Wachukueni Manabii Kuwa Kielelezo—Sefania
1. Ni katika hali zipi Sefania alitumikia akiwa nabii, na yeye ni mfano mzuri kwetu kwa njia gani?
1 Ilikuwa katikati ya karne ya saba K.W.K., na watu walikuwa wanaabudu Baali waziwazi huko Yuda. Mfalme mbaya Amoni alikua ameuawa muda mfupi uliopita, na Mfalme Yosia mwenye umri mdogo ndiye alikuwa anatawala. (2 Nya. 33:21–34:1) Wakati huo, Yehova alimtuma Sefania atangaze ujumbe wa hukumu Yake. Ingawa Sefania alitoka katika familia ya kifalme ya Yuda, hakupunguza uzito wa ujumbe wa Yehova wa kushutumu utawala wa Yuda. (Sef. 1:1; 3:1-4) Vivyo hivyo, tunajitahidi kuiga ujasiri wa Sefania na haturuhusu watu wa familia waingilie kati ibada yetu kwa Yehova. (Mt. 10:34-37) Sefania alitangaza ujumbe gani, na matokeo yalikuwa nini?
2. Tunapaswa kuchukua hatua gani ili tuweze kufichwa katika siku ya hasira ya Yehova?
2 Mtafuteni Yehova: Ni Yehova tu anayeweza kuwaokoa watu katika siku ya hasira yake. Kwa hiyo, Sefania aliwahimiza wakaaji wa Yuda wamtafute Yehova, watafute uadilifu, na kutafuta upole kukiwa bado na wakati. (Sef. 2:2, 3) Jambo hilo ni kweli wakati wetu pia. Kama Sefania, tunaweza kuwatia moyo wengine wamtafute Yehova, lakini sisi pia tunapaswa kuazimia ‘kutorudi nyuma na kuacha kumfuata Yehova.’ (Sef. 1:6) Badala yake, tunamtafuta Yehova kwa kujifunza Neno lake kwa makini na kusali tupate mwongozo wake. Tunatafuta uadilifu kwa kuishi maisha yaliyo safi kiadili. Tunatafuta upole tunapositawisha unyenyekevu na tunapofuata kwa utayari mwongozo wa tengenezo la Yehova.
3. Kwa nini tuwe na maoni yanayofaa tunapohubiri?
3 Matokeo Mazuri: Ujumbe wa hukumu aliotoa Sefania uliwachochea baadhi ya watu katika Yuda, lakini hasa ulimchochea kijana Yosia, ambaye alianza kumtafuta Yehova akiwa angali mvulana. Baadaye, Yosia aliongoza kwa bidii kampeni ya kuondoa ibada ya sanamu katika nchi ya Yuda. (2 Nya. 34:2-5) Leo, ingawa mbegu fulani za Ufalme zinaanguka kando ya barabara, kwenye miamba, au katikati ya miiba, nyingine huanguka kwenye udongo mzuri na huzaa matunda. (Mt. 13:18-23) Tuna uhakika kwamba Yehova ataendelea kubariki jitihada zetu tunaposambaza mbegu za Ufalme kwa bidii.—Zab. 126:6.
4. Kwa nini ‘tunapaswa kuendelea kumtarajia Yehova’?
4 Baadhi ya wakaaji wa Yuda walifikiri Yehova hatachukua hatua kamwe. Hata hivyo, Yehova aliwahakikishia kwamba siku yake kuu ilikuwa karibu. (Sef. 1:12, 14) Wale wanaomtumaini Yehova ndio tu waliookolewa. (Sef. 3:12, 17) Tunapoendelea ‘kumtarajia Yehova,’ Mungu wetu mkuu, acheni tumtumikie kwa shangwe na umoja, pamoja na waabudu wenzetu!—Sef. 3:8, 9.