Uongo wa Kwanza—Jinsi Matokeo Yake Yamekupata Wewe
KATIKA India, mwaka 1981, gari-moshi lilikuwa linakaribia daraja wakati mhandisi (injinia) kwa ghafula alipomwona ng’ombe juu ya reli. Alipiga breki mara moja. Gari-moshi hilo likatoka juu ya reli na mabehewa saba yaliyokuwa yamesongamana watu yakatumbukia ndani ya mto uliokuwa chini. Watu zaidi ya 800 walikufa. Kwa njia hiyo kitu kidogo tu—ng’ombe mmoja juu ya reli—akafanya msiba mkubwa utokee. Jambo kama hilo lilitokea katika Edeni, bustani ya Mungu.
Lazima Edeni pawe palikuwa mahali pa kupendeza. Palikuwa na miti, maua, wanyama na ndege tofauti-tofauti. Palikuwa na upatano na utulivu. Kweli kweli palikuwa paradiso. Lazima Adamu na Hawa wawe waliifurahia kazi ya mikono ya Mungu. Na walikuwa na taraja lenye kusisimua. Mungu aliwaambia: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.” (Mwanzo 1:28) Pamoja na hayo, walikuwa na dini rahisi iliyo bora zaidi: kufanya mapenzi ya Mungu.
Hata malaika walipendezwa sana na mwanzo huo wenye furaha wa jamii ya kibinadamu. Walakini malaika mmoja alikuwa tofauti. Kupendezwa kwake kulikuwa kwa choyo. Yeye alitamani sana kuabudiwa na wanadamu na akatunga hila ya kuwa “mungu,” au mtawala, wa ulimwengu huu. Kwa njia hiyo akawa Shetani, jina ambalo maana yake ni “mpinzani.”—Ona Luka 4:5-8; 2 Wakorintho 4:4.
Yehova Mungu alimwambia Adamu asili lo lote la matunda ya mti fulani. Hilo lilikuwa jaribu rahisi. Kwa kulikabili, Adamu na mke wake wangeweza kuonyesha kwamba kweli kweli walitaka kumwabudu Mungu. Zaidi ya hayo, Yehova alionya hivi: “Siku utakapokula matunda ya mti huo [uliokatazwa] utakufa hakika.” (Mwanzo 2:17) Waasi wasiotii hawangepewa zawadi ya uzima wa milele.
Hapo ndipo Shetani alipoona nafasi yake. Kupitia nyoka yeye alimjaribu Hawa achukue tunda lililokatazwa, kwa kusema: “Hakika hamtakufa.” Halafu kuhusu mti huo akasema: “Kwa maana Mungu anajua ya kamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” (Mwanzo 3:4, 5) Hilo lilikuwa toleo lenye kuvutia kama nini—ai! kuwa kama Mungu! Walakini Shetani alisema uongo. Hata hivyo, Hawa alisadiki yale aliyosema na kwa kutokutii akala kati ya matunda yaliyokatazwa. Baadaye, akampa Adamu, ambaye alijiunga pamoja naye katika kutenda dhambi. Matokeo yalikuwa nini?
Tendo hilo lenye kuamua mambo “likaondoa juu ya reli” jamii yote ya kibinadamu na kutokeza msiba. Wenzi hao wa kwanza wakaipoteza paradiso mara moja. Baada ya wakati, vilevile walipoteza maisha zao wakarudi kwenye mavumbi ambayo kwayo walikuwa wameumbwa. (Mwanzo 3:19) Kwa kusikitisha, watoto wao wote—jamii ya kibinadamu—kwa njia hiyo walizaliwa nje ya paradiso, na ndani ya dhambi na mauti.—Warumi 5:12.
Ilionekana Shetani ameshinda. Sasa yeye alikuwa “mungu” fulani, na jamii ya kibinadamu ilikuwa ikimfuata yeye badala ya kumfuata Muumba. Lakini kwa kweli yeye hakuwa ameshinda. Yeye alikuwa ametupa tu ngumi ya kwanza katika shindano linaloendelea hata leo. Mara moja Yehova akajiingiza ili ayaondoe matokeo ya uongo wa Shetani. Yeye alimwambia Shetani: “Nami nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.”—Mwanzo 3:15.
Katika unabii huo wa kwanza katika Biblia, imetabiriwa kushindwa kwa Shetani mwishowe, ambako kutaletwa kupitia “uzao” fulani. Uzao huo ni nani? Kwa muda mrefu uzao huo uliendelea kuwa siri.
Mungu wa Ulimwengu Huu
Wazao wote wa Adamu na Hawa, isipokuwa wachache tu, walichagua kuwaiga wazazi wao katika kumwasi Mungu. Wao walipendelea kujitegemea kama walivyoambiwa na Shetani. Hatimaye, makao makuu ya kumpinga Mungu yakaja kuwa katika eneo linalojulikana kuwa Mesopotamia, katikati ya Mito Tigri na Frati.
Kiongozi wa kibinadamu wa upinzani huo alikuwa mwanamume ambaye jina lake aliitwa Nimrodi. Katika Biblia anaelezwa kuwa ndiye mfalme wa kwanza na mwundaji wa milki. Utendaji wake wote ulikuwa wa kumpinga Mungu; kwa hiyo, Biblia inasema: “Yeye alijionyesha mwenyewe kuwa mwindaji hodari wa kumpinga Yehova.” Mwanzo wa milki yake ulikuwa Babeli, ambao baadaye ulipata kuwa katikati ya mji wa Babiloni.—Mwanzo 10:9, 10, NW.
Kwa hiyo uonezi na ukatili wa kisiasa ulisambaa kutoka Babeli. Mawazo mageni ya kidini yalisitawishwa hapo pia. Uongo wa kwanza—kwamba Hawa mwenye dhambi hangekufa kweli kweli—ulifunuliwa wazi, kwa kuwa Hawa alikufa. Sasa nyongeza ya uongo huo ilifundishwa. Ilisemekana sehemu isiyokufa ya mwanadamu iliokoka wakati wa kufa na kuendelea kuishi katika ulimwengu fulani usioonekana. Fundisho hilo lilielekeza kwenye sadikisho la moto wa mateso, kupashana habari na roho waovu, kuabudu mizimwi (mababu waliokufa) na chungu nzima ya mafundisho mengine ya uongo.
Mawazo ya kidini yenye asili yake katika Babeli ya kale, au Babiloni, yalisambaa ulimwenguni pote. Mtu mmoja mwenye maarifa, aliona mafanani ambayo yameenea mbali sana kati ya dini nyingi za ulimwengu, alisema kwamba “lazima zote ziwe zilipata mawazo yazo ya kidini kutoka chanzo kimoja.” (The Worship of the Dead, cha Kanali J. Garnier) Chanzo hicho kilikuwa ni Babiloni ya kale. Mfumo huu wa kidini wa ulimwenguni pote uliotoka Babiloni unatajwa katika Biblia kuwa “Babuloni mkuu, mama wa wazinzi na wa mambo yote ya kuchukiza sana duniani.”—Ufunuo 17:5, HNWW.
Basi, uongo wa kwanza wa Shetani uliongoza kwenye uonezi wa kisiasa na dini ya uongo, ambayo ni mambo yaliyoenea kote. Lakini ni mambo gani yalikuwa yakisitawi kuhusiana na “uzao” ule ambao Mungu alitabiri ungeharibu Shetani na mipango yake?
[Picha katika ukurasa wa 5]
Kama gari-moshi hili, jamii yote ya kibinadamu ‘imeondolewa juu ya reli.’ Unajua ni kwa jinsi gani?