Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 1/15 kur. 14-19
  • Ibada ya Mungu Mmoja wa Kweli Tayari Inaendelea Kuinuliwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ibada ya Mungu Mmoja wa Kweli Tayari Inaendelea Kuinuliwa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JINA LA KIBINAFSI LA MUNGU WA PEKEE WA KWELI LATANGULIZWA MBELE!
  • Tutatembea Katika Jina la Yehova Milele!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Kitabu Cha Biblia Namba 33—Mika
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Watumishi wa Yehova Wana Tumaini la Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • ‘Watu wa Mataifa Wataiendea Makundi Makundi’ Ibada Yenye Kutoa Uzima
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 1/15 kur. 14-19

Ibada ya Mungu Mmoja wa Kweli Tayari Inaendelea Kuinuliwa

1, 2. Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya kwanza, ibada ya yule Mungu mmoja wa kweli ilishuka kwenye kiwango cha chini namna gani, nalo jambo hilo lilionyeshwaje katika Mika 3:12?

VITA ya Ulimwengu ya Kwanza ulikuwa ni wakati wa giza ambalo wanadamu walikuwa hawajapata kuliona hapo mbele. Ilikuwa kama kwamba nguvu za giza zilikuwa zimepata ushindi kote kote ulimwenguni. Ilionekana kama kwamba “mkuu wa ulimwengu” alikuwa ameshinda. (Yohana 14:30) Milki yake ya ulimwenguni ya dini ya uongo, kutia ndani Jumuiya ya Wakristo, ilipojitokeza kwa kutukuza taifa ikaunge mkono mataifa yenye wazimu wa kufanya vita, mkazo mkubwa sana ulielekezwa juu ya watu wote wenye kufuata dini. Kwa hiyo, hata ibada ya Mungu wa pekee wa kweli anayeishi ilirudi kwenye kiwango cha chini. Wenye kuitegemeza waliteswa na wakawekwa chini ya vizuizi, hata wakafungwa gerezani. Hali yao ikawa yenye msiba, kama ile inayosimuliwa katika Mika 3:12:

2 “Sayuni utalimwa kama shamba lilimwavyo, na Yerusalemu utakuwa magofu; na mlima wa nyumba [hekalu] utakuwa kama mahali palipoinuka msituni”​—kama shamba lililoachwa pasipo mtu lenye kufunikwa na vichaka virefu kama miti kwa sababu ya wakati mwingi sana kupita.

3. Waabudu wa Mungu huyo wa kweli walijiruhusu waamini maoni gani, walakini ni jambo gani lililobaki wapate kulifanya kulingana na unabii kabla ya “mwisho” kuja?

3 Ilionekana kama kwamba mwisho ulikuwa umefika​—juu ya taratibu nzima ya mambo duniani. Waabudu wa Mungu wa Biblia wakajiruhusu waamini hivyo ndivyo mambo yalivyokuwa, kwani walikuwa “watu wa kuchukiwa na mataifa yote.” (Mt. 24:9) Hata hivyo, walikuwa wameanza tu kuingia kwenye “mwisho wa taratibu ya mambo.” Walikuwa wangali na kazi nyingi ya kufanya ya kuokoa maisha kabla hawajaingia kwenye kumalizika kwa hiyo “taratibu ya mambo.” Kama vile Gavana (Liwali) mkuu kutoka Bethlehemu alivyokuwa ametabiri, “habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:3, 14, NW) Unabii wa Mika ulipatana na hayo, hata ingawa Mika alikuwa ameuandika mamia ya miaka kabla.

4. Baada ya masimulizi ya ukiwa ambao ungekuja juu ya Yerusalemu na nchi ya Yuda, Mika 4:1-4 inatabiri badiliko gani zuri ambalo lingemletea Yehova utukufu?

4 Baada ya Mika kusimulia uharibifu ambao ungeletwa na Wababeli, juu ya nchi ya Yuda na mji wake mkuu, Yerusalemu (au, Sayuni), aliendelea kusema hivi: “Lakini itakuwa katika siku za mwisho, ya kwamba mlima wa nyumba [hekalu] ya [Yehova] utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na watu wa mataifa watauendea makundi makundi. Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova], na nyumbani kwa Mungu wa Yakobo; naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake; kwa maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno la [Yehova] litatoka Yerusalemu. Naye atafanya hukumu kati ya watu wa kabila nyingi, naye atawakemea mataifa wenye nguvu walio mbali; nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe. Bali wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu; kwa kuwa kinywa cha [Yehova] wa majeshi kimesema hivi.”​—Mik. 4:1-4.

5. Leo, ni jengo gani lililo juu ya mlima wa nyumba ya Yehova, na je! hiyo Inatimiza Mika 4:1-4?

5 Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilipokuwa ikiendelea Yerusalemu wa kidunia ulitekwa na majeshi ya Uingereza chini ya jemadari Allenby, na ukikubali jambo hilo Ushirika wa Mataifa uliipa Uingereza mamlaka ya kuongoza eneo hilo, mpaka mwaka 1948. Mamlaka hiyo ya kuongoza ilipokwisha, vita vilifuata kati ya Wayahudi na Waarabu, na leo taifa la Israeli linashikilia hata mji wenye kuzungukwa na kuta wa Yerusalemu. Walakini je! hekalu la kumwabudu Yehova liko juu ya kilele cha mlima ule ambako nyumba ya ibada ya Yehova ilikuwako kufika mwaka 70 W.K.? Hapana, walakini Kuba la Mwamba la kuabudia mungu wa Mohamedi, Allah, ndilo lililoko hapo, na watu wa mataifa mengi hulitembelea likiwa ni mahali panapovutia watalii. Haiwezi kukanushwa hata! kwamba huko si kutimizwa kwa unabii wa Mika 4:1-4.

6. Hata hivyo, ni kwa nini Mika 4:1-4 inatimizwa, na kwa sababu gani Yerusalemu wa kidunia hauhusiki katika utimizo huo?

6 Hata hivyo, unabii huo umekuwa ukitimizwa tangu mwaka wa 1919 uliofuata vita vile vikuu. Namna gani hivyo? Kwa sababu Yerusalemu wa juu zaidi unahusika. Na tukumbuke namna katika Nisani 9, 33 W.K., Yesu Kristo akiwa Gavana aliyetoka Bethlehemu alivyopanda mwana-punda kwa ushindi akaingia Yerusalemu lakini asikubaliwe kuwa Mfalme. Siku mbili baadaye, katika Nisani 11, aliguswa moyo akaulilia Yerusalemu huo wa kidunia, akasema hivi: “Ni mara ngapi nimetaka kuwakusanya pamoja watoto wako, kama vile kuku avikusanyavyo pamoja vifaranga vyake chini ya mabawa yake, lakini hamkutaka! Angalieni, nyumba yenu [hekalu] mmeachiwa [ninyi watu] hali ya ukiwa.” (Mt. 23:37, 38) Siku tatu baadaye, katika Nisani 14 Yesu alifia imani katika Kalvari nje ya Yerusalemu. Kisha, kwa upande wake, Yehova Mungu akaliacha hekalu hilo hata ingawa lilikuwa limewekwa wakf kwake. Sasa halikuwa tena mahali pa ibada inayokubaliwa. Kuharibiwa kwalo mwaka wa 70 W.K. kulikazia jambo hilo!

7. Yerusalemu wa kimbinguni ulipata kuwa mama ya wanafunzi wa Yesu wakati gani, naye Paulo anatajaje jambo hilo?

7 Siku arobaini (40) baada ya Yesu kufufuliwa alipaa akarudi mbinguni na siku 10 baadaye, siku ya Pentekoste, alimimina roho takatifu juu ya wanafunzi wake waliokuwa wakingojea katika Yerusalemu wa kidunia. Wakati wa tukio hilo Yerusalemu wa juu ukawa mama yao. Kwa habari hiyo, mtume Mkristo Paulo aliandika hivi katika barua aliyoyaandikia makundi katika Galatia: “Yerusalemu ya juu mbinguni ni mji ulio huru, nao ni mama yetu.” (Gal. 4:26, HNWW) Hata hivyo, baadaye, alipokuwa akiandikia Wakristo wote Waebrania, mtume uyo huyo aliandika hivi: “Bali ninyi mmeufikilia mlima Sayuni, na mji wa Mungu aliye hai, Yerusalemu wa mbinguni, na majeshi ya malaika elfu nyingi, mkutano mkuu [wa kundi] la wazaliwa wa kwanza walioandikwa mbinguni, na Mungu mwamuzi wa watu wote.” (Ebr. 12:22, 23; Ufu 21:2) Mika 4:1-4 inatabiri kuhusiana na huo Yerusalemu Mpya, Yerusalemu wa kiroho, ulio juu ya Mlima Sayuni wa kiroho. Leo unabii wa Mika unatimizwa juu ya Yerusalemu huo wa kiroho ufalme wa Kimasihi!

8. Ibada ya Mungu mmoja wa kweli imeinuliwa kwa kadiri gani kuhusiana na dunia tangu mwaka 1914?

8 Tangu miaka ya uharibifu wa vita ya 1914-1918 ibada ya Mungu ambaye ibada yake ilikuwa ikifanywa katika “nyumba,” au hekalu, lililokuwa juu ya mlima mojawapo wa Yerusalemu ya kale, inaendelea kuinuliwa. Ibada ya Yehova ‘imewekwa imara juu ya milima’ ambayo juu yake kulikuwa au kungali kuna mahekalu ya miungu ya uongo ya hii taratibu. Kwa njia hiyo ibada ya Mungu wa pekee aliye hai na wa kweli ‘imeinuliwa juu ya vilima.’

9. Baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, hali iliwekwaje wazi ili ibada ya Yehova iinuliwe, na Mika 2:12, 13 ilisema nini kuhusu jambo hilo?

9 Hasa baada ya kumalizika kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza katika vuli ya mwaka 1918 ibada ya Yehova akiwa ndiye Mungu Aliye Juu Zaidi iliinuliwa juu kufika mbinguni. Ilikuwaje hivyo? Kwa sababu, kwanza katika kipindi kilichofuata vita ile kuu iliwezekana waabudu wa Yehova wakarudishwa kutoka hali ya kuonewa, kutawanywa na ya kuzuiwa ambayo ilifanana na hali ya wahamishwa Wayahudi katika Babeli wakati wa miaka! 607-537 K.W.K. Unabii wa Mika ulitabiri kukusanywa tena kwa Waisraeli wa kiroho na kuwafungulia njia watoke katika utumwa huo wa Kibabeli, alipokuwa akisema hivi: “Hakika nitakukusanya, Ee Yakobo, nyote pia; bila shaka nitawakusanya waliobaki wa Israeli; nitawaweka pamoja kama kondoo [katika zizi ]; kama kundi la kondoo kati ya malisho yao; watafanya mvumo kwa wingi wa watu; [apasuaye njia] amekwea juu mbele yao; wamebomoa mahali, wakapita mpaka langoni, wakatoka nje huko; mfalme wao naye amepita akiwatangulia, naye [Yehova] ametangulia mbele yao.”​—Mik. 2:12, 13.

10. Yule “mfalme” katika unabii wa Mika ni nani, naye ‘alipasua njia’ namna gani na wakati gani na kwa ajili ya nani?

10 Katika mwaka 537 K.W.K., Waisraeli walipoondoka Babeli kwa kupatana na amri ya mshindi Mwajemi, Koreshi Mkuu, hakukuwako mfalme wa kibinadamu wa nyumba ya kifalme ya Daudi mwenye kuwaongoza wakitoka. Sedekia, mfalme wa mwisho wa nasaba ya Daudi kutawala katika Yerusalemu wa kale, wakati huo alikuwa amekwisha kufa, na kuzikwa katika Babeli. Kwa wazi, basi, lazima unabii wa Mika uwe una utimizo wa kiroho, Kwa hiyo “mfalme” huyo ni nani? Ni Mfalme yule ambaye angetawazwa kwenye mkono wa kuume wa Mungu huko mbinguni mwishoni mwa “nyakati za Mataifa” (au, “nyakati zilizowekwa za mataifa”) katika vuli ya mwaka 1914 W.K. (Luka 21:24, Authorized Version, New World Translation; Zab. 110:1, 2) Huyo alikuwa “mfalme” mkuu zaidi ya Koreshi mshindi wa Babeli. Alikuwa ndiye “Mfalme” aliyetawazwa karibuni, Yesu Kristo. Ndiye ‘aliyepasua njia’ (NW) kwa Waisraeli wa kiroho wenye kuonewa, “waliobaki” wa Israeli, au Yakobo wa kiroho. Kwa hiyo katika mwaka uliofuata vita kuu wa 1919 ndipo Yesu Kristo aliyetukuzwa ‘alipopasua njia’ kwa wanafunzi wake waliojiweka Wakf na kubatizwa ambao walikuwa wamekuwa “watu wa kuchukiwa na mataifa yote” kwa ajili ya jina lake wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza.​—Mt. 24:9.

11, 12. Ni nani aliyekuwa akitangulia mbele ya mabaki walipokuwa wakipiga hatua kuelekea kwenye uhuru, nao walikuwa wanatii amri gani iliyotolewa naye?

11 Wanafunzi hao waliofunguliwa walikuwa tayari kumfuata yeye akiwa Mfalme wao aliyetawazwa kwenye mkono wa kuume wa Yehova. Akiwa kwenye ‘lango’ la kutokea ambalo alikuwa amepasua ‘akapita akiwatangulia.’ Akawaongoza kwenye uhuru wa kweli wa Kikristo. Yehova alikuwa ‘akitangulia mbele yao,’ kwa sababu Yehova ndiye Aliyekuwa Mkuu aliyewawezesha wapige hatua za kwenda kwenye uhuru. Ndiye aliyekuwa ametoa mwito kwa waabudu wake waliokuwa wamefungwa katika Babeli ya kidini, akisema hivi:

12 “Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake.”​—Ufu. 18:4; Yer. 50:8, 9; Isa. 48:20.

JINA LA KIBINAFSI LA MUNGU WA PEKEE WA KWELI LATANGULIZWA MBELE!

13. Wakati ulikuwa umefika kwa Mungu mmoja wa kweli alifanyie nini, nalo toleo la Mnara wa Mlinzi la Novemba 15, 1919, lilionyeshaje jambo hilo wazi?

13 Kufika wakati huo Yehova alikuwa ameanza kujifanyia jina. Kwa kufaa jina lake likaanza kutangulizwa mbele, likiwa ni jina lililo juu zaidi ya lile la Mwanawe Yesu Kristo aliyetukuzwa. Kwa mfano, Mnara wa Mlinzi na Mtangazaji wa Kuwapo kwa Kristo (Kiingereza), katika toleo lake la Novemba 15, 1919, lilichapisha makala za kwanza za mfululizo wa makala zenye kichwa “Usemi Mchangamfu wa Isaya,” na katika Sehemu ya Kwanza iliendelea kusema hivi:

Katika hii mistari kumi na moja ya sura ya arobaini tunapewa mifano mitatu ya Yehova: kwanza, anafananishwa na Mfariji baada ya mateso ya muda mrefu; pili, anafananishwa kuwa Ndiye wa Kweli, ambaye neno lake lasimama ingawa mengine yote yanashindwa; tatu, akiwa Mchungaji anayeongoza watu wake kwenye ulinzi kama ule mzazi awapao watoto wake.

Sababu ya pili ya faraja inapatikana katika maneno haya “kwamba uovu wake mwingi umesamehewa”. Kwa hekima yake Mungu aliona kwamba ile miaka sabini ya kuaibishwa kwa taifa lote la Wayahudi ingetosha kusawazisha haki ya hukumu katika maandishi ya kimungu ili kuondoa maelekeo ambayo walikuwa wameyaonyesha kwa karne nyingi ya kuingia kwenye ibada ya sanamu, au kuabudu miungu mingine kando ya Yehova.

. . . Walakini twajua kwamba Yehova asingeweza kamwe kuleta adhabu isiyo ya haki. Hawezi kujikana. . . .

. . . Mapendekezo [ya jina la gazeti lililochapishwa na Sosaiti] yalionyesha kwamba neno la Kiyiddi linalolingana na “sauti” lingefahamika mara moja na Wayahudi wote kuwa linaonyesha ujumbe fulani wa pekee kutoka kwa Yehova.

Kwa hakika jamii yo yote ambayo itatumiwa na Yehova kwa ajili ya kusudi hilo lililotukuzwa la kurithi pamoja na Kristo inahitaji kuwa imefanyiwa matayarisho mengi sana ya muda mrefu kabla ya kufanywa wawe “watu wanaoufaa urithi wa watakatifu katika nuru.”

. . . Lakini ukiwa ni uhakikisho maradufu wa utimizo wa mambo yaliyo juu yaliyoahidiwa Yehova kwa mara nyingine anatia jina lake, au kutia sahihi hati yake mwenyewe​—“neno la Mungu wetu litasimama milele,” hata kuwe na vipingamizi, vya halisi au vya kuwazia.​—Ukurasa 343, fungu 5; ukurasa 344, mafungu 5-7; ukurasa 345, fungu 4; ukurasa 346, fungu 4.

14. Vilevile, kitabu The Harp of God, kilichochapishwa mwaka 1921, kilitangulizaje mbele jina la Mungu?

14 Vilevile, katika kitabu cha kwanza kilichofungamanishwa pamoja na Sosaiti baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, yaani, The Harp of God (Kinubi cha Mungu), kilichotolewa mwaka 1921, maelezo ya utangulizi ya waandikaji yalisema hivi katika fungu la 2: “Yehova alikuwa na mpango mkuu kabla ya msingi wa ulimwengu kuwekwa; walakini hakuna ye yote aliyejua juu yake. Wakati wa miaka ya kwanza elfu nne ya historia ya wanadamu mpango wa Mungu ulitunzwa ukiwa siri.”

15. Miaka saba baadaye, ni azimio lenye tangazo kwa nani lililopitishwa na wahudhuriaji wa kusanyiko la mataifa yote katika Detroit, Michigan?

15 Kwenye kusanyiko la mataifa yote lililofanywa huko Detroit, Michigan, Julai 30 mpaka Agosti 6, 1928, maelfu waliohudhuria kwa umoja walipitisha azimio lenye kichwa “Tangazo la Kumpinga Shetani na Kumwunga Mkono Yehova,” lililopendekezwa na aliyekuwa msimamizi wa Sosaiti wakati huo.​—Tazama Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) wa Septemba 15, 1928, kurasa 278, 279.

16. Tukio lenye kuleta upeo wa mambo lilitokeaje miaka mitatu baadaye kwenye kusanyiko la mataifa yote katika Columbus, Ohio?

16 Hata hivyo, tukio lenye kufikisha kwenye upeo lilitokea mwaka 1931. Hiyo ilikuwa siku ya Jumapili, Julai 26, wakati maelfu wenye kuhudhuria kusanyiko la mataifa yote katika Columbus, Ohio, walipopitisha azimio lenye kichwa “Jina Jipya.” Kwa azimio hilo waabudu hao waliojiweka wakf na kubatizwa wa Mungu Aliye Juu Zaidi walichukua jina ambalo msingi wake ni Maandiko, yaani, “mashahidi wa Yehova.”​—Isa. 43:10, 12, NW.

17. Kwa kukubali hivyo jina hilo jipya, wahudhuriaji hao wa kusanyiko walifanya nini, na baada ya hapo makundi kuzunguka dunia yote yalifanya nini, na wakawa na wajibu gani?

17 Kwa njia hiyo Wakristo hao wakaondolea mbali majina yote ya kuwashutumu ambayo walikuwa wamebandikwa na Jumuiya ya Wakristo na wakakubali jina la heshima ambalo Biblia Takatifu ilionyesha kuwa lawafaa. Baada ya kusanyiko la Columbus azimio lililopitishwa huko lilipelekwa kwa makundi yote ya wanafunzi waliojiweka wakf na kubatizwa wa Bwana Yesu Kristo duniani pote, katika lugha zao mbalimbali. Makundi yote yenye kupitisha azimio hilo yaliripoti yamefanya hivyo kwenye makao makuu ya Sosaiti. Watu wote mmoja mmoja wenye kushiriki katika tendo hilo walijiweka chini ya wajibu mkubwa sana mbele ya Yehova Mungu. Kushindwa kuishi kulingana na jina hilo jipya kungemaanisha matokeo makali juu yao. Kuliheshimu kungetukuza jina la Mungu.​—Toleo la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Septemba 15,1931, kurasa 278, 279.

18. Je! tendo kama hilo limechukuliwa na Jumuiya ya Wakristo na dini ya Kiyahudi, na kwa hiyo ni nani ambao Mungu ametumia kutimiza Miaka 4:1-4?

18 Je! historia ya kibinadamu tangu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza inaripoti juu ya madhehebu yo yote ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo au dini ya Kiyahudi ikichukua tendo lo lote linalofanana na hilo la Mashahidi wa Yehova? Hapana! Kwa hiyo, ni kupitia Mashahidi hao Yehova Mungu ametimiza unabii ulioandikwa katika Mika 4:1-4. Kwa hiyo, kweli kweli, ibada ya Mungu mmoja wa kweli anayeishi imeimarishwa, “juu ya milima,” maana imeonyeshwa kuwa ni bora sana kuliko namna nyinginezo zote za ibada. Ibada hiyo ni “imara” na kwa hiyo haitaangushwa kamwe kutoka mahali pake palipo juu. Inatukuzwa na Mashahidi wa Yehova, na hivyo, kwa kusema kwa njia ya mfano, ‘inainuliwa juu ya vilima.’

19. Kuinuliwa kwa ibada ya kimungu, kama kwamba ni “juu ya vilima,” kuliifanya ionekane na nani na, kwa kupatana na hayo, ni hotuba gani yenye kushtua iliyotolewa katika Los Angeles, California, mwaka 1918?

19 Kuinuliwa huko kwa ibada ya Mungu wa pekee wa kweli aliye hai, kunakoifanya ionekane kwa mbali sana, kulikusudiwa kuwe kwa faida ya watu wa kutoka kwa mataifa yote na rangi zote za watu. Kwa hiyo, chini ya uongozi wa kimungu, siku ya Jumapili, Februari 24, 1918, katikati ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, aliyekuwa msimamizi wa Sosaiti wakati huo alitoa hotuba iliyokuwa imetangazwa sana katika Los Angeles, California, U.S.A. Kichwa chake cha habari kilikuwa chenye kushtua walakini kilipatana na zilivyokuwa nyakati hizo za maana sana zinapoangaliwa kulingana na maoni ya Biblia. Kichwa cha mazungumzo kilikuwa “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe.” Kichwa hicho kilitegemea fundisho la Biblia kwamba kutakuwako waokokaji wa kibinadamu wa “dhiki kubwa” ambayo itakomesha taratibu hii ya mambo iliyohukumiwa maangamizi. (Ufu. 7:9, 14) Waokokaji hao waliopendelewa wangeingizwa kwenye Kipindi cha Mileani chini ya ufalme wa Kristo. Kupitia serikali hiyo wangeweza kupata uzima wa milele juu ya dunia itakayofanywa kuwa paradiso.

20. Katika mwaka 1923, ni mfano gani wa Yesu uliozungumzwa kwenye kusanyiko la Los Angeles, na ilionyeshwaje namna unahusika?

20 Miaka mitano baadaye kusanyiko lingine lilifanywa katika mji uo huo wa Los Angeles, katika Agosti 18-26, 1923, na siku ya Jumamosi, Agosti 25, msimamizi wa Sosaiti alizungumza juu ya mfano wa Yesu wa Kondoo na mbuzi. Kwa kuwa mfano huo ni sehemu ya unabii wa Yesu juu ya “ishara” inayoonyesha “mwisho wa taratibu ya mambo,” msemaji alionyesha kwamba mfano huo unahusu “siku za mwisho”; alionyesha unahusu kabla ya mileani. Basi, ni nani wanaofananishwa na “kondoo” wanaofanyia mema “ndugu” za kiroho za Mfalme kulingana na mahitaji yao? Ni wale wanaoitwa ‘watu wa nia njema’ ambao watathawabishwa kwa kuokoka uharibifu wa taratibu ya mambo iliyopo na wahifadhiwe waingie kwenye taratibu ya mambo ya Mileani chini ya ufalme wa Kristo! (Tazama toleo la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) Novemba 1, 1923, ukurasa 326; pia lile la Oktoba 15, 1923, ukurasa 307.) “Kondoo” hao wa mfano wa leo ndio wale “watu” wanaoliendea makundi makundi hekalu la kiroho la ibada ya Yehova, ambalo linawakilishwa na mabaki ya “ndugu” za Kristo, Waisraeli wa kiroho.​—Mik. 4:1; Mt. 24:3; 25:31-46.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki