Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 8/1 kur. 11-17
  • Ukristo na Matendo ya Dini ya Kweli

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ukristo na Matendo ya Dini ya Kweli
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JE! WAKRISTO WA LEO WANGEMSULIBISHA YESU MARA YA PILI?
  • YESU NA DINI YA KWELI
  • YESU NA NAFSI
  • WAKRISTO NA AMRI ALIZOPEWA NUHU
  • WENYE KUUNGA UFALME MKONO KWA UMOJA
  • MAANA YAKE NINI
  • Dini ya Kweli—Namna ya Kuitambua
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Je! Umeipata Dini ya Kweli?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Ibada Ambayo Mungu Anakubali
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Kuzoea Dini Safi Kwa Ajili Ya Kuokolewa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 8/1 kur. 11-17

Ukristo na Matendo ya Dini ya Kweli

1, 2. Kinachoitwa “Ukristo” kiko namna gani kikilinganishwa na dini ya Yesu Kristo?

Gazeti la Detroit linaloitwa Free Press la Desemba 24, 1976, liliuliza hivi;

JE! WAKRISTO WA LEO WANGEMSULIBISHA YESU MARA YA PILI?

Katika makala iliyofuata, Sydney J. Harris, mwandikaji wa magazeti aliandika hivi:

“Ikiwa [Yesu] angekuja mara ya pili Siku ya Krismasi, je! hangesulibishwa mara ya pili bila kukawia? Wale ambao wangemsulibisha wakati huu si Warumi wala Wayahudi, bali ni wale wanaojiita kwa kujisifu kuwa Wakristo?

“Sijui namna sisi leo tungemfikiria na kumtenda mtu huyu mwenye mafundisho mageni na yenye kuogofya na ‘yasiyoweza kufuatwa’ juu ya mwenendo wa wanadamu na hali za kijamii. . . .

“Je! watu wanaopenda vita kati yetu wasingemshambulia wakisema ni mwoga asiyetaka vita kwa sababu anatusihi tusipinge mabaya bali turudishe mema mahali pa mabaya?

“Je! watu wanaotetea mataifa yao kati yetu “asingemshambulia wakimwita kuwa mtu wa hatari anayetaka kupindua serikali kwa sababu anatuambia kwamba sote ni ndugu? . . . Je! watu wenye kuvutwa vyepesi na fikira kati yetu “asingemkataa wakisema ni mtu anayelaumu kufurahia anasa kwa sababu anatuonya kwamba njia ya wokovu ni nyembamba na yenye taabu? . . .

“Sijui, sijui kama Wakati wa Ukristo umeanza.”

2 Makala hii inakazia sana mojawapo ya tofauti kubwa zilizo kati ya mafundisho ya Yesu Kristo na maoni ya watu wengi leo wanaojidai kuamini dini ya kweli inayoelezwa katika Biblia.

YESU NA DINI YA KWELI

3, 4. Maoni ya watu wengi juu ya Adamu na Hawa yako namna gani yakilinganishwa na imani ya (a) Yesu? (Mwa. 1:26) (b) wanafunzi wake?

3 Basi, tumekwisha kuona kwamba kitabu cha Biblia cha Mwanzo kinafundisha kwamba Yehova Mungu aliumba wanadamu wa kwanza, Adamu na Hawa. Ijapokuwa makasisi na wanakanisa wengi wanaopendelea makisio ya mageuzi wanaiona habari ya kitabu cha Mwanzo kuwa hadithi ya uongo, namna gani Yesu, Mwanzishi wa Ukristo?

4 Ni kweli Yesu alikuwa na hakika kwamba Mungu aliumba Adamu na Hawa, wazazi wa kwanza wa jamii ya wanadamu. Vilevile wanafunzi wake walisadiki hivyo. (Mwa. 2:21-24; 1 Kor. 6:16; 15:45; Efe. 5:31; Luka 3:23-38) Wakati mmoja Yesu alipokuwa akijibu ulizo la talaka alisema hivi:

“Hamkusoma ya kwamba yeye aliyewaumba mwanzo, aliwaumba mtu mume na mtu mke, akasema, Kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja? Hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe . . . Nami nawaambia ninyi, Kila mtu atakayemwacha mkewe, isipokuwa ni kwa sababu ya uasherati, akaoa mwingine, azini.”​—⁠ Mt. 19:4-9.

5. Ni maoni gani juu ya Biblia yanayotusaidia tuitambue dini ya kweli?

5 Twaweza kuhakikishwa na maneno hayo ya Yesu kwamba yeye na wafuasi wake waliikubali Biblia kuwa imeongozwa na Mungu na inategemeka. Ukubali huo ni alama ya maana ya kutambulisha dini ya kweli. (2 Tim. 3:16, 17) Basi, labda kila mmoja wetu atauliza hivi, ‘Je! dini yangu inaikubali Biblia kuwa imeongozwa na Mungu nayo ni ya kweli, kutia na yale ambayo inasema juu ya uumbaji? Je! mimi mwenyewe ninasadiki kama Yesu na mitume?’

6. (a) Yesu alionaje ndoa na talaka, na dini ya kweli iko namna gani ikilinganishwa na habari ya kitabu cha Mwanzo juu ya mazungumzo hayo? (b) Wakristo wa kwanza walifuata mwenendo gani juu ya ngono na ndoa? (Ebr. 13:4)

6 Yale ambayo Yesu alisema katika Mathayo 19:4-9 yanaonyesha vilevile namna dini ya kweli inavyoendelea kuwa na mwenendo mwema bila kugeuka. Yesu alikubali kwamba ndoa ni takatifu na kwamba mapatano ya ndoa ni yenye kuendelea muda mrefu; Maandiko yanaruhusu talaka na kuoa au kuolewa upya ikiwa mwenzi anafanya uzinzi au uasherati tu. Kwa kufuata sana kanuni hii ya kimungu, dini ya kweli inaongoza watu waliooana wafanye bidii kufanikisha ndoa yao. Haiwapasi waone ndoa kuwa mapatano ya urafiki ambayo ni ya muda tu, yanayoweza kuvunjwa na Serikali. Kwa hiyo, Wakristo wa kwanza waliepuka uasherati walipokuwa wakifuata dini ya kweli, wakifuata maoni ya Muumba kwamba ndoa ni kifungo kitakatifu, cha muda mrefu. Kwa hiyo, Dakt. C. J. Cadoux aliandika habari za Wakristo waliokuwa katika karne ya pili W. K. hivi:

“Kufanya ngono na mtu asiye mwenzi wa ndoa kulikatazwa kabisa. Mara nyingi Wakristo walilaumu vikali matendo ya kupita kiasi yaliyokuwa kawaida ya wapagani waliowazunguka.” ​—⁠The Early Church and the World, uku. 283.

7, 8. Kulingana na unavyojua, je! unaona wana-kanisa wakifuata kanuni ya Biblia juu ya mwenendo mwema. Au, haiwezekani kuifuata leo?

7 Je! wewe unaona kwamba makanisa mengi yanafuata kwa bidii kanuni hiyo ya Biblia inayopasa mwenendo mwema? Au, ni kawaida ya watu wanaojidai kuwa Wakristo kupeana talaka na kuoa au kuolewa upya ijapokuwa hakuna msingi wa Maandiko wa kufanya hivyo? Tena, je! dini nyingi hazikubali hata watu wanaoishi pamoja katika hali ya uasherati na watu wenye ndoa za wake wengi?

8 Bila shaka, wengi wangesema kwamba ijapokuwa kanuni ya Biblia juu ya mwenendo mwema ni nzuri zaidi, kwa kweli haiwezekani katika wakati wetu kuifuata. Lakini inawezekana sana kwa watu wa dini kufuata kanuni za mwenendo mwema ijapokuwa ‘matendo ya kupita kiasi ambayo ni kawaida ya watu wanaotuzunguka.’ (Ebr. 13:4) Angalia ripoti hii kutoka gazeti la Uingereza Daily Telegraph juu ya mamia ya maelfu ya watu wanaoishi katika bara ya Afrika:

“Katika Afrika, Mashahidi wa Yehova wamejionyesha kuwa raia wenye adabu na wenye utaratibu, wakifuata mwenendo bora wa maisha . . . Mashahidi hawafuati mwenendo wa uasherati na wa kuwa na wake wengi kama ilivyo kawaida ya Waafrika. Madhehebu hiyo inaweka mkazo juu ya kuzoea kutumia fedha kwa uanzalifu, kutokuchelewa, kutokudanganya na utii.”​—⁠Oktoba, 26, 1972.

9. (a) Ni kwa sababu gani mambo ambayo Biblia inasema juu ya mwenendo mwema kati ya wanaume na wanawake na wivi yanakamatana? (Kum. 5:19,21; 1 The. 4:4-6) (b) Dini ya kweli inajulikana kwa hatua gani juu ya mtu anayekuwa mkosaji asiyetuba na kuendelea na kosa?

9 Basi, tangu mwanzo tunaona mkazo wa mwenendo mwema na kuheshimu ndoa kuwa alama za kutambulisha ibada ya kweli. Hii inatia ndani hata maoni ya Biblia juu ya haki za kuwa na mali na wivi. Hayo yangetia vilevile kuiba mwenzi wa ndoa wa mtu mwingine au usafi wa mwenendo wa mtu mwingine. (Mwa. 2:24; Efe. 4:28) Zaidi ya hayo, Biblia inaeleza waziwazi kwamba watu wanaojidai kuwa na dini ya kweli lakini wanaoendelea kuwa ‘waasherati, ‘wazinzi, wevi au watamanio’ bila kutubu, lazima wafukuzwe watoke katika kundi la Kikristo kupatana na takwa hili la Mungu: “Ninyi mwondoeni yule mbaya miongoni mwenu.” (1 Kor. 5:11-13; 6:9, 10) Kufuata sana kanuni hiyo ya kimungu juu ya mwenendo mwema kumetambulisha dini ya kweli. Tuulize hivi, Ibada yetu ya Mungu inalinganaje na kanuni hiyo?

YESU NA NAFSI

10. Maandiko ya Kikristo yanapatanaje na kitabu cha Mwanzo juu ya “nafsi”?

10 Kumbuka kwamba katika mazungumzo yetu yaliyotangulia juu ya Adamu, tuliona kwamba Biblia haikusema kwamba Adamu alikuwa na nafsi isiyoweza kufa, bali yeye alikuwa nafsi. Je! huo ndio ufahamu ule ule unaopatikana katika Maandiko ya Kikristo au “Agano Jipya”? Ndio. Mtume Paulo hata alitumia maneno ya habari ya kitabu cha Mwanzo katika kuzungumza juu ya ufufuo, akisema: “Ndivyo ilivyoandikwa, Mtu wa kwanza, Adamu, akawa nafsi iliyo hai; Adamu wa mwisho [Yesu Kristo] ni roho yenye kuhuisha.” (1 Kor. 15:45) Kwa hiyo, shauri hili laonyesha vilevile imani zisizogeuka za dini ya kweli.

11. Wanafunzi wa Yesu walikuwa na tumaini gani, na waliwezaje kuwa na hakika kwamba ni la kweli wala si jambo la kuwazia tu? (1 Pet. 1:3, 4; Matendo 10;30, 40; 17:31; 1 Kor 15:3-8)

11 Wafuasi wa kwanza wa Kristo walikuwa na hakika ya ufahamu huo kwa sababu ya mambo yaliyompata Yesu mwenyewe. Yeye akiwa nafsi ya kibinadamu, aliuawa. Aliendelea hali hiyo ya kufa muda wa siku tatu ambao katika huo hakuwa akiishi mahali penginepo. (Matendo 2:22-27, NW; 1 Kor. 15:3, 4) Alikuwa kaburini mpaka Mungu alipomfufua siku ya tatu akiwa na mwili wa roho, kisha akarudi mbinguni. (1 Pet. 3:18) Hapo mwanzoni, alipokwisha kufananisha mauti na usingizi ambao katika huo mtu hafahamu cho chote, Yesu aliwaambia watu walioamini hivi: “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi.” (Yohana 11:11-14, 25; 5:28) Basi, wanafunzi wake hawakuwa na sababu ya kuamini wazo lo lote la Wagiriki la kwamba mtu anayo nafsi isiyoweza kufa.

12. Kwa sababu gani imani inayopasa “nafsi” ni ya maana juu ya dini?

12 Kupatana na hayo, kila mmoja wetu anaweza kuchunguza mambo ambayo dini yetu inafundisha. Je! fikira zetu za kidini zimepatanishwa na yale ambayo dini ya kweli inaendelea kufundisha, kwamba mtu ni nafsi na ya kwamba uzima wo wote wa wakati ujao unategemea ufufuo? Hilo si jambo la kufanyia mchezo; tumaini letu linategemea jambo hilo.

WAKRISTO NA AMRI ALIZOPEWA NUHU

13, 14. Kwa sababu gani habari ya damu ni ya maana juu ya ibada ya kweli?

13 Tunaweza kutazamia kwamba kama vile mafundisho ya Yesu yalivyopatana na habari ya kitabu cha Mwanzo juu ya Adamu, ndivyo yangepatana na yale tunayosoma katika Biblia juu ya Nuhu. Nayo yanapatana. Utakumbuka kwamba katika Mwanzo 9:3-6 Muumba alitoa maagizo yaliyokuwa amri zilizopaswa kufuatwa na wanadamu wote. Wakati huo Mungu alikataza kula nyama pamoja na damu iliyobaki ndani yake na kukataza kuua wanadamu wengine.

14 Tangu wakati huo, dini ya kweli ilitia ndani kuheshimu damu ambayo Mungu mwenyewe alisema ilipaswa ifananishe uhai uliotoka kwake na ni mali yake Yeye. (Law. 17:13, 14; Zab. 36:9) Kupatana na hayo, ni damu ya Yesu iliyomwagwa iwe dhabihu kwa ajili ya wanadamu wote. (Efe. 1:7; Ebr. 9:11-14; 1 Pet. 1:19), Lakini je! Wakristo vilevile wanatakiwa kuepuka kula damu au nyama isiyoondolewa damu yake? Tukiyachunguza Maandiko ya Kikristo, tunaona kwamba Matendo sura ya 15 ina uamuzi wa lazima wa mitume na wanaume wazee wa Yerusalemu waliokuwa sehemu ya baraza kuu au baraza inayoongoza ya wazee Wakristo. Biblia inatuambia kwamba, wakisaidiwa na roho takatifu ya Mungu, walihakikisha kwamba inawapasa Wakristo waepuke damu kama ilivyoamriwa kupitia kwa Nuhu.​—⁠Matendo 15:28, 29; 21:25.

15, 16. Mwenendo wa Wakristo wa kwanza juu ya damu uko namna gani ukilinganishwa na mwenendo wa Mashahidi wa Yehova?

15 Wakristo wa kwanza walifuata sana sheria hii ya Mungu. Kulingana na Tertuliano mwandikaji Mrumi, Wakristo wa karne ya pili na ya tatu ‘hawakutumia hata damu ya wanyama katika vyakula vyao vya kawaida; waliepuka vitu vilivyonyongwa na vilivyojifia vyenyewe.’ Hata watesi walifahamu kwamba wale wanaofuata dini ya kweli ya Kikristo hawangekula nyama ambayo damu yake ingekuwa imebaki ndani yake. Kwa hiyo ‘waliwajaribu Wakristo kwa kuwapa utumbo wenye damu, kwa sababu walijua kabisa kwamba Wakristo waliona kuwa haramu kile kitu ambacho kwa hicho walikuwa wakijaribu hivyo kuwakosesha.’​—⁠Kitabu cha Tertuliano, The Apology, Sehemu ya I, Sura ya 9.

16 Je! tangu wakati huo alama hii ya kutambulisha dini ya kweli imeachwa? Ijapokuwa makanisa mengi hayafuati wala kufundisha yale ambayo Biblia inasema juu ya jambo hilo, ingali ni alama inayotambulisha Ukristo wa kweli. Taarifa moja iliyotokana na taifa moja la Kiafrika ilisema habari ya Mashahidi wa Yehova waliokuwa wamefungwa gerezani kwa sababu ya kutokuwamo kwao katika siasa kama Wakristo wa kwanza. Askari zao wa gerezani waliijaribu imani yao kwa kutaka kuwalazimisha ‘waandike barua ya kuonyesha kwamba wanakana imani zao, wabadili dini yao, wakubali kanuni ya kuwa na wake wengi au wale nyama isiyoondolewa damu.’ Tunafurahi kueleza kwamba Wakristo hao walijibu kama mitume, wakisema: “Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu.”​—⁠Matendo 5:29.

17. Ni ushuhuda gani mwingine wa dini ya kweli ambao Wakristo wanaweza kuchunguza kwa habari ambazo Mungu alimwambia Nuhu?

17 Vilevile ushuhuda zaidi wa dini ya kweli ambao inatupasa tufikirie unapasa yale ambayo Mungu alimwambia Nuhu. Wakati huo, jamaa nzima ya wanadamu ilipokuwa yenye nafsi nane tu, Mungu alieleza wazi kwamba haiwapasi wapigane na kuuana. (Mwa. 9:5, 6) Kuona wanadamu wote hivyo kama ndugu na kuheshimu uhai wa kibinadamu ni alama mojawapo yenye nguvu kuliko zote, inayotambulisha dini ya kweli,​—⁠Kut. 20:13.

18. (a) Ni nini ambacho Yesu mwenyewe alisema kingetambulisha wanafunzi wake? (b) Wakristo wa kwanza walikuwa na maoni gani juu ya vita kwa sababu ya maneno ya Yesu? (Mt. 5:43-45; 26:52)

18 Upesi kabla ya kufa kwake, Yesu alisema hivi: “Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo. Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:34, 35) Kwa hiyo, Wakristo wa kwanza walikataa kujiunga na majeshi ya Kirumi wala kupigana katika majeshi ya lo lote la mataifa mengine ya kale. Katika habari yake inayosema “Uchunguzi wa Kupatana kwa Vita na Kanuni za Ukristo,” Jonathan Dymond alitoa taarifa ya uchunguzi wake wa jambo hili, akisema:

“Wakristo walioishi karibu na wakati wa Mwokozi wetu walisadiki pasipo mashaka kwamba yeye alikuwa amekataza kabisa vita​—⁠ya kwamba waliikubali imani hii waziwazi, na kwa kuhakikisha hivyo, walikuwa tayari kutoa, nao walitoa mali na maisha zao.

“Walakini, mwishowe Wakristo wakawa askari.​—⁠Wakati gani? Wakati uaminifu wao wote kwa Ukristo ulipokuwa dhaifu;​—⁠Walipovunja kanuni zake katika mambo mengine; . . . Wakawa askari walipokwisha kuacha kuwa Wakristo.” ​—⁠Kur. 60, 61.

19. Yohana, mwandikaji wa Biblia alikazia alama gani ya kutambulisha dini ya kweli?

19 Mtume Yohana aliweka mkazo juu ya upendo kama sifa ya lazima ya dini ya kweli alipoandika hivi: “Maana, hii ndiyo habari mliyoisikia tangu mwanzo, kwamba tupendane sisi kwa sisi; si kama Kaini alivyokuwa wa yule mwovu, akamwua ndugu yake . . . Watoto wadogo, tusipende kwa neno, wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.”​—⁠Yohana 3:11, 12, 18.

WENYE KUUNGA UFALME MKONO KWA UMOJA

20. Ili tumsaidie mtu aitambue ibada ya kweli, tungeweza kueleza nini juu ya Ufalme?

20 Sababu nyingine inayoonyesha umoja wa duniani pote wa udugu wa Kikristo inapatikana katika habari kuu ya mahubiri ya Yesu: ufalme wa mbinguni. Wakristo wa kweli wanaunga mkono na kutolea mamlaka hii ya ufalme maisha zao po pote wanapoishi juu ya uso wa dunia. Ijapokuwa mamilioni ya wanakanisa wa leo wanaisema mara nyingi “sala ya kielelezo” ambayo Yesu alitoa, wakisali “Ufalme wako uje,” je! wanafahamu kwamba Ufalme huo ni serikali kweli kweli itakayotawala dunia hii kwa faida ya wakaaji wa dunia, iletee wanadamu haki, amani, afya na uzima? (Ufu. 21:3, 4; 2 Pet. 3:11-13) Alipokuwa mbele ya liwali wa Kirumi Pontio Pilato, Yesu alisema habari za ufalme huo hivi:

“Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa wa ulimwengu huu, watumishi wangu wangenipigania, nisije nikatiwa mikononi mwa Wayahudi. Lakini ufalme wangu sio wa hapa.”​—⁠Yohana 18:36.

21. Wakristo wa kweli wanaonyesha ushikamanifu na bidii zao kwenye nini?

21 Ufalme huo ni wa mbinguni. Kwa hiyo, ijapokuwa Wakristo wanaheshimu bidii za wanadamu za kuleta amani, wanatumia nguvu zao zote na mali zao ili wahubiri ufalme huo na tumaini ambalo unatolea wanadamu wote. (Mt. 24:14; 28:18-20) Kwa hiyo, mambo yaliyo ya maana zaidi katika maisha za wafuasi wa kweli wa Kristo ni kushikamana na Ufalme huo.

22. Ni maoni gani ambayo Wakristo wa kwanza walikuwa nayo juu ya serikali za ulimwengu? (Tito 3:1; 1 Pet. 2:17)

22 Wakristo wa kwanza waliamini maneno hayo ya Kristo hata wakati mitume walipokwisha kufa. Walilipa kodi zao, wakatii sheria za nchi nao walikuwa raia bora kwa mambo yote ya kawaida katika nchi zao. (Mt. 22:17-21; Rum. 13:1-7) Lakini hawakuwamo katika vikundi na magombano ya siasa ya wakati wao. Historia imeandikwa hivi:

“Wakristo walikuwa wageni na wasafiri katika ulimwengu uliowazunguka; uraia wao ulikuwa mbinguni; ufalme waliotazamia haukuwa wa ulimwengu huu. Basi ilionekana wazi tangu mwanzo kwamba kutopendezwa na mambo ya utawala ilikuwa hali ya Ukristo.”​—⁠Christianity and the Roman Government, cha B. G. Hardy, uku. 39.

23. Sababu gani kutokuwamo kwa Mashahidi wa Yehova kwafaa kuchunguzwa tunapofikiria dini ya kweli? (Yohana 15:19)

23 Basi, katika kuwatambua wafuasi wa dini ya kweli leo, imetupasa tutafute wale wanaojitenga na mambo ya serikali za wanadamu, si kwa sababu zo zote za kibinafsi, bali kwa sababu wao wanatazamia hatua itakayochukuliwa na ufalme wa Mungu kuondoa matendo yasiyo ya haki na mateso ya wakati wetu. Je! Wakristo kama hao wanaweza kuwako leo? Kitabu cha karibuni chenye habari juu ya Ukristo kilisema hivi:

“Kujitenga kwa Mashahidi wa Yehova na siasa, vita na mambo ya kijamii kumefasiriwa na adui zao kuwa na maana ya kuchukia wanadamu, na hiyo imekuwa ndiyo sababu kubwa kuliko zote za kuteswa kwao vikali mara nyingi.” ​—⁠American Christianity, An Historical Interpretation.

Vilevile kitabu From State Church to Pluralism (1971), cha F. H. Littel, kinasema hivi:

“Walakini, ijapokuwa mafundisho mageni ya Mashahidi wa Yehova juu ya Ufalme yanaonekana kuwa upuzi tu na ya kuchukuliwa namna yalivyo, tusisahau kwamba katika dini ya Biblia kuja kwa Ufalme ni kipindi cha kuenea kwa nguvu na mageuzo makubwa ya kawaida ya matazamio ya wanadamu.”​—⁠Uku. 212.

Mafundisho ya Ufalme yako tofauti sana na maoni ya ulimwengu kama yalivyokuwa wakati Yesu alipokuwa akihukumiwa mbele ya Pontio Pilato. Lakini Yesu alisema vilevile hivi: “Hekima imejulikana kuwa ina haki kwa kazi zake.” Inafaa sana kuzichunguza kazi za wale wanaofuata maoni ya Biblia ikiwa tunataka sana kuitambua dini ya kweli.​—⁠Mt. 11:19.

MAANA YAKE NINI

24. Kwa ufupi, ni alama gani chache za maana zinazoitambulisha dini ya kweli?

24 Katika mambo ambayo tumezungumza, hatukufikiria alama zote zinazotambulisha dini ya kweli. Walakini, mambo hayo yanatupatia msingi wa kufaa kuchunguzia imani na desturi za dini yetu na kujichunguza wenyewe. Kupatana na mambo ambayo tumeona katika Biblia na katika maisha za Wakristo wa kwanza, tutafahamu vyepesi kwamba dini ya kweli inatia mambo haya: Kwamba Mungu alimwumba mwanamume moja kwa moja aishi duniani; kwamba wanadamu hawana nafsi isiyoweza kufa, bali wafu watafufuliwa wakati ujao; kwamba inatupasa tuwe imara katika kuepuka uasherati na kutegemeza utakatifu wa mpango wa ndoa; kwamba ni jambo la maana sana kutii sheria ya Mungu inayokataza damu, tuwapende wanadamu wenzetu, ambalo ni jambo linalofanya maisha yafurahishe zaidi sana; na kwamba yawapasa Wakristo watangaze ufalme wa Mungu kwa kusudi la kusaidia wengine wawe na tumaini bora ambalo Mungu anatoa.

25, 26. Kwa sababu gani yampasa kila mmoja wetu atake sana kuchunguza alama hizi za ibada ya kweli? Matokeo yatakuwa nini?

25 Labda wengine wataona kwamba dini yao au imani na desturi zao wenyewe zinatofautiana na dini ambayo Biblia inatambulisha kuwa ya kweli. Ukijiona kwamba wahitaji kufanya maguezo fulani, usikawie kufanya hivyo. Fuata shauri hili lililoongozwa na Mungu katika 1 Petro 3:10-12: “Kwa maana, atakaye kupenda maisha, na kuona siku njema . . . na aache mabaya, atende mema; atafute amani, aifuate sana. Kwa kuwa macho ya [Yehova] huwaelekea wenye haki.”

26 Tunawezaje kufuata yaliyo mema? Si kwa kuacha yasiyopatana na dini ya kweli tu, bali vilevile kwa kuchukua hatua ili tuishi kulingana na mapenzi ya Mungu wetu. Kumbuka kwamba Nuhu hakuamini tu. Biblia inatuambia kwamba Nuhu alitembea pamoja na Mungu wa kweli naye alikuwa “muhubiri wa haki.” (Tafsiri ya Zaire) Vivyo hivyo, Yesu na mitume wake waliamini wakaishi kulingana na dini ya kweli. Hii ilitia ndani kuwagawia wengine habari njema za ufalme wa Mungu na za taratibu mpya ya amani duniani ambayo Mungu ameahidi. (Mt. 4:17; 10:7; 28:19, 20) Tukifanya kama hivyo kwa moyo wote tutapata furaha nyingi sana na kuwapa watu wengine tumaini, kusudi la kuishi na furaha ya kweli. Watapata baraka nyingi kwa sababu ya kutambua na kufuata dini ya kweli​—⁠Kutoka The Watchtower, April 15, 1978.

[Picha katika ukurasa wa 14]

Mahali pa kujitia katika vita, Wakristo wa kweli wamepata umoja duniani pote​—⁠ambao msingi wake ni tumaini lao wote katika ufalme wa Mungu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki