Kuadhimisha Kifo cha Mwanamume Mkuu Zaidi Aliyepata Kuwa Duniani
“TAZAMA! Mwanamume yule!” Maneno hayo yalisemwa, si wakati wa kuumbwa kwa mwanamume mkamilifu Adamu katika shamba la Edeni miaka zaidi ya 6,000 iliyopita. Yalisemwa, karibu miaka 4,058 baadaye, kuhusu mwanamume aliyelingana na Adamu kabisa. Mwanamume huyo alikuwa amezaliwa kimwujiza na bikira Myahudi, Mariamu bintiye Eli wa Bethlehemu. Yeye, ambaye jina lake aliitwa Yesu, alikuwa Mwana wa Mungu, ambaye uhai wake ulikuwa umehamishwa kwa uwezo wa Mungu kutoka mbinguni. Yeye alikuwa amezaliwa kwa roho ya Babaye wa kimbinguni, hivyo akatengenezewa njia ya kurudi mbinguni. Jambo hilo lilitokea mara tu alipobatizwa katika Mto Yordani na Yohana Mbatizaji, katika vuli ya mwaka 29 W.K. Hapo Mungu alisema kutoka mbinguni na kumtangaza Yesu aliyekuwa ametoka kubatizwa kuwa ni Mwanawe. Yohana Mbatizaji alishuhudia jambo hilo.—1 Yohana 1:29-36.
Miaka mitatu na nusu baadaye, katika Siku ya Kupitwa ya masika ya mwaka 33 W.K., alikuwa akihukumiwa mbele ya gavana (liwali) Mroma wa jimbo la Yudea, Pontio Pilato. Mahakma ya Kiyahudi katika mji mkuu wa Yerusalemu ilikuwa imemhukumu wakati wa usiku wa Siku ya Kupitwa nayo ilikuwa imempeleka kwa gavana Mroma akahojiwe ili kumhukumu kwao kifo kuungwe mkono na mamlaka ya Kiroma. Kwa kutimiza unabii wa Biblia katika Zaburi 41:9, yeye alikuwa amesalitiwa kwa adui zake Wayahudi na mmoja wa wale mitume 12 wake mwenyewe, Yuda Iskariote. Gavana Pilato hakumpata Yesu na hatia ya mashtaka aliyokuwa ameshtakiwa na mahakma kuu ya Kiyahudi. Alijulisha uhakika huo umati wa Wayahudi waliokuwa wamekusanyika nje ya jumba la gavana huyo. Itikio lao lenye uadui lilikuwa hili, “Mtundike! Mtundike!” Kichwa cha Yesu kilikuwa kimezingwa kwa taji la miiba, na alikuwa amefunikwa vazi lenye rangi ya zambarau na watesi wake Waroma. Kwa kupatana na kuvikwa kwa Yesu, akiwa na taji na mavazi yenye rangi ya zambarau, Gavana Pilato alijaribu kuwasihi Wayahudi, ambao muda mrefu uliopita walikuwa wamenyang’anywa ufalme wao, kwa kupaza sauti hivi: “Mwoneni! Mfalme wenu!” Kwa unafiki, Wayahudi, wakiongozwa na makuhani wakuu wao, kwa kujibu walipaza sauti hivi: “Sisi hatuna mfalme ila Kaisari.”—Yohana 19:5-15, NW.
Baadaye siku iyo hiyo Yesu akafa juu ya mti wa kufishia na maiti yake ikazikwa katika kaburi lililokuwa katika shamba. Kama vile mwana-kondoo yule wa Siku ya Kupitwa aliyeliwa na mitume wake usiku uliokuwa umetangulia, yeye akafa, walakini hata mfupa mmoja wa mwili wake haukuvunjwa. (Kut. 12:46; Zab. 34:20) Mitume hao waaminifu walikuwa wamepewa wajibu wa kuadhimisha kifo chake kila mwaka katika Siku ya Kupitwa. Akiwa amekwisha kutimiza wajibu wake mwenyewe chini ya sheria ya Kiyahudi ya kuadhimisha chakula cha jioni cha Siku ya Kupitwa akiwa na mitume wake, mara moja Yesu akaanzisha kitu kati yao cha kusherehekea kifo chake. Kitu hicho kikaja kuitwa Chakula cha Jioni cha Bwana, au Kijio cha Jioni. Masimulizi yaliyoongozwa na Mungu juu ya kuanzishwa kwa hicho chakula cha jioni na Yesu yanasema hivi:
“Walipoendelea kula [chakula cha jioni cha Siku ya Kupitwa], Yesu akatwaa mkate na, baada ya kutoa baraka, yeye aliuvunja na, alipokuwa akiwapa wanafunzi wake, yeye akasema: ‘Chukueni, leni. Huu unafananisha mwili wangu.’ Pia, akachukua kikombe na, akiisha kutoa shukrani, yeye aliwapa, akasema: ‘Nyweni kutoka kwacho, ninyi nyote; kwa maana hii inamaanisha “damu ya agano” yangu, ambayo itamwagwa chini kwa ajili ya wengi kwa msamaha wa dhambi. Walakini mimi nawaambia ninyi, mimi sitakunywa tena kamwe tangu sasa na kuendelea yo yote ya tokeo hili la mzabibu mpaka siku ile nitakapolinywa likiwa jipya pamoja nanyi katika ufalme wa Baba yangu.’ Mwishowe, baada ya kuimba sifa, wakatoka nje waende kwenye Mlima wa Mizeituni.”—Mt. 26:26-30, NW.
Yesu alikuwa amemwondosha mwanafunzi yule msaliti, Yuda Iskariote, katika chakula cha jioni cha Siku ya Kupitwa. Kwa hiyo maneno ya Yesu hayakumhusu mwanafunzi huyo mwenye kukosa uaminifu alipowaambia hivi wale wanafunzi 11 waliobaki: “Mimi sitakunywa tena kamwe tangu sasa na kuendelea yo yote ya tokeo hili la mzabibu mpaka siku ile nitakapolinywa likiwa jipya pamoja nanyi katika ufalme wa Baba yangu.” (Mt. 26:29) Maneno hayo hayangeweza kumaanisha ndivyo ingalivyokuwa wakiwa duniani na wakiwa na mwili kama raia wa Ufalme huo wakati wa utawala wa Masihi Yesu wa miaka 1,000. Kufikia wakati huo wangekuwa wamekwisha kufa kwa muda mrefu na wangehitaji kufufuliwa kwenye uzima wa kibinadamu duniani baada ya “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–Magedoni. (Ufu. 16:14-16) Hata hivyo, Yesu hakumaanisha hivyo kwa habari ya wanafunzi waaminifu, kama hao 11. Yeye alikuwa anamaanisha kuwa kwao katika ufalme wa kimbinguni pamoja naye kwa kufufuliwa kutoka kwa wafu na kuingizwa kwenye uzima wa roho.
Wakati wa mwaka uliotangulia (32 W.K.), yeye alikuwa amewaambia hivi wanafunzi hao: “Baba yenu anajua mnahitaji vitu hivyo. Hata hivyo, tafuteni wakati wote ufalme wake, na vitu hivyo mtaongezewa. Msiogope, kundi dogo, kwa sababu Baba yenu amekubali kuwapa ufalme.” (Luka 12:30-32, NW) Kupewa kwao ufalme wa kimbinguni na Baba wa kimbinguni kungehusu ‘agano la Ufalme,’ na juu ya jambo hilo Bwana Yesu alisema alipowaambia hivi wale mitume waaminifu 11 kuhusiana na chakula cha jioni cha kukumbuka kifo chake: “Hata hivyo, ninyi ndio mlioshikana nami katika majaribu yangu; nami nafanya agano pamoja nanyi, kama vile Baba yangu alivyofanya agano pamoja nami, la ufalme, ili mweze kula na kunywa penye meza yangu katika ufalme wangu, na kuketi juu ya viti vya enzi na kuhukumu yale makabila kumi na mawili ya Israeli.”—Luka 22:28-30, NW.
Kutokana na hilo ni wazi kabisa kabisa kwamba wale walioshiriki kula katika mwadhimisho huo wa kwanza wa Chakula cha Jioni cha Bwana wangeshiriki pamoja na Bwana Yesu Kristo aliyetukuzwa katika ufalme huo wa kimbinguni. Vivyo hivyo, washiriki wote wa baadaye katika mwadhimisho wa Chakula cha Jioni cha Bwana wangepaswa kuwa ni wale waliopewa mwito wa kimbinguni na ambao Yesu Kristo angeleta kwenye ‘agano la Ufalme.’
Mtume Paulo alipeleka barua yake kwa Wakristo wa jamii hiyo, karibu miaka 22 baadaye (karibu mwaka 55 W.K.), barua ambayo katika hiyo anazungumza juu ya Chakula cha Jioni cha Bwana na ufufuo wa wafu, yaani, “ufufuo wa kwanza.” Katika maneno aliyowaandikia aliendelea kusema hivi: “Kadhalika na [ufufuo wa] wafu. Hupandwa katika uharibifu; hufufuliwa katika fahari; hupandwa katika aibu; hufufuliwa katika fahari; hupandwa katika udhaifu; hufufuliwa katika nguvu; hupandwa mwili wa asili; hufufuliwa mwili wa roho. Ikiwa uko mwili wa asili, na wa roho uko. . . . Na kama alivyo yeye wa mbinguni, ndivyo walivyo walio wa mbinguni. Na kama tulivyoichukua sura yake yule wa udongo [Adamu], kadhalika tutaichukua sura yake yeye aliye wa mbinguni.”—1 Kor. 15:42-49; Ufu. 20:5, 6.
Hata hivyo, kabla ya kuzungumza juu ya ufufuo, mtume Paulo aliandika juu ya mwadhimisho wa kila mwaka wa Chakula cha Jioni cha Bwana, akasema: “Kwa maana mimi nalipokea kwa Bwana niliyowapa nanyi, ya kuwa Bwana Yesu usiku ule aliotolewa alitwaa mkate, naye akiisha kushukuru akaumega, akasema, Huu ndio mwili wangu ulio kwa ajili yenu; fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu. Na vivi hivi baada ya kula [mkate wa chakula cha jioni] akakitwaa kikombe, akisema, Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu; fanyeni hivi kila mnywapo, kwa ukumbusho wangu. Maana kila mwulapo mkate huu na kukinywea kikombe hiki, mwaitangaza mauti ya Bwana hata ajapo.”—1 Kor. 11:23-26.
Kulikuwa ubora wa kiroho wa wao ‘kutangaza mauti ya Bwana’ kwa njia hiyo, kwa maana kwa njia hiyo walikuwa tofauti na Wayahudi wa asili. Mahali pa kuadhimisha chakula cha jioni cha Siku ya Kupitwa kila mwaka na kukombolewa kutoka nchi yenye uonezi ya Misri, wangeadhimisha kifo cha yule aliyefananishwa na mwana-kondoo wa Siku ya Kupitwa huko Misri. Huyo mwana-kondoo wa Siku ya Kupitwa wa kale alitumika kwa ajili ya ukombozi wa Waisraeli wa asili watoke utumwani Misri, walakini hakuwaondolea laana ya dhambi. Kwa upande mwingine, kifo cha “Mwana-kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu” kinawaondolea wanafunzi wa Yesu Kristo laana na dhambi na kinawaletea ukombozi wasiwe sehemu ya taratibu hii ya mambo ya kilimwengu, Misri ya kisasa. Vilevile kinawakumbusha wanafunzi juu ya msingi wa agano jipya, mpango wa Mungu ambao kupitia huo anachukua kutoka ulimwenguni watu kwa ajili ya jina lake, kwa sababu Yesu Kristo, Musa Mkuu Zaidi, ndiye mpatanishi wa hilo “agano jipya.” (Yer. 31:31-33) Vilevile kinawakumbusha juu ya ‘agano la ufalme,’ agano ambalo wameingizwa ndani yalo. Hawapaswi kusahau uhakika wa kwamba wameitwa kwenye ufalme huo wa kimbinguni wawe warithi washirika pamoja na Yesu Kristo, mzao wa Mfalme Daudi, “Mfalme wa Wafalme na Bwana wa Mabwana.”—Ufu. 19:16.
WATAZAMAJI WENYE MFANO WA KONDOO WA MWADHIMISHO HUO
Leo, karibu na mwisho wa hii taratibu ya mambo iliyohukumiwa maangamizi, kuna mabaki tu ya wanafunzi wa Kristo ambao ni warithi pamoja naye wa ufalme wa kimbinguni. Walakini mwadhimisho wao wa Ukumbusho kila mwaka ni maana sana kwa umati wa watu wenye kuongezeka kutoka mataifa yote. Wao wana furaha sana kualikwa wahudhurie mwadhimisho wa Chakula cha Jioni cha Bwana kinachoadhimishwa na mabaki ya Waisraeli wa kiroho, ambao wamo katika agano jipya na pia katika agano la Ufalme. Wao pia wameupa kisogo ulimwengu huu wenye kuongozwa na Ibilisi nao wanapiga hatua pamoja na mabaki ya Waisraeli kiroho kuelekea kwenye Nchi ya Ahadi iliyo bora zaidi, taratibu mpya ya mambo ya Mungu ikiwa chini ya uongozi wa ufalme wa Yesu Kristo na warithi washirika wake 144,000. Wao walitangulia kufananishwa na umati mkubwa sana uliochanganyika wa watu wasio Waisraeli walioondoka Misri yenye kuongozwa na mashetani wakati wa usiku huo wa kwanza wa Siku ya Kupitwa, wakajiweka upande mmoja na Waisraeli hao wenye kuondoka na wakafuata ibada ya Yehova Mungu. (Kut. 12:38) Hilo “kundi kubwa la watu waliochangamana” walipita Bahari Nyekundu (Shamu) pamoja na Waisraeli waliokuwa wakitoroka nao wakawa mashahidi wa ukombozi wa Yehova wa watu wake huko na wakawa washiriki pamoja nao, Wangeweza kufurahia jambo hilo pia!
“Kundi kubwa la watu waliochangamana” la kisasa la wenzi wa mabaki ya Waisraeli wa kiroho lilifananishwa na “mkutano mkubwa” usio na hesabu ambao mtume Yohana aliona wakifurahi kwenye hekalu la kiroho la Yehova. Wakiwa wamekwisha kujitenga na ulimwengu huu wa kale ulio najisi (chafu), walifananishwa kama kwamba ‘wamevaa mavazi meupe’ na kama kwamba wana “matawi ya mitende mikononi mwao.” Kama vile mabaki ya Waisraeli wa kiroho, wamejiweka wenyewe wakf kwa Yehova Mungu bila kumwekea masharti, kupitia Mwana-kondoo wake, Yesu Kristo, na wameuonyesha wakf huo kwa ubatizo wa maji. “Wanatazamia kutoka katika “dhiki ile iliyo kuu” ambayo iko mbele tu ya ulimwengu huu uliohukumiwa maangamizi, na baada ya hayo kwa maana kamili wataweza kupaza sauti kwa shangwe hivi: “Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-kondoo.” (Ufu. 7:9, 10) Basi, ukiwa na sababu kubwa sana, huu “mkutano mkubwa” utataka kukusanyika pamoja na mabaki ya kiroho katika usiku wa kukikumbuka kifo cha Mwana-kondoo huyo.
Tangu mwadhimisho wa Ukumbusho wa masika ya mwaka 1936, washiriki wa “mkutano mkubwa” wamejiona huru kuhudhuria sherehe ya Chakula cha Jioni cha Bwana, ingawa hawali mkate wa mfano wala kunywa divai ya mfano.a Tangu washiriki wa huo mkutano mkubwa wa Ufunuo 7:9-17 watambulishwe Mei 31, 1935, kwenye kusanyiko la Washington (D.C.) la Mashahidi wa Yehova, wamealikwa kipekee na mabaki waliotiwa mafuta wahudhurie Chakula hicho wakiwa watazamaji. Wamefanya hivyo kwa sababu ya kuthamini kutoka moyoni dhabihu ya ukombozi ya Bwana Yesu Kristo. Kutokushiriki kwao kula si kizuizi cha kujifanyia tu, kilichofanyizwa na wanadamu kiwazuie, bali ni kutenda kulingana na Neno la Mungu.
Sababu gani ni kweli hivyo? Ndivyo ilivyo kwa sababu Mwanzilishi wa mwadhimisho huo aliuanzisha usherehekewe na wale ambao alifanya pamoja nao agano la ufalme wa kimbinguni. Ingawa wamejiweka wakf na kubatizwa, wale wa “mkutano mkubwa” wanatambua kwamba hawajaingizwa kwenye agano hilo la Ufalme. Wao si Waisraeli wa kiroho, kwa kuwa hawajaingizwa kwenye “agano jipya” hilo, ambalo linafanywa pamoja na Waisraeli wa kiroho kupitia Mpatanishi Yesu Kristo. Hawajazaliwa kwa roho takatifu iliyoanza kumwagwa juu ya wale wanafunzi 120 huko Yerusalemu siku ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K. Kwa njia ya mfano, ‘hawajakufa pamoja na Kristo’ kwa kuacha kuwa na mataraja yote ya uzima ya kidunia ya wakati ujao katika dunia iliyo paradiso chini ya usimamizi wa ufalme wa Mungu. Hawatazamii ‘kuzikwa’ pamoja na Kristo, ili wawe katika ‘mfano wa kufufuliwa kwake.’ Kwa hiyo iwapo wangeshiriki kula mkate na kunywa divai ambayo kwa msingi inafananisha mwili wa kibinadamu na damu ya Yesu Kristo, wangekuwa wakidanganya, kwa sababu wao hawamo katika mipango kama hiyo na Yesu Kristo, Mwana-kondoo wa Mungu. Kwa sababu hiyo wanajiepusha kushiriki kula mifano hiyo pamoja na mabaki waliotiwa mafuta. Hata hivyo, kutokushiriki kwao kula hakuwazuii wasipate uzima wa milele, kwa maana unapatikana kupitia imani kwa Yesu Kristo na mpango wa dhabihu ya ukombozi.—Rum. 6:4, 5; Kol. 2:12, 20; 1 Yohana 2:1, 2.
Hata hivyo, wao, wakiwa washiriki wa wale “kondoo wengine,” wamekusanywa pamoja na yule Mchungaji Mwema Yesu Kristo, nao wanafanyiza “kundi moja” wakiwa pamoja na mabaki wa kondoo hao wa kiroho ambao wamo katika “zizi hili” ambalo Yesu alisema juu yake katika Yohana 10:16. Wanafahamu kwamba wokovu wao na kuingizwa kwenye uzima wa milele juu ya Paradiso ya kidunia iliyoahidiwa kunatokana na Mungu kupitia Mchungaji Mwema wake, ambaye sasa wanakuwa kundi lake. Basi, wanawezaje wakati wo wote kupuza kutoa heshima zao kwa Kristo kwa kutokuwapo na kutokusherehekea chakula cha jioni alichokianzisha ili kuadhimisha kifo chake, ambacho kupitia kwacho wokovu huu wa rehema unapatikana? Kwa kufaa hawawezi kufanya hivyo! Hawataki kufanya hivyo. Maadamu mwadhimisho huo unaendelezwa duniani na mabaki ya warithi wa ufalme wa kimbinguni wa Mungu, wanatambua kwamba wana wajibu wa kuhudhuria Chakula cha Jioni cha Bwana wakiwa watazamaji. Hata ingawa katika sehemu nyingi huenda kusiwe ye yote wa mabaki apate kushiriki kula mifano hiyo, Mashahidi wa Yehova wanataka kupangia mwadhimisho huo kwa sababu ya kuheshimu sana yale ambayo unafananisha na kutoa nafasi kwa ye yote anayehudhuria, ambaye huenda akawa mmoja wa mabaki, ashiriki kula mifano hiyo.
Mwaka huu Chakula cha Jioni cha Bwana kitasherehekewa na Mashahidi wa Yehova baada ya jua kutua Aprili 8, 1982. Watu wote wanaotaka kuhudhuria ili kukikumbuka kifo cha Mwana-kondoo wa Mungu, Yesu Kristo, wanapaswa kupasha habari kundi la Mashahidi wa Yehova la mahali pao.
[Maelezo ya Chini]
a Tazama The Watchtower, Aprili 15, 1936, ukur. 123, maf. 44, 46.