Kumwonyesha Mungu Kuthamini Kwetu
Asante Yehova, Mungu daima,
Kwa kutoa nuru ya thamani!
Asante kwa pendeleo la sala,
Twaweza kukujia na shida!
Asante, Yehova, kwa Mwana wako,
Aliyeshinda kifo na Hades!
Twapiga asante kwa uongozi,
Hivyo twazitimiza nadhiri!
Asante, Yehova kwa udugetu,
Tupatapo rafiki za kweli!
Asante kwa kutupa roho yako,
Hutusaidia mwendo wetu!
Asante, Mungu wetu, kwa heshima
Kuhubiri jina lako kubwa!
Asante shida zote zitakwisha,
Baraka za Ufalme hudumu!
HAYO ni maneno ya wimbo “Asante, Yehova!” Yamo kichapo “Kuimba na Kufuatana Wenyewe kwa Muziki katika Mioyo Yenu,” kitabu cha wimbo katika kinachotumiwa na Mashahidi wa Yehova. Wimbo huo unashuhudia wana tamaa ya kumwonyesha Mungu kuthamini, na hilo linapatana na kitia moyo cha Kimaandiko cha ‘kuimba kwa muziki katika mioyo yetu kwa Yehova,’ hivyo “katika jina la Bwana yetu Yesu Kristo tukipiga asante sikuzote kwa Mungu wetu na Baba kwa ajili ya mambo yote.” (Waefeso 5:18-20, NW) Lakini ni nini baadhi ya sababu za kupiga asante, za kuonyesha kumthamini Yehova Mungu?
Kwa Sababu Gani Tumwonyeshe Mungu Kuthamini Kwetu
Maisha yenyewe ni zawadi kutoka kwa Mungu ambayo twapaswa kupigia asante. Kwa kweli, Yehova anatoa vitu vyote vikiwa vizuri na vyenye kufaidi. (Matendo 17:24, 25) Kati ya mambo mazuri yaliyotajwa katika wimbo huo ni haya: nuru ya kiroho ya thamani (Zaburi 43:3; Yohana 17:3); pendeleo la sala (Mithali 15:8); dhabihu yenye kuondoa dhambi ya Mwana wa Mungu, Yesu Kristo (Warumi 6:23; 1 Yohana 2:1, 2); uongozi wa Kimaandiko katika kufanya mapenzi ya kimungu (Zaburi 40:8; 119:9-16, 105); udugu wa Kikristo wenye upendo (1 Petro 2:17); roho takatifu ya Mungu yenye kuongoza, au nguvu ya utendaji (Zaburi 143:10); na baraka za ufalme za milele ambazo zitachukua mahali pa shida zote za dunia. (Mathayo 6:9, 10; Ufunuo 11:15-18; 12:9-12) Hayo ni baadhi ya mambo ambayo kwa ajili yayo Mashahidi wa Yehova wanampigia Mungu asante wanapoimba katika kusanyiko la kikundi.
Kuna sababu nyingi sana za kumwonyesha Mungu kuthamini kwetu. Ai, ebu waza juu ya kuamka wakati wa asubuhi yenye kupendeza! Jua linaangaza mng’ao mwingi, unasikia kuimba kwa ndege, na unanusa harufu tamu ya maua au nyasi zilizokatwa karibuni. Kwa msisimuko, unasema: “Ni vizuri kama nini kuwa hai!” Hata hivyo, inafaa kama nini kumwonyesha kuthamini Yule aliyefanya yote hayo yawezekane!
Hakika, Mungu ametoa mipango mingi kwa faida na furaha ya wanadamu. Fikiria juu ya jua, mwezi na nyota zinazotupa mwangaza. Kuna hewa ya kupumua na mimea ya kuifanya safi. Yehova ametoa chakula na maji kwa wingi. Na ebu waza juu ya ndege na wanyama wote wanaofanya safari ya kupitia mashambani ipendeze. (Ayubu 37:5-16; Zaburi 8:3-9; Matendo 14:15-17) Zaidi ya hayo, Mungu ametupa uwezo wa kuona, kusikia, kugusa, kuonja na kunusa mambo ambayo yanatuwezesha tufurahie maandalizi hayo kikamilifu. Twapaswa kuwa wenye shukrani kama nini!
Wa maana zaidi kwa Wakristo walio wakf ni utoaji wa kiroho wa Yehova. Utoaji kadha wa kadha unatajwa katika wimbo uliotangulia kutajwa. Hakika inafaa kumshukuru Mungu kwa ajili ya baraka hizo za kiroho.
Vilevile ni vizuri kutafakari kwa ukawaida juu ya utoaji wote mwingi wa Yehova Mungu wa kiroho na kimwili. Bila shaka kutafakari huko kutatuchochea tufanye jambo fulani. Inaelekea sana kutatuchochea tumwonyeshe Mungu kuthamini kwa kusema na kutenda.—Zaburi 1:1-3; 77:11, 12.
Maneno na Matendo ya Kuthamini
Sala ya moyo mweupe ni njia moja ya wazi ya kumwonyesha kuthamini Mtoaji wa “kila zawadi njema na kila utoaji mkamilifu.” (Yakobo 1:17, NW) Kwa hiyo, je, tunampigia Mungu asante kwa ukawaida kwa maneno ya sala? Huenda tukachochewa kufanya hivyo sawa na mtunga zaburi Daudi, ambaye alitangaza hivi: “Umefanya vitu vingi wewe mwenyewe, Ee Yehova Mungu wangu, hata kazi zako za ajabu na mawazo yako kutuelekea sisi; hakuna ye yote wa kulinganishwa nawe. Kama nikiwa na maelekeo ya kueleza na kusema juu yayo, yamekuwa mengi sana kuliko ninavyoweza kusimulia.”—Zaburi 40:5, NW.
Vilevile Daudi alikuwa ameazimia kumwonyesha Mungu kuthamini kwa maneno aliyowaambia wengine. Hivyo, yeye alisema: “Nitamshukuru [Yehova] kwa moyo wangu wote; nitayasimulia matendo yako yote ya ajabu.” (Zaburi 9:1) Hali moja na hiyo wimbo “Asante, Yehova!” unasema: “Asante, Mungu wetu, kwa heshima kuhubiri jina lako kubwa!” Ndiyo, kweli kweli, kusema na wengine juu ya Mungu, kwa kushiriki kusema na wengine juu ya ile kweli kutoka Neno lake, yaelekea sana ndiyo njia bora zaidi ya kumwonyesha shukrani zetu.
Tafadhali, rudia kufikiria juu ya yule mkoma mmoja aliyerudi kushukuru kwa ajili ya kuponywa. Yeye alifanyaje hivyo? Tunaambiwa hivi: “Na mmoja wao alipoona kwamba amepona, alirudi, huku akimtukuza Mungu kwa sauti kuu; akaanguka kifudifudi miguuni pake, akamshukuru.” (Luka 17:15, 16) Si kwamba tu mtu huyo alimpigia Yesu asante kwa kumponya bali pia yeye alimtukuza Mungu, Chanzo cha uhai na uponyaji wa kweli. Na mtu huyo aliyeponywa alimtukuza Mungu “kwa sauti kuu.” We, lazima awe alimsifu Yehova na kuzungumza juu ya jambo hilo kwa juma nyingi, hata miezi mingi! Jambo hilo linaonyesha vizuri jinsi tunavyoweza kutoa shukrani zetu kwa kuzungumza juu ya yale ambayo tumeona, tukasikia na kujifunza juu ya Mungu.
Hasa, hiyo ndiyo sababu Mashahidi wa Yehova wanakwenda nyumba kwa nyumba. Shukrani kwa Mungu zinawachochea washiriki katika kazi njema, matendo ya kimungu. (Yakobo 2:26) Kazi hizo ni kutia na kutangaza habari njema za ufalme wa Mungu. Mashahidi wana shauku ya kuwaambia wengine juu ya yale ambayo wamejifunza katika Neno la Mungu, Biblia, na kueleza jinsi maarifa hayo yamewapa tumaini kwa wakati ujao. Kama yule mkoma mwenye kuthamini, wao, pia, wanataka kumtukuza Mungu.
Je! wewe pia unahisi ukichochewa uzungumze juu ya baadhi ya mambo ambayo umejifunza katika Maandiko? Usiizuie tamaa hiyo. Unaweza kuanza kwa kuzungumza na washiriki wa jamaa, jirani, wafanyi kazi wenzi na marafiki. Unapofanya hivyo, utaona kwamba kuthamini kwako mwenyewe mambo ya kiroho kutaongezeka, ufahamu wako utaongezeka sana, na tamaa yako ya kujifunza zaidi itakua. Mithali moja ya Kimaandiko inasema hivi: “Mwelimishe mwenye hekima, naye atazidi kuwa na hekima; mfundishe mwenye haki, naye atazidi kuwa na elimu.” (Mithali 9:9) Mamilioni mengi ya watu kuthamini Mungu katika njia hiyo, na wanafanya hivyo wakiwa Mashahidi wa Yehova.
Basi, ni wazi kwamba tunaweza na tunapaswa kuonyesha kumthamini Mungu na wanadamu wenzetu. Twaweza kutoa shukrani kwa Mungu katika sala na kwa kutukuza sifa zake katika nyimbo. Zaidi ya yote, twaweza kumwonyesha Yehova Mungu kuthamini kwa kuzungumza na wengine juu ya kazi zake za ajabu.
Ikiwa unataka msaada wa kujifunza na kufanya mapenzi ya Yule aliyefanya vitu vyote, Mashahidi wa Yehova wako tayari kukusaidia. Ukiwa pamoja nao, unaweza kujua furaha inayoletwa na kuonyesha Mungu kuthamini kutoka moyoni.
[Picha katika ukurasa wa 7]
“Ni vizuri kama nini kuwa hai!”