Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 9/1 kur. 6-8
  • Uongo wa Kwanza—Kuondoa Matokeo Yake

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uongo wa Kwanza—Kuondoa Matokeo Yake
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ukristo na Ukafiri wa Kidini
  • Upotovu Kutoka Ndani
  • Paradiso Yarudishwa Tena
  • Kichwa Kitukufu cha Biblia
    Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
  • Upatano wa Biblia Yote
    Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?
  • Serikali Itakayoleta Paradiso
    Serikali Itakayoleta Paradiso
  • Ukristo—Je! Yesu Alikuwa Ndiye Njia ya Kuongoza kwa Mungu
    Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 9/1 kur. 6-8

Uongo wa Kwanza—Kuondoa Matokeo Yake

SI KILA mtu aliyemfuata Shetani wala kukubali mabuni yake ya kidini. Kwa mfano, Ibrahimu, aliendelea kumwabudu Mungu wa kweli. Yeye aliamini kwamba msingi pekee wa uzima ulitegemea kumtii Mungu. Kwa sababu hiyo Yehova alimbariki, akasema: “Na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia.” (Mwanzo 22:18) Maana ya hayo ilikuwa nini? Kwa wazi, “uzao” huo ulioahidiwa hapo mbele sana katika Edeni ungetokea kati ya watoto wa Ibrahimu.​—Wagalatia 3: l6

Baaadye, mambo mengine ya undani juu ya “uzao” huo walifunuliwa watu waaminifu. Yeye angezaliwa katika kabila la Yuda, ili awe mzao wa Mfalme Daudi. Yeye angezaliwa na bikira, katika mji wa Bethlehemu. (Mwanzo 49:10; 2 Samweli 7:16; Isaya 7:14; Mika 5:2) Wakati wenyewe ulipofika, “uzao” ulioahidiwa ulizaliwa mahali pale kabisa katika jamaa ile kabisa. Uzao huo alikuwa ni Yesu, ambaye baadaye aliitwa jina Kristo.​—Luka 2:8-11.

Wakati wa kuzaliwa kwa Yesu ulimwengu wa Shetani ulikuwa ndani ya giza nene la kidini. Chini ya utawala wa Roma, ambayo ilikuwa milki yenye nguvu zaidi wakati huo, dini nyingi mbalimbali za Kibabeli zilikuwa zinasitawi. Wazao wengi wa Ibrahimu mwaminifu, Waisraeli, walikuwa wamekengeuka wakaiacha ibada ya kweli. Viongozi wao wa kidini walikuwa wakijionyesha kuwa wenye haki na walikuwa wenye kiburi. Wengine walikuwa wameangukia mafundisho ya Kibabeli. Kulingana na mwanahistoria Myahudi, Yosefo, Mafarisayo (madhehebu moja ya kidini iliyokuwa maarufu) walisadiki kwamba “nafsi zina nguvu isiyokufa ndani yazo” na “kwamba nafsi za watu wabaya zinapatwa na adhabu ya milele.”

Yesu aliweza kurudisha wengi kwenye ibada safi. Yeye aliwafunza wafuasi wake ‘wasiwe sehemu’ ya taratibu ya mambo ya Shetani, ama kwa njia ya kidini ama kwa njia ya kisiasa. (Yohana 15:19, NW) Yeye aliwaponya wagonjwa akawafufua wafu na akawahurumia sana wale maskini. Watu hao walimpenda Yesu, lakini makuhani wengi walimchukia kwa sababu alifunua wazi njia zao za uonezi na mafundisho ya uongo. Kwa hiyo, mwishowe walimwua.

Baada ya Yesu kufa lazima Shetani awe aliona ameshinda, lakini, kama ndivyo, ilikuwa ni kwa muda mfupi tu. Karibuni Mungu alimfufua Yesu kutoka kwa wafu na kumwingiza kwenye uzima wa roho. Na kupitia kifo na ufufuo wa Yesu, Mungu alichukua hatua kubwa ya kuelekea kuondoa matokeo mabaya zaidi ya uongo wa Shetani. Yeye alitoa uwezekano kwa wale wote waliotaka kufuata njia ya ile kweli ili waupate tena uzima ambao Adamu alikuwa amepoteza kwa kutokutii kwake. “Kwa kuwa kama katika Adamu wote wanakufa,” ndivyo alivyosema mtume Paulo, “kadhalika katika Kristo wote [watafanywa hai].”​—1 Wakorintho 15:22-26.

Ukristo na Ukafiri wa Kidini

Sasa ikawa inawezekana wanadamu kupata wokovu kutokana na dhambi na mauti. Paradiso itarudishwa kupitia ufalme wa Mungu, ambao mtawala wake atakuwa ni Yesu Kristo aliyefufuliwa. Hata wanadamu wengine wangekuwa na pendeleo la kushiriki katika utawala huo wa Ufalme. Ujumbe huo wenye mkazo mwingi, uliotangazwa katika karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida wetu, ulichochea mioyo ya watu wengi. Kundi la wafuasi wa Kristo—ambao baadaye waliitwa Wakristo—lilifanyizwa katika Yerusalemu, na karibuni hesabu ikakua kufikia maelfu mengi.

Akiwa ameghadhibika, Shetani alishambulia. Karibuni Wakristo wakawa wanafia Yerusalemu kwa ajili ya imani yao. Mateso yaliwafukuza wengi kutoka mji huo, walakini walikwenda pamoja na “habari njema.” Wasamaria, kisha watu wa Mataifa, walibatizwa kuwa Wakristo. Kwa makumi machache ya miaka ujumbe huo ulikuwa umesambaa katika ulimwengu wote uliokuwa umejulikana wakati huo. Hizo zilikuwa nyakati zenye kujaa matukio!​—Matendo 17:6; Wakolosai 1:23.

Mwishowe, katika siku za bedui (mkatili) Mtawala Nero, nguvu za Milki ya Roma zilielekezwa juu ya Wakristo. Miili yenye kuchomeka ya Wakristo ilitumika kama viangaza kwenye sherehe za Kiroma. Wanyama-mwitu walifunguliwa juu yao katika viwanja. Hata hivyo, Ukristo uliendelea kuenea. Walakini Shetani alikuwa na njia nyingine za kutumia.

Upotovu Kutoka Ndani

Mtume Paulo alikuwa amewaonya hivi Wakristo Wakolosai: “Angalieni mtu asiwafanye mateka kwa elimu yake ya bure na madanganyo matupu.” (Wakolosai 2:8) Yeye alikuwa amewaambia hivi wazee Waefeso: “Najua mimi ya kuwa baada ya kuondoka kwangu mbwa-mwitu wakali wataingia kwenu, wasilihurumie kundi; tena katika ninyi wenyewe watainuka watu, wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao.” (Matendo 20:29, 30) Sasa onyo lake likaanza kutimizwa. Watu wadanganyifu waliingia ndani ya kundi na, kwa hoja za werevu ambazo zilionekana zinafaa kwa juu-juu, polepole wakaharibu juhudi ya washiriki wengi.

Baada ya karne chache namna ya Ukristo wenye kupendwa na watu wengi uliokuwa umepotolewa na mafundisho yasiyo ya Kimaandiko ukawa umesitawi. Fundisho la Kibabiloni la nafsi isiyokufa likatia mizizi. Utatu wa miungu uliabudiwa, sawa na miungu watatu walioabudiwa wakati mmoja katika Babiloni. Mafundisho ya moto wa mateso na, baadaye, purgatori (matohara) watu wakafundishwa. Sala zilitolewa kwa “Mama ya Mungu.” Katika siku za Mtawala Mroma Konstantino, namna hiyo ya Ukristo ulioasi imani, ulikuwa dini ya serikali ya milki hiyo, mahali pa kujitenga na ulimwengu.

Yesu alikuwa ametabiri kwamba baada ya kifo cha mitume mbegu ya Ukristo wa uongo ingepandwa ulimwenguni, na kwamba mpaka wakati wa “mavuno” Wakristo wa uongo na wa kweli wangeendelea kuwapo pamoja. (Mathayo 13:24-30, 36-43) Sasa jambo hilo lilikuwa linatokea. Ukristo wa uongo ulipokuwa wenye nguvu, uliwageukia kwa ukatili mwingi wale waliokataa kufuata njia yake. Wengine wenye kufanya madai ya kuwa ni Wakristo walichomwa wakiwa hai kwa ajili ya imani yao, walakini wakati huu miili yao yenye kuchomeka iliangaza nyuso za watawa na makuhani waliokuwa wakitazama

Kwa karne nyingi, nuru yenye kutoka Biblia iliangaza kwa njia hafifu tu. Neno la Mungu lilikuwa limeandikwa katika Kilatini, ambacho kilikuwa lugha iliyokuwa ikitokomea, na wenye kulitafsiri kwenye lugha zenye kusemwa na watu wengi waliteswa kwa ukatili mwingi. Walakini Biblia iliokoka hayo. Na hata Ukristo wa kweli ukaokoka, kama alivyosema Yesu. Na hata leo Biblia ipo na Ukristo wa kweli pia.

Paradiso Yarudishwa Tena

Ule uongo wa kwanza uliosemwa maelfu mengi ya miaka iliyopita katika bustani ya Edeni uliiletea jamaa ya kibinadamu msiba kweli kweli. Ulielekeza kwenye taabu isiyoelezeka. Kwa furaha, wanadamu hawatakuwa na lazima ya kuvumilia matokeo yake mabaya kwa muda mrefu zaidi.

“Uzao” ambao ungeharibu Shetani na mipango yake ulikuwa ni Yesu. Baada ya Yesu kufa alifufuliwa kwenye uzima wa roho na akapaa kwenda mbinguni, “akingojea hata adui zake wawekwe kuwa chini ya miguu yake.” (Waebrania 10:13) Ushuhuda unaonyesha kwamba kipindi hicho cha kungojea sasa kimekwisha, Unabii mbalimbali na orodha ya miaka ya Biblia inaonyesha mwaka 1914 kuwa wakati ambao Yesu ‘alifika kwenye utukufu wake’ ili atawale akiwa mfalme wa kimbinguni.​—Ona Mathayo 24, 25; Marko 13; Luka 21.

Hiyo maana yake ni kwamba Shetani, mwanzilishi wa ule uongo, amebaki na wakati mchache tu. (Ufunuo 12:12) Michomo ya utungu ambayo wanadamu wameipata tangu 1914 inashuhudia hasira yake nyingi kwa sababu ya jambo hilo. Karibuni yeye, pamoja na mifumo yake ya kisiasa na kidini yenye kuonea ambayo ilisitawi kutokana na uongo wake, ataharibiwa milele.​—Danieli 2:44; Ufunuo 18:4-8,

Hiyo itakuwa faraja kama nini kwa wanadamu! Amani, uzuri na furaha ya lile shamba la Mungu la kwanza itarudishwa tena mwishowe, na paradiso itaenezwa duniani pote. (Ufunuo 21:3, 4) Je! ungependa kuona jambo hilo? Mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wote waokolewe, na kupata kujua yaliyo kweli.” (1 Timotheo 2:4) Kwa sababu gani usitumie kwa faida fadhili za Yehova Mungu ambazo amekuonyesha? Epuka uongo wa Shetani na kutafuta ile kweli kutoka Neno la Mungu, Biblia. Kisha utashuhudia kuondolewa kwa mwisho kamili kwa matokeo yenye msiba ya ule uongo wa kishetani wa kwanza.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki