Dini ya Kweli—Namna ya Kuitambua
“Mjazwe maarifa ya mapenzi yake . . . mkimpendeza kabisa.”—Kol. 1:9, 10.
1-4. (a)Watu wengi wanaonaje juu ya kuamua mambo ya kidini? (Matendo 18:12-17) (b) Sababu gani wewe au wengine mngeona hivyo?
IKIWA watu wangekuwa wakibishana juu ya dini ya kweli ni dini gani wakakuomba ‘uamue’ kati yao nani anayesema kweli, ungetaka ufanye hivyo?
2 Dini ni mazungumzo yanayotokeza ubishi mwingi kuliko mengine. Historia inatoa mfano mmoja unaojulikana sana na huo unatia mtume Paulo mmojawapo wa viongozi wa kwanza wa Ukristo. Paulo alikamatwa ilipokwisha kutokea ghasia kidogo kwa sababu ya maoni mbalimbali ya kidini. Shauri lake lilisikilizwa na Festo, liwali wa jimbo la Kirumi la Uyahudi. Watu waliomshtaki Paulo walikuwa viongozi wa kidini Wayahudi, kutia na kuhani mkuu Anania. Wakati uliofuata hayo Festo alimpasha Mfalme Herode Agripa wa Pili habari za mambo yaliyotukia akisema:
3 “Walipopingana [na Paulo], washtaki wake hawakumshtaki makosa yo yote niliyokuwa nimetazamia; lakini walikuwa wakibishana naye tu hivi na hivi juu ya dini yao wenyewe.”—Matendo 25:18, 19, Jerusalem Bible.
4 Kama unavyoweza kufahamu, Liwali Festo hakutaka kujitia katika ubishi wa dini. Watu wengi wanadhani kwamba lisingekuwa jambo la hekima kujidai kuwa na dini ya kweli wala kujaribu kuamua kama dini yo yote ni ya kweli. Labda umepata kusikia maoni yanayoonekana kuwa ya hekima ya kwamba, ‘Acha kila mtu aamini anavyotaka. Dini zote ni nzuri.’
5. Ni kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba kila mtu anatiwa ndani ya shauri la dini?
5 Hata hivyo, sisi sote tunatiwa ndani, haya si mazungumzo ambayo kila mmoja wetu anaweza kuepuka. Ijapokuwa Wakomunisti wanaweka mkazo juu ya sayansi na kutokuamini Mungu, dini ni sehemu ya hali yetu ya moyoni. Kama kitabu kimoja cha maarifa yote kilivyoeleza:
“Kati ya jamaa nzima ya kibinadamu ambayo imekuwako vizazi vyote na kutawanyika katika kila pembe ya dunia, hakuna jambo linalopinga kwamba mwanadamu haabudu kitu fulani anachodhani ni mungu, akivutwa bila kufikiri na kuongozwa na ufunuo au mapokeo.”
6, 7. Kila mtu ana sababu gani za kuchunguza dini ya kweli?
6 Kitabu kinachoitwa Religion and Philosophy kinasema hivi juu ya dini wakati wa zamani sana: “Mwanzo wa ulimwengu na kuwako kwa mwanadamu ndani yake ulikuwa jambo gumu kufahamika kama mauti. Maelezo ya maulizo hayo yalitofautiana sana, lakini yangali ya msingi wa dini ya kisasa. Ijapokuwa sayansi inaweza kutoa maelezo juu ya matukio ya sasa, wanadamu kila mahali wangali wakitafuta tumaini litakalofuata makumi machache ya miaka ya kuishi kwa kila mmoja.”
7 Bila shaka hatutaki tutegemee wazo au hadithi ya uongo ili tupate majibu ya maulizo hayo ya msingi na tumaini la wakati ujao. Kwa hiyo, tuna sababu inayofaa kulichunguza jambo hili la kuitambua dini ya kweli.
8. Huenda mtu akakumbuka nini anapoufikiria ulimwengu wote?
8 Maoni ya mtu mmoja ni ya kwamba hakuna Mungu, lakini yule mwingine anasema kwamba hakuna anayejua sana habari hizo, yaani, habari za kuwapo kwetu. Lakini je! maoni hayo yanafurahisha kweli au yanapatana na mambo ya hakika? Wengine wana mawazo yaliyoonyeshwa na Will Durant mwanahistoria ya filosofia, aliyetajwa kuwa akisema hivi:
“Katika vitu vyote vilivyo hai naona kuna nguvu ya muumba, nami nadhani kuna kitu kama hicho hata katika chembe ndogo sana katika nguvu zake zote zenye kupasuka. Chembe si kitu kilichokufa. Ni kitu [kilicho] na uhai. Kwa hiyo mimi sidhani ulimwengu ni kama mashine. Mashine haina uhai. Inasimama kimya isipokuwa iendeshwe na kitu kilicho hai.”
Watu wengi hata pamoja na wale wanaosema kwamba hakuna anayejua habari za Mungu, wamesumbuliwa na mawazo hayo wakitafuta jibu la uzima, nao wamewaza kwamba Muumba huyu mwenye akili nyingi zaidi angetolea viumbe vyake majibu au kuvipasha habari, kama vile sisi wanadamu tunavyowapasha habari watoto wetu wenyewe.
KUTAFUTA DINI YA KWELI
9. Sababu gani mwendo ambao Mwajemi fulani alichukua ili aichunguze Biblia, unafaa? (Ayubu 35:9-11)
9 Kwa kawaida wale wanaotafuta sana kweli wanakubali kwamba bila shaka kuna Mungu na kwamba angefunua mapenzi yake na kutupa majibu ya sababu gani tupo, maana ya uzima na tumaini letu wakati ujao. Ebu ifikirie habari ya Mwajemi mmoja aliyekuwa katika Berlin Magharibi. Miaka ya zamani baba yake alikuwa mwanasiasa mkuu, lakini yalipokwisha kutukia mapinduzi ya siasa aliipeleka jamaa yake Urusi, ambako mwanawe alipata masomo akawa fundi wa kuunda vitu. Mwishowe kijana huyo alihamia Berlin Mashariki kisha akakimbilia Berlin Magharibi. Anaeleza hivi:
“Ijapokuwa nilikuwa mtu wa dini ya Mashariki, nilikuwa sifuati dini kwa matendo. Hata hivyo, nilimwamini Mungu tangu utoto wangu na kuwaza sana mara nyingi juu ya kusudi la uzima na sababu gani kuna dini nyingi sana, Mnamo kiangazi cha mwaka 1975 nilikutana na wanafunzi wa Biblia wawili nikaongea nao. Kwa maelezo yao niliweza kuamua kwamba Biblia iliongozwa na Mungu. Walinitembelea nyumbani kwangu tukazungumza sana habari za tofauti zilizo katika dini. Wakaniachia kitabu What Has Religion Done for Mankind?a Maelezo ya kitabu hicho yaliyotegemea Biblia yaligeuza maoni yangu yote ya maisha. Mambo niliyojifunza, na kugeuka kwa fikira na matendo yangu, yameniletea furaha nyingi.”
Ilimfaa kama nini fundi huyu wa kuunda vitu aifikirie Biblia! Biblia ni kitabu kilicho kati ya maandishi yote ya zamani sana ambayo ni matakatifu na yanayoenezwa sana kuliko mengine. Biblia peke yake ndiyo inayoweza kujibu maulizo yetu haya—Sababu gani tupo? Sababu gani tunakufa? Wakati ujao una tumaini gani?
10. Ni jambo gani linaloweza kusemwa Juu ya kama dini zote zinazotumia Biblia zinafundisha jambo lile au sivyo?
10 Tunapoitaja Biblia, je! unasema, ‘Karibu watu wote wanaoikubali Biblia wanaamini yale yale’? Wengi wanadhani hivyo. Lakini, sivyo kabisa. Kama yule fundi wa kuunda vitu aliyekuwa Berlin Magharibi, mamilioni ya watu wenye mioyo minyofu na wenye akili ambao wamelichunguza ulizo hili lenye maana sana juu ya ibada ya kweli wanajua kwamba kuna tofauti kubwa sana kati ya mafundisho na desturi za dini mbalimbali zinazojidai kuitegemea Biblia. Kwa kweli, kuna tofauti kubwa sana vilevile kati ya dini nyingi hizo na Biblia yenyewe. Tofauti hizo zinaweza kutia ndani maoni yako yote juu ya uzima na dini. Changanua dini yako mwenyewe au imani zako tunapochunguza mambo machache ya msingi na yenye maana sana. Jiulize hivi, ‘Je! mimi mwenyewe ninatafuta ibada ya kweli?’ Na ukiona kwamba imani na desturi zako zinapingana na dini ya kweli, fikiria sana utakalofanya.
11. Sababu gani imetupasa sote tuwe na nia ya kufikiria kugeuza imani na mwenendo wetu?
11 Uhitaji wa kugeuza imani na mwenendo wetu usishangaze mtu ye yote anayeijua Biblia. Kwa mfano, Yesu Kristo alisema hivi juu ya wafuasi wa dini waliokuwako wakati wake, ‘ibada wanayotoa ni ya bure; mafundisho yao ni sheria tu za wanadamu.’ (Mt. 15:9, JB) Wala si shauri la mafundisho tu. Yakobo ndugu mzazi mmoja na Yesu aliandika hivi: “Ikiwa imani inatenganishwa na matendo mema, inakufa” naye “Mtu asidhani kwamba yeye ni mtu wa dini na huku angali akijidanganya mwenyewe naye hauzuii ulimi wake; mtu ye yote anayefanya hivyo hafahamu dini sawasawa.”—Yak. 2:26; 1:26, JB.
HABARI YA MAANA SANA
12, 13. Ili habari ya Adamu na Hawa ina mambo gani yanayoweza kusaidia mtu anayetaka kutambua dini ya kweli?
12 Wanapofikiria dini ya kweli, labda watu wengi watafikiria kwanza mambo ambayo Yesu alifundisha na kufanya. Lakini kabla hatujafanya hivyo, na tuangalie kidogo Mwanzo, kitabu cha kwanza cha Biblia. Duniani pote watu wanajua kinavyosema juu ya Adamu na Hawa. Ijapokuwa inaweza kuonekana kuwa habari nyepesi, ni ya maana sana kuichunguza tunapotafuta alama zinazotambulisha dini ya kweli.
13 Kwa ufupi, kitabu cha Mwanzo kinatupasha habari kwamba Mungu alimwumba mwanamume moja kwa moja, akimfanyiza kutokana na sehemu za asili za dunia kisha “akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.” (Mwa. 2:7) Muumba alichagua mmojawapo wa miti ya bustani alimokuwa akiishi Adamu ufananishe ujuzi wa mema na mabaya na kuamru hivi: “Matunda ya kila mti, wa bustani waweza kula [mpaka ushibe], walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” (Mwa. 2:16, 17) Kwa njia hiyo Mungu alionyesha haki yake ya kuamua yaliyo mema na yaliyo mabaya. Haikuwa juu ya Adamu kujaribu kuamua yaliyokuwa mema na yaliyokuwa mabaya au iliyokuwa dini ya kweli na iliyokuwa dini ya uongo. Vilevile Muumba alimfanya Hawa mwanamke, akamtoa kwa Adamu awe mwenzi wake daima. Tunasoma hivi: “Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.” (Mwa. 2:24) Basi, tunapotafuta kuitambua dini ya kweli tunaweza kujifunza mengi kutokana na habari hii inayojulikana sana.
14. Ungewezaje kumpa mtu sababu ya mambo yanayosemwa na kitabu cha Mwanzo na yale makisio ya mageuzi?
14 Kwanza, Biblia inasema waziwazi kwamba mwanamume aliumbwa na Mungu moja kwa moja. (Mwa. 2:7) Haisemi kwamba kwa muda wa mamilioni ya miaka yeye aligeuka-geuka kutokana na namna fulani ya mnyama. Twajuaje? Kwa sababu habari inaeleza kwamba wanyama walikuwa wakizaa “kwa jinsi zao.” (Mwa. 1:21, 24) Ni kweli kwamba kuna nafasi ya kutokea namna mbalimbali za wanyama katika jamii moja ya wanyama, kama vile namna nyingi na kadiri nyingi zilizo katika jamii ya paka. Lakini sheria ya Mungu iliweka mpaka uliozuia wanyama wasiweze kugeuka kutoka jamii moja wawe jamii nyingine ya wanyama, wala kugeuka kuwa wanadamu, jamii bora zilizoumbwa duniani. Zaidi ya hayo, hakuna viumbe ambavyo vimepata kuonekana wakati wo wote ambavyo namna nyingine zilitokana navyo kwa mageuzi. Je! dini yako inaikubali habari ya Biblia, au inafuata makisio ya watu wengi ya mageuzi ambayo si ya hakika?
15. Kitabu cha Mwanzo kinatuambia nini juu ya Adamu na Hawa? (Mwa. 1:28)
15 Pili, tunaweza kuona kwamba Adamu aliumbwa akiwa na tumaini la uzima wa milele hapa duniani. Mungu alisema kwamba angekufa ikiwa angekosa kutii. Ikiwa angemtii Mungu, hangekufa. Angeendelea kuishi duniani. Akiwa nini? Akiwa nafsi ya kibinadamu. Je! hatukusoma hivi, “mtu akawa nafsi hai”?—Mwa. 2:7.
16-18. Unapozungumza na mtu juu ya kuitambua dini ya kweli, ungewezaje kutumia yanayosemwa na kitabu cha Mwanzo juu ya nafsi ya kibinadamu na kama kuna kuishi baada ya kufa?
16 Mambo hayo ya hakika ni ya maana kwa sababu dini nyingi zinafundisha kwamba kila mwanadamu ana nafsi ndani yake isiyoweza kufa. Hayo yalikuwa mafundisho makuu katika Misri na Babeli ya kale, nayo bado yanapatikana katika dini nyingi. Lakini je! yanapatana na yale ambayo kitabu cha Mwanzo kinasema juu ya Adamu? Hata kidogo. Adamu hakuwa na nafsi ndani yake isiyoweza kufa, yeye alikuwa nafsi. Na wakati wa kufa kungetukia jambo gani? Je! angepokea uzima usioweza kufa kama roho? Sivyo! Mungu alisema kwamba angerudi kwenye ardhi, “kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.” (Mwa. 3:19) Kufa kwa Adamu kulikuwa adhabu ya kuvunja kwake sheria ya Mungu, hakukuwa hatua ya kufikia uzima usioweza kufa mahali pengine.
17 Jiulize mwenyewe hivi, ‘Je! hivyo ndivyo dini yangu imenifundisha?’ Hakuna mahali ambapo Biblia inafundisha kwamba wanadamu wana nafsi zisizoweza kufa, zinazoendelea kuishi mwili ukiisha kufa. Inatoa tumaini bora, yaani, kwamba Mungu aweza kumfufua mtu akiwa nafsi aishi duniani au katika makao ya kiroho.—Matendo 24:15; 1 Kor. 15:35-38.
18 Kulingana na mambo tunayosoma katika kitabu cha Mwanzo, je! dini yako inafundisha kwamba Mungu alikusudia wanadamu waishi duniani milele? Dini kubwa nyingi zinafundisha watu kwamba wataishi mbinguni wakiisha kufa, watapata raha mahali pengine au jambo kama hilo. Alama moja ya kutambulisha dini ya kweli ni kukubaliwa kwa mafundisho ya Biblia ya kwamba dunia ni makao ya wanadamu, ambapo Mungu anakusudia wanadamu waishi milele.—Isa. 45:18.
MWENENDO UNATIWA NDANI VILEVILE
19, 20. Ungewezaje kutumia yanayosemwa na kitabu cha Mwanzo juu ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya ili usaidie mtu achunguze desturi zilizo katika dini yake? (Kut. 20:15; Yos. 7:20-25)
19 Imetupasa tuchunguze vilevile kwamba, dini ya kweli inayofunuliwa katika kitabu cha Mwanzo inatia mwenendo, si mafundisho au imani fulani tu.
20 Adamu na Hawa walipovunja sheria ya Mungu iliyokataza kula tunda la mti huo, dhambi yao kubwa ilikuwa kutokutii. Lakini umepata kufikiria kwamba walipofanya hivyo walikuwa wakichukua vilevile kitu kisichokuwa mali yao? Maana yake tunaweza kusema kwamba huo ni wivi. Walifukuzwa katika bustani ya ibada ya kweli kwa sababu ya kutokutii kwao, dhambi yao iliyotia ndani wivi. Labda unajua kwamba dini nyingi zinapinga wivi, sivyo? Lakini kwa matendo yao, zinamchukulia hatua gani mwivi asiyetubu, kwamba ni mtu tu anayeiba vitu dukani au kwamba ni mtu mwenye mshahara mnono na mwenye kuvaa vizuri anayedanganya watu au anayetumia vibaya mali ya biashara ambayo ameagizwa kutunza? Je! zinawafukuza wevi wasiotubu watoke katika ‘kundi’ kama Mungu alivyomfukuza Adamu? Ebu fikiria.
21. Yanayosemwa na kitabu cha Mwanzo sura ya 2 juu ya ndoa yanatofautianaje na yaliyo kawaida ya dini nyingi? (Mwa. 20:1-9)
21 Ifikirie ndoa vilevile. Ijapokuwa katika mazungumzo yetu mpaka hapa tumeifikiria habari ya Adamu na Hawa tu, kulingana na yanayosemwa juu ya kuambatana kwao, tunaweza kujiuliza hivi, Dini yangu ina maoni gani juu ya ndoa na talaka? Je! mume na mke wanatazamiwa kuambatana, au talaka ndilo jambo la kawaida? Mungu anatajwa kuwa ‘anachukia kuachana’ (talaka). (Mal. 2:16) Je! hayo ndiyo maoni ya dini unazojua, labda hata dini yako?
YALIYOMPATA NUHU KATIKA DINI YA KWELI
22, 23. Ungewezaje kuwapa wengine sababu za hatua ambayo Nuhu alichukua na habari ya gharika ili uwasaidie watambue dini ya kweli? (Eze. 14:14; Ebr. 11:7)
22 Acheni tuzungumze habari nyingine ya Biblia inayoweza kutusaidia kuitambua dini ya kweli. Habari hii inatia ndani Nuhu, ambaye tunaambiwa kwamba “alikwenda pamoja na Mungu.” Wakati “maovu ya mwanadamu [yalipokuwa] makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote,” Nuhu hakufanya dini ya kweli iwe mali yake peke yake. Hakuiona kuwa jambo la kibinafsi na la kipekee. Yeye alikuwa “muhubiri wa haki.” Biblia inatuambia kwamba Mungu alileta gharika ya dunia nzima awaharibu waovu, lakini alilinda Nuhu, mke wake, watoto wake watatu wa kiume na wake zao.—Mwa. 6:5—8:2, UV; 2 Pet. 2:5, ZSB.
23 Labda wengine watajibu kwamba habari hiyo ya Nuhu ni hadithi tu ya uongo au fumbo tu la maneno (mfano.) Dini yako inasemaje juu ya hilo? Ikiwa ungeuliza mmojawapo wa viongozi wake, je! angesema kwamba habari hiyo ya Biblia juu ya Nuhu na gharika inapendeza sana lakini si ya kweli? Ikiwa hivyo, hilo lingekuwa wazi, kwa maana lingemweka katika hali ya kupingana na Yesu Kristo, Mwanzishi wa Ukristo. Yesu aliikubali habari hiyo ya Biblia juu ya Nuhu na gharika ya dunia kuwa ya kweli, ndivyo na mitume wake.—Luka 17:26, 27; 1 Pet. 3:20.
24-26. Ni amri gani ambazo Mungu alimpa Nuhu, na kwa sababu gani zinafaa sana?
24 Kulingana na habari iliyomo katika Mwanzo sura ya 9, Nuhu na jamaa yake walipotoka katika safina ambayo katika hiyo waliokoka gharika, Mungu alieleza amri fulani zilizo wazi zinazoweza kutusaidia tuitambue dini ya kweli leo. Tunasoma hivi:
“Kila kiendacho kilicho hai kitakuwa chakula chenu, kama nilivyowapa mboga za majani, kadhalika nawapeni hivi vyote. Bali nyama pamoja na uhai wake, yaani, damu yake, msile. Hakika damu yenu ya uhai wenu nitaitaka; na kwa mkono wa kila mnyama nitaitaka; na kwa mkono wa mwanadamu, kwa mkono wa ndugu ya mtu nitataka uhai wa mwanadamu. Atakayemwaga damu ya mwanadamu, damu yake huyo itamwagwa na mwanadamu; maana kwa mfano wake Mungu alimfanya mwanadamu.”—Mwa.9:3-6.
25 Ijapokuwa Mungu alisema hivyo maelfu ya miaka iliyopita, ilikuwa mwanzoni mwa kipindi kipya cha historia ya wanadamu. Jambo hili linaweka mkazo kwamba kusema hivyo ni kwa maana sana ili dini ya kweli ipate kutambuliwa. Kupitia kwa watoto wake wa kiume, Nuhu akawa babu ya wanadamu wote. Kwa hiyo, amri ambazo Mungu alimpa Nuhu zinahusu wanadamu wote walio duniani leo.
26 Amri hizo zilikuwa na maana gani kwa Nuhu na jamaa yake? Kwanza, hawakuruhusiwa kula nyama pamoja na damu ikiwa bado ndani yake. Kula damu iliyokuwa mfano wa uhai au nafsi ya mnyama kulikatazwa. Nuhu aliambiwa vilevile asiue watu. Kwa hiyo wanadamu wote wakiwa wazao wa Nuhu, wanatakiwa kuheshimu damu na uhai, ikiwa wanataka kupata kibali ya Mungu.
27. Ni uchunguzi gani zaidi unaotakiwa ili kutambua dini ya kweli, na ni kwa sababu gani imetupasa tuione ikiwa na mwendo uo huo unaopatana?
27 Ijapokuwa tumechunguza habari mbili tu za kwanza za Biblia mpaka hapa, tumeweza kutofautisha alama chache zinazotambulisha dini ya kweli. Kwa kuwa ndani ya mioyo yetu sote tunataka sana kuabudu, mambo ambayo tumechunguza mpaka hapa yatatufaa sana. Lakini tunaweza kusaidiwa zaidi tuitambue dini ya kweli kwa kuchunguza sehemu fulani za mafundisho ya Yesu Kristo na ya mitume wake wakati wa mwanzo wa Ukristo. Katika kufanya hivyo, tutaona upatano ulio kati ya mwanzo wa Biblia na sehemu zake za mwisho juu ya alama za kutambulisha dini ya kweli.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichapwa na Watchtower Bible and Tract Society mwaka 1951.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Biblia inasema wazi kwamba mtu aliumbwa na Mungu na ya kwamba mtu mwenyewe alifanywa kuwa “nafsi hai”—wala si kwamba ana nafsi isiyoweza kufa
[Picha katika ukurasa wa 9]
Maoni ya dini yako juu ya ndoa na talaka ni nini? Je! waume na wake wanatazamiwa kuambatana kama inavyofundisha Biblia?
[Picha katika ukurasa wa 10]
Biblia inatoa habari ya Nuhu na gharika kama jambo lililotokea kweli kweli—je! hivyo ndivyo umefundishwa?