Kufichwa Katika Siku ya Hasira ya Yehova
“Mtafuteni [Yehova], . . . Itafuteni haki, utafuteni [upole]; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya [Yehova].”—Sef. 2:3.
1. Ni kwa sababu gani jina pamoja na unabii wa Sefania unapendeza leo?
‘MFICHWA wa Yehova’—hilo ndilo wazo linalotolewa na jina la nabii wa Mungu, Sefania, jina ambalo linamaanisha “Yehova ameficha.” Je! ni tamaa yako kufichwa na Yehova? Inapasa kuwa, kwa maana ulimwengu wa leo unatumbukia zaidi na zaidi katika taabu na katika hali ya kutokuwa na tumaini. Mungu mwenye haki, Yehova, hataruhusu kwa muda mrefu hali hizo ziendelee. Siku yake ya Har–Magedoni imekaribia. Sisi sote twapaswa kupendezwa sana na unabii wa Sefania kwa maana unasema mengi juu ya siku hiyo ya uamuzi. Unaonyesha namna tunavyoweza kupata mahali pa kukimbilia, ili ‘tufichwe na Yehova.’
2. Kwa sababu gani nguvu ya unabii huo si ndogo?
2 Sefania alitabiri wakati wa sehemu ya kwanza ya utawala wa Mfalme Yosia wa Yuda, ulioanza mwaka 659 K.W.K., na, basi, kama miaka 50 kabla Yehova hajafanya Yuda na Yerusalemu ziwe mahame. Kwa ajili ya ufupi wa unabii wake, mara nyingi Sefania hutajwa kuwa mmoja wa “Manabii Wadogo,” walakini nguvu ya unabii wake si ndogo. Katika siku za Sefania, ulieleza ujumbe wa kimungu ambao haungeweza kupuzwa. Vivyo hivyo, unaeleza juu ya karne yetu ya 20 ukiwa na onyo lenye nguvu nyingi linalopasa kutiiwa na watu wote wanaotumaini kupata usalama wakati wa siku inayokaribia ya hasira yenye kuwaka ya Yehova. Ni sehemu ya “neno la unabii” lenye nguvu la Yehova ambalo mtume Petro anafananisha na “taa ing’aayo mahali penye giza.”—2 Pet. 1:19; tazama pia Warumi 15:4.
3. (a) Kutabiri kwa Sefania kuliletaje faida ya mara moja? (b) Kwa sababu gani haingedumu?
3 Inaonekana kwamba Sefania, alikuwa mjukuu wa Mfalme Hezekia aliyekuwa mwaminifu. Akiwa nabii mwenye damu ya kifalme, angepaswa kuwa mjasiri kweli kweli ili atangaze hukumu zenye kuwaka za Yehova juu ya wakuu wa Yuda. (Sef. 1:1, 8) Kwa wazi kutabiri kwake kulikuwa na matokeo mazuri katika siku za ujana za Mfalme Yosia, aliyesafisha nchi kwa kuondoa dini ya uongo na akaja kujulikana kwa ajili ya “matendo yake mema, sawasawa na yote yaliyoandikwa katika torati ya [Yehova].” (2 Nya. 34:3, 14, 19, 33; 35:26) Kwa sababu hiyo, kutekelezwa kwa hukumu za Yehova kulikuwako kwa muda. Hata hivyo, mwendo wa haki wa Yosia haukufagilia mbali uovu uliokuwa umewameza watu, wala haukuondoa dhambi za babu yake, Manase, aliyekuwa ‘ameujaza Yerusalemu damu zisizo na hatia.’ (2 Fal. 24:3, 4) Siku ya Yehova ya mapambano ilikuwa imekaribia!
‘NENO LA YEHOVA’
4. (a) Unabii huo unaanza kwa usemi gani wenye kukata maneno? (b) Unatambulishaje chanzo cha taabu ya Yuda, na namna gani?
4 Kupitia Sefania, Yehova alionyesha wazi kwamba angekomesha uovu kabisa. Unabii huo unaanza kwa maneno haya:
“Nitavikomesha kabisa vitu vyote, visionekane juu ya uso wa nchi, asema [Yehova].”
Huko kungekuwa ni kumaliza, kung’oa vitu vyote vyenye kuchukiza machoni pa Yehova. “Neno” hilo lilitaja jambo hilo wazi kwa kuonyesha kitu kilichotokeza taabu za Yuda—dini ya uongo! Kwa maana Yehova aliendelea kusema hivi:
“Nitaunyosha mkono wangu juu ya Yuda na juu ya watu wote wakaao Yerusalemu; nami nitayakatilia mbali mabaki ya Baali, yasionekane mahali hapa, na hilo jina la [makuhani hao wa mungu wa kigeni] pamoja na makuhani; na wale walisujudiao jeshi la mbinguni juu ya dari za nyumba; na hao waabuduo, waapao kwa [Yehova] na kuapa pia kwa Malkamu; na hao waliorudi nyuma na kuacha kumfuata [Yehova]; na hao wasiomfuata [Yehova] wala kumwulizia.”—Sef. 1:2-6.
5. (a) Kwa sababu gani ibada ya Baali haikuwa na mahali panapofaa kati ya watu wa Mungu? (b) Ilitia mazoea gani yenye kuchukiza?
5 Ulikuwa uovu kama nini! Wayudea hao walikuwa wameiacha ibada safi ya Yehova ili waifuate ibada ya Baali ya mataifa yaliyokuwa jirani. Ibada ya Baali—pamoja na kutolewa kwa dhabihu za kibinadamu, sherehe zake za kimalaya, ibada yake ya sanamu zisizoweza kusema na sherehe zake za sala za kuomba ufanisi wa mali—haikuwa na mahali panapofaa kati ya waabudu wa Yehova. (Hes. 25:1-5; Yer. 7:30, 31; 11-17; 19:3-5) Dini ya uongo ilikuwa imewaingiza katika namna zote za mazoea maovu. Makuhani wa Yuda walikuwa wamevunja Amri ya Kwanza kwa kushirikiana na ‘makuhani wa mungu wa kigeni.’ (Kut. 20:2, 3) Wakiufuata mfano mbaya wa Mfalme Manase, waliliabudu “jeshi la mbinguni,” na wakatafuta uongozi kwa wachawi. (2 Nya. 33:1-6) Kwa kupatana na wazo la uongo kwamba ‘kuna wema katika dini zote,’ walikuwa wakilinganisha mungu-sanamu Malkamu na Yehova. Kwa sababu ya kumwacha Mungu aliye hai, walikuwa wamesitawisha ‘moyo mbovu unaokosa imani.’—Ebr. 3:12, NW.
6. Ni ufanani gani mbalimbali wenye kutokeza tunaoona leo kati ya mazoea katika Yuda na katika Jumuiya ya Wakristo leo?
6 Je! kuna tofauti katika Jumuiya ya Wakristo leo? Mataifa ya Jumuiya ya Wakristo yangali yana hatia ya damu nyingi sana, kwa sababu ya mamilioni ya uhai uliotolewa dhabihu juu ya madhabahu ya vita wakati wa karne hii. Viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo katika pande zote waliunga mkono vita hivyo, na hatia yao ya damu ingalipo. (Linganisha Yeremia 2:34, 35) Kama vile Wayudea wale walivyoshiriki katika namna zote za ngono zilizopotoka, ndivyo tunavyopata watu wa Jumuiya ya Wakristo leo wakishiriki katika ngono kabla ya ndoa, ngono za ovyo-ovyo, kubadilishana wake, talaka, kulalana kwa watu wa namna moja na kadhalika, huku wengi wa viongozi wa kidini wakijifanya hawayaoni mambo hayo au wakiyaruhusu mazoea hayo. Ni tofauti kama nini na kanuni Biblia!—1 Kor. 6:9, 10; Ebr. 13:4.
7. (a) Leo, tunaona kulingana kupi kwa uchawi na tangamano la imani lililozoewa na Wayudea waasi-imani? (b) Kwa habari hii, ni shauri gani la wakati wake linalopatikana katika neno la Mungu?
7 Unajimu, ubashiri, uchawi—mambo hayo pia yanapatikana kati ya Wakristo wa kujidai. Kwa sababu ya kutoa kisababu kwamba ‘dini zote zinaongoza kwenye lengo lile lile,’ kuna zoea lenye kuenea sana la tangamano la imani katika Jumuiya ya Wakristo leo. Ushirikina wa dini ya uongo unachanganywa pamoja na Biblia. Kwa hiyo, mahali pa kutii amri ya Yesu ya kuadhimisha mara moja kila mwaka Ukumbusho wa kifo chake, Jumuiya ya Wakristo inakazia Easter, iliyoitwa hivyo kufuatia mungu wa kike wa ngono, Ashtoreth (Kigiriki, Astarte), na kuingiza sherehe na ishara za uwezo wa kuzaa, kama vile sungura na mayai ya Easter. Ye yote ambaye amehusika katika mazoea hayo angefanya vema kufuata shauri zuri la 1 Samweli 7:3: “Ikiwa mnamrudia [Yehova] kwa mioyo yenu yote, basi, iondoleeni mbali miungu migeni; nayo Maashtorethi [sanamu] yatoke kwenu; naye atawaokoa.” Ndiyo, kumheshimu Yehova, Neno lake na matakwa yake ni mambo ya lazima kwetu iwapo tunatamani kuwa kati ya wale wanaoalikwa washiriki katika siku yake ya kutetewa. Ni kama ambavyo Sefania mwenyewe anavyosema:
“Nyamaza kimya mbele za Bwana [Yehova]; kwa maana siku ya [Yehova] i karibu; kwa kuwa [Yehova] ameweka tayari dhabihu amewatakasa wageni wake.”—Sef. 1:7.
8. ‘Neno la Yehova’ linaonya juu ya kuwaza gani kwa hatari?
8 Katika siku za Sefania, Yehova aliwachunguza kikamilifu waabudu wake wa kujidai. Kwa hiyo ‘neno la Yehova’ linaendelea kusema hivi:
“Kisha itakuwa wakati ule, nitauchunguza Yerusalemu kwa taa; nami nitawaadhibu watu walioganda juu ya sira [machujo] zao; wasemao katika mioyo yao, [Yehova] hatatenda mema wala hatatenda mabaya.” (Sef. 1:1, 12)
Watu hao wenye kujifikiria wenyewe tu walikuwa wametosheka na hali ya mambo iliyokuwapo. Hawakutaka mtu ye yote akoroge machujo yaliyokuwamo ndani ya visanduku vyao vya divai. Walikuwa kama Jumuiya ya Wakristo isiyo na imani leo, na vilevile kama wengine ambao wameacha kumwabudu Yehova, na kusema, Kuna uthibitisho gani kwamba kweli kweli hizi ndizo “siku za mwisho”?’ Kuwaza kwa namna hiyo kulitokeza msiba katika siku za Sefania, na kunaweza kuwa hatari zaidi katika siku zetu, tunapoukabili mwisho wa mfumo wote wa mambo wa ulimwengu.—2 Pet. 3:3, 4, 10.
9. Kama vile katika siku za Yuda, kwa sababu gani ni jambo la maana sana sasa kusitawisha maoni ya kiroho mahali pa maoni ya kimwili?
9 Kuhusu watu hao wasio na imani wenye kufuatia mali, Yehova anaendelea kusema hivi:
“Na huo utajiri wao utakuwa mateka, na nyumba zao zitakuwa ukiwa; naam, watajenga nyumba, lakini hawatakaa ndani yake; nao watapanda mizabibu, lakini hawatakunywa divai yake.” (Sef. 1:13)
Mali za ulimwengu hazifai kitu katika siku ya hukumu ya kimungu! Mahali pa kutafuta mali hizo leo, inafaa zaidi kama nini kusitawisha maoni ya Kimaandiko juu ya maisha, na kwa vijana kujitayarisha kwa ajili ya utumishi wa wakati wote kwa Yehova! Sikuzote wenye furaha ni wale wanaochagua ‘hazina mbinguni’ mahali pa ‘kuweka hazina duniani’!—Mt. 6:19-21; Mhu. 12:1; 1 Tim. 6:6-8.
‘SIKU ILIYO KUU YA YEHOVA I KARIBU’
10, 11. Yehova ‘anaharakisha’ siku yake kuu namna gani na kwa sababu gani?
10 Halafu, Bwana Mwenye Enzi Kuu mwenyewe anatuhakikishia hivi:
“Hiyo siku ya [Yehova] iliyo kuu i karibu; i karibu, nayo inafanya haraka.”—Sef. 1:7, 14.
11 Mtu ye yote asidhani kwamba wakati wa Mungu kuhukumu ulimwengu huu mwovu u mbali sana katika wakati ujao. Leo, kuna tisho la uhai wote wa kibinadamu duniani kuharibiwa, walakini hilo ni jambo ambalo Yehova hataruhusu! Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ndiye atakayekomesha wazimu huu wa kizazi hiki chenye silaha za nyukilia, wala si wanadamu wenye kufikiria mambo ya kisiasa. Yeye ‘ataiharakisha’ siku yake ya Har–Magedoni. ‘Mtu hodari’ ye yote atakayejaribu kuzuia hukumu hiyo isitekelezwe hana budi kulia kwa uchungu, kwa maana Yehova mwenyewe anatangaza hivi:
“Siku ile ni siku ya ghadhabu, siku ya fadhaa na dhiki, siku ya uharibifu na ukiwa, siku ya giza na utusitusi, siku ya mawingu na giza kuu, siku ya tarumbeta na ya kamsa [ishara ya hatari], juu ya miji yenye maboma, juu ya buruji [minara ya pembeni] zilizo ndefu sana.”—Sef. 1:15, 16.
12. Kwa sababu gani tunaweza kuwa na furaha kwamba kutakuwako uharibifu wenye kuchagua katika siku hiyo?
12 Ngome za ulimwengu huu wa kijeshi, hata kama zingeweza kuzuia mizinga ya nyukilia, hazitafaa kitu juu ya silaha za zana za kimbinguni za Yehova. Zaidi ya hayo, utakuwa ni uharibifu wenye kuchagua, kwa kupatana na maneno ya kiunabii ya Daudi: “[Yehova] huwahifadhi wote wampendao, na wote wasio haki atawaangamiza.” (Zab. 145:20) Itakuwa siku mbaya sana ya kuhukumiwa, hakika, kwa wale ambao hawakunyamaza kwa heshima mbele za Yehova. Kwa maana kupitia Sefania yeye anaendelea kusema hivi:
“Nami nitawaletea wanadamu dhiki, hata watakwenda kama vipofu, kwa sababu wamemtenda [Yehova] dhambi; na damu yao itamwagwa kama mavumbi, na nyama yao kama mavi.”—Sef. 1:17.
13. Ni raslimali gani ambazo hazitafaa kitu katika siku hiyo ya ghadhabu?
13 Je! akiba kubwa ya fedha katika banki, hata ikiwa imewekwa katika nchi “isiyofungamana na upande wo wote,” au dhahabu iliyolundikwa, au raslimali nyingi (mali), au maficho yaliyo chini ya ardhi yatafaa katika siku hiyo? Wapi! Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mwenyewe anaonyesha jambo hilo wazi, kwa kusema hivi:
“Fedha yao wala dhahabu yao havitaweza kuwaokoa katika siku ile ya ghadhabu ya [Yehova]; bali nchi yote pia itateketezwa kwa moto wa wivu wake; maana atawakomesha watu wote wakaao katika nchi.” (Sef. 1:18)
Katika hii siku ya mwisho ya uamuzi, ‘dunia yote’ inatiwa katika kutekelezwa kwa mwisho kwa hukumu ya Mungu. Walakini kuna njia ya kuokokea! Ni njia gani hiyo?
“JIKUSANYENI”
14. Ni nini ushahidi wa kushindwa kutii kusihi kwa Sefania 2:1 (a) kwa Yuda? (b) kwa Jumuiya ya Wakristo?
14 Sasa nabii mwenyewe wa Mungu anawasihi wale ambao wangeokoka, kama kwamba ni kuwasihi mara ya mwisho, na kusema:
“Jikusanyeni, naam, jikusanyeni, Ee taifa lisilo na haya.” (Sef. 2:1)
Walakini je! Yuda ikiwa kama taifa ilikubali kwa njia nzuri kusihi huko? Kuangamizwa kwa taifa hilo katika moto na Yehova katika mwaka 607 K.W.K. kunaonyesha hawakufanya hivyo. Walakini kulikuwa watu mmoja mmoja—Wayudea na wengine, kutia Yeremia, Ebed-Meleki na nyumba ya Yonadabu—waliookoka kwa sababu ya kulitii neno la Yehova. (Yer. 39:11, 12, 16-18; 35:18, 19) Hali inafanana na hiyo leo. Bila haya, Jumuiya ya Wakristo imepinga ujumbe wa Ufalme ambao Mashahidi wa Yehova wamehubiri katika makao yayo yote. Imeukataa ufalme wa Mungu kupitia Kristo Yesu kuwa tumaini pekee la mataifa, na mahali pake ikafanya kitu kilichotengenezwa na watu kinachojulikana leo kuwa Umoja wa Mataifa uwe tumaini pekee la mataifa. Kukusanya ko kote ambako Jumuiya ya Wakristo inafanya kutaangamizwa katika Har–Magedoni.—Zab. 2:2, 3; Ufu. 16:13-16.
15. Ni kukusanywa gani kwingine kumekuwa kukiendelea katika siku za kisasa?
15 Hata hivyo, kukusanya kwingine kumekuwa kukiendelea katika “siku za mwisho,” ambazo sasa tumo ndani yazo. Kwanza, kumekuwako kukusanywa, kwa sehemu kubwa kutoka katika Jumuiya ya Wakristo, kwa Wakristo wa kweli waliotiwa mafuta. Huko kumefuatwa na kukusanywa kutoka katika “kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha,” kwa “mkutano mkubwa” usio na hesabu, ili waokoke dhiki ile inayokaribia. (Ufu. 7:1-4, 9,14; Isa. 2:2, 3) Ni nani wanaojumuishwa (wanaofanyizwa) kuwa huo “mkutano mkubwa”? Ni watu wapole walio na nia ya kujinyenyekeza kutii shauri la nabii wa Mungu.
16, 17. Ni kupita kwa wakati gani kunakoendelea sasa na, kwa hiyo, ni mwito gani unaopaswa kuitikiwa la kuokoka?
16 Bila kuacha, wakati uliobaki ili Har–Magedoni ifike unaendelea kupita. Basi, onyo la nabii wa Mungu kwa watu hao wapole ni la wakati wake:
“Kabla haijazaa hiyo amri, kabla haijapita siku ile kama makapi, kabla haijawajilia hasira kali ya [Yehova], kabla haijawajilia siku ya hasira ya [Yehova],”
mnapaswa kuchukua hatua!—Sef. 2:2.
17 Ni amri na agizo la Yehova kwamba lazima Jumuiya ya Wakristo iangamie kama vile Yerusalemu usio na imani ulivyoharibiwa mwaka 607 K.W.K., na kwa sababu zile zile. (Eze. 22:3-5) Ina hatia ya damu, na viongozi wayo wa kidini wameiacha sheria ya Yehova. Dini yake ni sehemu ya Babeli Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, ambayo juu yake mtume Yohana aliandika hivi: “Kwa kuwa mataifa yote walidanganywa kwa uchawi wako. Na ndani yake ilionekana damu ya manabii, na ya watakatifu, na ya wale wote waliouawa juu ya nchi.” Haishangazi kwamba wote wanaotamani kumpendeza Mungu wamepewa mwito huu: “Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake”!—Ufu. 18:4, 23, 24.
‘KUMTAFUTA YEHOVA’
18. Lazima wapole wachukue hatua gani nyingine?
18 Hata hivyo, je! imetosha kujitenga na ulimwengu na dini yake ya uongo? Sefania anaonyesha kwamba wapole lazima wachukue hatua nyingine, inayofaa.
19. ‘Kumtafuta Yehova’ kunatia nini?
19 Kwanza, nabii huyo wa Mungu anasema hivi:
“Mtafuteni [Yehova], enyi nyote mlio [wapole] wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake.” (Sef. 2:3a)
Lazima watafute kumjua Yehova, pamoja na sifa zake nzuri ajabu na makusudi yake pia, kama vile Mwanawe, Yesu Kristo, ameeleza juu yake. Kufanya kwao hivyo kwa unyenyekevu kunaleta zawadi bora sana, kama Yesu mwenyewe alivyosema: “Hii ndiyo maana ya uzima wa milele, wapate maarifa ya kukujua wewe, Mungu wa kweli peke yako, na ya yeye uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 1:18; 17:3, NW) Kwa kumtafuta Yehova wataongozwa wampende kwa ‘moyo wao wote, nafsi, akili na nguvu,’ na kufuata mfano wa Yesu katika kufanya “utumishi mtakatifu” ambao Yehova anataka kutoka kwao.—Marko 12:29, 30, NW; 1 Pet. 2:21; Mt. 4:17; Ufu. 7:15, NW.
20. Tunapaswa kutafuta haki ya namna gani, na tukiwa na uhakika gani?
20 Halafu, Sefania anasema hivi:
“Itafuteni haki.” (Sef. 2:3b)
Hapana, si kujionyesha kuwa haki kwa Kifarisayo! Hakumfaidi ye yote kuwa na ‘juhudi kwa ajili ya Mungu’ ikiwa haipatani na maarifa sahihi ya Neno lake. Twahitaji ‘kuijua haki ya Mungu ili tujitiishe chini ya haki hiyo.’ Twahitaji kupatanisha maisha zetu na kanuni za Mungu—wala si za wanadamu—na kuuvaa utu wa Kikristo ‘ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika haki na ushikamanifu.’ (Rum. 10:2, 3; Efe. 4:22-24, NW) Haki na ushikamanifu huo wa kweli unatutaka tusiruhusu mawazo yaliyopotoka au njia za ulimwengu zipenye maishani mwetu. Kama alivyoshauri Yesu, tunahitaji ‘kuendelea, basi, kutafuta kwanza ufalme [wa Mungu] na haki yake,’ tukiwa na hakika kwamba, tunapoendelea kumtumikia, atatupa yaliyo ya lazima ili kuruzuku maisha zetu na kutulinda tuipite siku ya hasira ya Yehova.—Mt. 6:31-33, NW.
21. (a) Unabii huo unakaziaje sifa ya upole? (b) Kwa habari hii, twapaswa kujihadhari sana na nini?
21 Tatu, nabii wa Yehova anasema hivi:
“Utafuteni [upole].” (Sef. 2:3c)
Tayari Sefania amekwisha kusimulia wale watakaoutii unabii huo kuwa “[wapole] wa dunia.” Kwa hiyo sasa anarudia kukazia sifa hiyo. Ni jambo la maana kama nini tuendelee ‘kutafuta upole,’ kwa kuwa tumezungukwa na nia ya ulimwengu ya kiburi, kudai mno, mtu kufuatia maoni yake, “mimi kwanza!” Sikuzote kuna hatari kwamba twaweza kuwa na sehemu ya nia hiyo. Twahitaji kujihadhari, sikuzote tukiwa na nia ya kukubali adabu kutoka kwa Yehova na tengenezo lake, na kujipatanisha wenyewe na mapenzi yake. Tusidhani kwamba sisi “tukiisha kuokolewa, tumeokolewa daima,” kwa maana zawadi ya wokovu watapewa wale ‘wanaoendelea katika kweli.’—Mit. 22:4; Yohana 8:31, 32; 3 Yohana 3, 4, NW.
22. (a) Kwa sababu gani Sefania anasema “huenda”? (b) Matokeo ya mwisho yatakuwa nini kwa ‘wafichwa wa Yehova’?
22 Halafu Sefania anawaambia hivi ‘wapole wa dunia,’:
“Huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya [Yehova].” (Sef. 2:3d)
Kwa sababu gani “huenda”? Ni kwa sababu wokovu wa mwisho unategemea mwendo wa mtu mmoja mmoja, kama vile Yesu alivyoonyesha, kwa kusema hivi: “Yeye ambaye amevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” Vumilieni, basi, ninyi nyote mlio wapole, katika kufanya kwa unyenyekevu mapenzi ya Mungu ya wakati huu, ambayo yanatia kuhubiri habari njema hizi za ufalme wa Mungu uliosimamishwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote. (Mt. 24:13, 14, NW) Kwa kufanya hivyo, huenda ukawa kati ya wale ‘wafichwa wa Yehova’ katika siku ya hasira yake. Mtunga zaburi Daudi anaandika hivi juu yao: “Wenye upole watairithi [dunia], watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zab. 37:11.
[Sanduku katika ukurasa wa 15]
“HUENDA UKAWA UMEBAKI WAKATI MCHACHE TU”
Katika hotuba yake ya kustaafu, aliyekuwa rais wa United States Jimmy Carter alikiri hivi kuhusu silaha za nyukilia: “Hatari inaongezeka zaidi. Kwa kadiri zana za mataifa yenye nguvu nyingi zinavyozidi kuwa kubwa sana na kwa kadiri zinavyokuwa za ufundi mwingi sana na kwa kadiri serikali nyingine—pengine hata, katika wakati ujao, serikali nyingi—zinavyopata silaha hizo, huenda ukawa umebaki wakati mchache tu kabla wazimu, kukata tumaini, pupa au kukosea hakujatokeza nguvu hiyo yenye kuharibu sana.” Na tayari kuna wazimu mwingi ulimwenguni! Makala moja ya mhariri katika gazeti “Times” la New York la Januari 31, 1981, ilionya kwamba “Ikiwa Zaidi, Kuna Mwaka Mmoja Tu, wa Silaha Kupunguzwa” na mataifa yenye nguvu nyingi, ama sivyo watapoteza “nafasi zote zinazoonekana za kupunguza silaha za nyukilia.”