Misaada Katika Kujiendesha Wenyewe kama Watu Wadogo Zaidi
1. Ni habari gani za ki-Maandiko zilizoangaliwa hapo kwanza zinazoweza kutusaidia tujiendeshe kama watu wadogo Zaidi?
NI JAMBO gani litakalotusaidia tujiendeshe kama watu wadogo zaidi? Kwa uhakika mambo yote ambayo tumeona katika makala iliyotangulia juu ya matunda mabaya yaliyotokana na kukosa kufanya hivyo ni maonyo kwetu tujiendeshe kama watu wadogo zaidi. Kwa uhakika hatutaki kuondoka kwenye mbio ya uzima, au tunataka? Kwa upande mwingine, mifano yote myema ya ki-Maandiko ya wale waliojiendesha kama watu wadogo zaidi na thawabu walizopokea zinapasa zitutie moyo tutake kuwaiga.
2, 3. (a) Uhusiano mwema pamoja na Yehova unaweza kutusaidiaje tujiendeshe kama watu wadogo zaidi? (b) Kwa sababu gani unyenyekevu unaweza kutusaidia?
2 Ingawa huenda wengine wetu wakawa hawajaupata, mmoja wa misaada iliyo mikubwa zaidi katika habari hii ni kuwa na uhusiano mwema pamoja na Yehova Mungu, kumtumaini yeye kabisa. Tukifanya hivyo, hatutakuwa na hangaiko la bure juu ya kupungukiwa, kushushiwa heshima au kukosa kuonyeshwa na wengine kwamba wanatujali. Naam, tunataka ‘tumtumaini Yehova kwa moyo wetu wote, wala tusizitegemee akili zetu wenyewe. Katika njia zetu zote tukimkiri yeye, naye ataongoza mapito yetu tupate faida iliyo kubwa zaidi.’ (Mit. 3:5, 6) Halafu, tena, tunaweza kuwa na tumaini hakika kwamba atasawazisha vizuri kazi zake zote kwa faida yetu wenyewe.—Rum. 8:28.
3 Vilevile unyenyekevu unahitajiwa ili tuweze kujiendesha kama watu wadogo zaidi. Na kwa sababu gani tusiwe na nia ya kuwa wanyenyekevu? Tunaambiwa hivi: “Afadhali kuwa na roho ya unyenyekevu pamoja na maskini, kuliko kugawanya nyara pamoja na wenye kiburi.” Mwendo wa kiburi bila shaka utamletea mwenye kiburi hicho ushinde: “Kiburi hutangulia uangamivu; na roho yenye kutakabari hutangulia maanguko.” Zaidi ya hilo, kiburi humfanya Mungu atupinge, kama tusomavyo: “Mungu huwapinga wajikuzao, bali huwapa neema wanyenyekevu.” Mtume Petro anasema lile lile linalosemwa na mwanafunzi Yakobo: “Ninyi nyote jifungeni unyenyekevu” kuelekea mtu na mwenzake. Naam, imetupasa tujiendeshe kama watu wadogo zaidi—“kwa sababu “Mungu huwapinga wajikuzao, bali huwapa neema wanyenyekevu.”—Mit. 16:18, 19; Yak. 4:6; 1 Pet. 5:5; linganisha Warumi 12:16.
KANUNI YA UKICHWA
4, 5. (a) Kuthamini kwetu kanuni ya ukichwa kunaweza kusaidiaje katika jambo hili? (b) Jambo hilo linaweza kuonyeshwaje kwa mfano mzuri?
4 Msaada mwingine ni kwamba sisi tuithamini kanuni ya ukichwa. Wakati wo wote kunapokuwa na kazi ya kufanywa inayohitaji watu zaidi ya mmoja, kunahitajiwa mtu wa kuongoza na kufanya maamuzi ya mwisho au sivyo kunatokea mvurugo, na kazi inafanywa kwa makusudi yenye kuhitilafiana. Ndiyo kusema, kuna uhitaji wa kufuata utaratibu fulani uliotengenezwa. Utaratibu uliotengenezwa wenye watu wengi unaweza kufananishwa na mwili wa kibinadamu. Miili yetu ina viungo vingi sana vyenye kutofautiana, lakini bado vyote hivyo vinaongozwa na kile kile kichwa kimoja! Ni kweli kwamba huenda viungo vingine vikawa mashuhuri zaidi, vya maana zaidi ya vingine, lakini kama vile mtume aonyeshavyo wazi sana, hakuna hata kiungo kimoja kinachoweza kuambia kingine, “Sina haja na wewe.” Vyote vinahitajiwa sana. Tukifuata kielelezo hiki, je! haitupasi kuridhishwa na fungu la kushiriki katika utimizo wa kusudi la tengenezo?—1 Kor. 12:21.
5 Umaana wa kutambua kanuni ya ukichwa unaweza pia kuonyeshwa vizuri na mfano wa jamii ya muziki wa tarabu. Katika jamii kubwa ya muziki wa tarabu uliowekewa sehemu nyingi za kuukoleza vizuri, huenda kukawa na wanamuziki 100 wenye vipawa, na hata hivyo lazima kila mmoja wao ajiendeshe kama mtu mdogo zaidi. Hata kiongozi lazima ajiendeshe kama mtu mdogo zaidi, kwa maana yuko chini ya wajibu wa kuuimbisha muziki kama ulivyokusudiwa na mtungaji wake. Tena lazima wanamuziki wote walio katika jamii hiyo ya tarabu wamtii kiongozi, wawe wadogo zaidi yake. Si hivyo tu, bali katika kila upande, kunapokuwa na wanamuziki zaidi ya mmoja wenye kuimbisha chombo fulani, kunakuwa na “kiti cha kwanza,” nao wanamuziki wengine wote katika sehemu hiyo lazima wafuate mtindo wa mtu huyo aliye kiti cha kwanza kwa kadiri iwezekanayo. Hivyo kunakuwa na mkuu anayeitwa concertmaster kwenye Violin (mfano wa zeze) zile za kwanza. Ni kwa kufuata mpango wa namna hiyo tu inavyowezekana kutokeza muziki wenye kupendeza na kupatana. Naam, kuithamini kanuni ya ukichwa kutatusaidia tujiendeshe kama watu wadogo zaidi.
ROHO YA AKILI TIMAMU NA ROHO TAKATIFU YA MUNGU
6, 7. Ni kwa njia gani mbalimbali roho ya akili timamu inavyoweza kusaidia katika habari ya kujiendesha wenyewe kama watu wadogo zaidi?
6 Kuwa na roho ya akili timamu kutatusaidia pia katika jambo hili. Mtume Paulo anatushauri hivi: “Kupitia fadhili zisizostahilika zilizopewa kwangu mimi namwambia kila mmoja huko kati yenu asifikiri zaidi juu yake mwenyewe kuliko inavyohitajiwa kufikiri; bali afikiri ili awe na akili timamu, kila mmoja kama vile Mungu amemgawia yeye kipimo cha imani.” (Rum. 12:3, NW) Tukijichukua wenyewe kwa utimamu, bila kuacha maoni yetu yafunikwe na kiburi au kujitakia yetu wenyewe, tunaweza kujiendesha kama watu wadogo zaidi. Jinsi gani?
7 Kila mmoja wetu anafahamiana na nafsi yake mwenyewe zaidi ya vile anavyofahamiana na wengine. Zaidi ya vile wengine wanavyoona, imetupasa sisi tuweze kuona zaidi upungufu mwingi tulio nao katika kuwa vile tunavyopaswa kuwa na kutenda tunavyopaswa kutenda. Ni kama vile Paulo alivyoomboleza: “Lile nilipendalo, silitendi; bali lile nilichukialo ndilo ninalolitenda.” (Rum. 7:15) Zaidi ya hilo, kama Wakristo tuna wajibu wa kuepuka kuhukumu wengine vikali mno lakini tufahamu kwamba wanaweza kufanya makosa ya kutokukamilika, na wafanyapo mambo fulani tuwaachie kwa sababu hatujui vizuri sababu gani wameyafanya. Lakini bila shaka tunaumia moyoni kwa kuujua udhaifu wetu mbalimbali na mambo ambayo labda tumetenda kwa sababu ya kuwa na kusudi baya. Kwa sababu hiyo basi inatupasa tuwe na nia ya kujiendesha kama watu wadogo zaidi kuhusiana na wengine. Hakuna shaka: Kuwa na roho ya akili timamu kutatusaidia katika mambo haya.—2 Tim. 1:7.
8. Kuuthamini uwezo wa roho takatifu ya Mungu kunaweza kusaidiaje katika kujiendesha wenyewe kama watu wadogo zaidi?
8 Kuthamini kuzuri uwezo wa roho takatifu ya Mungu kutatusaidia pia tujiendeshe kama watu wadogo zaidi. Hata tuwe tunazaliwa na ujuzi wa kufanya mambo au kufikiria miradi fulani, jambo lililo la maana ndani ya tengenezo la Yehova ni roho takatifu ya Mungu. (Zek. 4:6) Hiyo roho takatifu iliwawezesha Wakristo wa kwanza kuwa na matokeo mazuri sana katika huduma yao hata adui zao wakalalamika kwamba watu hao ‘waliupindua ulimwengu.’ (Matendo 17:6) Ni kwa sababu ya roho ya Mungu waliweza kunena kwa njia ya wazi hivyo bila kuogopa, walipokabiliana na wapinzani wao wa kidini, ingawa kwa kuzaliwa walikuwa watu wasio na elimu nyingi na wa kawaida tu. (Matendo 4:13, 29-31) Kutambua kwamba ndugu zetu wote wana roho takatifu ya Mungu kutatusaidia tujiendeshe kama watu wadogo zaidi kuhusiana nao hata ingawa huenda tukawa tunawapita katika uwezo wa kufanya mambo fulani kulingana na maoni ya kilimwengu. Jambo hilo litafanya iwe vyepesi kwetu kulitii shauri hili: “Katika kuonyeshana heshima wekeni mfano.”—Rum. 12:10, NW.
9. Kuthamini kwetu kwamba ufalme wa Yehova ndio wenye umaana mkubwa zaidi kumepasa kuwa na matokeo gani juu yetu?
9 Kwa hiyo, je! tunauthamini umaana wa ufalme wa Yehova Mungu? Ikiwa tunauthamini tutakuwa na nia ya kutanguliza faida zake katika maisha zetu. Kufanya hivyo kutatusaidia pia tujiendeshe kama watu wadogo zaidi. Kwa sababu gani inaweza kusemwa hivyo? Kwa sababu tukithamini kwamba ile kazi ya Ufalme ambayo sisi sote tunaishiriki ndilo jambo la maana wala si sisi wenyewe tulio wa maana, hapo hatutakuwa na hangaiko la bure tukisahauliwa katika kupewa pendeleo la utumishi ambalo labda tungalitaka kupata. Tunataka tuichukue kazi ya Mungu kwa uzito, si kujichukua hivyo sisi wenyewe. Ingawaje, hesabu ya sehemu zilizo katika mikutano mbalimbali ya kundi ina kikomo, tena hesabu ya sehemu zilizo katika programu ya kusanyiko la mzunguko ina kikomo, tena hesabu ya sehemu zilizo katika programu ya kusanyiko la wilaya ina kikomo. Kwa hiyo bila shaka wengine wetu tutaachwa bila kupata sehemu. Ikiwa hivyo, acheni tufurahi pamoja na ndugu ambao wamepata mapendeleo badala ya kuwaonea kijicho. Acheni tuwe na nia ya akili ya mtunga zaburi aliyesema: “Kwa maana siku moja katika nyua zako ni bora kuliko elfu kwingineko. Mimi nimechagua kusimama kwenye kizingiti cha chini cha mlango katika nyumba ya Mungu wangu badala ya kuzurura-zurura katika hema za waovu.” Naam, ni afadhali zaidi kuwa mtu mdogo zaidi katika tengenezo la Yehova kuliko kuwa mtu mkubwa zaidi katika tengenezo bovu la Shetani lililohukumiwa maangamizi.—Zab. 84:10, NW.
HEKIMA YENYE MAFAA
10. Kujiendesha wenyewe kama watu wadogo zaidi kunaweza kutuepusha tusipatwe na aibu gani?
10 Neno la Mungu Biblia lina mengi ya kusema juu ya hekima yenye mafaa. Kwa mfano, linaonyesha wazi hekima ya kutumia vyombo vilivyonolewa ili mtu asitumie nguvu nyingi sana za bure. (Mhu. 10:10) Vilevile linatupa mashauri yenye mafaa juu ya kujiendesha kama watu wadogo zaidi. Yesu alitaja jambo hilo, kama tunavyosoma kwenye Luka 14:8-11: ‘Ukialikwa na mtu arusini, usiketi katika kiti cha mbele; isiwe kwamba amealikwa mtu mwenye kustahiwa kuliko wewe, akaja yule aliyewaalika wewe na yeye, na kukuambia, Mpishe huyu! Ndipo utakapoanza kwa haya kushika mahali pa nyuma. Bali ukialikwa, nenda ukaketi mahali pa nyuma, ili ajapo yule aliyekualika akuambie, Rafiki yangu, njoo huku mbele zaidi; ndipo utakapokuwa na utukufu mbele ya wote walioketi pamoja nawe. Kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa.”
11. (a) Kwa sababu gani kujiendesha wenyewe kama watu wadogo zaidi kunaleta uhusiano mwema pamoja na wengine? (b) Ni katika mambo gani mengine nia hii ya akili inasaidia?
11 Vilevile inaweza kusemwa kwamba ni hekima yenye mafaa kujaribu kuwa na uhusiano mzuri pamoja na wengine. Kujiendesha kama mtu mdogo zaidi ni njia moja ya kuutimiza mradi huo wenye kutamanika. Ni kawaida ya mwanadamu kuhangaikia faida zake mwenyewe, nasi tunapojitakia makuu au kutaka zaidi sana tuwapite wengine tunawafanya wajisikie vibaya. Lakini tunapojiendesha kama watu wadogo zaidi hatujaribu kunyakua cheo cha wengine, hatuwafanyi wajisikie wamekosa usalama au kwamba ni wadogo kuliko sisi. Hatuwafanyi wajaribu kulinda cheo chao. Kwa sababu hiyo, wao wataelekea zaidi kutuonyesha urafiki na upendo wenye shauku. Zaidi ya hilo, kujiendesha kama watu wadogo zaidi kutatuzuia tusijinyo-o-oshe mno katika kushindana na wengine ili tuwapite. Jambo hilo litatuzuia tusiwe vimbelembele kufanya mambo ambayo hatuna majaliwa au ujuzi wa kuyafanya; litatuzuia ‘tusijaze mdomoni lundo kubwa mno la ugali usioweza kumezeka,’ kwa usemi wa mfano. Au, ilivyosemwa kwa njia bora zaidi na Yesu, ni hekima kuihesabu gharama. Tena, hekima yenye mafaa itatuzuia tusiahidi watu mambo mengi kuliko tunayoweza kufanya.—Luka 14:28.
12. Kujiendesha wenyewe kama watu wadogo zaidi kunaweza kusaidiaje katika jamaa?
12 Hekima yenye mafaa inayotufanya tujiendeshe kama watu wadogo zaidi inahusika pia ndani ya jamaa. Kwa mfano, mke mwenye hekima ataridhika na kutimiza daraka la usaidizi na utii kuhusiana na mumewe, akijua kwamba kufanya hivyo kunaleta amani na furaha katika jamaa. Kuwa na nia ya kutimiza daraka hilo kunamfanya mumewe amwonee shauku na upendo, na kumfanya atake kumfanyia mambo. Tena hakuna jambo linaloweza kufurahisha mke zaidi ya kuonyeshwa na mumewe nia nzuri sana ya kumshukuru na kumpenda kwa shauku nyakati zote, kwa maneno na matendo. Katika habari hii, ni hekima yenye mafaa pia mume kukubali sehemu ambazo mkewe anampita kisha aridhike na kulitimiza daraka lile dogo zaidi, la kukubali anapitwa na mkewe kwa njia hiyo, mke akiwa chini ya ukichwa wake. Kufanya hivyo kutakuwa na matokeo mazuri juu ya mke pia.
UPENDO USIO NA UCHOYO NDIO MSAADA MKUBWA ZAIDI
13, 14. Katika habari hii, upendo usio na uchoyo ulimsaidiaje (a) Yonathani? (b) Yesu Kristo?
13 Je! kuonyesha shauku na upendo usio na uchoyo kutatusaidia katika kujiendesha kama watu wadogo zaidi? Ndiyo, tena kufanya hivyo ndiko kutakakotusaidia sana kuliko mambo mengine yote! Tuna mfano mwema wa Yonathani, mwana wa Mfalme Sauli. Tunasoma kwamba, mara tu baada ya Daudi kulichinja jitu Goliathi, nafsi ya Yonathani, ikaambatana na nafsi ya Daudi, Yonathani akampenda kama nafsi yake mwenyewe.’ (1 Sam. 18:1) Wakati ulipozidi kusonga, Yonathani alianza kujua kamba siye aliyechaguliwa na Yehova kumfuata Sauli kama mfalme katika Israeli, bali ni Daudi. Lakini kwa sababu ya upendo aliokuwa nao kwa Daudi, badala ya kumwonea Daudi kijicho hata kidogo, Yonathani alisema: “Usiogope, kwa maana mkono wa Sauli, babangu, hautakupata; na wewe utakuwa mfalme juu ya Israeli; na mimi nitakuwa wa pili wako.”—1 Sam. 23:17.
14 Yesu Kristo pia ni mfano mwema kwetu namna gani! Yesu alisema: “Nampenda Baba.” Kwa sababu ya upendo huo, hata dakika moja Yesu hakufikiria kuwa sawa na Baba yake, bali nyakati zote alithamini kwamba Yehova Mungu ndiye kichwa chake. (1 Kor. 11:3; Flp. 2:6) Zaidi ya hilo, kwa sababu ya Kristo kuwa na upendo mkubwa kwa wafuasi wa hatua zake waliotiwa mafuta, alikuwa na nia ya kuwafia. (Efe. 5:25) Mfano wa Yesu wa unyenyekevu na upendo unapasa kwa uhakika utusaidie tujiendeshe kama watu wadogo zaidi.
15. Mtume Paulo alitoa mfano gani mwema wa kujiendesha mwenyewe kama mtu mdogo zaidi?
15 Hapo kwanza tumeona kwamba mtume Paulo alijiendesha kama mtu mdogo zaidi kuhusiana na Wakristo wenzake. Kwa sababu gani? Ni kwa sababu ya upendo mkubwa aliokuwa nao kwao. Hivyo, alipokuwa akiwaandikia Wakristo wenzake huko Rumi, yeye hakutazamia kuitia nguvu imani yao tu bali pia kutiwa nguvu imani yake nao kwa kubadilishana kitia-moyo. (Rum. 1:8-12) Maneno aliyowaandikia ndugu zake huko Korintho yanashuhudia jambo ilo hilo: “Vinywa vyetu vimefumbuliwa kwenu, enyi Wakorintho; mioyo yetu imekunjuliwa. Hamsongwi ndani yetu, bali mwasongwa katika mioyo yenu. Basi, ili mlipe kadiri ile mliyopewa (nasema nanyi kama na watoto), nanyi pia mkunjuliwe mioyo.” (2 Kor. 6:11-13) Angalia misemo inayofanana na huo kwa habari ya Wakristo wa huko Filipi na Thesalonike.—Flp. 1:8; 4:1; 1 The. 2:7, 8.
16, 17. (a) Ni mambo gani yanayoweza kusemwa juu ya mifano ya ki-siku-hizi ya kujiendesha kama mtu mdogo zaidi? (b) Upendo unaweza kusaidiaje katika habari hii?
16 Je! hatuna mifano mingi myema ya jambo hili katika nyakati za ki-siku-hizi? Wengi walio katika vyeo vya madaraka wanaweka mifano myema katika kujiendesha kama watu wadogo zaidi. Kwa unyenyekevu wanakuwa tayari kuwatumikia ndugu zao wanaohitaji msaada. Hasa mikusanyiko yetu mikubwa. Halafu, ‘wanakunja mikono ya shati zao’ na kuitimiza kazi, bila kujali wamezaliwa wakiwa na vipawa gani au wana vyeo gani katika tengenezo.
17 Bila shaka, upendo usio na uchoyo utatusaidia tujiendeshe kama watu wadogo zaidi. Naam, ‘upendo haujigambi, haujitutumui kwa kiburi, hata hautafuti faida zake wenyewe.’ Hauhangaikii, mno kupata haki unayostahili kuipata. (1 Kor. 13:4, 5, NW) Kwa kweli upendo unaweza kutusaidia, kwa maana utatuongoza ‘tuendelee kutafuta, si faida yetu wenyewe, bali ile ya wenzetu.’ (1 Kor. 10:24) Ni kama vile Paulo alivyowaambia Wakristo Wagalatia: “Tumikianeni kwa upendo.” Kwa uhakika kutumikiana kunahitaji kwamba kila mmoja wetu ajiendeshe kama mtu mdogo zaidi!—Gal. 5:13.
18. Jambo hili la kujiendesha kama mtu mdogo zaidi linaweza kurudiwaje kwa muhtasari?
18 Kwa wazi maandishi ya Biblia, na vilevile historia ya kilimwengu ya kale na ya ki-siku-hizi, yanahakikisha kwamba kujiendesha kama mtu mdogo zaidi ndio mwendo wa hekima. Kunaleta uhusiano mwema na Yehova Mungu, na Wakristo wenzetu na washiriki wa jamaa zetu wenyewe. Tena, ndio mwendo wa furaha kwa “sababu unamaanisha kuwapa wengine faida na mapendo yao, na “ni heri kutoa kuliko kupokea.” (Matendo 20:35) Vile-vile, kuna misaada mingi ya kutuchochea tujiendeshe kama watu wadogo zaidi: kutii mifano ya ki-Biblia, kuitambua kanuni ya ukichwa, kuizoea roho ya akili timamu, kufuata vielekezo vya roho takatifu ya Mungu, na kuonyesha hekima yenye mafaa na upendo usio na uchoyo. Wakati wote na tulione kuwa pendeleo, kuwa baraka, kujiendesha wenyewe kama watu wadogo zaidi, kwa faida ya wengine na yetu wenyewe, na hasa sana kwa kumletea Yehova sifa. —Kutoka The Watchtower, June 1, 1981.
[Picha katika ukurasa wa 20]
Kama kila mtu angekuwa kiongozi, muziki wa tarabu ungekuwa wapi?