Mchezo wa Kuigiza wa Kusanyiko
[Sanduku/Pictures katika ukurasa wa 10]
Mchezo wa Kuigiza wa Kusanyiko: YEHOVA HUWABARIKI WASHIKAMANIFU WAKE
Mfalme wa kwanza wa Israeli, akawa mwasi—asimngojee Yehova, akafanya mambo kivyake. Kwa hiyo Yehova akamtia mafuta Daudi awe mfalme walakini akamwacha Sauli akiwa juu ya kiti cha enzi. (1 Samweli 13:9-14; 15:13-23; 16:11-23) Sauli akamwonea Daudi wivu na akajaribu kumwua.
Ushikamanifu wako kwa Yehova ungesimamaje chini ya hali kama hizo zenye kujaribu? Je! wewe ungalimngojea Yehova au ungalijaribu kusahihisha mambo kivyako?
“Sauli akajaribu kumpiga Daudi hata ukutani kwa mkuki wake, ila yeye akaponyoka kutoka mbele ya Sauli, nao huo mkuki akaupiga ukutani.”—1 Samweli 19:10.
Akiwa na wanaume 3,000 Sauli alikwenda kumwinda Daudi. Sauli mwenyewe akaingia ndani ya pango ambamo Daudi na watu wake walikuwa wamejificha. Daudi alisihiwa amwue Sauli, bali yeye alisema: “Ni jambo lisilowazika upande wangu, kwa maoni ya Yehova, kwamba nifanye jambo hili kwa mtiwa mafuta wa Yehova.”—1 Samweli 24:4, 6, NW.
Sauli alikufa akipigana na Wafilisti. Baadaye, “wazee wote wa Israeli . . . wakamtia Daudi mafuta awe mfalme juu ya Israeli.”—2 Samweli 5:1-3.
Daudi alikuwa kielelezo cha ushikamanifu kwa Mungu wake, Yehova. Yeye hakukimbia mbele Yake, ili afanye mambo kivyake. Yehova alimwita “mtu anayeupendeza moyo wangu, atakayefanya mapenzi yangu yote.”—Matendo 13:22.
Je! Yehova atasema vivyo hivyo juu yako? Je! sikuzote utamngojea atende? Je! utakuwa mshikamanifu kwa Yehova, watiwa mafuta wake anaowakubali na tengenezo lake la kitheokrasi na mipango yalo? Ukifanya hivyo, basi Yehova atakuthawabisha kama alivyomthawabisha Daudi.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]
Mchezo wa Kuigiza wa Kusanyiko: JIHADHARI NA MAZUNGUMZO YA UASI
Wana wa Israeli walikuwa wamekubali hivi: “Hayo yote aliyoyasema [Yehova] tutatenda.” (Kutoka 19:1-5, 8) Hata hivyo manung’uniko na malalamiko juu ya Musa yakatokea katika kambi hiyo. Wenye kuongoza katika mambo hayo walikuwa Kora, Dathani na Abiramu. Waliwavuta wengine na karibuni wengi wakawa wanampinga Yehova waziwazi.
Wewe ungalitendaje kwa sababu ya mazungumzo hayo ya uasi? Je! imani yako katika mtumishi wa Yehova Musa ingaliendelea kuwa imara kama ile ya Kalebu na Yoshua?
Mwanamume mmoja aliyekusanya kuni siku ya Sabato aliletwa mbele za Musa. Yehova aliamuru auawe, kwa maana huko kulikuwa ni kuvunja sheria ya Mungu—wala si ‘kijambo kidogo tu.’—Hesabu 15:32-36.
‘Mkutano wote waliamuru Yoshua na Kalebu wapigwe kwa mawe’ kwa sababu, kati ya wale wanaume 12 waliopelekwa wakaipeleleze Kanaani, wao peke yao ndio walioonyesha imani kwamba Yehova angewapa Waisraeli nchi hiyo.—Hesabu 13:25—14:10.
Yehova alimwamuru Haruni, vilevile Kora na wengine 250, watoe uvumba. Moto ulishuka chini na kuwameza waasi hao. Vilevile, Yehova aliifanya dunia imeze Dathani na Abiramu na watu wa nyumbani mwao pamoja na watu wa nyumba ya Kora. (Hesabu 16:32, 35) Kwa njia hiyo akaitatua suala la kuweka kwenye cheo kwa kitheokrasi.
Uasi unaweza kuanza kama jambo dogo tu —kulaumu uamuzi wa wazee au mpango fulani wa “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” Lakini unaweza kuongoza kwenye upinzani wa waziwazi. Yuda anatuonya hivi: “Ole wao, kwa sababu wao . . . wameangamia katika mazungumzo ya uasi ya Kora.” Ni vema zaidi kufuata shauri linalofuata baadaye la Yuda: “Lakini ninyi, wapendwa, . . . jidumisheni katika upendo wa Mungu.”—Yuda 11, 20, 21, NW.