Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 12/15 kur. 3-4
  • Ndoa Inashambuliwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ndoa Inashambuliwa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Hakuna Mtu Mkamilifu
  • Je, Ndoa Inaweza Kustahimili Msukosuko?
    Amkeni!—2006
  • Ikiwa Ndoa Imo Katika Hatua ya Kuvunjika
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Heshimu “Kile Ambacho Mungu Ameunganisha”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
  • Talaka Biblia Inasema Nini Hasa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 12/15 kur. 3-4

Ndoa Inashambuliwa

KUNA habari njema na habari mbaya kuhusu ndoa katika ulimwengu wa leo. Habari nzuri zatoka kwa mtaalamu wa maradhi ya akili kutoka Toronto, Dakt. Alan Lyall. Alimwambia ripota wa gazeti Toronto Star kwamba, ijapopatwa na mashambulizi mengi katika miaka ya karibuni, ndoa inarudia hali yake ya kawaida. Kwa sababu gani inakuwa hivyo? Yeye anajibu hivi: “Kwa kweli yaweza kuwa njia mojayapo ya maisha yenye kuridhisha na kutosheleza zaidi.”

Hata hivyo, habari mbaya ni kwamba ndoa nyingi ni zenye huzuni sana. Mwanamke mmoja kijana ambaye ni mwandishi wa habari za magazetini alisema: “Ninapotazama ndoa, sana sana ninaona maumivu. Na unapoacha kupatwa na maumivu unasikia vizuri sana.” Je! wewe una maoni kwamba ndoa ni njia ya maisha yenye kutosheleza au kwamba ni chanzo cha maumivu tu?

Haiwezi kubishwa kuna maumivu na mateso katika ndoa fulani-fulani. Mambo hayo yanaonekana katika hesabu kubwa sana ya talaka katika nchi ambazo talaka inaruhusiwa. Katika Marekani hesabu ya talaka iliongezeka mara tatu wakati wa miaka ishirini iliyopita. Katika Urusi yasemekana ndoa moja katika tatu mwisho wake ni talaka. Katika Australia hesabu ya talaka iliongezeka mara nne katika muda wa mwaka mmoja tu wakati sheria mpya ya talaka ilipoanzishwa. Kulingana na gezeti Financial Times la London, hesabu yenye kupanda juu ya talaka katika Uingereza iligharimu karibu dola bilioni mbili (pauni bilioni moja) kwa mwaka za malipo ya waliotalikwa pamoja na watoto.

Kwa sababu gani kuna msukusuko mwingi hivyo katika ndoa?

Hakuna Mtu Mkamilifu

Gumu moja ni kwamba hakuna mtu mkamilifu. Sisi sote tuna kasoro-kasoro zinazoweza kuudhi wengine. Tunapowaona watu pindi kwa pindi tu, kasoro hizo si za maana. Lakini tunapoishi na mtu katika ndoa, zaweza kuonekana kubwa sana. Zaweza kutokeza ugomvi wenye kuharibu. Au uhusiano huo waweza kutokeza jeuri. Katika Kanada, kwa mfano, mke mmoja katika kumi yasemekana anapigwa na mumewe.

Tofauti za nyutu, au za miradi, zaweza kutokeza matatizo makubwa. Inakuwaje mtu mwenye kusema-sema anapofunga ndoa na mtu anayependelea kunyamaza? Au wakati mwenzi mmoja anapothamini sana mali zaidi ya yule mwingine? Pengine mke aweza kuona ameshushiwa heshima iwapo mumewe hampi anasa zile zile alizokuwa akifurahia kwa babaye. Au huenda mume akatumia saa nyingi sana kazini na kumwacha mkewe peke yake, na hivyo kumfanya ajione mpweke.

Ulevi ni kisababishaji kingine kikubwa cha kuvunjika kwa ndoa. Uasherati ni kisababishaji kingine. Wengine, katika kizazi cha wakati huu chenye wendekevu, wana maoni kwamba kutokuaminika pindi kwa pindi kwaweza kufaidi. Walakini wachunguzi wanasema: “Kutokuaminika hakufai. Watu wengi sana wanafikiri uzinzi unaweza kuongeza ladha ya ndoa, lakini sikuzote uzinzi ulikuwa ishara ya kuwa na matatizo kweli kweli. Hilo halijapata kuwa jambo lisiloleta maumivu.” Ikithibitisha hilo, ripoti moja kutoka Uingereza ilionyesha uzinzi kuwa msingi wenye kutokeza talaka mara nyingi huko. Kwa kweli, mzinzi ‘anaiangamiza nafsi yake.’—Mithali 6: 32.

Je! umekwisha kufikiria pia, jinsi hali ya uchumi yenye kuharibika inavyoweza kuharibu ndoa? Wakati wote wawili, mume na mke, wanapokwenda kufanya kazi—kama wanavyofanya wengi leo—jamaa inakuwa na maelekeo ya kutengana. Na wakati wenzi wanapoingia katika deni kubwa, wasiwasi, uchungu na kulaumiana-laumiana kunatokea.

Tena, maelekeo ya kisasa ya watu ‘kufanya watakavyo’ yanaharibu imara ya ndoa. Wenzi wa ndoa wanaona vigumu kufaana katika mambo yenye kupendeza na yasiyopendeza mtu na mwenzake. Mara nyingi wanatazamia uhuru ule ule katika ndoa waliokuwa nao walipokuwa waseja. Watu waliofunga ndoa ambao hawawezi kusitawisha nia ya kutoa wana gumu kubwa.

Halafu watu wa ukoo wanaweza kuwa gumu, sana-sana katika nchi ambazo ndoa huonwa kuwa mwungano wa jamaa mbili mahali pa kuwa mwungano wa watu wawili tu. Katika sehemu hizo mkazo kutoka kwa watu wa ukoo waweza kuwa mkubwa. Mama ya mume huenda akawa mwenye kupiga ubwana, hata kwamba anakuwa kichwa, badala ya mume wa mke. Au pengine wazazi wa msichana mwenyewe wanasisitiza kumwambia anayopaswa kufanya, badala ya kuruhusu wenzi hao wachanga waishi maisha yao wenyewe.

Hayo ni baadhi ya magumu ambayo huenda wenzi wakapatwa nayo wanapofunga ndoa. Kwa hiyo, tunaweza kusema kwa kweli kwamba ndoa ingali inashambuliwa, ingali chini ya mkazo mkubwa. Je! itaokoka? Ndiyo, mpango wenyewe wa ndoa utaokoka, kwa sababu kweli kweli unaweza kuwa “njia mojayapo ya maisha yenye kuridhisha na kutosheleza zaidi.” Lakini bila shaka ndoa moja moja zaweza kushindwa na vita hiyo. Je! wewe unajua jinsi ya kuepuka matokeo hayo yenye huzuni?

[Picha katika ukurasa wa 3]

ULEVI

KUTOKUAMINIKA

KUPENDA MALI

MKAZO KUTOKA KWA WATU WA UKOO

DENI

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki