Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 2/15 kur. 9-14
  • Kujiweka Wakf—Kwa Nani? kwa Sababu Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kujiweka Wakf—Kwa Nani? kwa Sababu Gani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “NIMEKUJA . . . KUYAFANYA MAPENZI YAKO”
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Walizaliwa Katika Taifa Teule la Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Maana ya Ubatizo Wako
    Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
  • Mtakuwa “Ufalme wa Makuhani”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 2/15 kur. 9-14

Kujiweka Wakf​—Kwa Nani? kwa Sababu Gani?

“Walakini ninyi ni ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu [taifa lililotakaswa; taifa lililowekwa wakf], watu walio mali ya pekee.’”​—1 Petro 2:9, New World Translation; The Jerusalem Bible; The New English Bible.

1, 2. (a) Je! Abraham Lincoln alikuwa mshiriki wa mojalapo la makanisa ya Jumuiya ya Wakristo, na hata hivyo katika hotuba yake katika Gettysburg alilitajaje taifa lile ambalo yeye alikuwa rais walo? (b) Ni tendo gani linaloonyesha tumaini la taifa hilo kwa Mungu, na serikali itakayofuatia taabu ya ulimwengu itakuwaje “kwa watu”?

KATI ya makanisa yote ya Jumuiya ya Wakristo, hakuna lo lote lingeweza kudai rais wa 16 wa United States ya Amerika alikuwa mshiriki walo. Hata hivyo, alipokuwa akitoa hotuba ile ijulikanayo sana ya Gettysburg katika Novemba 15, 1863, mwanamume huyo msomaji wa Biblia, Abraham Lincoln, alisema maneno haya yenye mkazo:

“Miaka 87 iliyopita baba zetu walitokeza katika kontinenti hii, taifa jipya, lililozaliwa katika Uhuru, na lililowekwa wakf kwa shauri la kwamba watu wote wameumbwa wakiwa wanalingana. . . . Walakini, kwa maana kubwa zaidi, hatuwezi kuweka wakf​—hatuwezi kutakasa​—ardhi hii. Wanaume hodari, walio hai na waliokufa, waliong’ang’ana hapa, wameitakasa, hata kidogo hatuwezi kuongeza au kutoa kwa uwezo wetu mdogo.. . . Mahali pake, sisi tulio hai, ndio tunaopaswa kujiweka wakf kwa kazi ambayo haijakamilishwa bado ambayo wao waliopigana hapa wameifikisha hatua hii kwa uhodari. Mahali pake sisi ndio tunaopaswa kujiweka wakf kwa kazi ngumu sana ambayo imebaki mbele yetu . . . ”

2 Tangu hotuba hiyo yenye kukumbukwa katika makaburi ya taifa katika Gettysburg, Pennsylvania, United States haistahili dai la usemi ulio katika noti yao ya dola, “Twamtumaini Mungu.” Kujapokuwa kujiweka wakf kwa usemi huo kwa rais huyo na Waamerika wengine wenye moyo mnyofu, “serikali ya watu, kupitia watu,” ‘itaangamia kutoka duniani.’ Kwa furaha, “kwa watu” huo hautakuwa msiba wa kudumu (kuendelea milele), kwa sababu serikali kuu ya kifalme ya Mungu kupitia Mfalme wake aliyewekwa, Yesu Kristo, itafuata ilete baraka kwa wakaaji wote wa dunia hii, kutia kontinenti ambayo sasa ni Amerika.

3, 4. (a) Halafu ni “taifa” gani litakalotokea? (b) Kwa habari ya “taifa” hilo jipya Petro alikuwa akitaja maneno gani ambayo Yehova aliiambia Israeli?

3 Kisha taifa jipya litatokea. Hilo ni taifa jipi? Ni lile ambalo maneno yafuatayo yaliyoongozwa na Mungu yalielekezwa kwalo: “Walakini ninyi ni ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu walio mali ya pekee.’”​—1 Pet. 2:9, NW.

4 Kwa maneno hayo mtume Petro anataja misemo inayotumiwa na Mungu kuhusu watu Wake waliochaguliwa wa Israeli ambao wakati huo walikuwa katika Mlima Sinai huko Uarabuni, kama ilivyoandikwa katika Kutoka 19:5, 6. Hapo twasoma hivi: “Sasa basi ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli, na kulishika agano langu, hapo ndipo mtakapokuwa [mali ya pekee] kwangu kuliko makabila yote ya watu; maana dunia yote pia ni mali yangu, nanyi mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani na taifa takatifu.”

5. Kulingana na matumizi ya Biblia, je! “kutakasa” na “kuweka wakf” ni jambo lile lile?

5 Katika Kutoka 19:6 na 1 Petro 2:9, NW, maandiko ambayo maneno yayo yametangulia kutajwa, tafsiri fulani zinakazia usemi huo mfupi “taifa takatifu” kwa kuutafsiri kuwa “taifa lililotakaswa” au “taifa lililowekwa wakf.”a (Tazama The Jerusalem Bible; The New English Bible.) Kukubali na kuishi kupatana na kanuni za Yehova kungewatenga Waisraeli wawe watu waliotakaswa au waliowekwa wakf. Mungu anaweza “kutakasa” au “kuweka wakf” kitu au mtu au kikundi cha watu. Kwa Mungu maneno hayo mawili yanaweza kumaanisha jambo lile lile. Hata hivyo, ingawa wanadamu wasiokamilika hawawezi “kutakasa” kitu cho chote, wakifanye safi kwa kusudi takatifu, kwa kufaa na kwa upendo wanaweza “kuweka wakf” kitu, kutia wao wenyewe.

6. (a) Kwa kusema, “maneno yote aliyoyanena [Yehova] tutayatenda,” ni tendo gani lililochukuliwa na taifa la Israeli, wakiwa watu mmoja mmoja na wakiwa jamii? (b) Mungu aliwaingiza katika mpango gani bila kuwalazimisha?

6 Mungu alipendekeza kwa Waisraeli waliokuwa wameokolewa kwamba wangekuwa taifa takatifu kwake, mradi ‘waitii sauti yake na kulishika agano lake.’ Wao walijibu hivi: “Maneno yote aliyoyanena [Yehova] tutayatenda.” Kwa hiyo, wakiwa mtu mmoja na pia kama jamii, walijiweka wakf unaodumu kwa Mwokozi wao, Yehova Mungu. Ingawa Yehova alikuwa amekwisha kuwachagua kwa sababu walikuwa wazao wa asili wa Ibrahimu, na alikuwa amewaokoa kimwujiza kutoka Misri kupitia Bahari Nyekundu (Shamu), hata hivyo alingojea Waisraeli wajiweke wakf wenyewe kwake na kwa ibada yake kwa moyo wa kupenda. Kwa msingi huo walifanywa watu wa agano wa Yehova. Juu ya hilo, twasoma hivi:

“Kila amri ilipokwisha kunenwa na Musa kwa hao wafu wote, kama ilivyoamuru sheria, aliitwaa damu ya ndama na ya mbuzi, pamoja na maji na sufu nyekundu na hisopo, akakinyunyizia kitabu chenyewe, na watu wote, akisema, Hii ni damu ya agano mliloamriwa na Mungu.”​—Ebr. 9:19, 20; Kut. 24:1-8.

7. (a) Katika vizazi ambavyo vingefuata hali ya Wayahudi ingekuwa nini? (b) Wangewezaje kupoteza msimamo wao uliowekwa wakf?

7 Vizazi vya Wayahudi vilivyofuata vingezaliwa katika taifa hilo lililowekwa wakf na kwa hiyo, vikiwa na uhusiano uliowekwa wakf na Mungu. Lakini wakiwa mtu mmoja mmoja, wakiisha kukua na kufikia umri wa kuwa na daraka wangepaswa kuwaiga Wayahudi wale katika Mlima Sinai kwa kuvithibitisha vichocheo vyao vya moyo na matendo kwamba kweli kweli walikuwa wamejiweka wakf kwa Yehova ili waendelee kuwa na msimamo mzuri katika taifa hilo takatifu. Hivyo ndivyo ilivyo kwa sababu Mungu anaweza kuuondoa msimamo mtakatifu anaowapa watu, iwapo wanajionyesha hawastahili, na kuuhamisha kwa wale wanaojionyesha kuwa wanaustahili. Ndiyo sababu mtume Petro alielekeza maneno ya awali (kwanza) ya Mungu kwa Israeli wa asili, kwamba wangekuwa kwake “ufalme wa makuhani na taifa takatifu,” kwa taifa jipya la Kikristo lililotokezwa katika Pentekoste mwaka 33 W.K. Kuhamishwa huko kwa ukubali mtakatifu kulitokeaje?

8. (a) Petro alipoiandika barua yake ya kwanza iliyoongozwa na Mungu, ni msiba gani uliokuwa umekaribia kuipata Israeli, na sasa Wayahudi hawakuwa tena na uhusiano gani na Yehova Mungu? (b) Basi ni nani waliojumuishwa (waliofanyizwa) kuwa hilo “taifa lililotakaswa”?

8 Mtume huyo alipoyaandika maneno ya 1 Petro 2:9, NW, Wayahudi walikuwa wanakaribia msiba wa taifa zima. Mji wao wa Yerusalemu uliokuwa na hekalu ulikuwa karibu kuharibiwa na majeshi ya Waroma nao wangetawanywa kwenye mataifa yote, kama Yesu alivyokuwa ametabiri. (Luka 21:20-24) Inasikitisha kusema kwamba katika mwaka 33 W.K., walikuwa wamemkataa Yesu Kristo Mpatanishi wa agano jipya la Mungu, na bila shaka agano la kale la Torati lililokuwa limepatanishwa kupitia nabii Musa halikuwa likifanya kazi tena. ‘Waliokuwa Waisraeli kwa njia ya mwili’ sasa walikuwa wakikataliwa. (1 Kor. 10:18; Mt. 23:38) Taifa jipya la Israeli wa kiroho lilikuwa limetokezwa na Yehova Mungu. (Rum. 9:6; Gal. 6:15, 16) Hilo “taifa lililotakaswa” jipya lilikuwa lenye kujumuishwa na wanafunzi wa Yesu Kristo ambao Paulo aliwaandikia barua yake, yaani, “wale waliochaguliwa kulingana na maarifa ya mbele ya Mungu Baba, pamoja na kutakaswa kwa njia ya roho.”​—1 Pet. 1:1, 2, NW.

9. Je! Mungu alitangulia kujua watu mmoja mmoja ambao wangekuwa washiriki wa taifa hilo takatifu, na wao walikuwaje “jamaa” iliyochaguliwa?

9 Hiyo haimaanishi kwamba Mungu alikuwa anawajua washiriki mmoja mmoja na kutangulia kuwaweka kwa jina. Mahali pake, alijua kimbele kwamba angetokeza taifa jipya, “taifa takatifu,” na alijua kimbele mambo ambayo yangetakiwa kwa kila mshiriki mmoja mmoja ili achaguliwe na kuingizwa katika taifa hilo takatifu. Vilevile, taifa hilo la kiroho lingefanywa takatifu kipekee kwa roho takatifu ya Mungu, na washiriki wa taifa hilo wakiwa wamezaliwa kupitia roho takatifu ili wawe wana wa kiroho wa Mungu. (Tito 3:4-7) Wakiwa na msimamo huo mtakatifu, au uliotakaswa, wangeweza kutumikia wakiwa “ukuhani wa kifalme.” Wakiwa wamezaliwa kwa roho, wao walikuwa “jamii,” “jamii iliyochaguliwa.”

10. Kwa kuwa Mungu anashughulika na Wakristo waliotiwa mafuta kama “taifa” au kikundi, ni maulizo gani yanayotokea kuhusu daraka la mtu mmoja mmoja?

10 Walakini kujiweka wakf kwa Yehova kunakofanywa na washiriki mmoja mmoja kunahusuje jambo hilo? Ingawa Mungu “anawatakasa” au “kuwaweka wakf” wakiwa kikundi au taifa, je! ni lazima kila mmoja ajiweke wakf kwa Mungu bila kumwekea matakwa yo yote ili akubaliwe kuwa mshiriki wa taifa hilo jipya? Je! kwa kweli Maandiko hayasemi kwa ufupi hivi: ‘Msadiki Bwana Yesu Kristo nawe utaokolewa’? Au, kwa ufupi, ‘Tubu na uongoke’? Basi, je! kusadiki tu, kutubu na kuongoka siyo mambo yanayotajwa kuwa yanatakiwa ili kuwa mwanafunzi wa Yesu, Mkristo? Je! Yesu, Mwana wa Mungu alichukua hatua ya kujiweka wakf alipokuwa duniani? Ebu tuone.

“NIMEKUJA . . . KUYAFANYA MAPENZI YAKO”

11. Yesu alizaliwa chini ya mpango gani wa agano pamoja na Mungu, na hiyo ilikuwaje hivyo?

11 Kwa habari ya kuzaliwa kwa kibinadamu kwa Yesu, Wagalatia 4:4, NW, inatuambia hivi: “Wakati kipimo kamili cha wakati kilipofika, Mungu alimtuma Mwanawe, ambaye alitoka kwa mwanamke na ambaye alikuwa chini ya sheria [ya Musa].” Baada ya kuzaliwa kwake kwa kimwujiza na bikira Myahudi, kutahiriwa kwake katika siku ya nane kulithibitisha kwamba kwa kuzaliwa yeye alikuwa mmoja wa watu wa agano wa Mungu, na kwa habari hiyo Yusufu na Mariamu “walimpeleka mpaka Yerusalemu wakamtoe kwa Yehova.”​—Luka 2:22-24, NW.

12. Yohana aliwabatiza Wayahudi waliomjia kwa wonyesho wa nini, lakini kwa sababu gani hapo kwanza alikataa kumbatiza Yesu?

12 Mtangulizi wa Yesu Kristo, Yohana Mbatizaji alitumwa kwa taifa hilo lililowekwa wakf alielekeze kwenye toba. Hata Yesu alisema hivi: “Sikutumwa ila kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” (Mt. 15:24) Ujumbe waliopewa watu hawa wa Mungu waliowekwa wakf ulikuwa wa pekee, ambao haukuhusu mataifa yasiyo ya Waisraeli. Yohana Mbatizaji aliwasihi “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli” watubu dhambi zao walizofanya kwa agano la Torati. (Mt. 3:1-6) “Yohana alibatiza kwa ubatizo wa toba, akiwaambia watu wamwamini yeye atakayekuja nyuma yake, yaani, Yesu.” (Matendo 19:4) Hata hivyo, Yesu alipokwenda kwa Yohana abatizwe kwa maji, bila shaka huo haukuwa wonyesho wa kutubu, kwa maana Yesu hakuwa na dhambi wala hakuvunja agano la Torati alilozaliwa chini yalo. Yohana akiwa anajua jambo hilo, alisita kumbatiza Yesu, walakini alilikubali ombi lake alipoambiwa hivi: “Acha tu iwe hivyo kwa sasa, maana kwa namna hii inafaa tuyatekeleze yale yote Mungu anayotaka.” (Mt. 3:13-17, HNWW) Alikuwa na maana gani?

13. (a) Yesu alitimizaje Zaburi 40:7, 8? (b) Ubatizo wa Yesu ulifananisha nini?

13 Yesu alikuwa akitenda kupatana na unabii unaomhusu katika Zaburi 40:7, 8: “Ndipo niliposema, Tazama nimekuja, kuyafanya mapenzi yako, Ee Mungu wangu, ndiyo furaha yangu.” Katika Waebrania 10:5-10 unabii huo unaelekezwa kwa Yesu Kristo, kwa kuwa kwa habari ya Yesu, Mungu hakutaka dhabihu zilizokuwa zikitolewa kwa kupatana na Torati ya agano la Musa, bali alitaka mwili mkamilifu wa kibinadamu ambao Mungu alimtayarishia Mwanawe utolewe dhabihu kama msingi wa agano jipya. Kwa hiyo alipokuwa akibatizwa, Yesu hakuwa akijiweka wakf kwa Mungu, kwa maana tayari yeye alikuwa mshiriki wa taifa lililowekwa wakf na akiwa hana dhambi, hakuhitaji kuongoka. (Ebr. 7:26) Mahali pake, ubatizo wake ulikuwa wonyesho wa kujitoa kwa Babaye wa kimbinguni ili ayafanye mapenzi Yake. Na kwa habari hiyo Yesu aliwekea wanafunzi wake kielelezo cha ubatizo.

14. (a) Baada ya Yohana kuwekwa kifungoni, Yesu alianza kuhubiri ujumbe gani? (b) Toba na ubatizo wa wakati huo uliwatayarisha watu kwa ajili ya jambo gani?

14 Baada ya Yesu kusikia kwamba Yohana Mbatizaji alikuwa amewekwa kifungoni, alianza shughuli ya kuhubiria Waisraeli waliokuwa tayari wamejiweka wakf. “Tokea wakati huo Yesu alianza kuhubiri, na kusema, Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.” (Mt. 4:17) Ubatizo ukiwa wonyesho wa toba ukapata nguvu mpya. (Yohana 3:26; 4:1, 2) Wakati Musa Mkuu Zaidi, Yesu Kristo alipopaa kwenda mbinguni na akampa Yehova Mungu thamani (ubora) ya dhabihu yake ya kibinadamu yenye kustahili, agano la Torati ya Musa lilibatilishwa (liliacha kufanya kazi) na msingi wa kuanzisha “agano jipya” lililokuwa limetabiriwa uliwekwa. (Yer. 31:31-34) Kwa hiyo, katika siku ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K., wanafunzi Wayahudi wa Yesu walihamishwa kutoka agano la Torati ya Musa mpaka kwenye “agano jipya” ambalo Mpatanishi walo alikuwa Musa Mkuu Zaidi, Yesu Kristo.b

15. (a) Ni nini ambacho hakikumalizika mara moja kwa Wayahudi baada ya agano la Torati kuondolewa? (b) Mapenzi ya Mungu yalikuwa nini sasa kwa Wayahudi waliokuwa wanajali juu ya uhusiano wao uliowekwa wakf pamoja na Mungu?

15 Ingawa sasa agano la Torati lilikuwa limebatilishwa, kipindi cha wakati wa Mungu wa pendeleo la pekee na kukazia Wayahudi fikira, kwa msingi wa kwamba wao walikuwa wazao wa asili wa Ibrahimu, hakikuwa kimekwisha bado; kilikwisha kwanza katika mwaka 36 W.K. Kwa hiyo, hata baada ya kumwagwa kwa roho takatifu mara ya kwanza katika mwaka 33 W.K., mtume Petro aliyepakwa mafuta kwa roho aliambia hivi umati wa Wayahudi katika Yerusalemu: “Kwa hiyo, tubuni, na kugeuka [mkaongolewe] ili mfutishe dhambi zenu, kwamba majira ya kuburudisha yapate kuja kutoka kwa Yehova mwenyewe na kwamba apate kumtuma Kristo mliyewekewa ninyi, Yesu.” Ili kutengeneza upya uhusiano wao uliowekwa wakf kwa Mungu sasa kungetia kutubia dhambi zilizofanywa juu ya agano la Torati ambalo wangali walikuwa wanaona wamo ndani yalo walakini pia kujitoa wenyewe wawe washiriki wenye taraja wa taifa hilo jipya, ambayo ndiyo yaliyokuwa mapenzi ya Mungu kwa wote waliokuwa wanafunzi wa Yesu, Wakristo. Hilo linathibitishwa na yale ambayo Petro alitangulia kusema katika siku ya Pentekoste akiwaambia Wayahudi ‘waliochomwa kwenye moyo’ kwa sababu ya kushiriki kwao kutokeza kifo cha Yesu. Petro aliwaambia hivi: “Tubuni, na mwache kila mmoja wa ninyi abatizwe katika jina la Yesu Kristo kwa msamaha wa dhambi zenu, nanyi mtapokea zawadi ya bure ya roho takatifu.” Kwa hiyo mengi zaidi yalitiwa ndani zaidi ya kutubu tu na kuazimia kwa ujumla kufanya vizuri zaidi kwa msingi wa kumsadiki Yesu.​—Matendo 3:19, 20; 2:37-40, NW.

16. (a) Wakati ujumbe wa Ufalme ulipowafikia Wasamaria waliotahiriwa, ubatizo wao katika maji ulifananisha nini? Kwa sababu gani? (b) Ni nini kilichoonyesha wazi kwamba walikuwa wameingizwa katika uhusiano wa agano pamoja na Mungu?

16 Kabla ya kupaa mbinguni, Yesu aliwaambia mitume wake kwamba wangepanua utoaji wa ushuhuda uliomhusu ufike “Samaria na kwenye sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8, NW) Ingawa Wasamaria hawakuwa Waisraeli, ingawa walikuwa watu “wa taifa jingine,” walitahiriwa kwa sababu walivikubali vitabu vya Biblia vilivyoandikwa na Musa nao walimwona kuwa mpatanishi kati yao na Mungu. (Luka 17:16-18, NW) Kwa fadhili Zake zisizostahilika, Yehova aliona ni vema Petro atumie ufunguo wa pekee kwa ajili ya Wasamaria mapema zaidi ya kutumiwa kwa ufunguo ule wa Mataifa wasiotahiriwa katika kufungua nafasi zinazohusiana na ufalme wa mbinguni. Walakini kwa kuwa Wasamaria hao kwa kweli hawakuwa wamekuwa katika agano la Torati ya Musa, na walikuwa ‘wakiabudu wasichokijua,’ wao sasa, kwa kubatizwa, ilifaa kwanza wajiweke wakf wenyewe kwa Yehova Mungu katika jina la Masihi, Yesu akiwa ndiye Mpatanishi wa hilo agano jipya. Baadaye kubatizwa kwao kwa roho takatifu kulionyesha wazi kwamba walikuwa wamekubaliwa kwenye agano jipya hilo.​—Mt. 16:18, 19; Yohana 4:4-42; Matendo 8:5-25.

17. (a) Ni wakati gani na kwa namna gani Mungu aliwafikia watu wasiotahiriwa wasiokuwa Wayahudi “ili achague watu katika hao kwa ajili ya jina lake”? (b) Ubatizo wao katika maji ulifananisha nini?

17 Katika mwaka 36 W.K., wakati wa Mungu wa pendeleo la pekee kwa Wayahudi ulipokwisha, Yehova Mungu aligeuza fikira zake kwa watu wasiotahiriwa ambao hawakuwa Waisraeli, Mataifa, “Ili achague watu katika hao kwa ajili ya jina lake.” (Matendo 15:14-18) Akitumia mwingine wa zile “funguo” Petro alitumwa kwa watu wa nyumba ya akida Mroma aliyeitwa jina lake Kornelio, aliyekuwa anawaonyesha Wayahudi fadhili. Lazima iwe kwamba Mataifa hao waliukubali ushuhuda juu ya Yehova Mungu na Masihi wake aliyetukuzwa, kwa maana roho takatifu iliwaangukia na wakaanza kusema katika lugha mbalimbali. Kwa rehema Mungu alikuwa ameanza kuwapa “hata mataifa nao toba liletalo uzima,” kupitia Yesu Kristo, “Mwana-kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu.” (Matendo 11:18; Yohana 1:29) Yehova alikuwa amewakubali wao, vilevile, waingie katika taifa lake la kiroho kwa msingi wa kujiweka kwao wakf kwake walikokufanya mioyoni mwao. Roho takatifu ilithibitisha jambo hilo. Kwa hiyo hakuna ye yote wa Wayahudi wale waliokuwa wamekuwa Wakristo waliokwenda pamoja na Petro angeweza kupinga amri yake kwamba “wabatizwe kwa jina la Yesu Kristo.” Hiyo ilianzisha ‘kuongoka kwa watu mataifa.’ (Matendo 10:1-48; 15:3) Tangu wakati huo, wote ambao wametamani kumtumikia Mungu, wawe ni Wayahudi au wawe ni Mataifa, wamepaswa kujiweka wakf mioyoni mwao kwa Yehova. Na kwa habari ya ubatizo wao katika maji wanajitoa wenyewe wafanye mapenzi ya Mungu kwao, katika kumwiga Yesu.

[Maelezo ya Chini]

a Kuonekana kwa kwanza-kwanza kwa neno “-wekwa wakf” katika Maandiko ya Kiebrania kunaonekana katika Mwanzo 5:18-24, katika jina “Henoko,” jina ambalo maana yake ni “Wekwa wakf.” Katika maandishi ya Kiebrania jina hilo linaandikwa Hhanokh’, nalo linahusiana na neno la Kiebrania Han ukah, ambalo maana yake ni “Weka wakf.” Katika Yohana 10:22 “sherehe ya kuwekwa wakf” ambayo Yesu alihudhuria inatajwa. (Rotherham; Authorized Version) Mpaka siku hii Wayahudi huiita sherehe hiyo Han ukah, ambayo maana yake ni “Wakf,” kama inavyoonyeshwa na tafsiri za Kiebrania za Yohana 10:22.

b Hakuna maandishi yanayoonyesha wanafunzi hao wa kwanza wa Yesu walibatizwa tena kuwa mfano wa kujitoa kwao wakati fulani kabla ya roho takatifu kumwagwa juu yao katika Pentekoste. Kwa wazi ubatizo wao wa kwanza wa toba walipokuwa wangali chini ya Torati ulitia ndani jambo hilo, nalo hilo lingekuwa ni kumwiga Yesu, kwa kuwa ubatizo wa Yohana ulifanywa kwa kutarajia kutokea kwa Masihi nao uliwatayarisha kwa ajili ya mapenzi ya Mungu kwao kuhusiana na kuja kwake.

Kwa kurudia, je! unaweza kuyajibu maulizo haya?

□ Ni nani wanaojumuishwa (wanaofanyizwa) kuwa “taifa takatifu” au “lililotakaswa” linalotajwa katika 1 Petro 2:9?

□ Waisraeli wa kale walijiwekaje wakf kwa Yehova Mungu?

□ Yesu alipobatizwa, je! alikuwa anajiweka wakf kwa Mungu?

□ Ni nini kilichofananishwa na ubatizo wa maji wa Wasamaria na Mataifa walioamini?

□ Ili kuwa wafuasi wa hatua za Yesu, watu wasiotahiriwa ambao si Wayahudi walipaswa kufanya nini?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki