Mwabudu Mungu Katika Njia Yake
JE! WEWE umepata kuona ushuhuda wa ukweli huu kuhusu dini unaoelekea kujipinga?:
“[Miaka ya] kuanzia na wa 1980 itakuwa yenye ‘watu wengi zaidi wakivutwa kwenye imani ya Kikristo kuliko [wakati wa] historia yote iliyopita, na Wakristo wengi zaidi wakitoka kwenye matengenezo Kikristo kuliko kipindi kingine chote kilichotangulia.’”—Sydney “Morning Herald,” Julai 22, 1979.
Ripoti hiyo ya kutoka Australia, ambayo msingi wake ni uchunguzi uliofanywa juu ya dini 50 kubwa pamoja na vikundi 3,000 vya “Kikristo,” ulionyesha kwamba watu wanaacha makanisa yao kwa wingi sana. Huenda ukawajua wengi waliokuwa wakifuata dini sana na kuhudhuria kanisa na ambao sasa wameacha.
Hata hivyo watu wengi mmoja mmoja, wakiona uhitaji wa ndani wa kumwabudu Mungu, wanavutwa na dini fulani, mara nyingi inakuwa dini inayovuta maono yao ya ndani, pengine ikiwahimiza “waokoke.”
Wewe pia una uhitaji uliotiwa ndani yako na Mungu wa kuabudu Muumba wako. Lakini unapaswa kumwabuduje? Njia yake ya kuabudiwa ni njia gani?
UNAWEZA KUJUAJE?
Bila shaka, ni Mungu, wala si mwanadamu ye yote au kanisa linalopaswa kuamua kweli ni ipi na ni ipi iliyo ibada ya kweli. Yesu alimwambia hivi mwanamke iliyekuwa sehemu ya jamii ya kidini katika karne ya kwanza: “Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.” (Yohana 4:24) Hiyo inatupasa sisi leo pia.
Ndiyo, ili tumpendeze Mungu, tunahitaji kuwa na maelekeo ya ibada safi, tukiyaonyesha kwa moyo wote na kwa unyofu. Lazima vilevile tuwe tukitafuta kweli na kujitahidi kujipatanisha nayo. Hiyo inamaanisha kutenda kulingana na kweli iliyofunuliwa katika Neno la Mungu, badala ya kufuata mapokeo tu ya kanisa au mafundisho ya kidini yanayopingana na kweli ya Biblia.
Katika kuchunguza kama dini fulani—hata kanisa lako mwenyewe, au imani inayopendwa na wengi iliyo karibu yako—inapatana na kweli, sehemu nyingi mbalimbali zaweza kuchunguzwa. Lakini hata uchunguzi unaohusu sehemu tatu tu unaweza kukusaidia kumwabudu Mungu katika njia yake. Angalia:
IMANI INAYOPATIKANA POTE—LAKINI JE! NI KWELI?
Fundisho moja linalopatikana katika dini nyingi kuzunguka dunia yote ni lile la kwamba mwanadamu ana nafsi ndani yake inayookoka kifo cha mwili na kuendelea kuishi katika hali ya kutokufa ikiwa kama roho. Je! wewe unalitambua fundisho hilo? Mara nyingi linafungamanishwa na wazo la kwamba nafsi ya mtu mwema huenda mbinguni baada ya kufa. Nalo ndilo linalosababisha kuhangaika kunakoenea pote juu ya “roho” za watu wa ukoo waliokufa au mizimu. Kitabu Encyclopcedia Britannica kinasema hivi: “Imani katika kutokufa kwa kibinadamu kwa namna fulani inakaribia sana kuwa ya ulimwenguni pote.” Pengine unajua hivyo.
Lakini inafaa sana kwamba kitabu hicho kinasema kwamba “inakaribia sana kuwa ya ulimwenguni pote.” Sababu gani? Kwa kuwa Waebrania wa kale na Wakristo wa kwanza hawakuamini kwamba wanadamu wanazo nafsi zisizoweza kufa.
Huenda ukashangaa kusikia hivyo, kwa kuwa watu wengi wanafikiri kwamba fundisho hili la kanisa linatokana na Biblia. Walakini, angalia hili:
Kulingana na Biblia, uongo wa kwanza uliosemwa na Shetani Ibilisi, ulikuwa kwamba dhambi ya kibinadamu haingeleta kifo. (Mwa. 3:1-4) Hata hivyo, wazazi wetu wa kwanza walipokufa, nacho kifo kikaendelea kuwapata wote baadaye, ni jambo gani lingeweza kuwa lenye kudanganya zaidi kuliko kusema, ‘Kwa kweli wao hawafi—ni mwili wao tu unaokufa; nafsi yao inaendelea kuishi katika hali ya kutokufa’? Ndiyo, fundisho la kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu linaelekea kuendeleza uongo wa Shetani na limeongoza mamilioni mengi kuwaogopa wafu.
Hata hivyo, kusema kwa urahisi, Maandiko yanafundisha kwamba nafsi yako ni wewe. Tunapata kionyesho cha jambo hilo katika yale yanayoripotiwa na Biblia juu ya Adamu. Muumba alifanyiza mwili kutoka kwa mavumbi kisha akatoa uhai na pumzi iliyohitajiwa kuendeleza uhai. Matokeo? Adamu “akawa nafsi hai.” (Mwa. 2:7) Yeye hakupewa nafsi. Adamu alikuwa nafsi.—Linganisha 1 Wakorintho 15:45.
Kupatana na hilo, Biblia hufundisha kwamba nafsi (mtu) inaweza kufa. Angalia Ezekieli 18:4, NW. Hiyo inamaanisha kwamba wakati mtu anapokufa hana mawazo au maono? Barabara. Kwa kweli, Mhubiri 9:5 hutuambia hivi: “Walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote.”
Je! hiyo yamaanisha kwamba hakuna tumaini kwa watu wetu wa ukoo na rafiki waliokufa? Hapana, kwa kuwa Biblia hutupa mifano ya watu ambao Mungu alirudisha kwenye uhai, akawafufua. Kwa mfano, huenda ukawa tayari unajua kwamba Mungu alimfufua Yesu Kristo akiwa kiumbe cha kiroho katika siku ya tatu ya kufa kwake. (Matendo 10:39, 40; 1 Pet. 3:18) Kwa msingi huo pamoja na ahadi za Biblia zinazohusiana na jambo hilo, tunaweza kutazamia wakati ambapo Mungu atafufua wale walio katika kumbukumbu lake.—Matendo 17:31; 24:15.
Kwa hiyo, unapofikiria mambo, waweza kuona kwamba fundisho la nafsi isiyoweza kufa linalofundishwa na dini nyingi hupingana moja kwa moja na yale yanayosemwa na Biblia. Kwa hiyo jiulize: ‘Hilo linamaanisha nini kwangu? Je! nahitaji kufanya marekebisho fulani ili nimwabudu Mungu katika njia yake, katika kweli?’
MWENENDO UNAHUSIKA VILEVILE
Yesu Kristo alitupa msaada zaidi katika kutambua njia ya Mungu ya kumwabudu, Yeye aliwaambia wafuasi wake hivi: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:35) Je! makanisa mengi leo yanawahimiza kweli kweli wafuasi wake waonyeshe namna ya upendo kama ile aliyoonyesha Yesu?
Kwa mfano, Wakristo wa kwanza walijaribiwa kwa habari ya wao kuwa na upendo wa kweli walipoulizwa wajiunge na au waunge mkono jeshi la Kirumi. Walitaka kutii sheria za serikali, walakini hawangeweza kufanya hivyo wakati kufanya hivyo kungemaanisha kuvunja sheria ya Mungu, kama vile sheria yake juu ya kuua. (Mt. 22:21; Matendo 5:29) Na zaidi ya hayo, Mungu alikuwa amesema hivi kuhusu watu wake: “Watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu, taifa halitainua upanga juu ya taifa jingine wala hawatajifunza vita tena kamwe.”—Isa. 2:4.
Kupatana na hilo, Wakristo wa kwanza hawakupigana vita kwa ajili ya Milki ya Kirumi au taifa jingine lo lote.
Hata hivyo, ebu fikiria msimamo ambao umechukuliwa na makanisa ya wakati wetu pamoja na wahudumu na mapadri wao. Baada ya kutoa visababu fulani, wamevipa kibali na kuvibariki vita—vita ambavyo katika hivyo Wakatoliki huua Wakatoliki na Waprotestanti huua Waprotestanti. Hiyo si njia ya Mungu!
KANUNI ZA MUNGU ZA ADILI
Kama sehemu ya tatu ya kuchunguza ili kujua njia ya Mungu ya kuabudu, inatupasa kuona kama kikundi cha kidini kinategemeza kanuni zake za adili kuliko kuachilia tu makosa.
Yesu alifanya kazi ili kusaidia watu waliolemewa na dhambi, kutia na walevi na waasherati. Iliwapasa wanafunzi wake kufanya vivyo hivyo. (Mt. 9:10-13; 21:31; Luka 7:36-48; 1 Kor. 6:9, 11) Nayo Biblia huonyesha kwamba hata baada ya watu kutubu na kuwa Wakristo baadhi yao wanaweza kuteleza na kufanya dhambi nzito. (Gal. 6:1) Kwa mfano, mwanamume fulani katika kundi la Kikristo katika Korintho wa kale alipata kuwa mwasherati.—1 Kor. 5:1.
Ikiwa Mkristo angeangukia dhambi, iliwapasa Wakristo wengine wajaribu kumrudisha kwenye kibali ya Mungu na kwenye nguvu za kiroho. (Yak. 5:13-16) Lakini namna gani ikiwa mtu alizoea dhambi bila kutubu? Neno la Mungu lasema hivi kuhusu mwanamume huyo katika Korintho au ye yote aliye kama yeye:
“Msichangamane na mtu aitwaye ndugu, akiwa ni mzinzi au mwenye kuabudu sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi; mtu wa namna hii msikubali hata kula naye. . . . Mwondoeni yule mbaya miongoni mwenu.”—1 Kor. 5:11-13.
Kwa hiyo mtenda dhambi nzito akikataa msaada na kutubu, lazima afukuzwe au kutengwa na ushirika wa kundi la kweli la Kikristo. Pengine kufanya hivyo kutamshtua na kumrudishia fahamu zake. Hata hivyo, iwe hivyo au isiwe, kufukuzwa huko kunakoongozwa na Mungu kutoka kwa kundi kutawalinda Wakristo wanyofu.-—1 Kor. 5:2-8.
Lakini je! kuadibu kwa namna hiyo kunafanywa katika makanisa mengi unayojua? Au si kweli kwamba wanakanisa wengi wanaozoea dhambi waziwazi wanaendelea kukubaliwa kuwa sehemu ya kikundi hicho?
Ukurasa wa kwanza katika gazeti la Nigeria uliripoti karibuni hivi:
“Karibu theluthi moja ya wanaume waliooa wa Roma Katoliki katika eneo la askofu mkuu la Lusaka wana masuria wanaoishi nao . . . Ripoti hiyo, ambayo msingi wake ni uchunguzi uliofanywa na Askofu-mkuu Emmanuel Milingo, inasema kwamba kuna masuria katika [jamaa] 3,225 kati ya jamaa 10,903 za Kikatoliki.”—Sept. 14, 1980.
Kwa kukataa kufuata amri ya Mungu ya kutenga na ushirika watenda dhambi wasiotubu, makanisa huwafanya wengine wafikiri kwamba wanaweza kutenda dhambi vilevile na wasiadhibiwe. Au huenda wakaacha dini tu.—Mhu. 8:11.
Kijana mmoja aliandikia gazeti moja yafuatayo:
“Mimi nachukia kwenda kanisani kwa sababu naona watu humo ninaojua kwamba ni walevi, wapiga porojo, waongo na wadanganyaji, nao wamo mle kila Jumapili wakitoa sala zao na kuimba nyimbo. Siwaheshimu wanafiki hata kidogo nalo kanisa letu linajaa hao.”—Palm Beach “Post-Times,” May 27, 1979.
Kwa wazi Mungu hawezi kukubali watu au makanisa yanayozaa matunda ya namna hiyo na ambao hawamwabudu “katika roho na kweli.”—Yohana 4:24; Mt. 7:15-20.
WEWE UTAFANYA NINI?
Tumechunguza sehemu tatu tu. Lakini zinaonyesha waziwazi kwamba ikiwa tunataka kumwabudu Mungu katika njia yake, huenda ikawa lazima tufanye mabadiliko fulani katika imani na njia zetu, hata kama vile alivyofanya mtume Paulo pamoja na wengine wengi ambao wamepata kuwa Wakristo wa kweli. Kujitenga wenyewe na dini ambazo haziendelezi njia ya Mungu ya kuabudiwa ni jambo la lazima. Kwa kweli, Mungu hutuamuru ‘tutoke kwao ikiwa hatutaki kushiriki dhambi zao na kupokea sehemu ya mapigo yao yanayokuja kutoka kwa Mungu.’—Ufu. 18:4, 5; 2 Kor. 6:14-18.
Mashahidi wa Yehova wanapendezwa sana na kupatanisha maisha yao na Neno la Mungu, na hivyo kumwabudu Muumba “katika roho na kweli.” Watafurahia sana kukusaidia wewe, pia, katia tamaa yako ya kumwabudu Mungu katika njia yake.