Serikali za Wanadamu Zapondwa na Ufalme wa Mungu.
CHINI YA Mfalme Nebukadreza mwenye nguvu nyingi, Babeli ilifikia cheo cha kuwa Mamlaka ya Tatu ya Ulimwengu ya unabii wa Biblia. Serikali zote za Mashariki ya Kati ya kale zilizoipinga ziliangushwa na majeshi yake yenye nguvu nyingi. Hata serikali ya Yehova ya kitheokrasi ya mfano ya wakati huo iliruhusiwa na Mungu iharibiwe kwa sababu ya kutokuaminika kwa Waisraeli. Walakini, akilini mwake Nebukadreza, kuangushwa kwa Yerusalemu na kuharibiwa kwa hekalu lake la ibada ya kweli kulimfanya yeye na mungu wake Marduki kuwa wenye nguvu kuliko Yehova Mungu wa Waebrania pamoja na wafalme wao wa ukoo wa Daudi.
Kwa kuja kuuharibu mji mkuu wa Yerusalemu, Nebukadreza alionyesha nia iliyotabiriwa kwamba ingeonyeshwa na ufalme wa Babeli. Tunasoma hivi: “Nitapanda mpaka mbinguni, nitakiinua kiti changu [cha enzi] juu kuliko nyota za Mungu; nami nitaketi juu ya mlima wa mkutano [mahali ambapo Waisraeli walipofanyia ibada yao katika hekalu juu ya Mlima Sayuni] . . . Nitapaa kupita vimo vya mawingu, nitafanana na yeye Aliye juu.”—Isa. 14:13, 14.
Unabii huo uliendelea ukatabiri kwamba nasaba ya kifalme ya Babeli ‘ingeshushwa mpaka sheol (kuzimu), katika pande za mwisho za shimo.’ (Isa. 14:15) Makumi ya miaka kabla ya kuangushwa kwa nasaba ya kifalme ya Nebukadreza, Yehova alitweza mtawala huyu mwenye kiburi kwa kuruhusu apatwe na ugonjwa wa akili. Kwa muda wa miaka saba Nebukadreza alijidhania kuwa ng’ombe dume, akaenda huku na huku akila majani.
Nebukadreza uyu huyu ndiye ambaye hapo mbeleni alikuwa amepata ndoto ya sanamu na yenye “kutisha” ya unabii. Madini mbalimbali katika sanamu hii yalifananisha mfuatano wa serikali za ulimwengu ambazo zingesimama duniani kwa muda wa karne nyingi, na kufuatwa na enzi kuu ya Mungu iliyosimamishwa tena duniani kwa njia ya utawala wa ufalme wa Mwanawe, Kristo Yesu.
Baada ya kusahau ndoto hiyo alipoamka, Nebukadreza aliwaita wachawi na wanajimu wake wamwambie, si ile ndoto tu, bali hata na maana ya ndoto hiyo. Walishindwa kabisa. Lakini, Danieli akamwambia: “Yuko Mungu mbinguni afunuaye siri, naye amemjulisha mfalme Nebukadreza mambo yatakayokuwa siku za mwisho.”—Dan. 2:28.
Kabla ya kutoa maana, Danieli alimkumbusha Nebukadreza ndoto yake: “Kichwa chake kilikuwa ni cha dhahabu safi; kifua chake na mikono yake ni ya fedha; tumbo lake na viuno vyake ni vya shaba; miguu yake ni ya chuma na nyayo za miguu yake nusu ya chuma na nusu ya udongo.” (Dan. 2:32, 33) Ndoto hiyo ilikuwa na maana gani? Danieli alieleza kwamba Nebukadreza na nasaba yake ya kifalme wangekuwa wa kwanza katika mfululizo wa mamlaka za ulimwengu, akisema, “Wewe u kichwa kile cha dhahabu.” Kisha akaongeza: “Na baada ya zamani zako utainuka ufalme mwingine, mdogo kuliko wewe; na ufalme mwingine wa tatu wa shaba, utakaoitawala dunia yote. Na ufalme wa nne utakuwa na nguvu mfano wa chuma; kwa maana chuma huvunja vitu vyote na kuvishinda; na kama chuma kisetavyo vitu hivi vyote, ndivyo utakavyovunja-vunja na kuseta.”—Dan. 2:38-40.
Lakini namna gani juu ya miguu ya chuma na udongo? “Na kama vile ulivyoziona hizo nyayo za miguu na vidole vyake, kuwa nusu udongo wa mfinyazi, na nusu chuma, ufalme ule utakuwa umegawanyika . . . utakuwa nusu yake una nguvu, na nusu yake umevunjika.” Ni jambo gani litakalosababisha kuvunjika-vunjika huku katika “ufalme” ulio kama chuma au serikali ya ulimwengu uliofananishwa na nyayo na vidole vya miguu? “Na kama vile ulivyokiona kile chuma kimechanganyika na udongo wa matope, [wale washiriki wa “ufalme wa nne”] watajichanganya nafsi zao kwa mbegu za wanadamu; lakini [wale wanaofananishwa na chuma na udongo wa matope] hawatashikamana kama vile chuma kisivyoshikamana na udongo.”—Dan. 2:41-43.
Tukifuatisha mfululizo huu wa mamlaka za ulimwengu kupitia kwa ile sanamu, kuanzia na kichwa mpaka kwa nyayo katika muda wa wakati, twaona kwamba zilianza na Babeli, na kuendelea kupitia kwa Umedi na Uajemi, Ugiriki na Rumi. Ule “ufalme wa nne,” uliofananishwa na miguu na nyayo, ulianza na milki ya Kirumi. Wakati ulipoendelea, nguvu za milki hii zilipunguka na Milki ya Uingereza ikainuka, ikiwa kwa kweli imetokana na Milki ya Kirumi. Hii ilikuwa hivyo ijapokuwa kulikuwako kushindania mamlaka ya ulimwengu pamoja na mabaki ya Milki ya Kirumi. (Dan. 7:19, 20) Inaelekea kwamba hakuna maana yo yote ya kiunabii ya sanamu hii kuwa na vidole kumi vya mguu. Hili ni jambo la kawaida katika wanadamu, kama vile hii sanamu ilivyokuwa na mikono miwili, miguu miwili na kadhalika.
Milki ya Uingereza ilisitawi ikawa ufalme wenye kutawalwa na nasaba ya kifalme nayo iliendelea kuonyesha tabia kama za chuma za Milki ya Kirumi ya kale. Na ijapokuwa koloni 13 za Amerika ziliasi Milki ya Uingereza, serikali ya United States of America imekuwa sehemu ya utawala wa mfano wa chuma, nayo mamlaka hii imeshirikiana sana na serikali ya Uingereza katika mambo ya ulimwengu. Hivyo tukifuatisha mfululizo wa mamlaka ya ulimwengu kupitia kwa sehemu ile kufikia kwa nyayo na vidole vyake, twaona namna ilivyo lazima kwamba Mamlaka ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika yatiwa ndani ya kile “chuma.” Hata katika wakati wa mwisho ulioendelea sana, ingali ndiyo Mamlaka ya Ulimwengu, hata ingekuwa kumetokea washindani wengi wenye nguvu.
Kuhusiana na ile sanamu ya ndoto, hakukutajwa kwamba ‘ufalme wa tano’ ulitokea, hata ingawa njozi nyingine ya Danieli ya baadaye ilionyesha “mnyama wa nne” mwenye kuogopesha akifananisha Milki ya Kirumi ambayo kutoka kwake ilitokea “pembe ndogo” ambayo ilikua ikawa kubwa sana ikifananisha Milki ya Uingereza. (Dan. 7:7, 8, 19-26; 8:9-11, 23-25) Ili zifikie nguvu za utawala, Milki za Rumi na Uingereza na Amerika zilikuwa kwa kweli kama chuma kwa ‘kuvunja-vunja na kuseta’ falme nyingine pamoja na watu.
Ni kweli, katika karne ya 19 na ya 20 kumekuwako matukio fulani katika mambo ya ulimwengu ambayo yamedhoofisha utawala wa mfano wa chuma wa Mamlaka ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika. Vikundi vya kijamii vyenye kutaka mabadiliko vimetokea navyo vimedhoofisha mwundo, maongozi na nguvu za hii Mamlaka ya Saba ya Ulimwengu. Ilisemekana kwamba “ufalme ule utakuwa ufalme uliogawanyika . . . kama vile ulivyoona kile chuma kimechanganyika na udongo wa matope.” Ungekuwa ‘umejichanganya nafsi zao na mbegu za wanadamu; lakini hautashikamana, kama vile chuma kisivyoshikamana na udongo.’ Hivyo, “udongo” wa ile sanamu ungefananisha vikundi vya watu wanaoinuka na kupinga mamlaka iliyosimamishwa. Kupitia kwa vyama vya wafanya kazi, maandamano, migomo na vitendo vingine vya kupinga, watu wa vivi hivi wamejaribu kudhoofisha namna ya serikali ya kibepari iliyosimamishwa pamoja na maeneo yaliyo chini ya maongozi ya Mamlaka ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika.
Ingawa serikali za nje za Kikomunisti za mataifa mengine mara nyingi huchochea na kutoa njia za kusitawisha huu “udongo” ndani ya Mamlaka ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika, pamoja na maeneo yaliyo chini ya maongozi yake, zenyewe hazikufananishwa katika ile sanamu. Lazima ikumbukwe kwamba sanamu hii inafananisha mfululizo wa mamlaka ya ulimwengu duniani kwa ujumla, sana sana kama vile inavyohusiana na watu wa Yehova, kuendelea mpaka wakati sanamu inapoharibiwa na ufalme wa Mungu kupitia kwa Kristo kuchukua mahali pa serikali zote za dunia. Kumekuwako serikali na falme zenye nguvu zilizopata kuinuka duniani tangu wakati wa Babeli kama vile milki za kale za Mashariki, sehemu za Ulaya, Afrika na bara za Amerika. Walakini hizi hazikufananishwa katika ile sanamu, kwa sababu hazikuwa mamlaka za ulimwengu zenye nguvu zaidi mpaka wakati wa mwisho wa Nyakati za Mataifa katika mwaka 1914 kuhusiana na watu wa Yehova. Kinyume chake, katika Ufunuo 13:1 serikali zote za kisiasa zimetiwa ndani ya “mnyama mwenye vichwa saba na pembe kumi.” Si kwamba tu ana vichwa saba zikifananisha mamlaka saba za ulimwengu kuanzia na ya Misri mpaka ya Uingereza na Amerika, bali vilevile ana mwili unaotia ndani sehemu nyingine zote za kisiasa, mnyama wote akifananisha taratibu ya utawala wa kisiasa duniani kurudi nyuma mpaka mwanzo wake katika siku za Nimrodi.
Basi “udongo” haufananishi serikali za Kikomunisti kama vile sehemu nyingine za hiyo sanamu zisivyofananisha serikali na milki nyingine ambazo hazikutawala ulimwengu wote katika muda wote wa wakati uliopita. Walakini uhakika wa kwamba sanamu hiyo imefikia wakati wake wa mwisho pasipo kuwa na nafasi kwa mamlaka nyingine ya ulimwengu kutokea, na vilevile uhakika wa kwamba “mnyama” huyo ana vichwa saba tu, wala si vinane, unaonyesha kwamba hakutakuwako mamlaka nyingine mpya ya ulimwengu itakayotawala dunia yote kabla ya kuondolewa kwa taratibu yote ya kisiasa. “Udongo” haufananishi mamlaka nyingine ya ulimwengu ikitokea, wafananisha tu kitu chenye kudhoofisha.
Ufunuo sura ya 17 husimulia juu ya yule “mnyama mwekundu sana” akiwa mzima ‘ndiye mfalme wa nane,’ walakini inasemekana kwamba “ni mmoja wa wale saba”—yaani zile mamlaka za ulimwengu. Kwa kweli yeye hana mamlaka yo yote ya utawala, isipokuwa ile anayopewa atumie duniani na zile “saba.” Ukweli ni kwamba, Mamlaka ya Saba ya Ulimwengu ndiyo iliyoongoza katika kutokeza hiyo “sanamu” ya yule mnyama. (Linganisha Ufunuo 13:11-18.) Huyu “mnyama mwekundi sana,” akiwa “sanamu” ya yule “mnyama mwenye pembe kumi, na vichwa saba,” atokaye katika “bahari” ya wanadamu, kwa wazi afananisha kwanza Ushirika wa Mataifa na kisha Umoja wa Mataifa. Yeye ni ‘mfalme wa nane’ kwa vile lilivyo tengenezo la ulimwenguni pote, walakini halichukui mahali pa ile Mamlaka ya Saba ya Ulimwengu. Lenyewe si ile sehemu ya dunia ya mataifa ya Kikomunisti, kama vile udongo wa ile sanamu usivyofananisha mamlaka mpya ya ulimwengu ikitokea kutokana na ile sanamu inayofananisha mfululizo wa mamlaka za ulimwengu.
Bila shaka wakati lile “jiwe” lililokatwa kutoka katika mlima linapopiga ile sanamu katika miguu yake na kuiangusha kwa kuiharibu, jiwe hilo litavunja-vunja, si ile mamlaka ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika pamoja na mabaki yaliyopo duniani leo ya zile mamlaka nyingine za ulimwengu za nyakati zilizopita tu, bali vilevile na zile tawala zilizoshirikiana na mamlaka hizo za ulimwengu zilizofananishwa na ile sanamu pamoja na zile zinazounga mkono na kusaidia ule “udongo” katika miguu na vidole vya miguu vya ile sanamu. Serikali hizi zote za wanadamu pamoja na vikundi vyenye kutaka mabadiliko lazima ziondolewe duniani ili kuiachia nafasi serikali ya Ufalme inayosimamiwa na Yesu Kristo, mfalme aliyewekwa na Mungu.
Biblia inaonyesha kwamba jambo hili halitatimizwa pasipo vita, kwa sababu mataifa yote yanataka kushikilia enzi kuu zao. Unabii unaolingana wa Ufunuo 17:12-14 unaonyesha kwamba watawala wenye kutokeza zaidi wa wakati wa mwisho (kama vile wanavyofananishwa na zile “pembe kumi” za yule mnyama) “wapokea mamlaka kama wafalme muda wa saa moja [au muda mfupi] pamoja na yule mnyama. Hawa wana shauri moja, nao wampa yule mnyama [Ushirika wa Mataifa na mrithi wake, Umoja wa Mataifa] nguvu zao na mamlaka yao. Hawa watafanya vita na Mwana-Kondoo [Kristo Yesu], na Mwana-Kondoo atawashinda, kwa maana Yeye ni Bwana wa Mabwana na Mfalme wa Wafalme.”
Lo! mwisho wenye aibu namna gani wa mwendo wa mamlaka za ulimwengu! Utawala wazo wa ukatili na wenye uonezi utaondolewa, usirudi tena kuwalemea wanadamu duniani. Ufalme wa Mungu utaleta serikali ya ulimwenguni pote itakayotawala kwa unyofu na amani. Italeta afya pamoja na uzima wa milele kwa wanadamu watiifu, walio raia za ufalme huo. Hii inaonyeshwa waziwazi sana mwishoni mwa ule unabii wa ndoto ya sanamu aliyopewa Nebukadreza: “Ndipo kile chuma, na ule udongo, na ile shaba, na ile fedha, na ile dhahabu, vilivunjwa vipande vipande pamoja, vikawa kama makapi ya viwanja vya kupepetea wakati wa hari; upepo ukavipeperusha, hata pasionekane mahali pake; na lile jiwe [linalofananisha ufalme wa Mungu mikononi mwa Kristo Yesu] lililoipiga hiyo sanamu likawa [mlima] mkubwa, likaijaza dunia yote.”—Dan. 2:35.
Unabii wa Biblia waonyesha kwamba wakati huu wa furaha u karibu. Leo watu wa mataifa yote wanakaribishwa wajiweke upande wa enzi kuu ya Yehova badala ya kuzitumaini serikali za kibinadamu. (Zab. 146:3) Mashahidi wa Yehova watafurahia kukusaidia ujifunze mengi zaidi kuhusu serikali hii ya Ufalme.