Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 1/15 kur. 19-24
  • ‘Watu wa Mataifa Wataiendea Makundi Makundi’ Ibada Yenye Kutoa Uzima

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Watu wa Mataifa Wataiendea Makundi Makundi’ Ibada Yenye Kutoa Uzima
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • WAOKOKAJI WA HAR-MAGEDONI WASONGA MBELE NA IBADA YA KWELI
  • KINACHOHITAJIWA SASA KATIKATI YA ULIMWENGU MPOTOVU
  • “Roho ya Uhai Itokayo kwa Mungu Ikawaingia”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • “Israeli Wote” Wanaokolewa Wabariki Wanadamu Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Ibada ya Mungu Mmoja wa Kweli Tayari Inaendelea Kuinuliwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 1/15 kur. 19-24

‘Watu wa Mataifa Wataiendea Makundi Makundi’ Ibada Yenye Kutoa Uzima

1, 2. (a) Yohana aliposimulia njozi yake katika Ufunuo 7:9-17, hali ya hekalu katika Yerusalemu ilikuwa nini? (b) “Mkutano mkubwa” ulitambulishwa wakati gani na wapi, na itikio la wahudhuriaji wa kusanyiko lilikuwa nini?

WAKATI kitabu cha mwisho cha Biblia, Ufunuo, kilipoandikwa na mtume Yohana aliyekuwa Mkristo-Myahudi, karibu na mwaka 96 W.K., hekalu la Kiyahudi katika Yerusalemu lilikuwa limekwisha kuharibiwa na askari-jeshi Warumi chini ya Jemadari Tito. Hata hivyo, mtume Yohana anasimulia, katika Ufunuo 7:9-17, “mkutano” usio na hesabu ukitolewa kwa watu wa rangi zote, mataifa yote, mbari zote na lugha zote, nao walionekana wakimtolea Mungu akiwa juu ya kiti chake cha enzi utumishi mtakatifu kwenye nyua za hekalu lake. Bila shaka, hekalu la kiroho la Yehova Mungu ndilo lililokuwa linamaanishwa hapo.

2 Mashahidi wa Yehova pamoja na watu wenye nia njema walikuwa na furaha nyingi sana katika mwaka 1935 wakati wale wa huo “mkutano” usio na hesabu wa watu wa mataifa yote walipotambulishwa kuwa ndio “kondoo” wanaoelezwa katika mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi. (Mt. 25:31-46) Ndiyo, walitambulishwa kuwa ni wale wale kama “kondoo wengine” waliotajwa katika mfano wa Yesu Mchungaji Mwema. (Yohana 10:16; tazama kitabu Kinubi cha Mungu katika Kiingereza, kilichochapishwa mwaka 1921, ukurasa 338, fungu 577; pia, toleo la Mnara wa Mlinzi wa Kiingereza la Oktoba 15, 1923, ukurasa 310, chini ya kichwa kidogo “Jamii Mbili.”) Kutambulishwa kwa washiriki wa “mkutano mkubwa” wa Ufunuo 7:9-17 kulitokea kwenye kusanyiko la Mei 30 mpaka Juni 3, 1935, huko Washington, D.C., U.S.A., kupitia maelezo ya kisasa ya mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi. Siku hiyo (Jumamosi) baada ya mazungumzo hayo kulikuwako ubatizo wa wahudhuriaji 840 walioongozwa na ufahamu wao mpya juu ya mambo kulingana na maelezo ya mfano wa Yesu.

3. Mika 4:2 ilianza kutimizwa wakati gani, na wenye kushiriki utimizo huo walikuwa wakitazamia Yerusalemu gani?

3 “Kondoo wengine” waliojiweka wakf na kubatizwa wanashiriki pamoja na ndugu za kiroho za Mfalme Yesu Kristo katika kuhubiri “habari njema hizi za ufalme” kila mahali, “katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14, NW) Kwa njia hiyo Mika 4:2 ilianza kutimizwa: “Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova], na nyumbani kwa Mungu wa Yakobo; naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake; kwa maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno la [Yehova] litatoka Yerusalemu.” Si kwa Yerusalemu wa kidunia, ambao wakati huo ulikuwa umetwaliwa na majeshi ya Uingereza, bali kwa Yerusalemu Mpya ukiwa juu ya Mlima Sayuni wa kimbinguni ndiko “kondoo wengine” wa “mkutano mkubwa” walitazamia “sheria” ambayo msingi wake ni Biblia na kutazamia “neno la [Yehova]” kupitia mashahidi wake waliotiwa mafuta, Waisraeli wa kiroho.

4. Mika 4:3, 4 ilianza kutimizwa juu ya nani wakati huo?

4 Utimizo wa maneno ya Mika 4:3, 4 ulianza kati ya wenye mfano wa kondoo wa “mkutano mkubwa” wa mataifa yote wala si katikati ya mataifa ya kilimwengu yaliyokuwa yakilundika zana za vita kwa ajili ya Vita ya Ulimwengu ya Pili, maneno hayo yakiwa yanasema hivi: “Naye [Yehova] atafanya hukumu kati ya watu wa kabila nyingi, naye atawakemea mataifa wenye nguvu walio mbali; nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe. Bali wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu; kwa kuwa kinywa cha [Yehova] wa majeshi kimesema hivi.”

5. Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, walichukua msimamo juu ya jambo gani, na; kwa kusema kwa njia ya mfano, wamekuwa wakikaa kwa namna gani?

5 Bila woga, pasipo kukubali mtu ye yote wa ulimwengu huu awafanye watetemeke kwa woga, hata baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili kuanzwa katika Septemba 1, 1939, Mashahidi hao wametangaza waziwazi na kujulisha waziwazi hali yao ya kutokuwamo kuhusiana na mataifa yote yaliyokuwa yakishiriki katika vita vyenye ukatili. (Tazama toleo la Mnara wa Mlinzi katika Kiingereza la Novemba 1, 1939, lenye makala kuu yenye kichwa “Kutokuwamo.”) Tangu wakati huo wameendelea kushikilia msimamo huo wa kutokuwamo. Katika visa vingi, hiyo imefanya wafungiwe kwenye kambi za mateso, au katika magereza, au hata kuuawa kwa kuwa wao hawatukuzi mataifa. Wanakataa kuwa sehemu ya ulimwengu, kama vile tu Yesu Kristo alivyokataa. Kwa kufaa, basi, lazima Mashahidi hao watazamiwe kuwa wenye amani ndani ya makundi yao, wakikaa pamoja kama ndugu na ndugu. (Zab. 133) Kwa kusema kwa mfano, kila mmoja wao anaketi “chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake,” kwa usalama, kama vile walivyokaa Waisraeli wakati wa utawala wa amani wa miaka 40 wa Mfalme Solomoni, mwana wa Daudi. (1 Fal. 4:25) Wakati wa huu “mwisho wa taratibu ya mambo,” kwa amani wanahubiri “habari njema hizi za ufalme . . . katika dunia yote inayokaliwa na watu.”​—Mt. 24:3, 14, NW.

WAOKOKAJI WA HAR-MAGEDONI WASONGA MBELE NA IBADA YA KWELI

6, 7. Toleo la Mnara wa Mlinzi la Desemba 15, 1928, lilisema nini kuhusu Mika 5:6-9, juu ya namna hayo yangetimizwa?

6 Kwa hiyo kati ya watu wa mataifa yote Mashahidi ni kitu chenye kuburudisha. Hivyo ni kama tu ilivyotabiriwa katika Mika 5:6-9: “Naye [Yehova] atatuokoa na Mwashuri [milki ya ulimwengu ya Ashuru], atakapoingia katika nchi yetu, na kukanyaga ndani ya mipaka yetu. Na hayo mabaki ya Yakobo yatakuwa kati ya kabila nyingi mfano wa umande utokao kwa [Yehova], mfano wa manyunyu katika manyasi; yasiyomngojea mtu, wala kuwakawilia wanadamu. Na hayo mabaki ya Yakobo yatakuwa kati ya mataifa, kati ya kabila nyingi, mfano wa simba kati ya wanyama wa msituni, kama mwana-simba kati ya makundi ya kondoo, ambaye, akiwa anapita katikati, hukanyaga-kanyaga na kurarua-rurua, wala hakuna wa kuokoa. Mkono wako na uinuliwe juu ya adui zako, na adui zako wote wakatiliwe mbali.”

7 Ikitaja jambo hilo, makala “Mtawala kutoka Bethlehemu,” katika toleo la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Desemba 15, 1928, ilisema hivi:

Huo unaweza kufahamika kuwa wonyesho wa kwamba wengine wa mabaki watakuwa duniani hata baada ya Har–Magedoni kupiganwa na kisha watakuwa na kazi ya kufanya katika jina la Bwana na ifanywe kwa sifa na utukufu wake. Hao watu, wakiwa wamekwisha kuiokoka ile taabu kubwa na yenye kuogopesha sana, sasa hawatatumainia tena wanadamu wawasaidie wala kuwaangalia wana wa watu wawaletee msaada na faraja bali watamgeukia Bwana na kulisikia Neno lake kwa furaha. Viumbe wengine watakuwa na pendeleo, wakiwa mawakili na wajumbe wa Bwana, wa kushuhudia ujumbe huo wa amani kwa watu.

Mabaki ya Bwana, kulingana na unabii huu, watasonga mbele na kushinda kwa nguvu za Yehova. Simba ndiye mfalme kati ya wanyama wa mwituni, na hakuna ye yote anayeweza kusimama mbele yake. Makundi ya kondoo yanakuwa bila uwezo kukabili simba mchanga mwenye nguvu aliye kati yao. Ndivyo mabaki waaminifu wa Mungu wanavyosimuliwa na nabii huyo. Wao watakuwa kati ya mataifa ya watu wengi wakiwa wenye nguvu na wenye kutenda kwa bidii katika jina la Bwana ili kusaidia wale wanaotaka msaada na kuonyesha wazi njia ya Mungu ya kuharibu wale wanaopinga.​—Ukurasa 376, mafungu 35, 36.

8. Likizungumza jambo hilo zaidi, toleo la Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 1929, liliendelea kusema nini?

8 Likiendelea kuzungumza zaidi juu ya jambo hilo, toleo la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Machi 15, 1929, ukurasa wa 88, fungu la 41, liliendelea kusema hivi:

Hata jamii ya kundi kubwa lazima iongozwe kwenye chemchemi za maji ya uzima. (Ufu. 7:17) Huenda Bwana akatumia mabaki wawasaidie kwa njia hiyo. Kuna wengine wengi watakaonyenyekezwa na Har–Magedoni, nao watakuwa na nia ya kusikia. Baada ya Har–Magedoni huenda wengine wa mabaki wakatumiwa na Bwana kutoa ushuhuda na kusaidia wale wanaohitaji kufundishwa, na huenda wakafanya hilo kabla ya kutwaliwa kwa halisi kwenye nyua za utukufu wa milele. Ni hakika kwamba kazi ya mabaki sasa ni kutangaza habari njema wakiwa ndio mashahidi waliowekwa kwa kufaa na Mungu.

9. Hata hivyo, je! imekuwa lazima mabaki wangojee mpaka baada ya Yehova kupata ushindi kwenye Har–Magedoni ndipo wawe kama “umande” na kama “mwana-simba” kuhusiana na watu wa mataifa?

9 Hata hivyo, haijapata kuwa lazima mabaki ya Israeli wa kiroho wangojee mpaka baada ya “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye Har–Magedoni ili wawe kama “umande” wa kuburudisha watu wanaotafuta kumwabudu “Mungu wa Yakobo” kwenye hekalu lake la kiroho. (Ufu. 16:14, 16) Hapana, haijapata kuwa lazima mabaki wangojee mpaka baada ya Yehova kupata ushindi kwenye upeo wa vita hiyo ya mwisho ndipo wawe kama “mwana-simba” kati ya mataifa. Kama vile nabii Isaya alipokuwa akiona njozi yake ya Yehova kwenye hekalu Lake, wamekubali ulizo la Yehova, “Ni nani atakayekwenda kwa ajili yetu?” Mara moja baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza kumalizika mwaka 1918, walisema hivi: “Mimi hapa, nitume mimi.” (Isa. 6:8) Kwa kutii amri ya kimungu, ‘Enendeni,’ wamekwenda kwa watu wa mataifa yote.

10. Mabaki wamekuwa kama simba kati ya mataifa kwa kutangaza ujumbe gani wa Yehova?

10 Kwa njia hiyo wamehubiri ujumbe wa ufalme uliosimamishwa utakaobariki jamii ya “kondoo” na ambao utaharibu jamii ya “mbuzi.” (Mt. 25:31-46) Wakati wa kutangaza “siku ya kisasi cha Mungu wetu” wamekuwa kama simba kwa ujasiri, wakishauri adui za ufalme wa Mungu uliosimamishwa kwamba wataharibiwa kwenye Har–Magedoni na Mfalme Shujaa wa Vita wa Yehova, Yesu Kristo, “Simba aliye wa kabila ya Yuda.”​—Isa. 61:1-3 Ufu. 5:5.

11. Ni kwa sababu gani “mkono” wa mabaki waliotiwa mafuta umeendelea kuwa juu ya adui zao, na matokeo yake yamekuwa nini kwa habari ya matawi ya Sosaiti na hesabu ya “kondoo” waliokusanywa?

11 Kwa njia hiyo “mkono” wao wakuyatenda kwa bidii yanayosemwa neno la Mungu umekuwa “juu” kwa kuwashinda adui zote wanaojitahidi kuzuia ujumbe wa Ufalme. Onyo limetolewa juu ya adui hao kuhusu kushindwa na kuharibiwa kwao kunakokuja kwenye Har–Magedoni, wakati ambapo ‘watakatiliwa mbali’ milele. (Mik. 5:9) Kwa upande mwingine wa habari hiyo, watangazaji hao waliotiwa mafuta wa ufalme wa Mungu wamekuwa kama “umande” wenye kuburudisha kwa watu wenye mfano wa kondoo ambao wamejisikia kama “manyasi” yaliyokauka na kuwa makavu. Kwa sababu Yehova ameshikilia mkono wao, umeendelea kuinuka juu ya adui zao kwa miaka yote hii tangu kuchapishwa kwa makala hizo zilizotangulia kutajwa katika matoleo ya Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) ya 1928 na 1929. Kuonyesha ushuhuda wa jambo hilo, ni kwamba matawi ya nchi za ugenini ya Sosaiti yameongezeka katika hesabu kufika 97, yote yakitumiwa na “mabaki” waliotiwa mafuta. Vilevile “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wa Mchungaji Mwema, Yesu Kristo, umeendelea kuongezeka mpaka sasa. Ufunuo 7:9-17 hausemi mwishowe hesabu yao itakuwa nini.

12. Kazi ya mabaki waliotiwa mafuta pamoja na wenzi wao wenye mfano wa kondoo itaendelea mpaka kitu gani kiachiliwe, na kwa sababu gani?

12 Lazima utendaji mbalimbali wa mabaki waliotiwa mafuta pamoja na wenzi wao wenye mfano wa “kondoo” uendelee mpaka wale “malaika wanne” wanaosimama kwenye pembe nne za dunia waamriwe waachilie pepo zile nne ambazo zitatokeza ‘dhiki kubwa.’ Wakati wa dhiki hiyo wale watakaoendelea kuukataa ujumbe wa Ufalme ‘watakatiliwa mbali,’ waharibiwe, Kufika wakati huo hesabu ya mwisho inayohitajiwa kukamilisha warithi-washirika 144,000 wa Yesu Kristo itakuwa imekwisha ‘kutiwa muhuri’ kwenye vipaji vya nyuso zao. (Ufu. 7:1-8, 14) Wenzi wao wenye mfano wa kondoo ambao wametoka katika mataifa yote kusudi waitafute “nyumba” ya kiroho ya Yehova na ambao wamejiweka wakf ‘wakwende katika mapito yake’ watalindwa wakati wa hiyo ‘dhiki kubwa.’ (Mik. 4:1-4) Kwa hiyo wataokoka wakiwa duniani na kuingia kwenye utawala wa miaka elfu moja wa Yesu Kristo pamoja na warithi-washirika wake waliotukuzwa.

13. Ni wangapi kati ya mabaki waliotiwa mafuta watakaookoka Har–Magedoni, nao wataendelea kuwa kama nini kati ya waokokaji wenzao?

13 Hatujui ni wangapi kati ya mabaki waliotiwa mafuta wa warithi-washirika wa Kristo watakaookoka pamoja nao “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye Har–Magedoni, wala hatujui wataendelea kukaa nao muda gani baada ya hapo. Walakini hata iwe ni kwa wakati gani, wataendelea kuwa kama “umande” unaoburudisha kwa “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine.” Wao hawatatatiza mabaki kwa kuwa tayari “kondoo wengine” wamekwisha kufanywa kuwa “kundi moja” pamoja na mabaki walio katika “zizi hili” ambamo “kundi dogo” wamewekwa ndani yake na Mchungaji Mwema. (Yohana 10:16; Luka 12:32) Kwa hiyo si katikati ya “mkutano mkubwa” utakaookoka kwamba mabaki watatenda kama simba mkali katikati ya kondoo wasio na ulinzi.

14. Katika pindi hiyo, Sayuni wa kimbinguni utakuwa kama mnyama gani anayekanyaga-kanyaga vitu, nayo “pembe” itakuwa ngumu au yenye nguvu kadiri gani kuelekea adui?

14 Mabaki hawatashiriki kijeshi kamwe katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye Har–Magedoni. Kama vile Waisraeli katika siku za Mfalme Yehoshafati, watasimama tu na kuona wokovu wa Yehova kupitia “Simba aliye wa kabila ya Yuda,” Yesu Kristo. (2 Nya. 20:17) Katika pindi hiyo Yehova Mungu Mwenye Nguvu Zote atafanya “pembe” ya Sayuni wa kimbinguni iwe kama chuma na kama fahali, atakanyaga-kanyaga adui za Mungu kama kwamba ni juu ya sakafu ya kupuria. Hakika Sayuni huo “utaponda-ponda mataifa mengi” na kuyaharibu. (Mik. 4:13) Cho chote kitakachobaki baada ya kuharibiwa kwao kitakuwa cha kutumiwa na waokokaji wa Har–Magedoni.

KINACHOHITAJIWA SASA KATIKATI YA ULIMWENGU MPOTOVU

15. Je! mtu akitimiza takwa la Mungu lililoandikwa katika Mika 6:8 anaweza kubaki katika Jumuiya ya Wakristo? Na kwa sababu gani?

15 Mika 7:2, 6 inasema kuhusiana na Jumuiya ya Wakristo, mfano wa kisasa wa Israeli isiyo na ushikamanifu: “Mtu [mshikamanifu] ametoweka, asionekane katika nchi, wala hapana mtu mwenye adili katika wanadamu, . . . adui za mtu ni watu wa nyumbani mwake mwenyewe.” Ili hata Wakristo wa kujidai ambao ni sehemu ya Jumuiya ya Wakristo ya kisasa waokoke matokeo ya hali hii iliyopotoka, wanapaswa kufanya nini? Je watoe sadaka za mali wakati wangali sehemu ya tengenezo hilo la kidini lililopotoka? Hapana! Mahali pake, lazima watende kupatana na yale yanayosemwa katika Mika 6:8: “Ee mwanadamu, yeye amekuonyesha yaliyo mema; na [Yehova] anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!” Ili kutimiza takwa hilo la kimungu lazima mtu atoke hata ndani ya Jumuiya ya Wakristo, kwa kuwa madai yake ya kusema ni ya Kikristo ni ya uongo. Upotovu wake wa kidini na wa kiadili unathibitisha jambo hilo. Mtu akikaa ndani yake na kujaribu kuibadili iwe nzuri hatafanikiwa. Imehukumiwa maangamizi na Mungu yule ambaye inadai kumtumikia.

16, 17. (a) Mtu anapaswa kujiunga na makundi makundi ya watu gani leo, naye anapaswa kufanya uchaugzi gani kwa habari ya uungu? (b) Kwa kuimba wimbo wa Musa na wa Mwana-Kondoo, mtu huyo anatukuza mungu gani?

16 Nyumba ya ibada ya Jumuiya ya Wakristo itafagiliwa mbali kama vile tu hekalu huko Yerusalemu katika siku za Mika lilivyoharibiwa katika mwaka 607 K.W.K. Kwa hiyo, ili “kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako,” mtu aliye katika Jumuiya ya Wakristo, sawa na mtu aliye katika milki yote ya ulimwengu ya dini ya uongo, lazima ajiunge na watu wa mataifa yote ambao sasa wanauendea makundi makundi ‘mlima wa Yehova, na nyumba ya Mungu wa Yakobo.’ Lazima mtu huyo akubali mafundisho ya Yehova kutoka Sayuni wa kimbinguni na lazima atembee katika njia ile ambayo Yeye anaionyesha sasa. Hiyo haimaanishi kuwa mwongofu wa Kiyahudi. Inamaanisha kuwa mwanafunzi wa Mwana-mzaliwa-pekee wa Yehova na kuwa namna ya shahidi ambaye yeye alikuwa. Ati? Kuwa shahidi aliyejiweka wakf na kubatizwa wa Yehova? Ndiyo! Inamaanisha mtu afanye uchaguzi ulioandikwa katika Mika 4:5: “Kwa maana mataifa yote watakwenda, kila moja kwa jina la mungu wake, na sisi tutakwenda kwa jina la [Yehova], Mungu wetu, milele na milele.” Lazima mtu ajiunge kuuimba “wimbo wa Musa, mtumwa wa Mungu, na wimbo wa Mwana-Kondoo,” akisema:

17 “Ni makuu, na ya ajabu, matendo yako, Ee [Yehova] Mungu Mwenyezi; ni za haki, na za kweli, njia zako, Ee Mfalme wa mataifa. Ni nani asiyekucha, Ee [Yehova], na kulitukuza jina lako? kwa kuwa wewe peke yako u [mshikamanifu]; kwa maana mataifa yote watakuja na kusujudu mbele zako! kwa kuwa matendo yako ya haki yamekwisha kufunuliwa.”​—Ufu. 15:3, 4.

18. Sababu gani ulizo la kumalizia na jibu la Mika yanafaa kuhusiana na Yehova?

18 Kwa ushikamanifu, Yehova atatimiza ahadi zake zote alizotuahidi, kama ile aliyomwahidi mzee wa ukoo Abrahamu na mjukuu wake, Yakobo, au Israeli, kufikia hatua ya kubariki jamaa zote na mataifa yote ya dunia kupitia Mwanawe, Yesu Kristo. Kwa kufanya hivyo, Yehova mwenyewe atatenda akiwa ndiye Abrahamu aliyefananishwa, akiwa ndiye Abrahamu Mkuu Zaidi. Kwa sababu ya ushikamanifu wake usioyumba-yumba kwetu, mpaka sasa hata sisi tunaweza kutumia, maneno ya kumalizia ya Mika na kusema hivi:

“Ni nani aliye Mungu kama wewe, mwenye kusamehe uovu, na kuliachilia kosa la watu wa urithi wake waliosalia? hashiki hasira yake milele, kwa maana yeye hufurahia rehema. Atarejea na kutuhurumia; atayakanyaga maovu yetu; nawe utazitupa dhambi zao zote katika vilindi vya bahari. Wewe utamtimilizia Yakobo kweli yako, na Ibrahimu rehema zako, ulizowaapia baba zetu tangu siku za kale.​—Mik. 7:18-20.

19. Ni nani Mungu asiyelinganika, na ni ibada ya nani tutakayoiinua juu kabisa hata “siku za mwisho” zipite?

19 Hakuna Mungu anayelingana na Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu, Mungu na Baba ya Bwana yetu Yesu Kristo. Na tuiinue ibada yake safi, sasa, “katika siku za mwisho,” na hata milele.​—Kutoka The Watchtower July 15, 1981.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Lazima ‘watu waiendee makundi makundi’ ibada yenye kutoa uzima

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki