Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 5/1 kur. 3-5
  • Sala Iliyo Mfano wa Kufuatwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sala Iliyo Mfano wa Kufuatwa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • THAMANI
  • PANDE MBALIMBALI
  • YENYE KUDUMU
  • Sala ya Bwana Inachomaanisha Kwako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Tunapaswa Kusali kwa Mungu Jinsi Gani?
    Amkeni!—2012
  • Yehova Hutuandalia Mahitaji Yetu ya Kila Siku
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Jinsi ya Kusali—Je, Kukariri Sala ya Bwana Ndiyo Njia Bora Zaidi ya Kusali?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 5/1 kur. 3-5

Sala Iliyo Mfano wa Kufuatwa

“Basi ninyi salini hivi; Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe, ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni. Utupe leo riziki yetu. Utusamehe deni zetu, kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu. Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu.”

UNAWEZA kuiita hiyo Sala ya sala. Inajulikana mahali pengi kuwa sala ya “Baba Yetu” na “Sala ya Bwana” kwa sababu Bwana Yesu Kristo aliwatolea wanafunzi wake sala hiyo iwe mfano wa kufuatwa. (Mathayo 6:9-13) Kwa kufaa inaweza kulinganishwa na kito cha thamani.

THAMANI

Mawazo yenye thamani kubwa yametiwa katika maneno hayo machache ya sala hii. Sawa na jiwe lenye thamani kubwa, thamani ya sala hiyo ni kubwa sana. Kwa mfano, ni vigumu mara 120 kupata almasi kuliko kupata dhahabu. Thamani ya almasi inaongezwa na pande zake mbalimbali.

PANDE MBALIMBALI

Hizi zinapatikana kwa kuikata madini hiyo kwa uangalifu. Ni lazima zile pembe zilingane kabisa ndipo madini hiyo iweze kung’aa vizuri kabisa. Vivyo hivyo, kila upande wa Sala Iliyo Mfano wa Kufuatwa unang’aa kwa fahari yake wenyewe.

YENYE KUDUMU

‘Almasi ni za milele.’ Je! wewe ulijua kwamba karibu miaka 2,000 imepita tangu Sala Iliyo Mfano wa Kufuatwa ilipotokezwa? Ustahili wake haujafifia. Kwa hiyo acheni tukichunguze kwa makini zaidi kito hiki cha thamani. Sala yenyewe ina maana gani?

Mambo yanayohusiana na Mungu yanatajwa kwanza

Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe (litakaswe).

Jina la kibinafsi la Mungu ni Yehova. Yesu ‘alidhihirisha jina la Baba yake’ kwa wanafunzi wake kwa kutumia jina la kibinafsi la Mungu na kuwafahamisha sifa za Mungu. Nao pia wangelitakasa jina hilo kwa kulichukua kama kitu kitakatifu, kueleza wengine habari za jina hilo na kujulisha kusudi la Mungu la kutakasa jina lake mwenyewe mbele ya uumbaji wote. Wakiwa ni ‘watu walio kwa ajili ya jina la Mungu,’ Wakristo wanapaswa sikuzote wajitahidi kujiendesha kwa namna inayolistahili Jina hilo.​—Zaburi 83:18; Yohana 17:6; Matendo 15:14, NW.

Ufalme wako uje.

Ufalme ni serikali ya kimbingu ya Mungu, chombo ambacho kupitia hicho wanadamu watawezeshwa kupata usalama wa kweli na ufurahiaji kamili wa maisha. Tayari umesimamishwa mbinguni, naye Mfalme wake, Kristo Yesu, aliyetiwa mafuta na Yehova Mungu mwenyewe, karibuni ataitawala dunia. Kwa kuwa ni serikali yenye nguvu nyingi, Ufalme huo utachukua hatua ya kuiondoa mifumo isiyo mikamilifu na yenye uonezi iliyopo sasa. “Utavunja falme hizi zote [mamlaka za kisiasa za sasa] vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”​—Danieli 2:44; 7:13,14.

Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.

Mapenzi ya Mungu ni kwamba uovu wote usafishwe katika ulimwengu mzima. “Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo,” Biblia inasema. Mungu ana kusudi la pekee kwa sayari hii. “Utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso,” Yesu akamwambia mwanamume mmoja aliyetundikwa mtini pamoja naye, na hivyo akampa mtu huyo tumaini la kuishi katika dunia itakayokuwa paradiso. Kusudi la Mungu linatia ndani ufufuo wa wafu, wa “wenye haki na wasio haki pia.” Mapenzi yake ni kwamba “namna zote za watu waokolewe.”​—Zaburi 37:10; Luka 23:43, NW; Matendo 24:15; 1 Timotheo 2:3, 4, NW.

Mambo yanayohusiana na mahitaji yetu ndiyo yanayochukua nafasi ya pili

Utupe leo riziki yetu.

Ombi letu la mahitaji ya maisha linapasa lifanywe kwa kiasi kidogo. Omba chakula kinachoitosha “leo” tu. Kama vile Yesu alivyosema kwa kweli, “uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo.” Ikiwa tunamwamini yeye, hatutatumia maisha zetu zaidi sana katika kujipatia mali za kimwili. “Tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo.” Alipokuwa akisema, “Utupe,” Yesu alikuwa akitufundisha pia tuyakumbuke mahitaji ya wengine.​—Luka 12:15; 1 Timotheo 6:8.

Utusamehe deni zetu, kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu.

Tunahitaji msamaha wa Mungu. “Tukisema kwamba hatuna dhambi, twajidanganya wenyewe, wala kweli haimo mwetu. Tukiziungama dhambi zetu, [Mungu] ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.” “Tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki”​—mradi, bila shaka, tuna imani ya kweli katika mpango alioufanya Mungu ili watu wasamehewe kupitia Yesu Kristo. Pia, ni lazima sisi wenyewe tuwe wenye kusamehe wengine.​—1 Yohana 1:8, 9; 2:1, 2.

Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu.

“Ulimwengu mzima uko katika uwezo wa yule mwovu,” yaani, Shetani Ibilisi. Mungu hashawishi mtu ye yote afanye ubaya, lakini huenda tamaa zetu zikatuvuta tutake kufanya yasiyofaa. Mungu anatutolea kanuni zinazofaa za Biblia na ushirika wa Kikristo unaojenga ili kutusaidia tuondoke kwenye kishawishi na kutulinda na uovu. Kwa hiyo tunahitaji kutenda kupatana na sala yetu. “Enyi mmpendao [Yehova], uchukieni uovu;... [Huwaokoa] na mkono wa wasio haki” washikamanifu wake.​—1 Yohana 5:19, NW; Zaburi 97:10.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki