Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 3/15 kur. 18-22
  • Kumtumikia Yehova “Bega kwa Bega”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kumtumikia Yehova “Bega kwa Bega”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘KITU CHA KUSTAAJABIWA’
  • ‘OLE WAKE . . . MJI WA UONEZII’
  • NJIA YA KUOKOKEA
  • WAKATI WA UTENDAJI WENYE FURAHA
  • Watu wa Yehova Waliorudishwa Wamsifu Duniani Pote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Kitabu Cha Biblia Namba 36—Sefania
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Kufichwa Katika Siku ya Hasira ya Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • “Mikono Yako Isilegee”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 3/15 kur. 18-22

Kumtumikia Yehova “Bega kwa Bega”

“Nitabadilishia vikundi vya watu wawe na lugha safi, ili wote waliitie jina la Yehova, ili wamtumikie bega kwa bega.”​—Sef. 3:9, NW.

1. Tuna mahakikisho gani juu ya neno la unabii la Yehova?

NENO la unabii la Yehova sikuzote linatimia bila kukosea. Yeye mwenyewe anatuambia hivi: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.” (Isa. 55:11) Ndivyo imekuwa kwa mambo mengi ya ndani-ndani ya unabii mkuu wa Sefania.

2. (a) Ni vikundi vya mataifa gani vinavyotajwa katika Sefania 2:4-8? (b) Kuzuru leo mahali vilipokuwa, kunawezaje kuthibitisha usahihi wa unabii huo?

2 Kwa mfano, Sefania anaandika, mmoja baada ya mwingine, semi za Yehova za maangamizi juu ya miji ya Filistia, taifa la Wakerethi, nchi ya Wafilisti, na Moabu na Amoni. (Sef. 2:4-8) Unabii wote huo mbalimbali ulitimia kwa njia yenye kutokeza wakati wa miaka na karne zilizofuata. Leo, li wapi taifa la Filistia, pamoja na miji yake, na wa wapi Wakerethi waliokuwa wakiwategemea? Hawapo kamwe. Namna gani Moabu na Amoni? Unabii huo unasema hivi:

“Basi kama niishivyo, asema [Yehova] wa majeshi, Mungu wa Israeli, Hakika Moabu atakuwa kama Sodoma, na wana wa Amoni kama Gomora, yaani, milki ya upupu, na mashimo ya chumvi, ukiwa wa daima.” (Sef 2:9)

Ukisafiri leo kupitia maeneo ya Yordani ambako mataifa yenye kiburi ya Moabu na Amoni yalisitawi wakati mmoja, unakuta nini? Ukiwa​—kama vile Yehova alivyotabiri! Historia inaonyesha kwamba Ethiopia vilevile, pamoja na Misri, zilionyeshwa chamtema-kuni na wavamiaji Wababeli.​—Sef. 2:12.

‘KITU CHA KUSTAAJABIWA’

3, 4. (a) Usemi wa Yehova kuhusu Ashuru na Ninawi ulikuwa nini? (b) Kwa sababu gani hilo lingeweza kuonekana kuwa jambo lisilowezekana? (c) Ushuhuda ni nini juu ya utimizo wenye kutokeza wa unabii huo?

3 Wenye kustaajabisha sana ni utimizo wa usemi wa Yehova kuhusu Ashuru na Ninawi. Sefania alitabiri wakati mji mkuu wenye kiburi wa Ashuru, Ninawi, ulipokuwa ukisitawi katika utukufu wake, miaka isiyopungua 15 kabla taifa hilo halijapinduliwa kutoka cheo chake likiwa mamlaka ya ulimwengu ya pili ya historia ya Biblia. Ni nani angeweza kuwazia jambo kama hilo? Walakini Yehova alikuwa anaupinga huo “mji wa damu” wenye kutukuza taifa. (Nah. 3:1, 5) Kupitia Sefania alizungumza juu ya kuutoza hesabu, kwa kusema hivi:

“Naye atanyosha mkono wake juu ya upande wa kaskazini, na kuiangamiza Ashuru; naye ataufanya Ninawi kuwa ukiwa, kuwa mahali pakavu kama jangwa. . . . Huu ndio mji ule furaha, uliokaa pasipo kufikiri, uliosema moyoni mwake, Mimi niko, wala hapana mwingine ila mimi. Jinsi [umekuwa kitu cha kustaajabiwa], mahali pa kulala pa wanyama wa bara! Kila mtu apitaye atazomea, na kutikisa mkono wake.”​—Sef. 2:13-15.

4 ‘Haiwezekani!’ huenda wakawa walisema watu wa siku hizo. Hata hivyo kizazi icho hicho kiliishi kikayaona mambo hayo! Katika mwaka 632 K.W.K. Nabopolasa wa Babeli na Siaksare Mmedi waliuzingira na kuushinda Ninawi. Mambo ya Nyakati ya Wababeli yanatuambia hivi: “Nyara nyingi za mji na hekalu walizichukua na [wakaugeuza] mji ukawa chungu ya magofu.” Kuharibiwa kwa Ninawi kulikuwa kamili kabisa hata kwamba mahali ulipokuwa hapakujulikana kwa karne nyingi. Katika miaka iliyoanzia na wa 1800 mahali ulipokuwa palitambuliwa tena, na maktaba inayojulikana sana ya Ashurbanipali wa Pili ilifukuliwa. Walakini kufikia siku hii eneo hilo ni ukiwa mtupu ambapo mara nyingi mifugo hupumzikia. Neno la unabii la Yehova lilikuwa sahihi kama nini katika utimizo!

5. Unabii huo unatoa ujumbe gani wenye nguvu sana kwa siku zetu?

5 Hata hivyo, la maana zaidi ni kwamba maandishi hayo ya kiunabii yanatoa ujumbe fulani leo. Ni ‘onyo kwetu sisi tuliofikiliwa na miisho ya mifumo ya mambo.’ (1 Kor. 10:11,12, NW; Rum. 15:4; 2 Tim. 3:16, 17) Yanatutia moyo tuepuke kiburi, kufikiria kujitafutia anasa, mawazo ya kupata mali na maelekeo ya jeuri ambayo yalifanya Mungu alete hukumu juu ya mataifa hayo. Vilevile, tukumbuke kwamba unabii huo mbalimbali unahusu sana leo, na kwamba utimizo wake wa kumalizia unaharakishwa sana. Yehova, Mungu aliye hai, hakuuhifadhi mpaka siku hii ili uwe maandishi ya kihistoria tu. Mataifa hayo ya kale yana mifano yayo ya kisasa, sana-sana mamlaka za kisiasa na kijeshi zinazofanana na Ashuru, ambayo yanajivunia nguvu yayo ya kijeshi. Kwa hakika Yehova atalipa kisasi juu ya wapinzani hao wa ufalme wake.​—Nah. 1:2; Sef. 1:2, 9.

‘OLE WAKE . . . MJI WA UONEZII’

6. Ni ulizo gani linaloulizwa sasa, na kwa sababu gani linafaa?

6 Serikali za kisasa zenye kugandamiza na kuamrisha zinafanana sana na Ninawi mkatili wa Milki ya Ashuru yenye nguvu sana. Hata hivyo Yehova anaonyesha wazi kwamba kuna sehemu ya huu mfumo wa mambo uliopo ambayo ni yenye lawama kubwa zaidi machoni pake. Hiyo ni sehemu gani?

7. (a) Ni ‘mji wa uonezi’ gani unaofanana na Yerusalemu wa kale, na unafanana nao katika njia gani? (b) Imekataaje adabu?

7 Ni ile sehemu ya ulimwengu inayodai kuwa watu wa Mungu mwenyewe, kama vile Yuda na Yerusalemu zilivyodai katika siku za Sefania. Sehemu hiyo inadai kuwa ya “Kikristo,” na kwa ujumla inajulikana kuwa “Jumuiya ya Wakristo.” Walakini viongozi wayo wa kidini wameasi-imani ya mafundisho safi ya Neno la Mungu, Biblia, na mataifa na vikundi vya watu wa sehemu hiyo wamepotoka wakaacha kufuata kanuni bora za adili zilizoandikwa katika Neno hilo. Kwa hiyo, Sefania mwenyewe sasa anazungumza juu ya huo “mji” wenye kumvunjia Mungu heshima, kwa kusema hivi:

“Ole wake yeye aliyeasi na kutiwa unajisi, mji wa [uonezi]! Hakuitii sauti; hakukubali kurudiwa; hakumwamini [Yehova]; hakumkaribia Mungu wake.”

Yehova amewatuma mashahidi wake katika Jumuiya ya Wakristo yote, kwenye miji na vijiji vyake, na nyumba kwa nyumba. “Kila asubuhi,” wamezitangaza hukumu zake. “Wakati wa mchana,” (NW), matakwa yake ya haki yamesemwa wazi. Walakini viongozi na makasisi wa Jumuiya ya Wakristo wamekuwa ‘wajeuri’ (NW) na ‘hawaoni haya’ kupinga wajumbe hao wa Yehova mwenye haki na wa ufalme wake.​—Sef. 3:1-5.

8, 9. (a) Sasa Yehova mwenyewe anatoa tangazo gani? (b) Tangazo hilo linahusu nani? (c) Kwa sababu gani twapaswa kushukuru kwa ajili ya hayo?

8 Katika kumwunga mkono nabii wake mwaminifu, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova sasa anatoa tangazo la maangamizi, na kulifanya litie mataifa yote, na kulimalizia kwa maneno haya:

“Basi ningojeni, asema [Yehova], hata siku ile nitakapoondoka kuteka mateka; maana nimeazimia kuwakusanya mataifa, ili nizikutanishe falme, nipate kuwamwagia ghadhabu yangu; naam, ukali wote wa hasira yangu; kwa maana dunia yote itateketezwa kwa moto wa wivu wangu.”​—Sef. 3:6-8.

9 Kwa hiyo kutekelezwa kwa hukumu ya Yehova hakukomi wakati wa kufanywa ukiwa kwa Jumuiya ya Wakristo, ambayo lazima dini yayo iangamie pamoja na milki ya ulimwengu yote ya dini ya uongo, inayosimuliwa kuwa “Babeli Mkuu.” (Ufu. 18:2-4) Hiyo siku ya ‘ukali wa hasira’ yake na ya ‘moto wa wivu wake’ itaondoa uovu wote katika dunia. (Tazama pia Isaya 34:2-8; Yeremia 25:32, 33.) Tunapaswa kuwa na shukrani kama nini kwamba hii dhiki kubwa kushinda za wakati mwingine wo wote itakuwa ya mwisho, kulingana na ushahidi wa Yesu mwenyewe katika Mathayo 24:21! Itakuwa imekwisha kutimiza kusudi la Yehova la ‘kukomesha kabisa,’ kama vile Ninawi wa kale. “Mateso hayatainuka mara ya pili.”​—Nah. 1:9; Dan. 12:1; Ufu. 19:11-21.

NJIA YA KUOKOKEA

10. Ni ‘lugha chafu’ gani inayozungumzwa ulimwenguni sasa?

10 Je! kuna njia ya kuokokea wakati wa huo msiba wa ulimwengu? Ndiyo kabisa! Katika maneno yanayofuata ya unabii huo, Yehova Mungu mwenyewe anaonyesha hiyo ni njia gani. Yeye anasema hivi:

“Kwa maana ndipo nitabadilishia vikundi vya watu wawe na lugha safi, ili wote waliitie jina la Yehova, ili wamtumikie bega kwa bega.” (Sef. 3:9)

Hata yawe yanatumia lugha gani kati ya mamia ya lugha za taifa, mataifa ya kilimwengu yanapiga porojo katika “lugha” inayomchukiza Yehova. Mahali pa kuushangilia ufalme wa Mungu, yanashangilia shughuli zayo za kutukuza taifa, yakijaribu kutumia Umoja wa Mataifa uliogawanyika ili yapate faida za kichoyo. Yanaukataa ufalme wa Yehova kupitia Kristo Yesu.

11. (a) Ni “lugha safi’’ gani inayosikiwa leo? (b) “Lugha” hiyo inazungumzwa kwa kadiri kubwa namna gani? (c) Wale wanaoizungumza ‘wanaliitiaje jina la Yehova,’ na kwa matokeo’ gani?

11 Basi, huko kubadilishwa kuwa na “lugha safi” ni nini? Ni kugeukia ujumbe wa kweli, “habari njema” zenye kuburudisha, “kielelezo cha maneno yenye uzima,” yanayomsifu Yehova na makusudi yake ya haki kupitia Kristo Yesu. (2 Tim. 1:13) Hiyo “lugha safi” inawaunganisha. Na inashuhudia kwamba, katika mwaka wenye kutokeza wa 1914, “ufalme wa dunia umekwisha kuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake, naye atamiliki hata milele na milele.” (Ufu. 11:15) Kwa kuusema ujumbe huo kwa midomo yao, Wakristo wa kweli ulimwenguni pote ‘wanaliitia jina la Yehova’ wakiwa wakf, kwa kupatana wakimtolea “utumishi mtakatifu.” Wakiwa ndio kikundi pekee cha watu chenye umoja duniani, wanaenda kwenye nyumba za watu, wakizishangilia “habari njema” za ufalme wa Yehova uliosimamishwa. Kwa njia hiyo wanamtumikia Yehova “bega kwa bega.” (Mt. 24:14; Rum. 12:1, NW) Je! wewe ni mmoja ambaye amejitenga na ulimwengu kwa njia hiyo, ili umtumikie Mungu kwa juhudi ukiwa wakf Kwake? Ni kwa kufanya kazi kwa njia hiyo pamoja na watu walio tengenezo wa Yehova, ndipo unapoweza ‘kuponywa.’​—Yoeli 2:32; tazama pia Hosea 14:1, 2; Waebrania 13:15.

12, 13. (a) Ni matatizo gani yanayoweza kuwapo katika kujifunza “lugha” hiyo? (b) Kwa sababu gani upole unahitajiwa ili kutumikia “bega kwa bega”?(c) Tunawezaje kusitawisha sifa ya upole?

12 ‘Kubadilishwa kuwa na lugha safi’ limekuwa jambo gumu kwa wengine kufanya. Si rahisi kutoka katika ulimwengu, wenye njia rahisi zenye kuruhusu ubaya, na kujinyima mambo yaliyo ya lazima ili ‘kuliitia jina la Yehova.’ Jambo hilo limetutaka tuondolee mbali mawazo yenye makosa, tabia mbaya na njia za maisha za kujitafutia faida za kichoyo na za upotovu, ili tujipatanishe na kanuni safi, zinazofaa za watu wa Mungu mwenyewe. (Efe. 4:17, 18, 29; 1 Pet. 4:3) Jambo hilo limetutaka tutambue inavyofaa tengenezo lile moja ambalo Yehova anatumia duniani leo, na twafanya hivyo kwa kushirikiana pamoja na “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” Jambo hilo limetutaka tuwe wapole, katika ‘kuchunguza kwa uangalifu’ Neno la Mungu kwa msaada wa vitabu vya huyo “mtumwa,” ili tuiimarishe imani yetu.​—Mt. 24:45; Matendo 17:11, NW.

13 Katika kumtumikia Yehova “bega kwa bega,” tunahitaji sifa ya upole, kama inavyokaziwa mara nyingi na Sefania. Tunapofanya makosa, kama wanavyokosa wanadamu wote wasiokamilika, na tuwe tayari kuyakiri, kama “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” ambaye amejumuishwa na watu wenye mwili wasiokamilika, alivyolazimika kufanya masahihisho. Hata hivyo, na tusilaumu kamwe kweli yote iliyo bora ambayo Yehova amesitawisha kati ya watu wake wenye umoja wakati wa miaka 100 iliyopita, na ambayo, kwa kusahihishwa na kurekebishwa, imepata kung’aa zaidi na zaidi penye “njia ya wenye haki.”​—Mit. 4:18.

14. (a) Ni nia gani iliyo kinyume cha upole, nayo inaonyeshwaje? (b) Watu hao wenye kujikweza wanatendaje, na tunapaswa kutii maonyo gani? (c) Ni wapi tutakapokuta hakuna ‘upungufu wa kitu cho chote’?

14 Pindi kwa pindi, kati ya watu wa Yehova kumetokea watu ambao, kama yule Shetani wa kwanza, wamesitawisha nia ya kujitegemea na ya kutafuta-tafuta makosa. Wao hawataki kutumikia “bega kwa bega” pamoja na udugu wa ulimwenguni pote. (Linganisha Waefeso 2:19-22.) Mahali pake, ‘wanageuzia bega’ maneno ya Yehova. (Zek. 7:11, 12) Kwa kutukana kielelezo cha “lugha safi” ambayo kwa neema nyingi Yehova amewafundisha watu wake wakati wa karne moja iliyopita, watu hawa wenye kujikweza wanajaribu kuwaondoa “kondoo” watoke kwa “kundi” pekee la mataifa yote ambalo Yesu amekusanya duniani. (Yohana 10:7-10,16) Wanajaribu kupanda mashaka na kuwatenga wasiojihadhari waondoke kwa “meza” ya chakula cha kiroho ambayo imeandaliwa kwenye Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova, ambako kwa kweli hakuna ‘upungufu wa kitu cho chote.’ (Zab. 23:1-6) Wao wanasema kwamba inatosha kuisoma Biblia peke yake, ukiwa peke yako au katika vikundi vidogo-vidogo nyumbani. Walakini, kwa kushangaza, kupitia ‘usomaji wa Biblia’ huo wamerudia kabisa mafundisho ya kuasi-imani ambayo ndiyo maelezo viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo walikuwa wakifundisha miaka 100 iliyopita, na hata wengine wamerudia kusherehekea sikukuu za Jumuiya ya Wakristo tena, kama vile sikukuu ya Kirumi ya Saturnalia ya Desemba 25! Yesu na mitume wake walionya juu ya watu hao wenye kuhalifu sheria.​—Mt. 24:11-13; Matendo 20:28-30; 2 Pet. 2:1, 22.

15. (a) Yehova anatendaje kwa habari ya wale ‘wanaojikweza’? (b) Hao ‘watu walioonewa na maskini’ wanatambulishwaje? (c) Yehova anawatolea hawa uhakikisho gani?

15 Kupitia nabii wake Sefania, Yehova anawaambia watu Wake namna atakavyofutilia mbali wale ambao bila haya wanajaribu kupanda mbegu ya mvurugo katika tengenezo Lake la kidunia, kwa kusema hivi:

“Nitawaondoa watu wako [wanaojikweza] na kujivuna, wasiwe kati yako, wala [hutajikweza] tena katika mlima wangu mtakatifu.”

Tofauti na hayo, Yehova anasema hivi:

“Nitasaza ndani yako watu walioonewa na maskini, nao watalitumainia jina la [Yehova].” (Sef. 3:11, 12)

Ndiyo, hao ndio wale wapole, wanaofanya kazi “bega kwa bega” wanaposhiriki katika “kazi takatifu ya habari njema.” (Rum. 15:15, 16, NW) Hawana kiburi kingi hata kwamba wasiweze kufanya kazi ya ki-maskini ya kwenda nyumba kwa nyumba kufuatia kielelezo ambacho wanafunzi wa Yesu walijifunza kwa Bwana yao. (Mt. 10:5-13; Luka 9:2-6; Matendo 5:42) Kwa kulifanya jina la Yehova liwe kimbilio (kulitumaini, UV) wanalitangaza jina hilo tukufu na kusudi lake la kulitetea kupitia ufalme wenye ushindi wa Kristo wake. (Eze. 38:23; Dan. 2:44) Watu wa Yehova wanapoendelea kutumikia na kuishi kulingana na haki yake, wao wana uhakika kwamba “hapana mtu atakayewaogofya.” (Sef. 3:13) Wanafurahia amani ya kweli ya akili!

WAKATI WA UTENDAJI WENYE FURAHA

16. (a) Sefania anaelezaje furaha yake? (b) Ni mwito gani wa kiunabii ambao umeitikiwa leo, na ni nani ambao wameuitikia?

16 Sefania mwenyewe anafurahishwa na uhakikisho wa namna hiyo kutoka kwa Yehova, hata kwamba anatolea watu wa Mungu mwito huo:

“Imba, Ee binti Sayuni; piga kelele, Ee Israeli; furahi na kushangilia kwa moyo wako wote, Ee binti Yerusalemu. [Yehova] ameziondoa hukumu zako, amemtupa nje adui yako; mfalme wa Israeli, naam, yeye [Yehova], yu katikati yako; hutaogopa uovu tena.” (Sef. 3:14, 15)

Tangu mwaka 1919, walipofunguliwa kutoka utumwa wa kiroho katika Babeli Mkuu, mashahidi waliotiwa mafuta wa Yehova wamemtumikia “bega kwa bega” katika kutoa ushahidi wenye furaha mbele ya watu wote. Yehova amewahukumu na kuwakubali watoto hao wa Yerusalemu wa kimbinguni. (Gal. 4:26; 1 Pet. 4:17) Magereza na kambi za kutumikisha watumwa zimeshindwa nguvu za kuweza kuwarudisha tena katika utumwa wa kiroho. Furaha yao sasa wanashiriki “mkutano mkubwa” wa Mashahidi wenzao, waliotambuliwa tangu mwaka 1935 wawe sehemu ya “kondoo wengine” wa Bwana.​—Yohana 10:16; Ufu. 7:9, 10.

17. (a) Ni uhakikisho gani unaowasaidia watu wa Yehova wavumilie katika “utumishi mtakatifu”? (b) Ni kwa njia gani Yehova ‘ametulia,’ na bado akiwa ‘anashangilia . . . akifurahia kwa kuimba,’ nasi tunapaswa kuitikiaje?

17 Sasa Yehova mwenyewe anasihi, moja kwa moja watiwa mafuta wake, wanaowakilisha Sayuni wa kimbinguni, na kupitia kwao wafanya kazi wenzao wa ule “mkutano mkubwa,” kwa kusema hivi:

“Usiogope, Ee Sayuni; mikono yako isilegee.” (Sef. 3:16)

Hata uhalifu na jeuri yawe mambo yenye kuumiza sana leo, hata matisho ya kizazi hiki chenye silaha za nyukilia yakiwa yenye kuogopesha namna gani, hata mateso yatakayowapata Mashahidi wa Yehova yawe yenye ukatili namna gani, urafiki wao pamoja na Yehova na kumtumaini Mungu wao kutawapitisha mambo hayo. Tukiwa tumekwisha kuweka mikono yetu kwenye jembe la “utumishi mtakatifu,” tusitazame nyuma kamwe kwenye mambo yaliyo nyuma na kuacha kulima mbele, “bega kwa bega”! (Luka 9:62; Ufu. 7:15, NW) Kwa sasa unabii huo unatoa uhakikisho zaidi wa kimungu:

“[Yehova], Mungu wako, yu katikati yako shujaa awezaye kuokoa; atakushangilia kwa furaha kuu, atatulia katika upendo wake. Atakufurahia kwa kuimba.” (Sef. 3:17)

Yehova ‘ametulia’ (‘amenyamaza,’ NW) kwa kutafuta starehe na kiburudisho kwa kuonyesha upendo watu wake aliowapata tena, waliorudishwa, naye anafurahi sana na kushangilia sana kwa ajili ya ukamilifu na juhudi yao katika utumishi wake. Katika hizi “siku za mwisho” twapaswa kujiona kuwa karibu sana na Mungu wetu aliye hai, Yehova, tunapotumikia bega kwa bega katika utumishi wake.​—2 Tim. 3:1.

18. (a) Watu wa Yehova wamefanywaje wakawa “sifa na Jina” tangu mwaka 1919? (b) Twawezaje kutumikia “bega kwa bega” kwa ajili ya maelfu mengi wengine?

18 Tangu mwaka 1919, imekuwa siku kuu ya kurudishwa kwa watu wote wa Mungu. Wakiwa mashahidi waaminifu wameendelea kuhubiri wakiwa na juhudi ya umisionari, hata kwamba tengenezo la Yehova likapanuka kufikia miisho ya dunia. (Rum. 10:10,18) Hakika umekuwa wakati wa kuwaleta pamoja watu wa Mungu, kuwakusanya pamoja. Na wanakusanywa kwa kusudi gani? Yehova mwenyewe anajibu hivi:

‘‘Nitawafanya ninyi kuwa sifa na jina, miongoni mwa watu wote wa dunia.” (Sef. 3:20)

Kwa furaha, mabaki waliotiwa mafuta wa watu wa Mungu wamekuwa “sifa na jina” katika kuliinua juu jina lenye thamani la Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, na sasa wengi wa hao “watu wote wa dunia” wanafanya kazi pamoja nao, “bega kwa bega,” katika kuyajulisha makusudi ya Ufalme. Badiliko tulilofanya la kuzungumza ile “lugha safi,” na kuendelea kwetu kushangilia “habari njema za ufalme” hizo, bado kutasaidia maelfu mengi zaidi ‘waliitie jina la Yehova,’ ili wao pia, wawe ‘wafichwa wa Yehova’ wakati wa ile siku ya hasira yake, na wajitokeze wamsifu kwa umilele wote.​—Kutoka The Watchtower, August 15, 1981.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki