Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 10/15 kur. 12-18
  • Uwe na Imani Katika Ule Ufalme!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uwe na Imani Katika Ule Ufalme!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MANENO YA DANIELI YA KUONYA
  • HISTORIA YATHIBITISHA ONYO LA DANIELI
  • ILE ‘PEMBE NDOGO’ YATOKEA
  • TUKO WAPI KATIKA MKONDO WA WAKATI?
  • Jitu la Kiunabii—Anguko Lalo Litamaanisha Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Serikali za Wanadamu Zapondwa na Ufalme wa Mungu.
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Kuinuka na Kuanguka Kwa Sanamu Kubwa Sana
    Sikiliza Unabii wa Danieli!
  • Sikiliza Neno la Mungu la Kiunabii kwa Wakati Wetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 10/15 kur. 12-18

Uwe na Imani Katika Ule Ufalme!

“Lakini, ndugu, kwa habari ya nyakati na majira, hamna haja niwaandikie. Maana ninyi wenyewe mnajua yakini ya kuwa siku ya Bwana yaja kama vile mwivi ajavyo usiku.”​—1 Wathesalonike 5:1, 2.

1, 2. Yehova ameendeleaje kumtumia Yesu Kristo aliyefufuliwa?

AKIWA ndiye “Neno,” au Logos, Yesu Kristo alitumiwa sana na Baba yetu wa kimbinguni. (Yohana 1:1-3; Kol. 1:16) Lakini Yehova Mungu aliendelea kumtumia Yesu hata baada ya kufa na kufufuliwa kwake. Jambo hilo linakaziwa vizuri na maelezo yenye kuelimisha ya mtume Paulo.

2 Mtume huyo alitangaza wazi kwamba Mungu amekusudia kufanya vitu vyote katika mbingu na juu ya dunia vipatane naye, akifanya hivyo kupitia damu ya Yesu Kristo iliyomwagwa. (Kol. 1:19, 20) Hilo linapatana na maneno ya Paulo yenye kusema kwamba Yehova amepanga ‘vikusanywe pamoja tena katika Kristo vitu vyote katika mbingu na juu ya dunia.’ (Efe. 1:10, NW; Flp. 2:9-11) Lakini matukio yenye kufikia upeo katika habari hii yangehusu pia kusimamishwa kwa ufalme wa Mungu wa Kimasihi na kuja kwa ‘siku ya Yehova’ kwa njia yenye kutazamisha. (1 The. 5:1, 2) Maandiko yanaonyesha wazi kwa wingi daraka la Kristo tangu kupaa kwake mbinguni miaka zaidi ya 1,900 iliyopita. Inatufaa tukaze sana sana fikira zetu kwenye cheo chake cha maana sana katika mpango wa Yehova.

3. Kwa sababu gani Yesu alikuwa na habari juu ya maneno ya kiunabii yaliyonenwa juu ya serikali ya Ufalme?

3 Kwa sababu ya daraka lake la kuwa Logos, au “Neno,” kabla ya kuja duniani, Yesu aliyajua sana maneno ya kiunabii yaliyohusu serikali ya ule Ufalme. Kwa hiyo, akiwa mwanadamu, Yesu alimkaribisha msomaji atumie ufahamu anapoyatafakari maneno ya Danieli juu ya “wakati wa mwisho.” (Dan. 12:4; Mt. 24:15-22) Basi, acheni tugeukie kitabu cha Danieli tuangalie mambo fulani ambayo bila shaka Yesu aliyafahamu akiwa ndiye Logos, au “Neno.” Kwa maana inaelekea Yeye ndiye aliyetumiwa na Baba yetu wa kimbinguni kuwafanya manabii wa zamani za kale waandike walivyoandika.

4. Kwa habari ya serikali ya Ufalme, tunaambiwa nini katika Danieli 2:44; 7:13, 14 na 12:1?

4 Tunapotazama ndani ya kitabu cha Danieli kwa jicho lenye ufahamu, tunaona semi tatu hasa zenye kupendeza. Wa kwanza unapatikana katika Danieli 2:44:

“Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele [kwa nyakati zisizojulikana, NW].”‏

Usemi unaohusiana na huo unapatikana katika Danieli 7:13, 14, nao unasema:

“Nikaona katika njozi za usiku, na tazama, mmoja aliye mfano wa mwanadamu akaja pamoja na mawingu ya mbingu akamkaribia huyo mzee wa siku, wakamleta karibu naye. Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ambayo haitapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa.”

Mwisho, Danieli 12:1 inasema hivi:

“Wakati huo Mikaeli atasimama, jemadari mkuu, asimamaye upande wa wana wa watu wako; na kutakuwa na wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo.”

Hapa, katika vifungu vitatu vya maneno ya unabii wake, Danieli anataja kusimamishwa kwa serikali ya ule Ufalme, si mikononi mwa mtu mwingine ila mwa ‘mwanadamu,’ au Mikaeli. Semi hizi kwa wazi zinamtaja Kristo Yesu katika mamlaka ya Ufalme.​—Ufu. 12:7-10.

5. Je! ni jambo la ki-Maandiko kufikiria wakati kuhusiana na kuchukua mamlaka kwa serikali ya Ufalme?

5 Utaona kwamba katika semi zilizotangulia za Paulo na Danieli wakati unatajwa wa kutokea na kuchukua mamlaka kwa serikali ya kimbinguni. Ikiwa sisi tunaweka fikira zetu juu ya wakati wenyewe, basi 1 Wathesalonike 5:1 inatuhusu sisi kikweli inaposema:

“Lakini, ndugu, kwa habari ya nyakati na majira, hamna haja niwaandikie.”

Kama tunaifahamu kwa ukamili maana ya Neno la Mungu, hasa tunapozidi kuingia sana katika “wakati wa mwisho,” hatutapatikana kwa ghafula bila kuwa tayari. Kwa uhakika tutakuwa watu wa ufahamu kuhusu matukio yanayohusu wakati wa “mwisho wa taratibu ya mambo.” (Mt. 24:3, NW) Basi, acheni tuzungumze hali zenye kuzizunguka semi zile tatu zilizosemwa na Danieli kuhusiana na kusimamishwa kwa serikali ya ule Ufalme.

MANENO YA DANIELI YA KUONYA

6. Katika Danieli 2:40, ni maneno gani yanayosemwa juu ya “ufalme wa nne”?

6 Wengi wetu tunafahamu sana ile sanamu ya ndoto inayosimuliwa katika Danieli sura ya pili, nasi tunajua kwamba kwa msaada wa roho takatifu ya Yehova nabii huyo alimwambia Mfalme Nebukadreza maana ya sanamu hiyo. Ilifananisha mfuatano wa falme za ulimwengu, kuanza na Babiloni. Sisi tunapendezwa hasa na ule “ufalme wa nne,” ambao juu yake Danieli alisema:

“Na ufalme wa nne utakuwa na nguvu mfano wa chuma; kwa maana chuma huvunja vitu vyote na kuvishinda; na kama chuma kisetavyo vitu hivi vyote, ndivyo utakavyovunja-vunja na kuseta [hata zote hizi, NW].”‏—Dan. 2:40.

7. Huu “ufalme wa nne” ni nini?

7 Ufalme huu wenye mfano wa chuma unakuwa upi? Katika historia ya Biblia, “ufalme wa nne;” au mamlaka ya ulimwengu, tukihesabu chini kuanzia Babeli, ndio Milki ya Kirumi, katikati yake ukiwako mwungano wa Umedi na Uajemi na Milki ya Ugiriki. Baada ya muda fulani Milki ya Kirumi iligawanywa sehemu mbili kwa makusudi ya kuwa na usimamizi bora, kukawako milki ya mashariki na milki ya magharibi. Milki ya Waingereza ilikua kutokana na milki hiyo ya magharibi. Kwa sababu ya mapinduzi ya makoloni ya Waamerika, United States ya Amerika ilianzishwa. Kwa sababu kubwa za msingi nchi mbili hizi ziliona inafaa kushirikiana pamoja kijeshi na kwa njia nyingine ili kufanyiza Mamlaka ya Ulimwengu ya Waingereza na Waamerika.

8, 9. Kuna ufanani gani mbalimbali kati ya Danieli 2:40 na Danieli 7:7

8 Walakini, kwa habari ya huo “ufalme wa nne”​—katika kujulikana kwake kwa asili kama Milki ya Kirumi—Danieli anatuambia hivi katika mwingine wa unabii wake:

“Baadaye nikaona katika njozi ya usiku, na tazama, mnyama wa nne, mwenye kutisha, mwenye nguvu, mwenye uwezo mwingi, naye alikuwa na meno ya chuma, makubwa sana; alikula na kuvunja vipande vipande, na kuyakanyaga mabaki kwa miguu yake; na umbo lake lilikuwa mbali kabisa na wale wa kwanza, naye alikuwa na pembe [kumi, NW].”​—Dan. 7:7.

9 Katika kuchunguza Danieli sura ya saba, itaonwa kwamba nabii huyo anazipanga falme zile zile nne, au mamlaka za ulimwengu, kama zile zilizoonyeshwa katika sura ya pili. Lakini badala ya kuzieleza mamlaka hizo kama sehemu za sanamu, kuanza na kichwa cha dhahabu, yeye anazieleza kuwa wanyama. Katika sura ya saba, anaanza na simba (Babiloni) na kumaliza na yule mnyama wa nne mwenye nguvu zisizo za kawaida mwenye meno ya chuma. Basi, Danieli 7:7 inalingana sana na Danieli 2:40 kwa sababu zilikusudiwa zilingane. Katika maandiko yote haya mawili, ni wazi kwamba kusaga (kuseta), kuvunja-vunja na nguvu za kutisha zenye mfano wa chuma zinashirikishwa na huu ufalme wa Rumi. Lakini ulizo linabaki: Ni kwa njia gani huu “ufalme wa nne” unapata kufananisha mamlaka za ulimwengu mbili?

10. Ile ‘pembe ndogo’ ina chanzo gani?

10 Acheni tuendelee kusoma, katika Danieli 7:8:

“Nikaziangalia sana pembe zake, na tazama, pembe nyingine ikazuka kati yao, nayo ilikuwa ndogo, ambayo mbele yake pembe tatu katika zile za kwanza zikang’olewa kabisa; na tazama, katika pembe hiyo mlikuwa na macho kama macho ya mwanadamu, na kinywa kilichokuwa kikinena maneno makuu.”

Ajabu namna gani! Huu ufalme wa nne, Mamlaka ya Ulimwengu ya Kirumi, unaanza kukuza pembe nyingine kwenye kichwa chake cha mfano kilicho kama cha mnyama. Kisha tatu kati ya zile pembe zilizokuwapo zinang’olewa ili nafasi ipatikane pembe hii nyingine iote. Yote haya yana maana gani? Acheni tuyatazame mambo ya hakika ya historia.

HISTORIA YATHIBITISHA ONYO LA DANIELI

11. Kwa sababu gani ni jambo la faida kuona jinsi Milki ya Rumi ilivyotimiza kirefu matukio yanayoelezwa na Danieli?

11 Kwa kweli sisi ‘hatuna haja ya kuandikiwa habari zaidi’ kwa sababu tayari zote zimekwisha kuandikwa katika Neno la Mungu lenye roho Yake. Tena, ikiwa sisi ni wenye macho ya kiroho yenye kuona vizuri kikweli, matukio yanayotukia katika ulimwengu mzima hayatatupata kwa ghafula kama vile mwivi anavyoweza kuwashtukia watu wasiojua neno. Lakini tunahitaji kujua habari za kutosha ki-Maandiko, na ni jambo lenye faida kuangalia jinsi Milki ya Kirumi ilivyoyatimiza kirefu matukio yanayoelezwa katika njozi za Danieli za kiunabii.

12. Usimamizi wa Rumi ulivihusu Visiwa vya Uingereza kwa kadiri gani?

12 Tangu mwanzo wake, Rumi ilikuwa sana mamlaka ya kijeshi, nayo ilipanua maongozi yake na usimamizi wake kwa mapana na marefu. Ikiwa chini ya maongozi hasa ya ufalme wa kikabila wakati huo, Uingereza ilipata kuwa sehemu ya Milki ya Kirumi, na katika sehemu zote za Visiwa vya Uingereza kuna ushuhuda mwingi wa kuonyesha ilitawalwa namna hiyo. Ushuhuda huo unatia ndani ule ukuta ambao Hadrian Mwenye Milki alijenga kupita kati ya sehemu yote ya kaskazini ya Uingereza.

13, 14. (a) Hapo kwanza, uwezo wa Rumi ulikuwa wa aina gani? (b) Lakini kulitokea nini katika karne za tatu na nne?

13 Rumi ilipozidi kuwa na utajiri na kuendelea kuwa na hali yenye kushuka kwa sababu ya umalaya wa jamii yenye kutawala, uwezo wake wa kijeshi ulitokomea. Kufika wakati wa Nero na viongozi wenye milki waliofuatana, ilikuwa wazi kwamba nguvu za kijeshi za Rumi zilikuwa zimepungua sana. Lakini wenye kutaka kuiendeleza milki hiyo walitunga mpango wa kuiendeleza iwe sehemu kuu yenye kuongoza mambo ya ulimwengu muda wa karne nyingi ambazo zingefuata, hata ingawa haingeendelea kuwa mamlaka ya kijeshi. Walifanyaje hivyo?

14 Tukija ndani ya karne ya tatu na ya nne W.K., inaonekana kwamba Rumi ilipata sana kuwa mamlaka yenye mwungano wa dini na siasa, zaidi ya kuwa mamlaka ya kijeshi. Kwa akili nyingi, mpango ulitungwa kwa hila hivi kwamba mamlaka ya kipapa katika Rumi iliweza kuendelea kwa mapana na marefu kusimamia sehemu kubwa ya dunia yenye watu iliyojulikana wakati huo. Mpango huo ulijulikana kama mpango wa kutumikishwa kwa vibaraka na mabwana wakubwa katika ardhi yao, nao uliisaidia Milki Takatifu ya Rumi kuamrisha ki-nguvu mwendo wa mambo ya ulimwengu kwa muda usiopungua miaka 1,000, Rumi yenye Mapapa ikiwa ndiyo sehemu kubwa yenye maongozi.

15. Usimamizi wa kipapa ulidumishaje uongozi kwa mamia kadha ya miaka?

15 Chini ya mpango huo wa vibaraka kutumikishwa na mabwana wakubwa, wingi mkubwa wa watu walijitafutia chakula cha shida wakiwa wakulima hohehahe wasiojua la kufanya. Kutokana na vitonge-tonge vya riziki yao, walitakwa wawasaidie mabwana wavivu wa majumba ya ki-ukubwa katika Ulaya yote, kutia na Visiwa vya Uingereza. Halafu, mabwana hao wenye kutumikisha watu katika mashamba yao walilazimika kumlipa ushuru au kodi mfalme ambaye walikaa katika sehemu ya usimamizi wake. Kisha kila mmoja wa wafalme hao, awe alikuwa katika Uingereza, Sakzoni au sehemu nyingine za Ulaya, alikuwa kama kibaraka tu na alitakwa kulipa deni zake au ushuru wake kwenye usimamizi wa kipapa uliokuwa Rumi. Kwa hiyo, usimamizi wa kipapa ulipata utajiri wa mali na mamlaka pia wakati wa kipindi chote hicho kirefu ambacho mara nyingi kinaitwa Zamani Zenye Ujinga.

16. (a) Milki Takatifu ya Rumi inaelezwaje kwa njia nzuri na Danieli? (b) Ni nini kinachoonekana kikiota (kikimea) kwenye kichwa cha yule “mnyama wa nne,” Rumi?

16 Kwa kulinganishwa na hali hizo zilizokuwako wakati huo, maelezo ya kiunabii ya Danieli ya ufalme uliofananishwa na miguu ya chuma ya ile “sanamu kubwa sana” yanaelekea kufaa sana. (Dan. 2:31) Tena yanamfaa sana yule mnyama wa kutisha, mwenye meno ya chuma, mwenye kuvunja-vunja na kula anayeonyeshwa katika Danieli sura ya saba! Kwanza, mnyama huyo alikwenda mbio kwa fujo nyingi katika Ulaya yote, akitiisha kila kitu kilichokuwa njiani pake kwa kutumia nguvu za kijeshi. Halafu akaudumisha na kuzidi kuuimarisha uwezo wake kwa kutumia shughuli na hila ya kisiasa, ya kidini na ya kibiashara. Lakini namna gani ile sehemu iliyoota na kutokeza, hii ‘pembe ndogo,’ ambayo inaonekana ikimea kwenye kichwa cha yule “mnyama wa nne” mwenye kutisha anayefananisha Rumi? Jambo hilo linatokea wakati gani?

ILE ‘PEMBE NDOGO’ YATOKEA

17. Ukuzi wa ile ‘pembe ndogo’ ulianzaje?

17 Mpaka mwaka wa 1533 W.K., ufalme wa Uingereza uliendelea kutumikishwa na usimamizi wa kipapa ukiwa kama kibaraka. Walakini, mwaka uliofuata Mfalme Henri wa Nane akawa ndiye mkuu mwenye mamlaka zaidi wa Kanisa Katoliki la Uingereza. Yeye alikata uhusiano na Rumi, nao pia wakakata uhusiano wao naye. Sasa utajiri wa Visiwa vya Uingereza, ambao sehemu yake kubwa ilikuwa hapo kwanza imevutwa na mrija wa Kanisa Katoliki la Rumi, ilikuwa inakusanywa kwa wingi chini ya uongozi wa mfalme wa Uingereza mwenye kusimamia Kanisa Katoliki la Uingereza. (Kanisa Katoliki la Uingereza liliendelea kuwa na mwundo ule ule kama Kanisa Katoliki la Rumi, na kwa kiasi kikubwa ndivyo lilivyo hata leo hii.) Uwezo wa Milki Takatifu ya Rumi ulikuwa unaanza kufifia, lakini ‘pembe ndogo’ ilikuwa inaota (inamea) kutokana nayo.

18. Uingereza ilikuwa katika hali gani wakati wa Malkia Elizabeti wa Kwanza, na jambo hilo lilimaanisha nini kwa Ufaransa, Netherlands na Spania?

18 Miongo michache ya miaka inapita, nayo Uingereza inajikuta chini ya utawala wa Malkia Elizabeti wa Kwanza. Kufika wakati huu utajiri mwingi wa ule mpango wa kutumikishwa kwa vibaraka na wakubwa wao ndani ya Visiwa vya Uingereza unapata matokeo. Kumetokea kikosi cha meli za vita zenye nguvu za kutosha. Baada ya kitambo kidogo, chini ya uongozi wa wanaume mashuhuri kama Drake, Raleigh, na Hawkins, kikosi hicho cha Uingereza kinaonyesha nguvu zake katika kupigana na vikosi vyenye nguvu vya meli za Spania, Netherlands na Ufaransa (zote hizo zikiwa bado chini ya usimamizi wa kidini wa Rumi), na kuvishinda vyote, hata kile kikosi cha meli ziitwazo Armada ya Spania. Basi, Uingereza yaitawala bahari na kujigamba.

19. Kwa kuweka kando kando sura za pili na saba za Danieli, ni kuhusu nini sasa tunaona utimizo mkubwa?

19 Danieli 7:8 inasema nini? Naam, kwamba “pembe” tatu zingeng’olewa mbele ya ile yenye kumea, ile ‘pembe ndogo,’ na kwamba ingenena “maneno makuu.” Basi hapa, Mamlaka ya Ulimwengu ya Waingereza ikiwa imetokea, na baadaye kuungwa mkono na Amerika, tunapata utimizo kamili wa unabii huu mkubwa. Mamlaka ya Ulimwengu ya Mwungano wa Waingereza na Waamerika ni sehemu iliyomea kutokana na Milki ya Rumi. Ni “kitoto-kizaliwa” cha Rumi. Kwa hiyo, kwa njia ya unabii inaonyeshwa kama ikimea kwenye “kichwa” cha Rumi, yule “mnyama wa nne” mwenye meno ya chuma. Kwa kuziweka kando kando sura za pili na saba za Danieli, ni vyepesi kuona jinsi ‘miguu ya chuma’ inavyofananisha mamlaka mbili za ulimwengu zenye kufuatana, wala si moja tu.​—Dan. 2:32, 33.

TUKO WAPI KATIKA MKONDO WA WAKATI?

20. Tunaweza kufuatishaje usitawi wa ile ‘miguu ya chuma’ mpaka ndani ya karne yetu ya 20?

20 Kulingana na Danieli 2:41-43, tunaona kwamba falme za ulimwengu zenye kutambulika waziwazi zingepita. Basi, je! kila mmoja wa ile ‘miguu ya chuma’ miwili unafananisha mamlaka ya ulimwengu iliyo tofauti na ile nyingine? La, sivyo, kwa maana hata ile ‘mikono ya fedha’ miwili katika sehemu ya juu ya sanamu haifananishi mamlaka mbili za ulimwengu katika siku zenye ufanisi za mwungano wa Umedi na Uajemi. Hiyo miguu miwili na kile chuma cha miguu vinakua pamoja kutoka kwenye Milki ya Rumi, na hasa kuanzia karne ya nne, wakati Konstantino anapouacha mji mkuu wake wa magharibi, Rumi, akaanze mji mkuu wa mashariki katika Konstantinopo. Kutokana na milki hii yenye kugawanyika yanatokea mataifa mbalimbali yenye kujitegemea, na mwishowe Mamlaka ya Ulimwengu ya Mwungano wa Waingereza na Waamerika ndiyo inayopata nguvu za kutawala. Wakati wa vile vita viwili vya ulimwengu vya karne yetu, “miguu” hiyo ilipata kuwa kama “chuma” kweli kweli kwa maana majeshi yenye nguvu ya Mamlaka ya Ulimwengu ya Mwungano wa Waingereza na Waamerika yalivunja-vunja majeshi mapinzani na kutumia silaha za nuklea vitani kwa mara ya kwanza.

21. Ni udhaifu gani unaotokea mwishowe kwenye mwisho wa ile sanamu?

21 Haya, tunashuka kwenye sehemu ya mwisho kabisa ya hii sanamu kubwa sana. Bado sehemu hiyo ya mwisho inafananisha Mamlaka ya Ulimwengu ya Mwungano wa Waingereza na Waamerika. Lakini sasa ina udhaifu. Nyayo na vidole vyake vimepoteza zile nguvu kamili za miguu zenye mfano wa chuma. Kwa maana vimefanyizwa kwa “nusu chuma na nusu udongo” wa kufinyangwa. Danieli analifasiri jambo hili, akisema:

“Na kama vile ulivyokiona kile chuma kimechanganyika na udongo wa matope, watajichanganya nafsi zao kwa mbegu za wanadamu; lakini hawatashikamana, kama vile chuma kisivyoshikamana na udongo.”​—Dan. 2:33, 43.

22. (a) Kwa sababu gani watawala wa ujamaa na ukomunisti hawahusiki hapa? (b) Basi, “mbegu za wanadamu” ni nani? (c) Kumetokea nini kwa habari ya kile “chuma” na ule “udongo”?

22 Je! hiyo maana yake ni kwamba watawala wa ki-siku-hizi wa ujamaa na ukomunisti wanakuwa mamlaka ya ulimwengu? Sivyo, kwa maana unabii wa Biblia unaonyesha kwamba sehemu hizo za kisiasa zenye kupendwa na watu wengi hazitatokeza kamwe zitawale ulimwengu. Wakati sehemu ya mwisho ya ile sanamu ya kutisha ifikiapo mwisho baada ya wakati kupita, bado inakuwa ya chuma katika sehemu yake kubwa. Bado ndiyo mamlaka ya ulimwengu iliyomea kutokana na Milki Takatifu ya Rumi. Lakini uwezo huo wenye mfano wa chuma unadhoofishwa mwishoni mwa kizazi kwa kuingiliwa na kitu chororo kama udongo—utendaji wenye kuwaomba watu wawe na sauti kubwa zaidi katika mambo, kama kupitia miungano ya kibiashara, matendo ya kugomea mambo na kadhalika. “Mbegu za wanadamu,” wale waitwao kina yahe, wanajaribu kutoa maoni yao juu ya vile mambo yanavyoendeshwa. Tunaona hivyo leo, si katika zile nchi za magharibi za Ulaya tu ambazo wakati mmoja zilikuwa sehemu ya Milki Takatifu ya Rumi, bali sana-sana katika makao ya Mamlaka ya Mwungano wa Waingereza na Waamerika. Katika sehemu hizo matendo ya kufanya kazi kivivu, kufanya migomo na fujo za ki-kazi yamedhoofisha sana mamlaka ya kiserikali ambayo wakati mmoja ilikuwa kama “chuma.” Wafanya kazi wanapopambana na wenye kutunza uchumi, hao “mbegu za wanadamu” wanajaribu kuamuru jinsi watakavyofanya kazi na kuishi. Je! kufanya hivyo kumeleta uthabiti kati ya wenye kufanya kazi na serikali? Neno la Mungu linasema hivi kwa maneno machache: “Lakini hawatashikamana.”

23. (a) Ina maana gani kwamba sasa tumevifikia “vidole” vya nyayo za ile sanamu? (b) Tunaweza kutazamia nini halafu? (c) Kwenye huu “wakati wa mwisho,” inatupasa tujisikie tukisukumwa kufanya nini?

23 Basi, tuko wapi katika mkondo wa wakati? Kwenye mwisho wa mstari wa 43 “sanamu” haipo tena. Tumeshuka kwenye “vidole” vyenyewe vya nyayo! Sisi tunaishi katika wakati huo ambapo usitawi wa serikali yenye kufanyizwa na mwanadamu unafikia mwisho wake wenye masikitisho. Upeo wa nyakati umetufikia! Danieli ametuambia jambo la kutazamia. Naam, ufalme wa Kristo utakaotawala makundi yote ya watu, yaani lile “jiwe” lililokatwa kwenye “mlima” wa enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu wote, u karibu kujivurumisha kwenye nyayo za ile sanamu ya kutisha, iibwage chini na kulibomoa kabisa umbo lote la utawala wa mwanadamu wenye uonezi. Huo ndio utakaokuwa “wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo.” Lakini wakati huo utafuatwa upesi sana na kipindi kilicho cha ajabu kuliko vipindi vyote vya historia ya kibinadamu, utawala wa Kristo wa miaka 1,000. Je! Mkristo ye yote wa kweli anaweza kukaa kwa ubaridi-ubaridi akiyatazama matukio ya huu “wakati wa mwisho” kwa utulivu tu, bila ya kujisikia akisukumwa kuiunga mkono serikali ya ule Ufalme? Huu ndio wakati wa kuonyesha tuko upande wa nani, wa Yehova au wa Shetani!—Dan. 2:44, 45; 7:14; 12:1, 4.

24. Sisi tutaendelea kuwa watu wa aina gani, na kwa sababu gani?

24 Kama isemavyo 1 Wathesalonike 5:1, hatuhitaji kuandikiwa lo lote kuzihusu nyakati na majira! Yote yameandikwa ndani ya Neno la Mungu. Tunalotakwa kufanya ni ‘kuyachimbua’ mambo hayo. Kwa hiyo acheni tufanye kama Waebrania 10:35-39 inavyodokeza: “Basi msiutupe ujasiri wenu [wa kunena, NW], kwa maana una thawabu kuu. Maana mnahitaji saburi, ili kwamba mkiisha kuyafanya mapenzi ya Mungu mpate [utimizo wa, NW] ile ahadi. Kwa kuwa bado kitambo kidogo sana, Yeye ajaye atakuja, wala hatakawia. Lakini mwenye haki wangu ataishi kwa imani; naye akisita-sita, [nafsi] yangu haina furaha naye. Lakini sisi hatumo miongoni mwao wasitao na kupotea, bali tumo miongoni mwa hao walio na imani ya kutuokoa [nafsi] zetu.” Acheni tuwe na imani yenye kudumu katika ule Ufalme, yenye kutusukuma tuchukue hatua! —Kutoka The Watchtower, May 15, 1981.

[Chati/Picha katika ukurasa wa 17]

ISHARA ZA MIFANO KATIKA UNABII WA DANIELI WA UFALME

Ile sanamu kubwa sana

(Danieli 2:31-45)

Wale wanyama wakubwa sana wanne

(Danieli 7:2-22)

BABILONIA

Kuanzia 625 K.W.K.

UMEDI-UAJEMI

Kuanzia 539 K.W.K.

UGIRIKI

Kuanzia 331 K.W.K.

RUMI

Kuanzia 30 K.W.K.

UINGEREZA NA AMERIKA

Kuanzia 1763 W.K.

VIKUNDI VINAVYOTAKA MABADILIKO MAKUBWA VIPENDWAVYO NA WATU WENGI

Ile pembe ndogo yatokea

(Danieli 7:8)

Konstantino Mwenye Milki (312-337 W.K.) aanzisha mji mkuu wa mashariki, zaidi ya kuwa na Rumi ambao kutoka huo Mamlaka ya Mwungano wa Waingereza na Waamerika yapanda

Henri wa Nane akata uhusiano na Rumi (1534 W.K.)

Kuanzia wakati wa Elizabeti wa Kwanza (1558-1603 W.K.), Uingereza yachukua hatua ya ‘kuzing’oa zile pembe tatu’ za Spania, Netherlands na mwishowe Ufaransa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki