Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 2/15 kur. 19-24
  • “Ni Nini Kinachonizuia Nisibatizwe?”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Ni Nini Kinachonizuia Nisibatizwe?”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • NAMNA GANI WEWE?
  • KUTUMIKIA MAHALI AMBAPO YEHOVA ANAKUWEKA WEWE
  • Ni Nini Kinachokuzuia Wewe Usibatizwe?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Kutimiza Matakwa ya Ubatizo wa Kikristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Je! Ubatizwe?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • ‘Je! Nibatizwe?’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 2/15 kur. 19-24

“Ni Nini Kinachonizuia Nisibatizwe?”

1. Filipo alitumwa kwa mtu wa namna gani?

ULIZO lililo juu liliulizwa na mtu aliyekuwa mwenye kujitoa sana ambaye tayari alikuwa anampenda Mungu, lakini alikuwa ametoka tu kuarifiwa juu ya “habari njema za Yesu.” Yeye alikuwa towashi Mwethiopia, aliyekuwa “amekwenda Yerusalemu kuabudu” akiwa mwongofu Myahudi. Yeye alikuwa akirudi Ethiopia akaendelee na kazi zake za cheo cha juu katika utumishi wa malkia wa Ethiopia wakati Filipo mwevanjeli (mweneza Injili) alipoongozwa na roho ya Mungu akamkaribie.

2. Filipo alimsaidiaje towashi huyo aufahamu unabii?

2 Akikimbia kando ya gari hilo, Filipo alimsikia mwanamume huyo akisoma kwa sauti kuu kutoka kitabu cha Isaya. Alipoulizwa kama alifahamu kifungu hicho cha Andiko alichokuwa akisoma, juu ya mwana-kondoo aliyekubali kuletwa machinjoni, towashi huyo Mwethiopia alilazimika kukiri kwamba hakufahamu kama nabii huyo alikuwa akisema juu yake mwenyewe au juu ya mtu mwingine. Ulikuwa mwanzo mzuri kama nini kwa Filipo! “Akianza kwa andiko lilo hilo akamhubiri habari njema za Yesu.” Ndiyo, unabii wa Isaya ulihusu “Mwana-kondoo wa Mungu aichukuaye dhambi ya ulimwengu”!—Matendo 8:26-35; Isa. 53:7, 8; Yohana 1:29.

3. Ufahamu huo mpya ulikuwa na matokeo gani kwake?

3 Tukio hilo lisilotazamiwa hata kidogo na lenye kustaajabisha sana lilikuwa na matokeo gani katika maisha ya towashi huyo? “Wakawa wakiendelea njiani, wakafika mahali penye maji; huyo towashi akasema, Tazama maji haya; ni nini kinachonizuia nisibatizwe?” Sana-sana kwa kuwa mwenendo wa maisha na ufahamu wa makusudi ya Mungu ni mambo yaliyomhusu Yesu akiwa Masihi na Mwokozi, kati ya mambo hayo Filipo hakuona jambo la kumzuia mwanamume huyo asibatizwe. Gari hilo likasimamishwa wakaenda kwenye maji pamoja na Filipo akambatiza kwa msingi wa ukubali wake wa dhabihu ya Yesu kwa msamaha wa dhambi.​—Matendo 8:26-39.

NAMNA GANI WEWE?

4.Ni wangapi kati ya wale wanaoshirikiana na Mashahidi wa Yehova wamechukua hatua ya ubatizo?

4 Watu wengi wanaoshirikiana na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote leo hawajabatizwa bado katika wonyesho wa wakf wao kwa Yehova. Kilele cha hesabu ulimwenguni pote cha wale wanaoshiriki kuhubiri “habari njema” katika 1981 kilikuwa 2,361,896 (kati yao karibu 25% hawajabatizwa bado). Walakini kwenye Chakula cha Jioni cha Bwana katika 1981 hudhurio lililounganishwa ulimwenguni pote lilikuwa 5,987,893. Hiyo maana yake ni kwamba zaidi ya nusu ya wale wanaohudhuria mikutano fulani ya Mashahidi wa Yehova hawajabatizwa bado. Je! hilo ni jambo la kututia wasiwasi? Hapana, walakini ni jambo la kuhangaikiwa kwa upendo. Wengine kati ya hawa wameshirikiana nasi kwa zaidi ya miezi michache.

5. Ni kwa njia gani yule towashi Mwethiopia ni mfano mzuri kwa wale ambao hawajabatizwa bado?

5 Pengine mmoja wa wale ambao hawajabatizwa bado ni wewe, ewe msomaji mpendwa. Sababu yako ya kutobatizwa bado yaweza kuwa nzuri, walakini kama sivyo, twakualika ufikirie kwa uangalifu na kwa sala mfano mwema wa yule towashi Mwethiopia ambaye hakukawia-kawia kubatizwa. Alichunguza akili na moyo wake mwenyewe, na akamwuliza Filipo iwapo yalikuwako mambo yo yote ya kumzuia asibatizwe. Alipojua hakuna cha kumzuia alibatizwa mara moja.

6. Ni hatua gani zinazopasa kuchukuliwa na wale wanaoona kwamba wanahitaji wakati mwingi zaidi?

6 Huenda ukawa hujabatizwa kwa ajili ya namna unavyokata maneno, kwa kutegemea namna unavyopima mambo kwa unyofu, kwamba wewe bado huna maarifa ya kutosha ya Neno la Mungu kufanya wakf kwa Yehova unaotoka moyoni. Ili kufanya hivyo bila kuweka masharti yo yote, wataka kumjua Yehova na makusudi yake vizuri zaidi. Hilo ni jambo la kusifika, nasi tunakutia moyo uendelee kufanya maendeleo mazuri katika mafunzo yako, huku ukikumbuka kwamba wakati unasonga mbele kila siku. Tumia vizuri zaidi nafasi zako za kujifunza Biblia faraghani na kwa msaada wa Mashahidi wa Yehova. (2 Tim. 3:16, 17) Sitawisha zoea la kawaida la kuhudhuria mikutano ya Kikristo, ambako utapokea maagizo ya lazima na ushirika unaohitajiwa pamoja na Wakristo wenzi na kitia-moyo kutoka kwao. (Ebr. 10:24, 25) Unapofuata kawaida hii ya kufanya mambo kwa kujitahidi, inaelekea kwamba haitapita miezi mingi kabla hujawa tayari kuuonyesha wakf wako kwa ubatizo wa maji. Baba yetu wa kimbinguni anakualika wewe uingie katika uhusiano huo wa pekee sana pamoja na yeye!

7. (a) Wengine wanaokawia-kawia kubatizwa huenda wakawa wanawaza namna gani? (b) Yesu anaonyeshaje kuwa hilo ni hatari?

7 Pengine wewe ni mmoja ambaye amekuwa akihudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova kwa miaka kadha walakini bado hujaamua kuchukua hatua za wakf na ubatizo. Unapochunguza akili ya siri ya moyoni, je! yaweza kuwa unakawia-kawia kwa sababu unaona kwamba kuishi kama Mkristo kungekuwekea vizuizi wewe? Je! unawaza kwamba maadamu hujabatizwa hutapatwa na vizuizi hivyo na utakuwa na “uhuru” fulani wa kufanya mambo fulani yasiyofaa wakati taratibu hii ya kale inapoendela kuwapo, ukitumaini kungojea mpaka dakika ya mwisho ili uchukue msimamo wako wa ibada ya kweli? Kuwaza kwa njia hiyo kwaweza kuwa hatari, kwaweza kuleta msiba kweli kweli! Yesu alisema hivi: “Jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo.”​—Luka 21:34, 35; 1 Kor. 15:33, 34; Rum. 13:11-14.

8. Twapaswa kuuonaje mwaliko wa upendo wa Yehova na kujiweka wakf wenyewe kwake?

8 Ukikawia-kawia isivyofaa kuukubali mwaliko wa upendo wa Yehova wa kuwa na kibali yake kwa kuweka maisha yako wakf kwake, wakati unaokubalika wa kuendeleza mwaliko huo huenda ukaisha kwa habari yako wewe. (2 Kor. 6:1, 2; Ebr. 12:25) Kwa hiyo usisite kuchukua zawadi ya uzima na kumkaribia yeye kwa kushukuru. Usiendelee kutazama nyuma kwa kutamani vivuta macho vya taratibu hii, ambayo karibuni itaangamia. Itikia upendo wa Mungu wakati ungali na nafasi. Ingawa yeye ni mteuzi kuhusu wale anaowaleta katika uhusiano wa karibu na yeye na ni mwenye kuweka vizuizi fulani juu ya mambo yanayoweza kufanywa na yasiyoweza kufanywa, kwa kadiri unavyomjua Yehova zaidi, ndivyo utakavyoona kwamba yale anayofanya au anayoyataka sikuzote ni bora kwako. Yeye hataki kukunyima cho chote ambacho kweli kweli ni chema au kitakachokupa furaha ya kuendelea. (Zab. 145:16, 19) Mwana mwenye heshima na mwenye utii huliona kuwa jambo la asili kabisa kuwa pamoja na baba yake wa kidunia na kushauriwa naye. Basi yapasa kuwa zaidi hivyo juu ya nia yako kwa Baba yetu wa kimbinguni mwenye upendo!—Yohana 14:23.

9. Twapaswa kuyaelekeaje matatizo ya kibinafsi?

9 Bila shaka, iwapo unapigana kweli kweli kutawala tamaa fulani ya mwili, na unajaribu kikweli kwa moyo wako wote na nguvu zako zote kuishinda, unaweza kuwa na hakika kwamba Mungu atakusaidia​—ushinde​—si kwa mwujiza wa kuondoa tatizo hilo, bali kwa msaada wa roho yake wa kusitawisha matunda yanayohitajiwa ya roho maishani mwako. Vile-vile, katika kundi utaonyeshwa huruma (ufahamu) na kusaidiwa kwa kuwafikia wanaume wazee. Wao wako hapo wakiwa ni msaada wa kukusaidia.​—Gal. 5:22-24; Efe. 4:11-15.

10, 11. (a) Mlinda-gereza Mfilipi na watu wa nyumba yake waliweka mfano gani mwema? (b) Ili ‘kuokolewa,’ je! mengi zaidi yalitiwa ndani zaidi ya kumsadiki Yesu tu?

10 Kwa hiyo usikawie-kawie kufanya yale unayojua wapaswa kuyafanya ili umpendeze Mungu. Ufuate mfano mzuri wa mlinda-gereza wa Filipi aliyewauliza Paulo na Sila: “Bwana zangu, yanipasa nifanye nini nipate kuokoka?” Alipoambiwa “mwamini Bwana Yesu, nawe utaokoka pamoja na nyumba yako,” masimulizi yanaendelea kutuambia kwamba “akabatizwa [bila kukawia-kawia], yeye na watu wake wote.”

11 Ingawa tetemeko la ardhi kutoka kwa Mungu hapo kwanza lilitumika kutia woga wa kimungu katika mlinda-gereza huyo, tusitazamie tuamshwe na jambo kama hilo la ajabu kutoka kwa Mungu leo ili turudiwe na fahamu zetu na kuondolea mbali hali yetu ya kutotaka. Kwa habari ya mwanamume huyo na watu wa nyumba yake hilo halikuwa jambo dogo tu la kumsadiki Yesu ambalo likawaweka katika hali ya kuokolewa. Wala halikuwa tendo la kila siku tu la njia ya maisha ya Kikristo. Hapana, kwa maana masimulizi yanasema kwamba Paulo na Sila walimwambia “neno la [Yehova], yeye na watu wote waliomo nyumbani mwake.” Hiyo ilitia kumjua Yehova vya kutosha ili kwanza wapate msamaha wa hali ya dhambi ya wakati uliopita kwa msingi wa kuikubali dhabihu ya ukombozi. Ni kweli kwamba jambo hilo lilichukua muda mfupi sana, kwa habari yao, kwa siku moja tu. Hayo yalifuatwa na kujiweka kwao wakf kwa kutoka moyoni kwa Bwana Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, Yehova Mungu, na kubatizwa katika wonyesho wa hilo. Ndiyo, mlinda-gereza huyo “akafurahi sana, yeye na nyumba yake yote, maana amekwisha kumwamini Mungu.”​—Matendo 16:25-34.

12. Je! ukosefu wa ufahamu kamili wa mambo fulani unapasa kumkawiza mtu asibatizwe?

12 Pengine wewe ni mmoja anayesita kwa sababu ya shaka au ulizo fulani linalosumbua-sumbua. Walakini ikiwa jambo fulani juu ya fundisho la kidini lingali halijatatuliwa, kuna kila sababu ya kuchunguza kupata jibu katika Neno la Mungu, ukisali bila kukoma kwa Mungu ili akupe ufahamu. Yeye atafanya hivyo, wakati unapomtumaini kabisa. Yeye hataweka “jiwe” au “nyoka” katika mkono wako ulionyoshwa. (Mt. 7:7-11) Usitoe udhuru wa kutoweka maisha yako wakf kwake kwa sababu ya mambo fulani machache ambayo pengine huyafahamu kabisa. Mkristo anaendelea kukua katika maarifa ya Mungu na makusudi Yake.​—Flp. 1:9-11; Ebr. 6:1-3.

13. (a) Ni jambo gani linalotambuliwa juu ya watoto wachanga walioko katikati yetu? (b) Mtu wa umri mdogo anapaswa kubatizwa wakati gani?

13 Na mwisho kabisa, huenda ukajiona kwamba wewe ni mchanga sana kuweza kujiweka wakf inavyofaa kwa ufahamu. Kwa wengi, hiyo yaweza kuwa kweli, kwa kuwa kuna maelfu ya watoto wachanga wanaoshirikiana na Mashahidi wa Yehova​—jambo ambalo kwetu ni la kufurahisha. (Mt. 19:13-15) Wanapokua wapate kukomaa vya kutosha, katika akili na mwili, ili wajichukulie wenyewe daraka la wakf na ubatizo, twaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu ‘anatia alama’ watoto hao wawe “watakatifu,” mradi wanaitikia na kuwatii wazazi wao wanaoamini. (1 Kor. 7:14) Walakini wakati hausimami mahali pale pale. Ikiwa umefuata namna wazazi wako wamekulea “katika adabu na rekebisho la akilini la Yehova,” nawe umejibidiisha kujifunza nyumbani na kundini, je! sasa wakati umefika ujiweke wakf kwa Yehova? Ikiwa ndivyo, baada ya kuzungumza jambo hilo pamoja na wazazi wako na wazee katika kundi lako, tunakutia moyo uendelee kushikamana na uamuzi wako wa kuweka wakf maisha yako kwa Yehova na kubatizwa.​—Efe. 6:1-4, NW; 2 Tim. 1:5-7.

KUTUMIKIA MAHALI AMBAPO YEHOVA ANAKUWEKA WEWE

14. Ni mambo gani yanayopasa kuangaliwa sasa kuhusu ‘kuvunwa’ kwa waliotiwa mafuta?

14 Baada ya kubatizwa sasa, je! kuna tumaini kwamba Mungu atakuita uwe sehemu ya bibi-arusi wa Kristo? Kwa wazi, Mungu ndiye mwamuzi, wala si wanadamu. Maono ya ndani na maelekeo ya mtu, kama yale ambayo huenda yakawa yalitiwa ndani yake alipokuwa katika madhehebu fulani ya Jumuiya ya Wakristo hayapasi kuamua. (Rum. 8:28-30; 9:16) Ni jambo la maana kukumbuka kwamba ‘kuvunwa’ kwa waliotiwa mafuta kunakaribia mwisho wake haraka sana. (Linganisha Mathayo 13:36-43.) Kwa karne 19 kulikuwako mwito mmoja tu, ule wa kimbinguni, na Yehova alikuwa mteuzi sana juu ya wale ambao wangetumikia na Mwanawe kuwa washiriki wa serikali ya kifalme. Wengi wangealikwa lakini ni wachache wenye thamani ambao wangechaguliwa. (Mt. 22:2, 14) Baada ya wakati hesabu iliyowekwa yenye kikomo ya 144,000 ingefikiwa. Baada ya hiyo hakuna wengine ambao wangetiwa mafuta kwa roho takatifu ikiwa ni ushuhuda wa kwamba walikuwa na tumaini la kimbinguni isipokuwa, jambo linalotokea mara chache sana, kutokuaminika kwa mmoja wa waliosalia wa ‘waliochaguliwa’ kufanye iwe lazima mahali pake pachukuliwe na mwingine.​—Rum. 8:16; 11:19; Ufu. 7:1-8; 14:1-5.

15, 16. (a) Ni jambo gani linaloonekana wazi kwa habari ya kumalizika kwa mwito wa kimbinguni na kukusanywa kwa ule “mkutano mkubwa”? (b) Katika wakati huu ulioendelea sana, ni nini lingekuwa jambo la akili kwa habari ya mahali pa mmoja kuchukuliwa na mwingine? (c) Hata hivyo, dai lo lote la mtu la kibinafsi la mwito wa kimbinguni lapasa lionweje?

15 Tunapochunguza namna Yehova amekuwa akishughulika na watu wake wakati wa hiki ‘kipindi cha mavuno,’ inaonekana wazi kwamba mwito wa kimbinguni kwa ujumla ulikwisha karibu mwaka 1935, wakati tumaini la ule “mkutano mkubwa” wa Ufunuo 7:9-17 lilipofahamika inavyofaa kuwa la kidunia. Matokeo yamekuwa kama vile Yehova alivyotangulia kujua kwamba yangekuwa. Kama ambavyo Ufunuo 7:3, 4 unavyoonyesha, kungekuwako ‘kutia muhuri’ kwa mwisho kwa waliosalia wa Israeli wa kiroho. Walakini, katika wakati huu unaotangulia ile “dhiki kubwa,” “mkutano mkubwa” usio na kikomo katika hesabu yake ungetokea. Wangeendelea kuwa na tumaini lao la asili la kuishi duniani, wala si kuzaliwa mara ya pili wakitazamia uzima wa kimbinguni.​—Zab. 115:16; Yohana 3:1-8.

16 Kwa habari ya uwezekano wa ‘kuzaliwa mara ya pili’ ili kuchukua mahali pa mwingine katika wakati huu ulioendelea sana, kwa kufahamika ni wachache sana tu kati ya hawa waliobaki waliotiwa mafuta wanaoweza kupoteza mwito wao wa kimbinguni kwa kukosa uaminifu. Hesabu zao zimepunguzwa sana sasa na kifo wakabaki maelfu machache tu. Je! ikiwa lazima mahali pa mmoja pachukuliwe na mwingine, Yehova angemwita nani? Yesu alisema juu ya wale walioalikwa wawe mitume wake: “Nanyi ndinyi mliodumu pamoja nami katika majaribu yangu.” (Luka 22:28) Ni jambo la akili, Yehova angechagua mtu ambaye amekuwa mshiriki kwa miaka mingi, na ambaye amekwisha kuonyesha uvumilivu na ushikamanifu chini ya jaribu, kuliko mtu aliyebatizwa hivi karibuni akawa mwanafunzi wa Yesu na pengine bado hajajaribiwa katika njia nyingi. Hayo hayasemwi yawe kanuni au yatoe msingi wa kuamua juu ya dai la kibinafsi la mtu, bali ili kuwasaidia wapya walioanza kushiriki waepuke kujitanguliza na kuwa na hakika juu ya namna Yehova anavyoshughulikia.

17. Wakf na ubatizo huanzisha uhusiano gani, ukiongoza kwenye thawabu gani?

17 Mtu awe ni wa “kundi dogo” la warithi wa Ufalme au awe ana tumaini bora sana la kuishi milele katika ukamilifu na furaha juu ya dunia, uhusiano huo unaanza tukiisha kupata kibali ya Baba yetu, Yehova. (Luka 12:32) Na tunaupataje msimamo unaokubalika mbele ya Mungu? Ni kwa kuyatwaa maarifa, kuiamini dhabihu ya Kristo, kutubu juu ya mwendo wetu wa kwanza katika ulimwengu, kugeuka inavyofaa ili kufanya mapenzi ya Mungu, kuweka maisha yetu wakf kwa Yehova na kubatizwa katika wonyesho wa jambo hilo. Kisha, tukiuhifadhi uhusiano wetu wenye thamani pamoja na Mungu, yeye ni mwaminifu kwa kuwa atatuthawabisha kwa uzima wa milele, ambao ni mali yenye thamani kubwa sana iwe ni katika mbingu au katika makao ya Ufalme huo hapa duniani.​—Ebr. 11:6; Rum. 6:23.

18. Ni katika njia gani kazi ya ‘kutia alama’ inaendelea sasa, na watu mmoja mmoja huonyeshaje kwamba ‘wametiwa alama’ ya kupata wokovu?

18 Hivi karibuni kutenga “kondoo” na “mbuzi” kutafikia mwisho. Wakati Mungu atakapoileta ile “dhiki kubwa” awafagilie mbali “wao wasiomjua Mungu, na wao wasioitii Injili ya Bwana wetu Yesu,” hakuna mtu atakayeachwa akiwa katika hali ya bila kuamua jambo mojalapo. (Mt. 25:31-46; 2 The. 1:6-9) Ni wale tu ‘waliotiwa alama’ ya wokovu watakaookoka na kuingia katika taratibu mpya yake. (Ufu. 7:3, 4, 9, 14; Eze. 9:2-6) Wale ambao wamekubali ‘kutiwa alama’ hiyo yenye kuleta wokovu watakuwa wenye furaha kama nini kwa sababu ya kukubaliwa waingie katika uhusiano uliowekwa wakf pamoja na Yehova Mungu kama unavyoonyeshwa na ubatizo wa maji, na kuendelea kuwa wakamilifu katika barabara nyembamba inayoongoza kwenye uzima!—Mt. 7:13, 14.​—Kutoka The Watchtower, Februari 15 1982.

Je! kwa kurudia wewe unaweza kuyajibu maulizo haya?

□ Towashi Mwethiopia aliwekaje mfano mwema katika kubatizwa?

□ Kwa sababu gani mtu hapaswi kukawia-kawia kuweka kando vivuta macho vya hii taratibu apendelee kuukubali mwaliko wa upendo wa Yehova?

□ Kumtumaini Yehova kutamsaidiaje mtu kunapokuwa shaka au ulizo linalosumbua-sumbua?

□ Unapaswa kuuonaje wakf na ubatizo?

□ Ni jambo la akili kwamba Yehova atamchagua nani ikiwa lazima mahali pa Mwisraeli mmoja wa kiroho pachukuliwe na mwingine?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki