizo gani juu ya namna Wakristo wanavyolishwa kiroho? (b) Kwa sababu gani ilifaa Yesu awaite wanafunzi wake “watumwa”?
MUNGU analishaje watu wake kiroho? Je! hilo lafanywa kwa watu mmoja mmoja, yaani, Wakristo wanapata chakula chao kama watu walio peke yao, wenye kujitegemea wenyewe, bila kuwa na lazima ya kushirikiana na Wakristo wengine wenye imani ya kweli? Je! wanaweza kujifunza Biblia wao wenyewe tu na kumtumikia Mungu bila kutegemea ye yote?
2 Twaweza kupata jibu la maulizo haya kwa kuangalia mambo ambayo Yesu Kristo aliwaambia mitume wake siku tatu tu kabla ya kufa kwake. Alipokuwa akizungumza juu ya mambo yatakayokuja, alikuwa ameeleza kirefu matukio ambayo yangekuwa “ishara” ya kuwapo kwake wakati ambapo angerudi akiwa na mamlaka na utukufu wa kimbinguni. Aliwaonya wakeshe wakitazamia awakague na kuwahukumu wanafunzi wake, ambao aliwaita “watumwa.” (Mt. 24:1-44, NW) Angeweza kutumia neno hili kwao kwa maana karibuni angewanunua kwa damu yake mwenyewe.—1 Kor. 6:20; 7:23.
“MTUMWA” NA “NYUMBA”
3, 4. Katika maneno ya Yesu katika Mathayo 24:45, yeye angewezaje kusema juu ya wanafunzi wake kwa kufaa kama “mtumwa” na “nyumba” pia?
3 Kwa habari ya onyo hili, Yesu alisema hivi pia: “Ni nani basi yule mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya nyumba yake, awape watu chakula kwa wakati wake?”—Mt. 24:25.
4 “Nyumba” ni watumishi au watumwa wa nyumbani. Wakiwa washiriki wa nyumba ya Mungu, hao wangelishwa kama kikundi, wakifanya kazi pamoja, wakijuana, wakishirikiana na kusaidiana. Tunapoyafikiria maneno ya Yesu ya mfano, tutaona kwamba neno “mtumwa” (katika umoja au singular) hapa lina maana ya watumishi wote wa nyumba wakiwa pamoja kama jamii, na kwamba usemi “nyumba” (wingi) unawamaanisha wao kama watu mmoja mmoja.
5. Twajuaje kwamba matumizi ya neno “mtumwa” kama Yesu alivyolitumia katika Mathayo 24:45 yalieleweka na wanafunzi wake?
5 Maoni haya ya kikundi cha watu, ndiyo, hata taifa zima, kuwa mtumwa au mtumishi, hayakuwa mapya kwa wanafunzi wa Yesu. Yehova Mungu mwenyewe alikuwa amesema kwa taifa la Israeli mara nyingi kama mtumishi wake. Alisema hivi: “Nawe, Israeli, mtumishi wangu; Yakobo, niliyekuchagua; mzao wa Ibrahimu, rafiki yangu; wewe niliyekushika toka miisho ya dunia, na kukuita toka pembe zake, nikikuambia, Wewe u mtumishi wangu; nimekuchagua wala sikukutupa.” (Isa. 41:8, 9) Akionyesha wazi kwamba “mtumishi” huyu ni watu wengi, Muumba alisema hivi kwa taifa la Israeli: “Ninyi ni mashahidi wangu, asema [Yehova], na mtumishi niliyemchagua. . . . Lakini sikia sasa, Ee Yakobo, mtumishi wangu; na Israeli, niliyekuchagua; [Yehova], . . . asema hivi . . . je! sikukuhubiri haya zamani na kuyaonyesha? na ninyi ni mashahidi wangu.”—Isa. 43:10; 44:1-8; pia 42:19; 44:21; 48:20; 49:3; Yer. 30:10.
6, 7. Baada ya Mungu kukataa Israeli wa asili, ni nani aliyetumiwa kama “mtumishi” wake? Twajuaje?
6 Baada ya Mungu kulikataa taifa la asili la Israeli lisiwe mtumishi wake kwa sababu ya kutokutii kwao, sasa nani angekuwa mtumishi wake, chombo chake cha kidunia, mashahidi wake duniani? Na tuone mtume Paulo asemavyo juu ya hili. Ilikuwa karibu na miaka ya 50-52 C.E. Paulo alipoandika juu ya shauri hili kwa kundi la Kikristo katika Galatia. Agano jipya lenye kuchukua mahali pa agano la Torati lilikuwa limekuwa likitenda tangu Pentekoste ya mwaka wa 33 C.E. Kwa hiyo kundi la Kikristo lilikuwa limekuwa likifanya kazi kwa karibu miaka kumi na minane. Paulo alisema hivi kwa Wakristo Wagalatia: “Kwa sababu kutahiriwa si kitu, wala kutokutahiriwa, bali kiumbe kipya. Na wote watakaoenenda kwa kanuni hiyo, amani na iwe kwao na rehema, naam, kwa Israeli wa Mungu.”—Gal. 6:15, 16.
7 Kundi la Kikristo lilikuwa la watu waliotembea kwa utaratibu kulingana na kanuni hiyo juu ya “kiumbe kipya.” Kwa njia hiyo wao wakiwa kundi lenye umoja walikuwa “mtumishi” wa Mungu, kama vile Israeli wa kale walivyokuwa wamekuwa. Kwa hiyo, fungu la maneno lililomo katika Isaya 43:10 laweza kuelekezwa kwa njia ya kiroho kwa kundi kama “Israeli wa Mungu”: “Ninyi ni mashahidi wangu, asema [Yehova], na mtumishi niliyemchagua.”
WAKATI JAMII YA “MTUMWA” ILIPOANZA
8. Onyesha ni wakati gani jamii ya “mtumwa” mwaminifu ilipotokea.
8 “Mtumwa” huyu mwaminifu alitokea wakati gani? Katika Pentekoste, mwaka wa 33 C.E. Watu wa kwanza 120 ambao juu yao roho takatifu ilimiminwa walianza mara hiyo kufanya kazi ya kulisha wengine walioalikwa kwenye karamu ya kiroho ya Mungu, yaani, Wayahudi ambao kati yao 3,000 walikikubali “chakula” cha kiroho kilichotolewa wakabatizwa. Baada ya hili watu hawa 3,000 waliendelea kula chakula cha kiroho mpaka walipopata nguvu kutosha. Ndipo wengi waliporudi makwao katika nchi nyingine, wakaanzisha makundi na kuendelea kushirikiana na kutenda kupatana na kufundisha kwa kweli kwa mitume.—Matendo 2:1-4, 37-42.
9. Kulishwa kwa “nyumba” kulipanuliwaje?
9 Baada ya miaka inayopungua mitatu u nusu jitihada za kulisha za “mtumwa mwaminifu mwenye akili” zilifikishwa kwa Mataifa Petro alipomweleza Kornelio na nyumba yake habari njema. Wanafunzi wapya walipozidi kuingia, wao kama “nyumba” walijiunga katika kulisha wengine. Mpango ulifanywa ambao mitume, hasa Paulo na “nyumba” ya washirika wenye kusafiri pamoja naye, walilisha watu wengi katika nchi nyingi kwa kuutumia. Walitimiza maneno ya Yesu: “Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na [roho takatifu]; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi.”—Mt. 28:19, 20.
10. (a) Ni msaada gani wa kudumu wa kazi ya kulisha ambao Mungu alitoa kupitia kwa Wakristo fulani wa karne ya kwanza? (b) Ni nini kinachofanyiza chakula cha kiroho kilichoongozwa na Mungu kwa Wakristo leo?
10 Ili kutoa msaada wa kudumu katika kazi ya kulisha kiroho, mitume na wanafunzi wengine wa karne ya kwanza wa Yesu Kristo waliongozwa na Mungu waandike vitabu 27 vyenye kufanyiza Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Hivi, pamoja na Maandiko ya Kiebrania ambayo yalikuwako, viliwatolea wao chakula cha kiroho kwa njia ya barua wakati huo, na Wakristo mpaka siku hii.
11. Je! kazi ya kulisha iliendelea karne zote hizo?
11 Yesu alikuwa amesema hivi: “Tazama, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, hata ukamilifu wa dahari.” (Mt. 28:20) Yesu Kristo ndiye Kichwa cha kundi, mtumwa wake, nayo maneno yake yaonyesha kwamba angewatia nguvu walishe “nyumba” yake karne zote hizo. Kwa wazi kizazi kimoja cha jamii ya “mtumwa” kililisha kizazi chake kilichofuata, na pia kikaendelea kujilisha chenyewe.
12. Toa mfano juu ya namna jamii ya “mtumwa” yaweza kulisha “nyumba” ingawa maneno yote mawili yana maana ya watu wale wale.
12 Huenda mtu akauliza, ‘“Mtumwa,” ambaye amefanyizwa na “nyumba,” awezaje kulisha “nyumba”? Hiyo ingeonyesha “mtumwa” anajilisha mwenyewe.’ Mfano wa jambo hili waweza kutolewa juu ya jamaa inayohamia shamba fulani. Mojawapo la mahitaji yao ya kwanza ni kutolewa kwa chakula. Je! baba anatoa chakula chote na kukitia vinywani mwa wale wengine wote? Sivyo. Kila mshiriki wa jamaa afanya kazi tofauti. Huenda mmoja akafanya kazi ya kulima. Wengine huenda wakachimba kisima. Wengine wanapanda. Wengine wanaangalia mifugo na kukamua maziwa. Bila shaka, wote waweza kusaidia katika sehemu fulani za kazi. Yaelekea wote wangefanya kazi ya mavuno. Halafu, wanawake wangetia vyakula katika mikebe viwe akiba ya wakati ujao. Wangepika na kupakulia jamaa chakula. Sasa, kama angalikuwa ni mtu mmoja wa kufanya kazi hiyo asingaliruzuku kwa njia nzuri hivyo. Lakini kwa jitihada ya jamaa, wote wanalishwa vema. Kama jamaa wao ni mwili mmoja, kama vile “mtumwa mwaminifu mwenye akili” alivyo. Lakini kama watu mmoja mmoja wao ni wafanya kazi wenye kukuza na kupakua chakula, kama watumwa katika nyumba. Mfano unaofanana na huo uliotolewa na mtume Paulo katika 1 Wakorintho 12:12-27 ni ule wa mwili wa kibinadamu na viungo vyake.
JAMII YA “MTUMWA” KATIKA NYAKATI ZA KISASA
13. Maneno ya Yesu katika Mathayo 24:46 yanatokeza ulizo gani?
13 Yesu alisema hivi juu ya “mtumwa” huyu: “Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo.” (Mt. 24:46) Hapa Yesu alizungumza juu ya kundi kwake akague jamii yake ya “mtumwa” aone kama watakuwa ‘wakifanya hivyo,’ yaani, kulisha nyumba yake chakula chao wakati ufaao. “Mtumwa” huyo ni nani leo?
14. “Mtumwa” wa karne ya kwanza alijihakikishaje?
14 Kwa msingi wa kanuni iliyotajwa na Yesu: “Kwa matunda yake mti hutambulikana,” twaweza kuamua “mtumwa” huyo ni nani. (Mt. 12:33) Karne kumi na tisa zilizopita, wakati jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ilipoanzishwa, ilitangaza habari njema za ufalme wa Mungu wa Kimasihi na uharibifu uliokuwa ukija wa taratibu ya mambo ya Kiyahudi. Jamii hii nyaminifu peke yake ndiyo iliyozaa matunda ya kweli ya Ufalme. Ingawa iliteswa, iliokoka kipindi cha wakati wenye jeuri uliokuja kutimiza unabii wa Yesu katika Mathayo 24:4-22, Marko 13:5-20 na Luka 21:8-24 kwa mara ya kwanza.
15, 16. Ni nani wanaoonekana kuwa “mtumwa” wa kisasa, na kwa njia gani?
15 Mwaka wa 1914 C.E. wakati wa utimizo kamili wa unabii wa Yesu juu ya “ishara ya kuwapo [kwake] na ya mwisho wa taratibu ya mambo” ulianza. Kwa hiyo imempasa “mtumwa mwaminifu mwenye akili” awe mwenye bidii sana katika wakati huu wa mwisho wenye haraka akiuhubiri ufalme wa Mungu wa Kimasihi na mwisho wa taratibu hii ya ulimwengu. Nao imewapasa wawe wanaendelea kuishi kama jamii ya “mtumwa” ya karne ya kwanza, yajapokuwa mateso yaliyoenea pote. Ni nani anayefanya hivi leo? Ni nani wanaozaa matunda yafaayo ya Kikristo? Mambo ya hakika yaonyesha ni jamii ndogo ya washiriki waliotiwa mafuta wa kundi la kweli la Kristo lililoko duniani wakati huu. Wao wametoa chakula cha kiroho kutoka katika Neno la Mungu kwa bidii nyingi, wakiiendeleza hali yao wenyewe ya kiroho.
16 Zaidi ya hayo, “mtumwa” wa kisasa ameleta watu wengine karibu 2,000,000 washirikiane naye. Yeye ameonekana kweli kuwa “mtumishi” wa Yehova, mashahidi wake. Wenye kushirikiana na “mtumwa” huyu wana tumaini la kuishi milele katika dunia ya paradiso. Wanalishwa kwa wingi na “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” Chakula cha kiroho wapatacho ni chakula “kwa wakati wake,” kwa sababu hali hazijapata wakati wo wote kuwa zenye hatari kama sasa wala haja ya kuikimbia taratibu hii ya mambo na kuutumaini mpango wa Mungu wa wokovu haijapata wakati wo wote kuwa ya haraka kama ilivyo sasa.
17. Je! kulisha kwa “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ni kielelezo cha kulisha kwa kiroho kutakakokuwako wakati wa utawala wa miaka elfu wa Kristo? Eleza.
17 Basi, twaona kwamba Yesu Kristo mwenyewe alikaza fikira kwenye njia hii ya kulishia watu wake—si kama watu mmoja mmoja walio peke yao na wenye kujitegemea wenyewe, bali kama jamii iliyoungana kabisa ya Wakristo wenye upendo wa kweli kwa mmoja na mwenzake na wenye kuangaliana. Hivi ndivyo ilivyo leo kati ya makundi ya mashahidi wa Yehova katika nchi zote. Lazima iwe hivyo sasa, kwa maana watu watakuwa wenye umoja bila shaka, wakishirikiana katika kuleta uzuri wa dunia wakati wa utawala wa miaka elfu wa Kristo. Hakuwezi kwa njia nyingine yo yote kuwa na furaha na kuzaliwa kwa matunda ya roho, ambayo ni “upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujiweza.” (Gal. 5:22, 23, NW) Sifa hizi zikiwamo katika watu ndipo tu kuwezapo kuwa na amani na kufurahia kuishi juu ya dunia hili.
—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.