Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 9/1 kur. 20-24
  • Kuokoka au Kuharibiwa kwenye ile “Dhiki Kubwa”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuokoka au Kuharibiwa kwenye ile “Dhiki Kubwa”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Si Wafu Wote Watakaofufuliwa
  • Yehova Akitoa Hukumu Ndio Mwisho wa Mambo
  • Wokovu au Uharibifu
  • Kuukimbilia Ufalme ili Kupata Wokovu
  • Siku ya Hukumu na Baada ya Hapo
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Ufufuo wa Uzima na Mwingine wa Hukumu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Nguvu za Tumaini la Ufufuo
    Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
  • Siku ya Hukumu Ni Nini?
    Amkeni!—2010
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 9/1 kur. 20-24

Kuokoka au Kuharibiwa kwenye ile “Dhiki Kubwa”

“Hawa Wataondoka wakaingie kwenye kukatiliwa mbali milele, bali wenye haki kwenye uzima wa milele.”​—Mathayo 25:46, NW.

1, 2. Wengine wamekuwa na maoni gani, na kwa sababu gani maoni hayo ni ya hatari na ya kupasa kuepukwa?

WENGINE wanakataa wazo la kwamba watu fulani wataharibiwa milele. Iko hivyo kwa wanaoamini kwamba mwishowe kila mtu ataokolewa. Nyuma huko-o-o katika karne ya tatu W.K., mwandikaji wa kidini Origen alicheza-cheza na wazo la wote kuokolewa mwishowe. Bila kwenda mbali sana, wengine leo wanaodai kuwa ni Wakristo wanatoa maoni ya kwamba pengine wanadamu wote watafufuliwa, kutia na wale watakaoharibiwa wakati ujao katika “dhiki kubwa.”​—Mathayo 24:21, 22.

2 Pasipo kujua, wale wanaofuata wazo lilo wanakaribia sana kwa hatari fundisho la kidini la Jumuiya ya Wakristo juu ya “ufufuo wa watu wote.” Makanisa makubwa-makubwa yanafundisha kwamba maiti za WOTE waliokufa zitafufuliwa zikajiunge na nafsi zao mbinguni au katika ‘moto wa mateso.” Hata hivyo Biblia, haifundishi juu ya huo “ufufuo wa watu wote” kama unavyofahamika na Jumuiya ya Wakristo, wala kwamba wafu WOTE, hata waovu, watafufuliwa au kurudishwa kwenye uzima.

Si Wafu Wote Watakaofufuliwa

3. Yesu alionyeshaje kwamba si wote wangefufuliwa?

3 Yesu alionyesha kwamba si kila mtu atakayefufuliwa. Yeye alikuwa akijibu ulizo la ujanja aliloulizwa na Masadukayo, ambao walikuwa wanaamini kwamba ha-kuna mtu atakayefufuliwa. Yeye alizungumza juu ya “wale ambao wamehesabiwa wanastahili kuipokea hiyo taratibu ya mambo na ufufuo kutoka kwa wafu.” (Luka 20:35, NW) Maneno yake yanadokeza kwamba si wote watakaokuwa wamejithibitisha wanastahili kufufuliwa katika taratibu ya mambo mpya ambayo Mungu ameahidi.

4. Kulingana na Ufunuo sura ya 20, wafu watatoka wapi, lakini ni mahali gani pa mfano pasipotoa wafu wake?

4 Katika Ufunuo sura ya 20, inayozungumza juu ya ufufuo wa “wafu waliosalia” ambao hawashiriki katika “ufufuo wa kwanza,” Biblia inasema kwamba “bahari” na “Hadeze” (ZSB) inatoa wafu waliomo ndani. Haisemi kwamba wafu wanatoka katika “ziwa la moto,” au “mauti ya pili,” ambapo mahali kwingine inaitwa “Gehena” (Kiebrania, Geʹi Hinnomʹ). (Luka 12:5, NW) Kama vile neno “bahari” linavyoonyesha kaburi la majini la ujumla la wale wote waliofia vilindini na ambao miili yao haikuonekana ipate kuzikwa duniani, neno la Kigiriki haʹdeze halimaanishi kaburi fulani moja bali, linamaanisha kaburi la kidunia la wanadamu la kawaida. Linalingana na neno “Sheol” linalopatikana katika Maandiko ya Kiebrania. Yesu anasema hivi: “Nami nilikuwa nimekufa, na tazama, mimi ni hai hata milele na milele. Nami nina funguo za mauti, na za Hadeze.” (Ufunuo 1:18, ZSB) Wakati wa utawala wake wa mileani atatumia “funguo” hizo kuweka huru kutokana na kifo wale “wanaohesabiwa wanastahili kuipata taratibu ya mambo hiyo na ufufuo kutoka kwa wafu.”

5. Ni nini kinachofananishwa na “Gehenna”?

5 Kwa upande mwingine, hakuna mahali po pote ambapo Maandiko yanasema kwamba Kristo ana funguo za Gehenna. Yeye alizungumza juu ya Gehenna na kusema hivi: “Msipate kuwaogopa wale wanaoua mwili bali wasiweze kuiua nafsi; bali mwogopeni yule [Yehova] anayeweza kuharibu vyote viwili, nafsi na mwili katika Gehena.” (Mathayo 10:28, NW) Akitoa maelezo juu ya kifungu hicho katika kitabu chake Kutokufa kwa Nafsi au Ufufuo wa Wafu? (Kifaransa), Profesa Oscar Cullmann anaandika hivi: “psy·kheʹ [nafsi] haimaanishi wazo la Kigiriki la nafsi bali lapasa kutafsiriwa kuwa ‘uhai’. . . . W. G. Kummel. . . vilevile anaandika hivi akiwa na sababu nzuri: Mt. 10:28 ‘haikazii kutokufa kwa nafsi, bali inakazia uhakika wa kwamba Mungu peke yake ndiye anayeweza kuharibu uhai wa kidunia na pia uhai wa kimbingu.’ “Ndiyo, Gehenna inafananisha uharibifu kamili ambao katika huo hakuna ufufuo unaowezekana. Kitabu The New Bible Commentary (Chapa ya Pili, ukurasa 786) kinaeleza Gehenna kuwa ndio “ufafanuzi wa ‘mauti ya pili.’”​—Ufunuo 21:8.

6. Onyesha kutoka kwa Biblia kwamba wengine wanakwenda Gehenna kabla ya Siku ya Hukumu ya miaka 1,000 na kwa hiyo hawana tumaini la ufufuo?

6 Basi, Biblia kwa uhakika inaonyesha kwamba wengine wanamalizikia katika Gehenna ya mfano kabla ya Siku ya Hukumu ya miaka 1,000 kuanza. Yesu aliwaambia waandishi na Mafarisayo wasiotubu kwamba wao pamoja na waongofu wao wa Mataifa walikuwa ‘wanaistahili Gehenna’ au, kwa halisi, ‘wana wa Gehenna.’ (Mathayo 23:15, 33-35, NW; ona pia Yohana 9:39-41; 15:22-24.) Na kama mwongofu wa Mafarisayo angestahili Gehenna ‘mara mbili kama wao,’ Yuda Iskariote aliyefanya muafaka wa uhaini pamoja nao wa kumsaliti Mwana wa Mungu aliistahili zaidi kama nini! Yesu alionyesha hilo alipomwita Yuda “mwana wa upotevu.” (Yohana 17:12) Vivyo hivyo, waasi-imani wasiotubu, wanakwenda kwenye Gehenna wanapokufa bali si katika Sheol, au Hadeze. (Waebrania 6:4-8; 2 Petro 2:1) Ndivyo ilivyo kwa Wakristo waliojiweka wakf wanaoendelea katika dhambi ya kukusudia au ‘wanaosita-sita.’ (Waebrania 10:26-31, 38, 39) Hiyo ni mifano tu ya kuonyesha kwamba wengine, hata katika “hii taratibu ya mambo,” wamefanya dhambi ambayo haina msamaha, wala hata katika taratibu ya mambo “itakayokuja.” (Mathayo 12:31, 32, NW; linganisha 1 Yohana 5:16.) Kwa hiyo, hawatafufuliwa.

Yehova Akitoa Hukumu Ndio Mwisho wa Mambo

7. Ni nini kinachothibitisha zaidi kwamba Yehova anawatolea wengine hukumu ya mwisho hata wakati wa hii taratibu ya mambo ya sasa?

7 Ukweli wa kwamba Yesu alisema kwamba mtu ‘akikufuru roho’ hangesamehewa “katika hii taratibu ya mambo wala katika ile itakayokuja” wapasa kusadikisha ye yote mwenye mashaka juu ya habari ya kwamba Yehova ndiye anayetoa hukumu ya mwisho juu ya wengine hata wakati wa “hii taratibu.” Wao ‘wana dhambi ya milele.’ ‘Hawana msamaha hata milele.’ (Marko 3:28, 29) Basi, kwa sababu gani wafufuliwe?

8. (a) Tunapaswa kuonyeshaje nia ile ile kama Yehova? (b) Kwa sababu gani tunapaswa kuwa na uhakika katika Yehova na Mwanaye wakiwa Mahakimu, na ni mfano gani unaoweza kutajwa kuonyesha hukumu ya kimungu kuwa ndio mwisho wa mambo?

8 Kama ilivyo, tukiwa mashahidi wenye kuheshimika wa Mungu Yehova wetu, hatwendi huku na huku tukiwatisha watu kwa uharibifu. Tunayaona mambo kama Yehova. Juu yake inasemekana kwamba yeye ni ‘mwenye subira,’ kwa sababu “hataki ye yote aje aharibiwe bali anataka sana wote wafikie hali ya kutubu.” (2 Petro 3:9, NW) Kwa upande mwingine, twapaswa kuepuka kuongozwa kupita kiasi na maono ya moyoni na pengine pasipo kujua, tulaumu njia ya Yehova ya kuendesha mambo. Yehova ni Hakimu mkamilifu. (Kumbukumbu la Torati 32:4) Kristo Yesu yuko vivyo hivyo. (Yohana 5:30) Kesi inapoletwa mbele ya mahakimu wasiokamilika wa kibinadamu na kufuata kawaida ya kisheria, kuanzia mahakama ya chini zaidi mpaka kwenye mahakama kuu zaidi nchini, watu wanaona kwamba hiyo ndiyo haki, na hakuna rufani nyingine inayoweza kukatwa. Basi, kwa sababu gani sisi tutilie shaka hukumu za Yehova na kwamba huo ndio mwisho wa mambo?​—Zaburi 119:75.

9. Mathayo 10:28 inaonyeshaje hukumu za Yehova kuwa ndio mwisho wa mambo?

9 Ingawa Yehova amejionyesha kuwa ni ‘mwenye subira’ sana kwa sababu “anataka sana wote wafikie hali ya kutubu,” yeye anajua kwamba si wanadamu wote watakaotubu. Ndiyo sababu Yesu alituonya ‘tumwogope yule anayeweza kuharibu nafsi na mwili katika Gehenna.’ Kikitoa maelezo juu ya kifungu hicho, kitabu New lnternational Dictionary of New Testament Theology kinasema hivi: “Mt. 10:28 inafundisha si uwezo wa nafsi kutokufa bali kutoweza kubadilishwa kwa hukumu ya kimungu kwa wasiotubu.”

10. Yesu alisema nini kuhusu “wengi” na “wachache,” na ni nini maana ya neno la Kigiriki linalotafsiriwi kuwa “upotevuni”?

10 Katika Mahubiri yake ya Mlimani Yesu alisema hivi: “Ingieni kwa kupitia mlango ulio mwembamba; maana mlango ni mpana, na njia ni pana iendayo upotevuni [Kigiriki, apoleia], nao ni wengi waingiao kwa mlango huo. Bali mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani, nao waionao ni wachache.” (Mathayo 7:13, 14) Kamusi za Kigiriki zinafafanua apoleia kuwa na maana ya “kuharibiwa kabisa,” “uharibifu wa milele” (ya Arndt na Gingrich) au “uharibifu wa kabisa, si kwa maana tu ya kukomeshwa kwa kuwapo kwa kimwili.” (Kitabu Theological Dictionary of the New Testament) Kwa hiyo, hakuna msingi wa Kibiblia wa kutuongoza tusadiki kwamba watu wanaoishi leo, wanaoikabili ile “dhiki” kubwa zaidi tangu ulimwengu ulipoanza, wana uchaguzi mwingine licha ya “uzima” au “uharibifu.”​—Mathayo 24:21, 22.

Wokovu au Uharibifu

11. (a) Usemi ‘siku ya Yehova’ unamaanisha nini (b) Ni ‘siku gani ya Yehova iliyo kuu’ ambayo iko mbele, halafu ni nini kitakachotokea wakati huo?

11 “Hiyo siku ya [Yehova] iliyo kuu i karibu.” (Sefania 1:14) Maneno hayo hayajapata kuwa ya kutisha kama katika wakati huu. Ni kweli kwamba kumekuwako vipindi vingine vya pekee katika historia ambapo katika hivyo Yehova alitekeleza hukumu yake na kulitukuza jina lake takatifu, na kila kimoja kilikuwa ‘siku ya Yehova’ iliyo ndogo. Yerusalemu usioaminika, Babiloni na Misri zilipatwa na “siku” kama hizo. (Isaya 2:1, 6-17; 13:1-6; Yeremia 46:1-10) Walakini ‘siku ya Yehova’ iliyo kuu zaidi ingali mbele. Ni “siku” ambayo hukumu za Yehova zitatekelezwa juu ya Jumuiya ya Wakristo, sehemu nyingine ya milki ya ulimwengu ya dini ya uongo ya Shetani na mfumo wake wote mbovu. “Siku ile ni siku ya ghadhabu, siku ya fadhaa na dhiki, siku ya uharibifu na ukiwa.” Unabii huo unaendelea kusema hivi: “Nami nitawaletea wanadamu dhiki, . . . wamemtenda [Yehova] dhambi... Fedha yao wala dhahabu yao havitaweza kuwaokoa katika siku ile ya ghadhabu ya [Yehova]; bali nchi yote pia itateketezwa kwa moto wa wivu wake; maana atawakomesha watu wote wakaao katika nchi hii, naam, ukomo wa kutisha. . . . Kabla haijawajilia hasira kali ya [Yehova], kabla haijawajilia siku ya hasira ya [Yehova]. Mtafuteni [Yehova], enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya [Yehova].”​—Sefania 1:15-2:3.

12. Je! unabii wa Sefania unahusu Yuda tu, au matumizi yake yanatia mengi zaidi?

12 Hata wachunguzi wengi wa Jumuiya ya Wakristo wanatambua kwamba unabii huo haukuhusu Yuda peke yake lakini ulitabiri “hukumu ya ulimwengu wote wa juu na chini ikiupata ulimwengu wote” (Keil-Delitzsch), “mwisho wa kipindi cha dhambi” (Ecumenical Bible ya Kifaransa), “‘siku’ ambapo hukumu ya ulimwengu wote wa juu na chini itakapoletwa juu ya uovu wote na ghadhabu ya Mungu kumwagwa juu ya wote wasiomjua Mungu na wasiotii injili ya Bwana yetu Yesu Kristo.”​—New Bible Commentary, Chapa ya Pili.

13. (a) Kulingana na Paulo, ‘siku ya Yehova’ itatokea wakati gani? (b) Ni nani “mtu mwenye kuvunja sheria,” na “mtu” huyo wa mfano anangojea hukumu gani?

13 Mtume Paulo alishirikisha ‘siku ya Yehova’ na “kuwapo kwa Bwana yetu Yesu Kristo.” (2 Wathesalonike 2:1, 2, NW) Akiisha kuzungumza juu ya “uasi-imani” ambao mwishowe ulimtokeza “yule mtu wa kuvunja sheria,” (“mtu wa kuasi,” UV)—jamii ya viongozi wa kidini yenye kuasi imani ya makanisa ya Jumuiya ya Wakristo—Paulo anaongeza hivi: “Hakika, ndipo, yule mtu wa kuvunja sheria atakapofunuliwa, ambaye Bwana Yesu atamfutilia mbali kwa roho ya kinywa chake na kummaliza kwa wonyesho wa kuwapo kwake.” (2 Wathesalonike 2:3, 8, NW) Viongozi wa kidini wenye kuasi ‘watafutiliwa mbali’ au ‘kumalizwa’ mwanzoni kabisa mwa “dhiki ile iliyo kuu.” (Ufunuo 17:1-5, 16, 17) Jamii hiyo inaitwa pia “yule mwana wa uharibifu [apoleia],” ambayo maana yake ni kwamba wanaelekea kwenye “uharibifu wa milele” katika Gehenna, kama waliofanana nao katika siku za Yesu.​—2 Wathesalonike 2:3, NW; Mathayo 23:33, NW.

14. Kwa sababu gani wengine wengi “watapotea,” kwa hiyo ni uchaguzi gani ulio mbele ya wanadamu wote?

14 Lakini namna gani watu wote ambao wamefuata viongozi wa kidini pamoja na ‘udanganyifu wao usio na haki’? Mtume Paulo anasema kuwa wao “wanapotea [kwa halisi: “wanajiharibu”], ikiwa ni adhabu kwa sababu hawakuukubali upendo wa ile kweli ili wapate kuokolewa. Kwa hiyo ndiyo sababu Mungu anaruhusu utendaji wa kosa uwaendee, ili wauamini uongo, kusudi wote wapate kuhukumiwa kwa sababu hawakuiamini ile kweli bali walipendezwa na uasi.” (2 Wathesalonike 2:10-12, NW) Leo, Ulimwengu umekuwa karai (bakuli) la uovu, mwenendo mchafu na ufisadi. Wanadamu walio wengi ‘wanapendezwa na uasi’ na ‘hawaukubali upendo wa ile kweli ili wapate kuokolewa.’ (Linganisha Ezekieli 9:4-7.) Kwa hiyo, ‘watahukumiwa’ na wataangamia “ikiwa ni adhabu.” Katika “dhiki ile iliyo kuu” inayokuja uchaguzi uko wazi kabisa. Ama ni wokovu ama ni uharibifu.

Kuukimbilia Ufalme ili Kupata Wokovu

15. Mfano wa “kondoo” na “mbuzi” unasema uchaguzi wa mataifa yote ya wanadamu ni nini?

15 Ndiyo, “hiyo siku ya [Yehova] iliyo kuu i karibu; i karibu, nayo inafanya haraka sana.” (Sefania 1:14) Tunaishi katika wakati wa hukumu wakati “mataifa yote” yamekusanywa mbele ya Kristo Yesu. Watu wa mataifa hayo yote wanatenganishwa katika jamii mbili, “kondoo” na “mbuzi.” Matokeo ya mwisho yanasemwa wazi: “uzima wa milele” kwa “kondoo,” na “kukatiliwa mbali milele” (NW) kwa “mbuzi.”​—Mathayo 25:31-33, 46.

16, 17. (a) 2 Wathesalonike 1:6-9 inaonyeshaje hukumu ya Yehova inayotolewa katika ile “dhiki kubwa” kuwa -ndio mwisho wa mambo? (b) Pamoja na watesi wa watu wa Mungu, ni nani wengine watakaoharibiwa, na kwa sababu gani?

16 Kwa mara nyingine akionyesha hukumu ya Yehova ambayo ndiyo mwisho wa mambo, Paulo anaandika hivi: “Kwa kuwa ni haki mbele za Mungu kuwalipa mateso wale wawatesao ninyi; na kuwalipa ninyi mteswao raha pamoja na sisi; wakati wa kufunuliwa [apokalypsis] kwake Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika wa uweza wake; katika mwali wa moto; huku akiwalipiza kisasi wao wasiomjua Mungu, na wao wasioitii Injili ya Bwana wetu Yesu; watakaoadhibiwa kwa maangamizi ya milele.”​—2 Wathesalonike 1:6-9.

17 Angalia kwamba ‘kuadhibiwa kwa maangamizi ya milele’ kunatekelezwa si tu juu ya wale ‘wanaowatesa’ watu wa Mungu bali pia juu ya wale “wasiomjua Mungu” na wale “wasioitii Injili.” Katika barua aliyowaandikia Warumi, Paulo anaeleza sababu gani wale “wasiomjua Mungu” hawana “udhuru” na sababu gani watahukumiwa. (Warumi 1:18-20; 2:5-16) ‘Malaika anayeruka katikati ya mbingu,’ anayezungumzwa katika Ufunuo sura ya 14, anawaalika wote “wakaao juu ya nchi” wamche “Mungu, na kumtukuza, kwa maana saa ya hukumu yake imekuja.” Kwa hiyo watu wanasihiwa wamwabudu “yeye aliyezifanya mbingu na nchi na bahari na chemchemi za maji.” Wale wanaoshindwa kufanya hivyo, na wale wote wanaoweka imani katika “mnyama” wa kisiasa wa Shetani badala ya ufalme wa Kimasihi wa Mungu, wataharibiwa pamoja na “mnyama” huyo katika ‘shinikizo kubwa la ghadhabu ya Mungu.’​—Ufunuo 14:6, 7, 9,10, 14-20; 19:11-21.

18. (a) Wo wote wanaotumaini kuokoka sasa wanapaswa kufanya nini? (b) Ni nani ambao Biblia inataja kuwa wanaokoka ile “dhiki kubwa,” na wana taraja gani mbele yao?

18 Wo wote wanaotumaini ‘kufichwa katika siku ya hasira ya Yehova’ lazima ‘watafute haki, unyenyekevu’ na ‘kuzitenda hukumu za Yehova,’ badala ya kuzilaumu. (Sefania 2:2, 3) Wo wote wanaotumaini kuonwa na Hakimu wa Yehova aliyewekwa kuwa ni “kondoo” wa kuokolewa kwenye ile “dhiki kubwa” lazima wajionyeshe kuwa ni “wenye haki,” wanaosaidia kwa matendo na kuunga mkono “ndugu” wa Kristo waliotiwa mafuta, ambao wanafanyiza jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mathayo 25:33, 40, 46; 24:45-47) Wale tu ambao Biblia inawapa tumaini la kuokoka ile “dhiki kubwa” ni “ndugu” wa Kristo, au “wateule,” na ule “mkutano mkubwa” wa “kondoo” ambao ‘wanatoa utumishi mtakatifu’ (NW) pasipo kuacha, wakati wote wakisema hivi ili wote wasikie: “Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo.” Wakiwa ni wanafunzi waliobatizwa ambao wametolewa kutoka kwa “watu wa mataifa yote,” huu “mkutano mkubwa” unachungwa na Mwana-kondoo Kristo Yesu, ambaye anawaongoza kwenye “chemchemi za maji yenye uhai” ambayo hayatakwisha kamwe. “Ni Mungu atayafuta machozi yote katika macho yao.”​—Mathayo 24:21, 22; 25:34 28:19, 20, NW; Ufunuo 7:9-17.

—Kutoka The Watchtower, April 1, 1982

MAULIZO YA KUJIKUMBUSHA

◻ Makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yanamaanisha nini na “ufufuo wa watu wote” waliokufa, lakini je! fundisho hilo la kidini ni la Kibiblia?

◻ Ni maandiko gani yanayoonyesha kwamba si wafu wote watakaofufuliwa?

◻ “Gehenna” ni nini?

◻ Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova anawatolea hukumu ya mwisho wengine hata wakati wa hii taratibu ya mambo ya sasa?

◻ Ni nini yatakayotokea katika ‘siku ya Yehova,’ na je! wale watakaoangamizwa watafufuliwa?

◻ Ni nini yanayopasa kufanywa ili kuokoka, kwa hiyo ni kazi gani yenye uharaka zaidi ya wakati mwingineo wote?

[Picha katika ukurasa wa 21]

Yuda, “mwana wa upotevu” atakuwa kati ya wale ambao hawatafufuliwa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki