Je! Dini Yoyote Ni Nzuri vya Kutosha?
“Hali ya nyakati zetu inahuzunisha. Tunahitaji dini, lakini hakuna mahali popote tunapopata Mungu awezaye kuifaa.” —Lucian Blaga, Mshairi na mwanafalsafa Mromania
“Dini na makasisi wamekuwa, na labda wataendelea muda mrefu wakiwa, miongoni mwa maadui wakubwa zaidi wa maendeleo na uhuru.”—Khristo Botev, Mshairi Mbulgaria.
MANUKUU hayo yanayoandama yanaonyesha tatanisho, ambamo watu wengi wenye mioyo myeupe hujipata wenyewe. Ndani sana moyoni, wanahisi uhitaji wa dini, lakini Mungu wa kifumbo ambaye makasisi wanafundisha juu yake si Mungu ambaye wanaweza kumfahamu na kumpenda. Isitoshe, wanatambua kwamba makasisi na dini zao wamefanya mengi kuzuia maendeleo na uhuru wa kibinadamu. Naam, ingawa uhitaji wa dini unazidi kutambuliwa, watu wanyofu hawatakubali dini yoyote tu.
Tofauti ya Maana
Dini ina sehemu kubwa katika umbo na historia ya ainabinadamu. The New Encyclopœdia Britannica husema juu ya dini “kuwa jambo la hakika katika maono, utamaduni, na historia ya kibinadamu” na huongeza hivi: “Ushuhuda mbalimbali wa mielekeo na uaminifu-mshikamanifu wa kidini umo katika kila sehemu ya maisha ya kibinadamu.” Lakini historia huonyesha kwamba hakuna hata moja ya dini kubwa za ulimwengu ambayo imekuwa baraka kwa ainabinadamu.
Mwanasiasa wa India Jawaharlal Nehru alieleza hivi wakati mmoja: “Tamasha ya ile iitwayo dini, au kwa vyoyote dini iliyopangwa kitengenezo, katika India na penginepo, imetujaza na hofu.” Unapofikiria vita ambavyo vimepigwa na uhalifu uliofanywa kwa jina la dini, je, waweza kwa unyofu kutokubaliana naye?
Katika karne ya 18, mwanafalsafa Mfaransa Voltaire alionyesha tofauti yenye kupendeza. Aliandika hivi: “Unasema, dini imetokeza matendo mengi yenye sifa mbaya. Badala ya hiyo, wapaswa kusema ushirikina ndio [umefanya hivyo], ushirikina unaotawala juu ya tufe letu lenye huzuni. Ushirikina adui mkatili zaidi wa ibada safi ambayo twadaiwa na yule Aliyeko Mkuu Zaidi.” Voltaire alishindana na kutokuvumilia dini kwa siku yake, lakini alidumisha imani yake katika Mungu akiwa Muumba wa ulimwengu wote mzima. Aliona tofauti kati ya dini ya kweli na bandia.
Uhitaji wa Kuchagua
Si wote wanaokubaliana na Voltaire. Wengine hudai kuona uzuri katika dini zote; kwa hiyo, wao hawahisi uhitaji wowote wa kweli wa kutafuta dini ya kweli. Watu kama hao wanapaswa kutii onyo lililotolewa na nabii Isaya, aliyeandika hivi: “Ole wao wasemao kwamba uovu ni wema, na kwamba wema ni uovu; watiao giza badala ya nuru, na nuru badala ya giza; watiao uchungu badala ya utamu, na utamu badala ya uchungu!” (Isaya 5:20) Dini bandia imetokeza lile lililo baya kwa wanadamu. Imesababisha giza la kiroho na kuwaacha watu wenye mioyo minyofu wakiwa na uchungu.
Kwa hiyo, uchaguzi si kati ya kuwa asiyemwamini Mungu na kuamini dini yoyote. Huo si rahisi jinsi hiyo. Mtu anapotambua uhitaji wa kuwa na Mungu, ni lazima atafute dini ya kweli. Kama mtafiti Émile Poulat alivyoeleza jambo hilo vizuri katika Le Grand Atlas des Religions (Atlasi Kubwa ya Dini): “Mambo ambayo [dini] hufundisha na kudai ni ya namna nyingi sana hivi kwamba haiwezekani kuyaamini yote.” Kwa kupatana na hilo, Encyclopœdia Universalis (Ensaiklopedia ya Ulimwengu Wote Mzima, 1989) ya Kifaransa yasema hivi: “Karne ya 21 ikirudia dini, . . . mwanadamu atapaswa kuamua kama mambo matakatifu anayotolewa ni ya kweli au ni bandia.”
Jinsi ya Kuchagua Dini ya Kweli
Ni nini kitakachotuongoza katika kuichagua dini ya kweli? Encyclopœdia Universalis ni sahihi inapokazia umaana wa kweli. Dini inayofundisha mambo ya uwongo haiwezi kuwa ya kweli. Nabii mkuu zaidi aliyepata kutembea duniani alitaarifu hivi: “Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.”—Yohana 4:24.
Nabii huyo alikuwa Yesu Kristo, naye pia alitangaza rasmi hivi: “Jilindeni dhidi ya walimu wa dini bandia, wanaowajia ninyi wakiwa wamejivalia kama kondoo walakini kwa kweli ni mbwa-mwitu wenye pupa. Mwaweza kuwatambua kwa matunda yao. . . . Kila mti mzuri hutokeza matunda mazuri, walakini mti mbovu hutokeza matunda mabaya.” (Mathayo 7:15-17, Phillips) Wakiona matunda mabaya ya dini “kubwa” za ulimwengu, na hata za mafarakano na madhehebu ambayo yametokea, watu wengi wenye mioyo myeupe wanaanza kuyaona yote hayo kuwa ‘miti mibovu,’ isiyo mizuri vya kutosha. Lakini wanaweza kupataje dini ya kweli?
Kwa wazi isingewezekana kujifunza maelfu yote ya dini zilizo ndani na nje ya Jumuiya ya Wakristo kabla ya kuchagua. Hata hivyo, ikiwa—kama Yesu alivyosema—tunatumia kweli na matunda kuwa mambo ya kuthibitishia, kutambulisha dini ya kweli kunawezekana.
Kweli na Matunda
Yesu alitaja kweli. Kwa habari hiyo, ni kikundi kipi cha waamini kinachokataa mambo ya uwongo wa kidini yanayotokana na hekaya ya kale na falsafa ya Kigiriki inayoenea katika dini nyingi? Uwongo mmoja wa jinsi hiyo ni lile fundisho kwamba nafsi ya kibinadamu kwa asili ni isiyoweza kufa.a Fundisho hilo limetokeza fundisho la moto wa helo lenye kumfanya Mungu asiheshimiwe.
Yesu alitaja matunda pia. Kwa habari hiyo, je, unajua dini ambayo imetokeza ushirika wa kweli wa kimataifa ambapo vizuizi vya rangi, lugha na taifa vinashindwa na upendo na kuelewana? Je! wajua jumuiya ya kidini ya ulimwenguni pote ambayo washirika wayo wangependelea kunyanyaswa kuliko kuruhusu wanasiasa au viongozi wa kidini wawachochee kuwachukia ndugu na dada zao na kuwaua kwa jina la utukuzo wa taifa au dini? Dini iliyokataa mambo hayo ya uwongo wa kidini na kuzaa matunda ya jinsi hiyo ingetoa ushuhuda wenye nguvu kuwa ndiyo ya kweli, sivyo?
Dini ya Kweli Inazoewa Leo
Je! kuna dini ya jinsi hiyo? Naam, kunayo. Walakini ni lazima ukiri kwamba si mojawapo ya dini kubwa za ulimwengu. Je! hilo lapasa kutushangaza? La. Katika Mahubiri yake ya Mlimani yenye umaarufu, Yesu alitaarifu hivi: “Ingieni kwa kupitia mlango ulio mwembamba; maana mlango ni mpana, na njia ni pana iendayo upotevuni, nao ni wengi waingiao kwa mlango huo. Bali mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani, nao waionao ni wachache.”—Mathayo 7:13, 14.
Kwa hiyo dini ya kweli itapatikana wapi? Kwa unyenyekevu na unyofu wote, ni lazima tuseme kwamba Mashahidi wa Yehova ndio wanaofanyiza jumuiya ya kimataifa inayotembea kwenye ‘njia hiyo iliyosonga.’ Ni kweli, zile dini kubwa kubwa huwaita Mashahidi wa Yehova farakano (madhehebu) kwa dharau. Lakini hivyo ndivyo viongozi wa kidini wa karne ya kwanza W.K. walivyowaita Wakristo wa mapema.—Matendo 24:1-14.
Kwa nini Mashahidi wa Yehova wana uhakika kwamba wao ndio walio na dini ya kweli? Wao hujumlika kuwa udugu wa kimataifa unaofikia nchi zaidi ya 200 na unaoshinda migawanyiko ya kitaifa, rangi, lugha na cheo cha kijamii. Na wao hukataa kuamini mafundisho—hata yawe ya kale jinsi gani—ambayo hupinga kwa wazi yale Biblia husema. Lakini waliingiaje katika hali hiyo yenye uvutio wa kuamsha wivu? Na kuzoea kwa dini ya kweli kunahusisha nini? Hilo na maswali mengine juu ya dini yatazungumziwa katika makala mbili zifuatazo.
[Maelezo ya Chini]
a Ili kupata uthibitisho wenye maelezo mazuri juu ya hilo, ona kitabu Mankind’s Search for God, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., kurasa 52-7.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Zile krusedi zilikuwa sehemu ya matunda mabaya ya dini bandia
[Hisani]
Bibliothèque Nationale, Paris
[Picha katika ukurasa wa 8]
Dini ya kweli hutokeza matunda mazuri