Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 3/1 kur. 5-8
  • Wewe Unaweza Kuwa Jirani Mwema

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wewe Unaweza Kuwa Jirani Mwema
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mambo Yanayopasa Kufanywa Katika Hali ya Ujirani
  • Mambo Yasiyopasa Kufanywa Katika Hali ya Ujirani
  • Uwezo wo Hali ya Ujirani
  • Majirani Wema Wanafaa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Hali ya Ujirani Imekwenda Wapi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • “Mpende Jirani Yako Kama Wewe Mwenyewe”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Hubiri Ukiwa Jirani Mwema
    Huduma Yetu ya Ufalme—2001
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 3/1 kur. 5-8

Wewe Unaweza Kuwa Jirani Mwema

WAKATI watu wa umri mkubwa wanaposema habari ya “zile zamani zenye mambo mazuri,” unafikiri wana maana gani? Zamani zilizopita hazikuwa “zenye mambo mazuri” kwa watu wengi upande wa utajiri wa kimwili, starehe na vifaa vyenye kurahisisha mambo au upande wa matibabu. Hakukuwa na televisheni, motokaa zilikuwa chache, hata simu au vitu vingine ambavyo watu wengi leo wanaona visipokuwapo maisha ni magumu. Basi, ni kitu gani kilichokuwa kizuri sana zamani hizo? Bila shaka wanachomaanisha ni hali ya ujirani iliyokuwako.

Ingawa usalama wa hali ya pesa ulikuwa mdogo, watu walikuwa wakisaidiana. Kama wanavyosema watu wengi wa umri mkubwa, hata kama mtu alikuwa maskini wa mwisho, sikuzote alikuwa na kitu cha kumkopesha jirani yake. Kama mtu alikuwa mgonjwa sana, jirani zake walikuwa wakimpa msaada wa matendo, kama vile kumpikia au kumtunzia watoto. Kama mtu alikuwa na kazi kubwa nyumbani kwake, jirani zake walikuwa na kawaida ya kuja haraka na kumsaidia.

Walakini, kwa kuwa wakuu wa kiserikali wanazidi nyakati zote kufanyia watu mambo, watu wenyewe wanapunguza nyakati zote hali ya kuhitajiana. Hata hivyo, tunalazimika bado kuishi pamoja na jirani zetu. Biblia ilionya zamani za kale kwamba “yeye anayejitenga mbali na wengine atatafuta tamaa yake mwenyewe ya kichoyo.” (Mithali 18:1, NW) Mtu anayekataa kuchangamana na wengine anakosa usawaziko mwishowe, hata anakuwa mtu kiajabu-ajabu.

Ni kweli kwamba kwa kawaida hatujichagulii watu tunaotaka wawe jirani zetu, wala sio wanaotuchagua sisi tuwe jirani zao. Na “mashirika mabaya yanaharibu” kikweli “mazoea mazuri.” (1 Wakorintho 15:33, NW) Lakini tukijifunza kuishi na jirani wa namna hiyo kwa hekima, wao watapata faida na hata sisi. Ili kufanya hivyo ni mambo gani yanayohitajiwa?

Mambo Yanayopasa Kufanywa Katika Hali ya Ujirani

Kuwa jirani mwema kunataka ufahamu. Mambo tofauti-tofauti yanakubalika katika namna tofauti-tofauti za ujirani. Ikiwa sisi tumetoka katika eneo la mashambani ambako watu wanatembeleana nyakati zote, huenda ikatupasa kubadilika tukihamia mji mkubwa ambako hatuwezi kutembeleana sana kama mashambani. Katika miji fulani mikubwa maeneo mbalimbali ya ujirani yanakuwa na mchanganyiko. Yanakuwa na watu waliotoka katika hali mbalimbali za maisha. Huenda wengine wakafanya mambo kwa njia ambayo haikuwa kawaida yetu kuiona, lakini mradi hawasumbui watu wote au kujaribu kuharibu jamaa yetu wenyewe, sababu gani tuwalaumu-laumu?

Jirani mwema anahitaji pia kuwa na urafiki. Je! kweli tunapoteza saa zetu ikiwa tunatabasamu kwa kuwasalimu “Habari ya asubuhi?” watu tunaopitana nao njiani? Hata uso mmoja tu wenye kuchangamka unaweza kufanya kikundi kizima cha watu kijisikie vizuri zaidi.

Tukiwa na urafiki, tutataka pia kujua majina ya watu wanaoishi karibu nasi. Tukiongea na jirani zetu kwa kuwataja majina, tunaonyesha kwamba tunawachukua kama watu mmoja mmoja, na inaelekea wataelekea zaidi kutuchangamkia sisi.

Jirani mwema anahitaji kuonyesha kuhangaikia watu, pia. Ikiwa mtu fulani wa karibu ni mgonjwa, mtu anaonyesha anamhangaikia kwa kukumbuka kuuliza sasa yukoje na kumwambia maneno machache ya kumfariji. Huenda hata kukawa na kazi fulani ndogo tunayoweza kumfanyia kusaidia kupunguza furushi lake. Pia, ikiwa karibu yetu anaishi mtu wa umri mkubwa, sababu gani tusijaribu kumwonyesha huyo hali ya huruma zaidi? Kwa mfano, ikiwa tunakwenda tukanunue vitu vyetu, labda tunaweza kumnunulia mzee huyo kitu fulani. Ikiwa taa fulani imeachwa ikiwaka katika nyumba yake kwa muda mrefu isivyo kawaida, au mlango umeachwa wazi, sababu gani tusiende kuangalia kuna nini tuhakikishe kwamba mambo yote ni sawa?

Na namna gani tukiona uhalifu ukiendelea kutendwa au jambo fulani linaloonekana kuwa kosa? Kwa kawaida si hekima kujitupa ndani ya jambo hilo moja kwa moja kidume na kujaribu kuimaliza hali hiyo. Watu waliopewa mazoezi ndio kwa kawaida wanaofanya vizuri zaidi jambo la namna hiyo kuliko vile sisi tunavyoweza kufanya. Lakini walau hangaiko la hali ya ujirani litatusukuma tujulishe upesi polisi, na labda tuchungulie mambo kwa urefu ambayo yanaweza kuwasaidia baadaye.

Uongozi wenye mafaa katika kushughulika na jirani zetu ni ile kanuni nzuri sana inayosema: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Hivyo, tukiona tatizo linalohusu jirani yetu, na tunashindwa kujua la kufanya, tujiulize hivi: “Mimi ningetaka mtu anifanyie nini kama ningekuwa katika hali hiyo?” Jibu la ulizo hilo litatusaidia kufanya uamuzi wa hekima.

Wakati mmoja mtu mwenye kusimama karibu na Yesu alimwuliza hivi: “Jirani yangu ni nani?” Yesu alijibu kwa kusimulia mfano wa yule “Msamaria mwema.” Alionyesha kwamba jirani halisi ni yule atakayesaidia mtu akimwona katika uhitaji. Tukiwaonyesha jirani zetu urafiki, ufahamu na hangaiko juu yao, tutakuwa tukiufuata mfano mwema huo.​—Luka 10:29-37.

Mambo Yasiyopasa Kufanywa Katika Hali ya Ujirani

Vilevile kuna mambo fulani ambayo jirani mwema hatafanya. Atayaepuka kwa sababu ni mwenye huruma ya kuwafikia wengine. Kwa mfano, yeye hatafungulia kinanda chake au televisheni (au radio) sauti kubwa sana ili jirani wote wajue kuna kinanda kinachoimba mahali fulani. Yeye ataweka nyumba na mazingira yake katika hali ya kupendeza macho na ya usafi, na hivyo hataharibu sura nzuri ya ujirani huo.

Mwanamume mmoja mwenye hekima aliandika hivi zamani za kale: “Mguu wako usiingie katika nyumba ya jirani yako ila kwa kiasi; asije akakukinai na kukuchukia.” (Mithali 25:17) Ndiyo, ingawa kutembelea jirani mara kwa mara ni jambo linaloweza kuwapendeza, wanaweza kuchoka upesi wakiwa na mtu wa kuwatembelea saa zote tuu.

Halafu tena mtume Paulo alionya tujihadhari na wale walioendelea ‘kuzunguka-zunguka nyumba kwa nyumba’ na wakawa ni “wachongezi na wadadisi, wakinena maneno yasiyowapasa.” (1 Timotheo 5:13) Tunaepuka kueneza porojo na malaumu juu ya watu wa mahali tunapoishi tukipunguza wakati tunaotumia tukiwa tumetembelea jirani zetu. Zaidi ya hilo, watu walio wengi leo wanalalamika wakisema hawana wakati wa kutosha kufanya mambo yote wanayotaka. Tukitumia wakati mwingi mno katika maongezi na matembezi ya kirafiki, huenda nafasi ikakosekana ya kufanya jambo fulani lililo la maana zaidi.

Jirani mwema anakuwa na heshima kwa wale walio karibu yake na anashughulika nao kwa upole. Basi yeye hatafanya vitatizo vidogo viwe magumu makubwa. Jioni moja wakati wa kiangazi huko Amsterdam baba mmoja aliudhika kwa sababu kelele yenye kufanywa na radio fulani upande mwingine wa barabara ilikuwa ikizuia watoto wake wasilale. Mke wake akatumia uanana (upole) kwa kupendekeza amwendee jirani huyo na kumweleza tatizo lenyewe. Jirani yake alipolisikia tatizo lenyewe alizungumza naye kwa kutumia kiasi, akafurahia kuonyesha ushirikiano. Aliifunga radio, akasema: “Hata hivyo mimi huwa sisikilizi siasa hizo!” Ingawa hali hiyo ingaliweza kuwa mbaya, iliepukwa kwa kuishughulikia kiupole, na wale jirani wawili wakawa rafiki wakubwa.

Mwishowe, tunahitaji busara na usawaziko. Huenda wengine wa jirani zetu wakawa wana tabia mbaya. Huenda wakawa wanavuta sigara, kusema mambo machafu au kuishi maisha za uasherati. Katika maeneo mengine matineja wanatumia dawa za kulevya na kujianzishia magenge (makundi-makundi) yao wenyewe. Kwa hiyo inatupasa tusawazishe hali yetu ya ujirani kwa kuhakikisha kwamba watoto wetu hawapakwi tabia mbaya na watoto jirani. Ndiyo, kuwa jirani mwema kunatia ndani mambo mengi.

Uwezo wo Hali ya Ujirani

Mapema katika mwaka wa 1980, John, mzee katika kundi la Mashahidi wa Yehova, alijikuta katika hali ambamo hali ya kujisikia akiwa na hali ya ujirani ilikuwa imevunjika kabisa. Jambo hilo lilitukia katika mji mmoja huko Oklahoma, United States (Amerika). Tineja (kijana) mweusi alikuwa ameuawa, na watu weusi wa huko walikuwa na wazo la kwamba polisi hawakuwa wakijali kuchukua hatua. Kukafyatuka ghasia kali sana zinazohusu ubaguzi wa rangi. Risasi zilimiminwa kweli kweli.

Hata hivyo makao ya John yalikuwa kama mahali penye starehe katika msukosuko huo. Ingawa ilimbidi yeye, mkewe na binti yake tineja, walale sakafuni muda wa saa kadha ili kuepuka kugongwa na risasi zenye kukosa shabaha, nyumba yao haikuwa na mikazo wala chuki yenye kusababishwa na ubaguzi wa rangi. Kwa kweli, jamaa hiyo ya weupe ilikubali msichana mweusi na jamaa ya watu wa kutoka Mexico ijifiche pamoja nao katika nyumba yao. Mke wa John alisema: “Najua kuna matata; mimi si kipofu. Lakini kwa kutegemea msingi unaofanya tushughulike pamoja na watu​—weusi kwa weupe​—kuna uhusiano mwema.”

Ndiyo, jamaa hii ilikuwa imekuwa jirani wema kwa watu waliokuwa karibu yao. Walikuwa wamewaonyesha heshima na huruma ya kuwafikiria hali zao, na basi wao pia waliheshimiwa na watu hao. Wao hawakuonyeshwa na watu chuki za ubaguzi wa rangi.

Siku chache baada ya ghasia hizo, walipokuwa wakihubiri nyumba kwa nyumba (utumishi wa ujirani ambao Mashahidi wa Yehova wote wanaushiriki), waliweza kuwakuta watu wa ukoo wa mvulana ambaye kifo chake ndicho kilizusha jeuri ile. Walitumia hali ya urafiki wakawapa pole na kuwatolea msaada mzuri zaidi ya wote ambao wangeweza kutoa. Wakawaeleza habari za tumaini hakika la ufufuo kutoka kwa wafu na taraja la kuishi hivi karibuni katika ulimwengu ambamo watu wote watakuwa ni jirani wema. Ulimwengu huo umeelezwa habari zake katika mstari mmoja katika kitabu cha Biblia cha Isaya: “Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua [Yehova], kama vile maji yanavyoifunika bahari.”​—Isaya 11:9.

Kwa hakika sisi sote tungependa kuishi katika ulimwengu wa namna hiyo. Lakini wakati tunapoungoja, inatupasa tuishi na mambo kama yalivyo. Hata hivyo, tukitumia usawaziko na hali ya ujirani kuwaelekea watu walio karibu yetu kama vile John na jamaa yake walivyofanya, kuwafikiria kwa huruma na kuwaheshimu, tutaona maisha yakifurahisha zaidi. Halafu nani ajuaye? Labda jirani zetu nao watatuonyesha zaidi hali ya ujirani.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki